Dini ya Uislamu Inatangazwa kupitia Dalili zitokanazo na Qur'ani na Sunnah za Mbora wa Viumbe. (⮫)


دين الإسلام تعرضه نصوص القرآن وسنة خير الأنام

 Dini ya Uislamu Inatangazwa kupitia Dalili zitokanazo na Qur'ani na Sunnah za Mbora wa Viumbe.

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa Rehema Mwenye kurehemu.

  Utangulizi

Hakika kila sifa njema zinamstahiki Mwenyezi Mungu, tunamhimidi yeye na tunamtaka msaada yeye, na tunamuomba msamaha, na tunajilinda kwa Mwenyezi Mungu kutokana na shari ya nafsi zetu, na ubaya wa matendo yetu, aliyemuongoza Mwenyezi Mungu hakuna wa kumpoteza, na aliyempoteza hakuna kipenzi wa kumuongoa, na ninashuhudia kuwa hapana Mola isipokuwa Mwenyezi Mungu, yeye pekee asiye na mshirika wake, na ninashuhudia kuwa Muhammadi ni mja wake na ni Mtume wake, Amani ya Mwenyezi Mungu iwe juu yake, amani na salamu nyingi.

Baada ya hayo

Leo hii Kwa hakika kuna haja kubwa ya kupatikana Kitabu kipana na kifupi, kinachoitangaza dini ya uislamu kwa ujumla wake, sawa sawa iwe ni katika mambo yanayohusu Itikadi, au Ibada, au Miamala au Adabu au mambo mengine, Kwa kupitia kitabu hicho anaweza msomaji kujijengea fikra iliyo wazi yenye kuenea iliyokamilika kuhusu dini ya uislamu, na apate marejeo ndani ya kitabu hicho yule aliyeingia katika dini ya uislamu marejeo ya awali kabisa katika kujifunza hukumu za uislamu na adabu zake na kujifunza maamrisho yake na makatazo yake, na kipatikane kitabu hicho kwa walinganiaji katika njia ya Mwenyezi Mungu, wakikifasiri kitabu hicho katika Lugha zote, na kumpatia kila mwenye kuuliza kuhusu dini ya uislamu, na kila mwenye kuingia katika dini ya uislamu, hivyo akaongoka kwa kitabu hicho yule aliyependa Mwenyezi Mungu kuongoka kwake, na wakati huo itasimama hoja na ufikishaji dhidi ya wapingaji na waliopotoka.

Na kabla ya kuanza kuandika kitabu hiki, ni lazima kuweka njia na vigezo ambavyo atashikamana navyo mtunzi; ili aweze kufikia lengo kuu la kitabu hiki, na tunataja miongoni mwa vigezo hivyo ni haya yafutayo:

Ni kuitangaza na kuidhihirisha dini hii kwa kupitia ushahidi wa Qur'ani tukufu na Sunnah za bwana Mtume zilizotakasika, na wala siyo kupitia mifumo ya Kibinadamu ya maneno ya kubishana na kukinaishana, na kufanya hivyo ni kwa kuchunga mambo mengi:

A- Nikuwa kwa kusikiliza maneno ya Mwenyezi Mungu Mtukufu, na kufahamu makusudio yake anaongoka amtakaye Mwenyezi Mungu kumuongoza na husimama hoja dhidi ya mpotevu mwenye kupinga, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na pindi yeyote, miongoni mwa washirikina, akiomba kuingia kwenye himaya yako, ewe Mtume, na akataka amani, basi mkubalie maombi yake ili apate kuisikia Qur’ani tukufu na auone uongofu wake, kisha mrudishe alikotoka akiwa kwenye usalama." [Al-Taubah:6], Na huenda hoja na ufikishaji usisimame kupitia usulubu wa kibinadamu na njia za maneno ambazo zimegubikwa na mapungufu.

B- Hakika Mwenyezi Mungu ametuamrisha kufikisha dini yake na wahyi wake kama alivyouteremsha, wala hakutuamrisha kuchagua njia za maneno yatokayo kwetu ili kuwaongoza watu tukidhani kuwa tutafika kwa maneno hayo kwenye nyoyo zao, kwa nini tunazisumbua nafsi zetu kwa kitu ambacho hatukuamrishwa kukifanya na tukaacha tulichoamrishwa kukifanya ?

C- Hakika njia nyingine ya Daa'wa, mfano kuwazungumzia kwa mapana kuhusu wendaji kombo wa wagomvi wetu, na kuwajibu hoja zao, katika nyanja za Itikadi au za Ibada au za Tabia au za kiadabu na uchumi, au kutumia mijadala ya kifikra na kiakili,kama kuzungumzia kuhusu kuthibitisha uwepo wa Mwenyezi Mungu- Ametukuka Mwenyezi Mungu utukufu wa hali ya juu kwa wanayomsingizia Madhalimu, au kuzungumzia mabadiliko yaliyopo katika Injili na Taurati na vitabu vya Dini zingine, na kuyaweka wazi mapungufu yake na ubatili wake. Na yote hayo yanafaa kuwa ndiyo njia ya kuweka wazi ubovu wa misingi na Itikadi za wagomvi wetu, na inafaa vilevile iwe ni akiba ya utamaduni wa muislamu- pamoja nakuwa haimdhuru kutoijua- lakini haifai moja kwa moja kuwa ndio msingi na muelekeo ambao unasimamia ujumbe wa Mwenyezi Mungu.

D- Ni kuwa wale ambao wanaingia katika uislamu kwa kupitia njia hizi zilizokwisha tajwa, siyo lazima kuwa wao watakuwa ni waislamu wa kweli, kwani hakika anaweza kuingia mmoja wao katika dini hii kwa kupendezwa na jambo fulani ambalo limezungumzwa kwa mapana, na huenda akawa haamini mambo mengine ya msingi katika mambo ya dini, kama mwenye kupendezwa - kwa mfano- pekee uliopo katika uchumi wa kiislamu, lakini haamini maisha ya akhera, au haamini kuwepo kwa majini na mashetani na vinginevyo.

Na Aina hii ya watu madhara yao katika uislamu ni makubwa kuliko manufaa yao.

E- Hakika Qur'ani ni mtawala wa Nafsi na nyoyo, Basi ikitokea kutenganishwa Qur'ani na nafsi, basi Nafsi zilizotakasika huitafuta Qur'ani na hupanda juu katika ngazi ya Imani na uchamungu, Basi ni kwanini itenganishwe kati ya Qur'ani na Nafsi?!.

Na kusiwe na muingiliano kati ya majibu ya kivitendo, na kubanwa kwa matukio, na kutumia uzoefu wa siku nyingi katika kuitangaza na kuidhihirisha dini hii, Bali dini hii hutangazwa kama ilivyoteremka, kwa kufuata muongozo wake nao ni kuwasemesha watu na kwenda nao hatua kwa hatua mpaka kufikia hatua ya kuwa na msimamo imara.

Na azingatie sana katika uandishi kutumia mfumo mpana, na kufupisha kwa kadiri iwezekanavyo, kiasi kwamba itakuwa rahisi kukibeba kitabu hicho na kukisambaza kwa watu.

Na tufanye kuwa tumeimaliza kazi hii, na tumekitafsiri kitabu hiki, na tumekichapisha nakala milioni kumi, na kikafika kitabu katika mikono ya watu milioni kumi, na wakaziamini Aya na Hadithi zilizomo ndani ya kitabu hiki asilimia 1% miongoni mwao, na wakazikufuru na kuzipinga aya na hadithi zilizoko humo watu asilimia 99%, na ikawa hii asilimia moja ni yenye kufanya bidii na kuwa na khofu, ikitarajia Imani na uchamungu, Hivi hujui ewe ndugu yangu mtukufu kuwa hii asilimia moja katika asilimia mia moja kuwa inamaanisha kuingia watu laki moja katika Dini ya Mwenyezi Mungu?. Na hili bila shaka ni mafanikio makubwa, Na ikiwa Mwenyezi Mungu atakuongozea mtu mmoja ni bora kwako kuliko kumiliki ngamia mwekundu.

Bali hata kama hakuamini yeyote katika hawa waliolinganiwa, na wote wakaipinga dini hii, kwa hakika tunakuwa sisi tumetekeleza amana na tumefikisha ujumbe aliotubebesha Mwenyezi Mungu.

Kwa hakika jambo la muhimu kwa walinganiaji katika njia ya Mwenyezi Mungu siyo kuwakinaisha watu kwa dini hii kwakuwa na pupa ya kuongoka kwao, kama ilivyo tajwa katika kitabu kitukufu. "Ikiwa utafanya pupa, ewe Mtume, kuwaongoa hawa washirikina, basi jua kuwa Mwenyezi Mungu Hamuongoi mpotoshaji" [Surat Nahli 37], Lakini jambo lao la muhimu zaidi ni lile jambo la muhimu kwa Nabii wao alilosemeshwa na Mola wake -Aliyetakasika na kutukuka- "Ewe Mtume, fikisha wahyi wa Mwenyezi Mungu uliyoteremshwa kwako kutoka kwa Mola wako. Na iwapo utapunguza bidii katika kuufikisha, ukaficha chochote katika wahyi huo, basi utakuwa hukuufikisha ujumbe wa Mola wako. Na Mwenyezi Mungu anakulinda na kukuokoa na maadui zako". [Al Maaida: 67].

Tunamuomba- Mwenyezi Mungu Mtukufu- Tuwe sote kwa pamoja ni wenye kusaidiana kufikisha Dini ya Mwenyezi Mungu kwa watu wote, na atufungulie milango ya Kheri na wenye kulingania katika mlango huo, na atufungie milango ya shari na kusimama mbele yake, na Mwenyezi Mungu ni mjuzi zaidi. Na Rehema na amani ziwe juu ya Mtume Muhammad.

 §  Kipenzi changu msomaji.

Kitabu hiki ambacho kiko mikononi mwako kinakufahamisha kuhusu uislamu, kwa Taswira pana na iliyoenea sehemu zake zote (Itikadi zake, Adabu, Sheria na Mafunzo yake yote).

Na kwa hakika nimechunga mambo mengi ya msingi katika kitabu hicho:

La Kwanza: Kutilia umuhimu misingi ya dini ambayo dini imesimama kwa misingi hiyo.

La Pili: Kufupisha kwa kadiri iwezekanavyo.

La Tatu: Kuutangaza uislamu kupitia vyanzo vyake asili (Qur'ani tukufu, Hadithi za Bwana Mtume- Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani-) pale ambapo msomaji anasimama moja kwa moja mbele ya Chemchem ya misingi ya uislamu akinywa moja kwa moja muongozo wake na mafundisho yake kutoka katika chemchem.

Na utakuta ewe kipenzi changu msomaji, baada ya kufika mwisho wa kitabu hiki, kuwa imejengeka kwako fikra iliyowazi kuhusu dini ya uislamu, kiasi kwamba utaweza baada ya hapo kupanda ngazi katika kuinua akiba ya elimu kuhusu dini hii.

Hakika kitabu hiki ambacho kiko mikononi mwako ni muhimu kwa kundi kubwa la watu, na kinawapa kipaumbele kwa daraja la kwanza wale wenye mapenzi makubwa ya kuingia katika uislamu, na kujifunza Itikadi zake na adabu zake na hukumu zake.

Kama ambavyo kinatoa kipaumbele kwa wenye kutilia umuhimu wa kuzitambua dini mbalimbali ambazo zinakimbiliwa na Mamilioni ya watu wengi, vilevile huwatilia umuhimu marafiki wa uislamu waliokaribu na uislamu na wenye kupendezwa na baadhi ya mambo yake, na pia kinawatilia umuhimu maadui wa uislamu na wenye kuuchukia na kukaa nao mbali, na wale ambao huenda ikawa kutokuujua uislamu ikawa ni moja ya sababu ya msingi ya kuufanyia uadui na kuuchukia uislamu.

Na miongoni mwa wanaopewa kipaumbele na kitabu hiki kwa nafasi ya juu kabisa ni wale waislamu ambao wanapenda kuifafanua dini ya uislamu kwa watu, Basi kitabu hiki kinawafupishia jitihada na kuwafanyia wepesi na kinawapunguzia kazi pia.

Na kwa hakika unaweza kukuta ewe msomaji mwenye akili timamu-kama ulikuwa huna fikra ya uislamu huko nyuma- kuwa wewe unahitajia kutilia umuhimu wa hali ya juu na kusoma kwa umakini ili ujue maana iliyogubikwa na kitabu hiki, na wala usione dhiki kwa hilo kwani kuna tovuti nyingi za kiislamu zinazojibu maswali yako.

  1- Neno la Tauhidi (Laa ilaaha illa llaahu) Hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu peke yake.

Msingi muhimu wa dini ya kiislamu ni neno la Tauhidi (Laa ilaaha illa llahu) na bila msingi huu madhubuti jengo la uislamu haliwezi kusimama imara, na hilo ni neno la kwanza ambalo anatakiwa kulitamka mtu mwanzo anapoingia katika uislamu akiwa analiamini neno hilo na kuamini maana zake zote na vyenye kutokana na maana yake. Basi ni nini maana ya (Laa ilaaha illa llahu)?

Hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu makusudio yake ni:

- Hakuna muumba wa Ulimwengu isipokuwa Mwenyezi Mungu pekee.

- Hakuna Mmiliki na muendeshaji wa huu Ulimwengu isipokuwa ni Mwenyezi Mungu pekee.

-Hakuna Mwenye kuabudiwa anayestahiki kufanyiwa ibada isipokuwa Mwenyezi Mungu pekee.

Mwenyezi Mungu ndiye aliyeuumba ulimwengu huu mpana na mzuri wa hali ya juu. Mbingu hizi na nyota zake kubwa na Sayari zake zenye kutembea, zinatembea katika nidhamu iliyopangika vyema, na harakati za kupendeza, hakuna mwenye kuzishika mbingu hizo isipokuwa Mwenyezi Mungu. Na Ardhi hii na milima yake na mabonde yake na mito yake, na miti yake na mimea yake, pamoja na hewa yake na maji yake, nchi kavu yake na bahari yake, na kila mwenye kuishi humo na mwenye kutembea juu yake, bila shaka kabisa vyote hivi ameviumba Mwenyezi Mungu na akavileta kutoka katika kutokuwepo.

Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu katika Qur'ani tukufu: "Na alama kwao (ya utendaji kazi wa Mwenyezi Mungu) ni jua ambalo linatembea hadi kituo chake Alichokikadiria Mwenyezi Mungu, halitakipita kituo hicho wala halitatulia kabla ya kukifikia. Huo ni mpango wa Mshindi Asiyeshindwa, Mjuzi Ambaye hakuna kitu chochote kinachofichikana katika ujuzi Wake". "Na mwezi ni alama katika viumbe vyake. Tumeukadiria uwe na njia za kupitia kila usiku. Unaanza ukiwa mwezi mwandamo mdogo sana na unaendelea kuwa mkubwa mpaka unakuwa mwezi mkamilifu mviringo, kisha unarudi kuwa mdogo kama shuke la mtende kuuku lililolegea". "Kila kimojawapo kati ya jua, mwezi, usiku na mchana, kina wakati ambao Mwenyezi Mungu Ameukadiria, na hakitangulii kikapita wakati huo. Haiwezekani kwa jua kuufikia mwezi likaufuta mwangaza wake au ukageuza njia yake ya kupitia. Na haiwezekani kwa usiku kuutangulia mchana ukauingilia kabla ya wakati wake kumalizika. Na kila kimojawapo kati ya jua, mwezi na nyota viko katika anga vinaogelea". [Surat Yaasin 38- 40].

"Na ardhi tumeipanua na kuitandika, na tukaweka humo majabali yaliyojikita, ili ardhi isiende mrama na watu wake, na tukaotesha humo kila aina ya mimea yenye mandhari ya kupendeza na yenye kunufaisha, inayomfurahisha mwenye kuiangalia". "Ili viwe ni mazingatio ya kumfanya mtu aone na atoke kwenye giza la ujinga, na ni ukumbusho kwa kila mja mnyenyekevu, mwenye kucha (kumcha Mungu) na kuogopa, mwenye kurejea sana kwa Mwenyezi Mungu Aliyeshinda na kutukuka". "Na tumeteremsha kutoka juu mvua yenye manufaa mengi, tukaotesha kwayo mabustani yenye miti mingi na nafaka za mimea ya nafaka zinazovunwa". "Na tukaotesha mitende mirefu yenye makarara yaliyojaza na kupandana". [Surat Qaaf 7-10]

Huu ndiyo uumbaji wa Mwenyezi Mungu Mtukufu, Ameifanya Ardhi kuwa ni tulivu na akaweka humo vyenye kuvutia kwa kiwango kinachoendana na uhitaji wa maisha, Basi hazidishi mpaka ikawa ni uzito kutembea juu yake, wala hapunguzi kiasi cha kushindwa kuenea humo viumbe hai na kila kitu kwake yeye kimewekwa kwa kiasi maalumu.

na ameshusha kutoka mawinguni maji yaliyo masafi na wala hayawezi kuendelea maisha isipokuwa kupitia maji. {Na tumejaalia kutokana na maji kila kitu kuwa Hai} [Al Anbiyaai 30]. Na akatoa kutokana na maji mimea na matunda na wakanyweshelezwa kwa maji hayo wanyama na wanaadamu, na akaiandaa ardhi ili iyahifadhi maji hayo na akafuatishia humo chemchem na mito.

Na akaotesha katika ardhi mabustani yenye kuvutia kwa miti na maua yake na uzuri wake wenye kuvutia Mwenyezi Mungu Ambaye ameumba kila kitu kwa namna nzuri na akaanza kumuumba mwanadamu kutokana na udongo.

Hakika mwanadamu wa kwanza aliyemuumba Mwenyezi Mungu ni Baba wa wanadamu naye ni Adam - juu yake amani- kisha akamtengeneza sawa na akamuwekea sura na akampulizia roho itokayo kwake , kisha akamuumba kutokana na huo udongo mke wake kisha, akakifanya kizazi chake kilichotokana na udongo kikatokana na maji madhalilifu (Manii).

Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na kwa hakika tulimuumba Ādam kutokana na udongo uliochukuliwa kutoka ardhi yote". "Kisha tukamuumba kwa tone la manii" "Kisha tukaliumba tone hilo kwa kuligeuza kulifanya pande la damu iliyo nyekundu, kisha tukaliumba pande la damu kwa kuligeuza kulifanya kinofu cha nyama kadiri ya kutafunika baada ya siku arobaini, na tukakiumba kinofu cha nyama kilicho laini kwa kukigeuza kukifanya mifupa, na tukaivisha nyama ile mifupa, kisha tukamfanya ni kiumbe kingine kwa kupulizia roho ndani yake. Ametukuka Mwenyezi Mungu Mwenye kheri nyingi Ambaye Ametengeneza umbo la kila kitu". [Al Mu'uminun: 12-14].

Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mnayaonaje maji ya manii mnayoyatupa ndani ya vizazi vya wake zenu", "Je nyinyi ndio mnaomuumba mwanadamu kutokana na hayo au ni sisi ndio wenye kuumba?" "Sisi tumekadiria kati yenu kifo na wala hatutoshindwa kuwafufueni" tena. "Na sisi si wenye kushindwa kubadilisha umbo lenu Siku ya Kiyama na kuwaumba kwa sifa na namna msizozijua". [Suratil Waaqiyah 58-68].

Zingatia kukuumba kwako Mwenyezi Mungu utaona maajabu makubwa kutokana na kuweka vyombo vidogo sana na nidhamu iliyo na mpangilio maalumu ambao haijulikani kazi yake isipokuwa twajua kidogo sana licha ya kujua mpangilio wake, kwa mfano hiki chombo kilichokamilika kwa ajili ya kumeng'enya chakula, mpangilio wake unaanzia kwenye mdomo kwa kukata chakula vipande vidogo ili iwe ni wepesi katika kusaga na kisha hatua ya kooni hutupa tonge kwenye koromeo na hufungua mlango wa kudaka tonge na kufunga mlango wa hewa kisha tonge huteleza kwenda tumboni kwa kupitia kidaka tonge chenye kutikisika mtikisiko kama mdudu, Na kwenye utumbo mpana kunaendelea kazi ya kumenge'nya chakula na hapo kinabadilika chakula na kuwa kimiminika kinachofungua tundu la utumbo mpana na kuelekea kwenye maingilio ya utumbo mwembamba na huko hundelea kazi ya kumeng'enya ambayo ni kazi ya kukibadilisha chakula kutoka kwenye hali yake ya uchakula (ghafi) na kukifanya kufaa kuwa lishe ya viungo vya mwili. Kisha kutoka katika utumbo mpana chakula huelekea kwenye utumbo mwembamba na hapo ndipo hukamilika umenge'nyaji wa mwisho na kwa sura hii chakula kinakuwa ni chenye kufaa kunyonywa kupitia nyuzinyuzi zilizopo kwenye Matumbo ili kipite pamoja na mfumo wa damu. Na hicho ni chombo kilichokamilika cha mzunguko wa damu ambao huzunguka katika mishipa ya damu iliyofungana na lau kama itanyooshwa urefu wake ungezidi zaidi kilomita elfu moja zilizoshikana katika pampu iliyopo katikati huitwa moyo. Moyo huo hauchoki katika kuhamisha damu kupitia mishipa hiyo imara.

Na kuna chombo kingine cha kupumulia, na cha Nne ni cha neva-Mishipa- na cha Tano ni cha kutoa uchafu, na cha Sita na Saba na mpaka cha Kumi ni katika vile ambavyo tunaendelea kuvijua kila siku na vile tusivyovijua ni vingi kuliko tunavyovijua. Basi ni nani aliyemuumba huyu mwanadam kwa namna hii nzuri asiyekuwa Mwenyezi Mungu?.

Kwa hivyo ni kosa kubwa sana hapa ulimwenguni kumfanyia Mwenyezi Mungu mshirika hali ya kuwa yeye ndiye aliyekuumba wewe.

Elekea kwa moyo mkunjufu na kwa roho safi na zingatia mwanzo wa uumbaji wa Mwenyezi Mungu Mtukufu hewa ambayo unayoivuta na inapenya kuja kwako toka katika sehemu pasi na kuonekana rangi yake, na lau kama ingekatika hewa hiyo kwa dakika chache ungekosekana uhai, Hakika haya maji ambayo unayoyanywa, na hicho chakula ambacho unakila, na mwanadamu umpendaye, na hii Ardhi ambayo unatembea juu yake, na ile mbingu ambayo unaiona, kila ambacho macho yako yanakiona na yasichokiona katika viumbe vikubwa au vidogo, vyote hivyo ni viumbe vya Mwenyezi Mungu Muumba aliye mjuzi wa mambo yote.

Hakika kufikiria viumbe vya Mwenyezi Mungu vinatujuza utukufu wa Mwenyezi Mungu na uwezo wake, na miongoni mwa watu wapumbavu wa hali ya juu na wajinga na waliopotea ni mwenye kuona huu uumbaji uanzilishi mtukufu ulioshikana uliopangika, wenye kujulisha juu hekima ya hali ya juu na uwezo usiokuwa na mipaka, kisha mtu huyo hamuamini muumba ambaye amemfanya awepo kutoka katika kutokuwepo. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Je, wameumbwa hawa washirikina bila kuwepo mwenye kuwaumba na kuwapatisha au wao wamejiumba wenyewe?" Na yote mambo mawili haya yametenguka na hayawezekani. Na kwa hivyo, inalazimika kuwa Mwenyezi Mungu Ndiye Aliyewaumba, na Yeye Peke Yake Ndiye Ambaye hakuna anayepasa kuabudiwa, wala kufaa kuabudiwa, isipokuwa Yeye. "Au wao wameumba mbingu na ardhi kwa ustadi huu wa kipekee? Bali wao hawaamini adhabu ya Mwenyezi Mungu, kwa kuwa wao ni washirikina". [Attur: 35-36].

Hakika Mwenyezi Mungu kutakasika na machafu ni kwakwe na mtukufu, linamtambulisha uwepo wake umbile salama pasina kuwa na haja ya kufundishwa, hakika amelifanya umbile ni lenye kujikuta katika kuumbwa kwake ni lenye kuelekea na kukimbilia kwake, lakini umbile hilo ni lenye kupotoshwa na kuwekwa mbali naye - Mwenyezi Mungu aliyetakasika na machafu.

Na hivyo ikiwa atapatwa na tatizo, msiba au dhiki ya hali ya juu na matatizo na yakampata majanga makubwa akiwa pwani au baharini, atakimbilia moja kwa moja kwa Mwenyezi Mungu kutaka kutoka kwake msaada na kuepushwa na aliyokuwa nayo, na Mwenyezi Mungu- kutakasika na machafu ni kwake- humjibu aliyedhurika pindi anapomuomba na humuondoshea mabaya.

Na huyu Muumba mtukufu ni mkubwa kuliko kila kitu, hapimishwi na chochote katika viumbe wake, naye ni mkubwa ambaye ukubwa wake hauna ukomo wala hakuna mwenye ujuzi uliokamilika kwa kujua hilo. Mwenye kusifika na sifa za utukufu wa hali ya juu zaidi ya viumbe wake juu ya mbingu zake. "Hapana kitu mfano wake, naye ni Mwenye kusikia Mwenye kuona" [Ash-shura: 11]. Hafanani na chochote katika viumbe vyake na lolote ulifikirialo akilini mwako kuhusu yeye basi Mwenyezi Mungu hayuko hivyo.

Anatuona Mwenyezi Mungu akiwa juu ya mbingu zake na sisi hatumuoni: "Macho hayamuoni Mwenyezi Mungu ulimwenguni. Ama kwenye nyumba ya Akhera, Waumini watamuona Mola wao bila kumueneza. Na Mwenyezi Mungu, kutakata na sifa za upungufu ni Kwake, anayafikia macho na kuyazunguka, na kuyajua vile yalivyo. Na Yeye ni Al-Latīf (Mpole) kwa mawalii Wake (vipenzi vyake), Anayejua mambo yenye upeo wa udogo, Al-Khabīr (Mtambuzi) Anayejua mambo ya ndani". [Suratul An'aam 103], Bali hisia zetu na nguvu hazistahamili kumuona hapa duniani.

Na kwa hakika mmoja miongoni mwa Manabii wa Mwenyezi Mungu alitaka kumuona, naye ni Nabii Mussa -Amani iwe juu yake- na Mwenyezi Mungu alipomsemesha mbele ya mlima Sinai: Akasema Ewe Mola wangu jitokeze ili nikuone, akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu kumwambia Mussa: «Hutoniona!»Yaani hutaweza kuniona ulimwenguni. «Lakini liangalie jabali, likitulia mahali lilipo ndipo nitakapojitokezea, basi utaniona.» Alipojitokeza Mola wake kwa lile jabali alilifanya lipondeke liwe sawa na ardhi. Hapo Mūsā alianguka akazimia. Alipopata fahamu kutoka kwenye hali ya kuzimia alisema, «Umetakasika, ewe Mola wangu, na kila sifa isiyolingana na utukufu wako, mimi natubia kwako kutokana na kuomba kwangu kukuona katika uhai huu wa kiulimwengu, na mimi ni wa mwanzo wa wenye kukuamini miongoni mwa watu wangu.» [Suratul Aaraf 143], Basi ule mlima mkubwa na mrefu ulisambaratika na kusagikasagika kwa kutokeza kwake Mwenyezi Mungu, basi vipi anaweza mwanadamu kuhimili kwa nguvu zake zilizo dhaifu na mnyonge.

Na katika sifa za Mwenyezi Mungu - kutakasika na machafu ni kwake - ni kuwa kwake yeye juu ya kila kitu ni muweza. {Na hakuwa Mwenyezi Mungu ni mwenye kushindwa na chochote kilichopo mbinguni wala Ardhini} [surat faatwir 44].

Mkononi mwake kuna uhai na kifo. Wanahitajia kutoka kwake viumbe wote, naye ni mwenye kujitosheleza kwa viumbe vyote Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Enyi watu! Nyinyi ndio wahitaji kwa Mwenyezi Mungu katika kila kitu, hamjitoshelezi Naye hata kiasi cha kupepesa jicho. Na Yeye, kutakasika na sifa za upungufu ni Kwake, Ndiye Mwenye kujitosheleza na watu na kila kitu miongoni mwa viumbe Vyake, Mwenye kushukuriwa kwa dhati Yake na majina Yake na sifa Zake", Anayeshukuriwa kwa neema Zake. Kwani kila neema waliyo nayo watu inatoka Kwake. Sifa njema zote ni Zake na shukrani kwa kila namna. [Surat Faatwir 15].

Na miongoni mwa sifa zake - kutakasika na machafu ni kwake - Ni ujuzi wake ulioenea katika kila kitu: "Na kwa Mwenyezi Mungu , Aliyetukuka na kuwa juu, kuna( mafātih al-ghayb), yaani: Funguo za hazina za mambo ya ghaibu yaliyofichikana, hakuna azijuwazo ila Yeye. Miongoni mwazo ni ujuzi wa Kiyama, kuteremka mvua, viliyomo ndani ya zao, matendo ya siku zinazokuja na mahala mtu atakapokufa. Na Anajua kila kilichoko barani na baharini. Na hakuna jani, linaloanguka kutoka kwenye mmea wowote, isipokuwa Analijua. Na kila chembe iliyofichikana ardhini na kila kibichi na kikavu, kimethibitishwa kwenye kitabu kilicho wazi kisicho na utatizi nacho ni Al-Lawh(Al-Maḥfūẓ ( Ubao Uliohifadhiwa) [Al An'am: 59]. Anajua yote yanayozungumzwa na ndimi zetu na yanayo fanywa na viungo vyetu bali yanayofichwa na vifua vyetu yote hayo anayajua. "Mwenyezi Mungu, Aliyetakasika na kila sifa ya upungufu, Anakijua kile kinachopitishwa na mtazamo wa macho kwa njia ya siri na kuiba na kile ambacho mtu anakidhamiria katika nafsi yake kizuri au kibaya". [Surat Ghaafir 19].

Na Mwenyezi Mungu ni mwenye kutufuatilia na mwenye kujua hali zetu hakijifichi kwake yeye chochote kilichopo Ardhini wala mbinguni haghafiliki wala hasahau wala halali, Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mwenyezi Mungu Ndiye Ambaye hakuna yeyote anayestahiki uungu na kuabudiwa isipokuwa Yeye. Ndiye Aliye hai Ambaye Amekusanya maana yote ya uhai mkamilifu unaolingana na utukufu Wake. Ndiye Msimamizi wa kila kitu. Kusinzia hakumshiki wala kulala. Kila kilichoko mbinguni na kilichoko ardhini ni miliki Yake. Na hatojipa ujasiri mtu yeyote kuombea mbele Yake isipokuwa kwa ruhusa Yake. Ujuzi Wake umevizunguka vitu vyote vilivyopita, vilivyoko na vitakavyo kuja. Anajua yaliyo mbele ya viumbe katika mambo ambayo yatakuja na yaliyo nyuma yao katika mambo yaliyopita. Na hakuna yeyote, katika viumbe, mwenye kuchungulia chochote katika elimu Yake isipokuwa kadiri ile ambayo Mwenyezi Mungu Amemjulisha na kumuonyesha. Kursiy Yake imeenea kwenye mbingu na ardhi. Kursiy ni mahali pa nyayo za Mola, uliyo mkubwa utukufu Wake, na hakuna ajuwaye namna ilivyo isipokuwa ni Mwenyezi Mungu Aliyetukuka. Wala hakumuelemei Mwenyezi Mungu Aliyetakata kuzitunza. (hizo mbingu na ardhi).Yeye Ndiye Aliye juu ya viumbe Vyake vyote, kwa dhati Yake na sifa Zake, Aliyekusanya sifa za utukufu na kiburi". Aya hii ni aya tukufu zaidi katika Qur’ani, na inaitwa Āyah al- Kursīy. [Al Baqara: 255].

Ana sifa zilizokamilika ambazo hazina mapungufu wala aibu.

Ana majina mazuri na sifa za hali ya juu. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na Mwenyezi Mungu, kutakata na sifa za upungufu ni Kwake na kutukuka ni Kwake, Ana Majina Mazuri yanayoonyesha ukamilifu wa uwezo Wake, na majina Yake yote ni mazuri. Basi ombeni kutoka Kwake, kwa majina Yake, mnachotaka na waacheni wale wanaogeuza majina Yake kwa kuzidisha na kupunguza au kupotoa, kama kumuita kwa majina hayo asiyeyastahiki, kama vile washirikina wanavyowaita, kwa majina hayo, waungu wao, au ayape majina hayo maana ambayo Mwenyezi Mungu Hakuitaka wala Mtume Wake. Basi watapata malipo ya matendo yao mabaya waliokuwa wakiyafanya ulimwenguni ya kumkanusha Mwenyezi Mungu, kuyapotoa majina Yake na kuwafanya waongo Mitume Wake". [Suratul Al-aaraf 180].

Na Mwenyezi Mungu -kutakasika na machafu ni kwake- hana mshirika wake katika ufalme wake wala hana msaidizi wala wa kufananishwa naye.

Ametakasika -kutakasika na machafu ni kwake- kuwa na mke na pia kuwa na mtoto, bali yeye amejitosheleza kwa hayo yote Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: Sema, ewe Mtume, «Yeye Ndiye Mwenyezi Mungu Aliyepwekeka kwa ustahiki wa kuabudiwa, uumbaji na utakatifu wa Majina na Sifa, Asiye na mshirika katika hayo". «Mwenyezi Mungu Ambaye Peke Yake Ndiye Mwenye kukusudiwa kwa kukidhi haja na matakwa. «Hakuzaa wala hakuzaliwa. «Wala hakuna yeyote katika viumbe Vyake mwenye kufanana wala kushabihiyana naye katika Majina Yake, Sifa Zake wala vitendo Vyake.» [Al Ikhlaswi: 1-4]. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na hawa makafiri walisema, «Mwenyezi Mungu amejifanyia mtoto.» "Kwa hakika mmeleta, enyi wenye wasemaji, kwa kusema neno hili, jambo kubwa lililo baya. "Zinakaribia mbingu kupasuka kwa ubaya mkubwa wa neno hilo, ardhi kuvunjika vipande-vipande majabali kuanguka kwa nguvu kwa kukasirika kwa ajili ya Mwenyezi Mungu" "kwa kumnasibishia mtoto, Mwenyezi Mungu". "Haifai kwa Mwenyezi Mungu na hainasibiani na Yeye Awe na mtoto, kwani kuwa na mtoto ni dalili ya upungufu na mahitajio, na Mwenyezi Mungu Ndiye Mkwasi Mwenye kuhimidiwa Aliyeepukana na sifa zote za upungufu". "Hakuna aliye mbinguni, miongoni mwa Malaika, wala aliye ardhini, miongoni mwa binadamu na majini, isipokuwa atamjia Mola wake Siku ya Kiyama akiwa ni mja mdhalilifu mnyenyekevu mwenye kukubali uja wake Kwake". [Mariam: 88-93].

Na yeye -aliyetakasika na machafu-ni mwenye kusifika na sifa za utakasifu na uzuri na nguvu na utukufu na utawala na ufalme na nguvu.

Na yeye vile vile husifika na sifa ya ukarimu na msamaha na huruma na hisani, hivyo yeye ni mwingi wa rehema ambayo imeenea rehema yake kila kitu.

Mwenye kurehemu ambaye huruma yake imeishinda hasira zake.

Na ni mkarimu ambaye ukarimu wake hauna ukomo wala hazina yake ya ukarimu haiishi.

Na majina yake yote ni mazuri yanajulisha juu ya sifa zilizokamilika ambazo hapasi kua na sifa hizo isipokuwa Mwenyezi Mungu.

Na kuzijua sifa zake kunauzidishia moyo mapenzi na utukufu, na kuogopa na kunyenyekea kwa ajili ya Mwenyezi Mungu.

Na kwa hivyo basi inakuwa maana ya Laa ilaaha illa llaahu ni kuwa kisifanywe chochote ambacho ni katika ibada isipokuwa kwa ajili ya Mwenyezi Mungu na hakuna mwenye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu, na Mwenyezi Mungu ndiye mwenye kusifika na sifa za Uungu na ukamilifu naye ndiye muumba mwenye kutoa riziki mwenye kuneemesha mwenye kuhuisha mwenye kufisha, aliye bora zaidi kwa viumbe wake basi yeye pekee ndiye anayestahiki kuabudiwa na hana mshirika wake.

Na yeyote atakaye kataa ibada ya Mwenyezi Mungu au akamuabudu asiyekuwa Mwenyezi Mungu, kwa hakika atakuwa ameshirikisha na amekufuru.

Na haipasi kusujudu na kurukuu na kunyenyekea na kusali isipokuwa kwa ajili ya Mwenyezi Mungu.

Na wala haombwi msaada isipokuwa Mwenyezi Mungu, wala haelekewi kwa dua isipokuwa Mwenyezi Mungu, wala usiombe haja yoyote isipokuwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu, na wala hakutafutwi ukaribu kwa namna yeyote wala utiifu wa kuabudiwa isipokuwa ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu. Sema,«Hakika Swala yangu na kuchinja kwangu wanyama, na uzima wangu na kufa kwangu yote ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu muumba wa walimwengu wote. «Asiye na mshirika katika uungu Wake wala katika Ulezi Wake wala katika majina Yake na sifa Zake. Kumpwekesha huko Mwenyezi Mungu kulikosafishika ndiko Alikoniamrisha mimi Mola wangu, Aliyetukuka na kuwa juu. Na mimi ni wa kwanza kumfuata Mwenyezi Mungu kikamilifu katika umma huu.» [Suratul An-am 162-163].

 §  B- Kwanini Ametuumba Mwenyezi Mungu?

Majibu ya swali hili zito yako katika umuhimu wa hali ya juu lakini ni lazima kutegemea majibu kutoka katika wahyi wa Mwenyezi Mungu, Basi Mwenyezi Mungu ndiye ambaye ametuumba na yeye ndiye ambaye anatupa habari kuhusu lengo lake la kutuumba sisi, amesema - aliyetukuka jambo lake- "Na sikuumba majini na binadamu na kutimiliza Mitume wote isipokuwa kwa lengo tukufu, nalo niabudiwe mimi Peke Yangu, na sio asiyekuwa mimi". [Adh Dhariyati: 56]. Hivyo Utumwa, ndiyo sifa inayowakusanya viumbe wote wa Mwenyezi Mungu viumbe ambao hakuna awezaye kuidhibiti idadi yake, miongoni mwao ni Malaika na wengineo, ni katika maajabu ya uumbaji wa Mwenyezi Mungu, umma wote huu una umbile uliloumbiwa kwa kujengewa maisha ya kuwa ni wenye kumuabudu na kumtakasa Mwenyezi Mungu Mola wa viumbe wote. "Zinamtakasa Yeye, kutakata ni Kwake, mbingu saba na ardhi na viumbe wote waliyo humo. Na kila kitu kilichoko katika ulimwengu huu kinamuepusha Mwenyezi Mungu Aliyetukuka na sifa za upungufu, maepusho yanayofungamana na kumsifu na kumshukuru, kutakata ni Kwake, lakini nyinyi, enyi watu, hamtambui hilo. Kwa kweli, Yeye ni Mpole kwa waja Wake, hawaharakishii adhabu wanaomuasi, ni Mwingi wa msamaha kwao". [Al- israa 44]. Na Malaika wanausiwa na kulazimishwa kujitakasa kama ambavyo wanadamu wanausiwa kuzitakasa nafsi.

Lakini Utumwa wa mja kumuabudu Mola wake ni wa hiyari na siyo wa kulazimishwa (Ni hiyari na hiyari hiyo ni mtihani) "Mwenyezi Mungu Ndiye Aliyewafanya nyinyi mpatikane kutoka kwenye hali ya kutokuwepo, kati yenu kuna wenye kuukanusha uungu Wake na baadhi yenu kuna wenye kuuamini na kufuata Sheria Zake kivitendo. Na Yeye, kutakasika na kila sifa za upungufu ni Kwake, ni Mwenye kuviona vitendo vyenu, hakuna chochote chenye kufichikana Kwake, na Atawalipa kwavyo". [Surat Taghaabun 2]

"Je hujui, ewe Mtume, kwamba Mwenyezi Mungu, kutakata na sifa za upungufu ni Kwake, wanamsujudia Yeye, katika hali ya kunyenyekea na kufuata amri, Malaika walioko mbinguni, viumbe walioko ardhini, jua, mwezi, majabali, miti na wanyama? Na wanamsujudia Mwenyezi Mungu, kwa kutii na kwa hiari, watu wengi, nao ni Waumini. Na kuna watu wengi imepasa adhabu juu yao, na kwa hivyo wao ni watwevu (madhalili). Na yeyote yule ambaye Mwenyezi Mungu Amemtweza (Amemdhalilisha) hakuna yeyote wa kumtukuza. Hakika Mwenyezi Mungu Anafanya kwa viumbe vyake Atakalo kulingana na hekima Yake". [Suratil Hajj 18]

Mwenyezi Mungu ametuumba ili tumuabudu na atupime ufaulu wetu katika kufanikisha ibada hii, Basi yeyote atakaye muabudu Mwenyezi Mungu na akampenda na akanyenyekea kwake na akatii maamrisho yake na akajiepusha na makatazo yake, Hupata radhi za Mwenyezi Mungu na rehema zake na mapenzi yake na Mwenyezi Mungu humlipa malipo yaliyo mazuri. Na atakaye kataa kumuabudu Mwenyezi Mungu ambaye amemuumba na akamruzuku, na akafanya kiburi kwa kuacha kufanya ibada, na akakataa kufuata maamrisho ya Mwenyezi Mungu na kujiepusha na makatazo yake, basi huyo atakuwa anastahiki Hasira za Mwenyezi Mungu na machukizo yake na adhabu yake iumizayo, na Mwenyezi Mungu Mtukufu hakutuumba bure bure na wala hakutuacha hivi hivi, na hakika mtu mjinga zaidi na mpumbavu kuliko watu wote ni mwenye kudhani kuwa yeye amekuja humu duniani na akapewa usikivu na uoni na akili, kisha akaishi katika maisha haya muda fulani kisha akafa, na wala hajui kwanini amekuja humu ulimwenguni na ni wapi atakwenda baada ya kufa, na Mwenyezi Mungu aliyetakasika na mtukufu anasema: "Je, mlidhania, enyi viumbe, ya kwamba sisi tuliwaumba nyinyi mkiwa mumepuuzwa: hakuna maamrisho wala makatazo wala malipo mema wala mateso, na kwamba nyinyi hamtorudishwa kwetu Akhera kwa Hesabu na Malipo?" [Al Mu'uminun: 115].

Na wala hafanani kwa Mwenyezi Mungu mwenye kumuamini yeye na akategemea kwake na akataka kuhukumiwa kwa sheria zake, na akawa anampenda anayenyenyekea kwake na anajikurubisha kwake kwa kufanya ibada mbalimbali na kutafuta yenye kumridhisha kila mahala, mtu mwenye kufanya hayo hafanani na mwenye kumkufuru Mwenyezi Mungu ambaye amemuumba na akamwekea sura na anazipinga alama zake na dini yake na anakataa kufuata maamrisho yake.

Huyu mtu wa kwanza anapata Ukarimu na Thawabu na mapenzi na Radhi, na huyu mwingine anapata kuchukiwa na adhabu.

pale ambapo Mwenyezi Mungu atawafufua watu baada ya kufa kwao kutoka makaburini mwao na akamlipa mwema wao neema mbalimbali na kumkirimu katika pepo yenye neema na kuadhibiwa mkosaji mwenye kiburi aliyekataa kumuabudu Mwenyezi Mungu kwa kumuadhibu katika nyumba ya adhabu.

Na ni wajibu juu yako kufikiria ukubwa wa takrima anayopewa mwema pindi zinapokuwa hizi thawabu na takrima kutoka kwa Mwenyezi Mungu aliye jitosheleza na mkarimu ambaye hana ukomo katika takrima zake na rehema zake na wala haiishi hazina yake. Hakika thawabu hizi zitakuwa na thamani kubwa peponi haziishi wala haziondoki (Na habari hizi ndizo tutakazozizungumzia hivi punde),

Na vile vile unatakiwa kufikiria adhabu kali na yenye kuumiza kwa kafiri, wakati itakapotoka adhabu toka kwa Mwenyezi Mungu mwenye nguvu ambaye hakuna ukomo wa nguvu zake.

  2- Muhammadi ni mjumbe wa Mwenyezi Mungu

Kuamini ujumbe wa Mtume Muhammad- rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- ndiye upande wa pili wa nguzo za msingi katika nguzo za uislamu, na msingi mkuu ambao jengo lake husimama juu yake.

Na mtu huwa muislamu kwa baada ya kutamka shahada mbili, hivyo atashuhudia kuwa hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu peke yake, na atashuhudia kuwa Muhammadi ni Mtume wa Mwenyezi Mungu.

 §  B- Basi ni nini maana ya Mtume? na ni nani huyo Muhammadi? na je kuna Mitume wengine wasiokuwa yeye?

Swali hili ndilo tutakalojaribu kulijibu katika kurasa hizi.

Mtume ni mtu aliye katika kilele cha juu kutokana ukweli wa maneno na tabia njema Mwenyezi Mungu anamchagua katika watu na humfunulia wahyi kwa akitakacho katika mambo ya dini na mambo yaliyofichikana na anaamrishwa kuwafikishia watu, hivyo Mtume ni mwanadamu, na mfano wake ni kama binadamu wengine, anakula kama wanavyo kula, na anakunywa kama wanavyokunywa, na anahitajia kila anachokihitajia mwanadamu, lakini yeye anatofautiana nao kwa kupewa wahyi ambao unamjia toka kwa Mwenyezi Mungu na akamuonyesha yatakayotokea katika mambo yaliyofichikana, na mambo ya dini ambayo anayafikisha kwa watu, na anatofautiana nao vile vile kwa yeye kuwa na ulinzi wa Mwenyezi Mungu unaomzuia kutenda madhambi makubwa na kila jambo ambalo linaharibu ufikishaji wa ujumbe wa Mwenyezi Mungu kwa watu.

Na tutaleta mfululizo wa baadhi ya visa vya Mitume waliotangulia kabla ya Mtume Muhammadi -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- ili iwe wazi kwetu kuwa ujumbe wa Mitume ni mmoja nao ni kulingania katika kumuabudu Mwenyezi Mungu peke yake, na tunaanza kuleta kisa cha mwanzo wa kuumbwa Mwanadamu na uadui wa Shetani kwa Baba wa wanadamu na kizazi chake.

 §  B- Mtume wa kwanza ni Baba yetu Adam- Amani iwe juu yake-

Amemuumba Mwenyezi Mungu Baba yetu Adamu -juu yake Amani- kutokana na udongo, kisha akampulizia roho itokayo kwake, Amesema Mwenyezi Mungu aliyetukuka jambo lake. "Na kwa hakika, tumewaneemesha nyinyi kwa kumuumba chanzo chenu - naye ni baba yenu Ādam- kutokana na kutokuwepo kamwe, kisha tukamtia sura ya umbo lake lililo bora kuliko lile la viumbe wengi. Kisha tuliwaamuru Malaika wetu, amani iwashukie, wamsujudie kwa ajili ya kumtukuza na kumuheshimu na kuonyesha ubora wa Ādam. Nao wakamsujudia wote, isipokuwa Ibilisi, ambaye alikuwa pamoja nao, hakuwa ni miongoni mwa wenye kumsujudia Ādam kwa kumuhusudu kwa heshima hii kubwa aliyopewa". Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka, Akasema hali ya kumkemea Ibilisi kwa kuacha kwake kumsujudia Ādam, «Ni lipi lililokuzuia usisujudu nilipokuamuru?» Ibilisi akasema, «Mimi ni bora kuliko yeye, kwa kuwa mimi nimeumbwa kwa moto na yeye ameumbwa kwa udongo.» Akaona kuwa moto ni bora kuliko udongo. "Mwenyezi Mungu Akasema kumwambia Ibilisi, «Shuka kutoka Peponi, kwani haifai kwako kufanya ujeuri humo; toka Peponi, kwani wewe ni miongoni mwa wanyonge walio madhalili". "Ibilisi akasema kumwambia Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka na kuwa juu, alipokata tamaa na rehema Yake, «Nipe muda mpaka Siku ya watu kufufuliwa, ili nipate kumpoteza ninayeweza kumpoteza kati ya wanadamu.» "Akasema Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka, «Wewe ni miongoni mwa wale niliowaandikia kucheleweshwa kipindi chao cha kufa mpaka Mvivio (mpulizo) wa Kwanza katika Parapanda pindi viumbe wote watakapokufa.» (Suratul -Aaraf 10-15)

Na akamuomba Mwenyezi Mungu amcheleweshe na wala asimfanyie haraka kumuadhibu na ampe idhini ya kumpoteza Adamu na kizazi chake kwa husda na kwa kuwachukia, basi Mwenyezi Mungu akamruhusu kwa hekima alizoziona akatawalia shetani upotoshaji wa kumpotosha Adam na kizazi chake isipokuwa waja wake wenyekumtakasia Mwenyezi Mungu ibada, na akamuamrisha Adam na kizazi chake wasimuabudu shetani na wala wasikubali upotoshaji wake na wajilinde kwa Mwenyezi Mungu kutokana na upotoshaji wake, Na ukaanza upotoshaji wa kwanza wa shetani kumpotosha Adam na mke wake Hawa (Ambaye Mwenyezi Mungu alimuumba kutokana na ubavu wake) katika kisa ambacho alikitaja Mwenyezi Mungu -kutakasika na machafu ni kwake.

«Na ewe Ādam, keti wewe pamoja na mke wako Ḥawā’ Peponi na kuleni matunda yaliyo humo popote mnapotaka na wala msile matunda ya mti huu (Aliwatajia mti huo), mkifanya hilo mtakuwa ni madhalimu wenye kukiuka mipaka ya Mwenyezi Mungu.» "Hapo Shetani aliwashawishi Ādam na Ḥawā’ ili awatokomeze kwenye kumuasi Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka, kwa kula matunda ya mti ule ambao Mwenyezi Mungu Aliwakataza kuula, ili mwisho wao uwe ni kufunukwa na tupu zao zilizokuwa zimesitiriwa. Na akawaambia, katika kujaribu kwake kuwafanyia vitimbi, «Hakika Mola wenu Amewakataza kula matunda ya mti huu ili msipate kuwa Malaika na ili msipate kuwa ni miongoni mwa wenye kuishi milele.» "Na Shetani Aliwaapia Ādam na Ḥawā’ kwa Mwenyezi Mungu kwamba yeye ni miongoni mwa wale wanaowapa nasaha kwa kuwashauri kula kutoka mti ule, huku yeye ni muongo katika hilo". "Hapo yeye aliwatia wao ujasiri na akawadanganya wakala kutoka mti huo ambao Mwenyezi Mungu Aliwakataza wasiukaribie. Walipokula kutoka mti huo, ziliwafunuka tupu zao na kikaondoka kile ambacho Mwenyezi Mungu Aliwasitiri nacho kabla ya wao kufanya uhalifu huo, wakawa wanayaambatisha majani ya miti ya Peponi kwenye tupu zao. Hapo Mola wao, Aliyetukuka na kuwa juu, Aliwaita, «Kwani sikuwakataza kula kutoka mti ule na nikawaambia kwamba Shetani, kwenu nyinyi, ni adui ambaye uadui wake uko waziwazi?» Katika aya hii kuna ushahidi kwamba kukaa uchi ni kati ya mambo makubwa na kwamba hilo ni jambo linalochukiza na linaloendelea kuchukiza katika tabia, na ni ovu kwenye akili za watu. "Ādam na Ḥawā’ walisema, «Ewe Mola wetu, tumejidhulumu nafsi zetu kwa kula kutoka kwenye mti ule. Na iwapo hutatusamehe na kuturehemu, tutakuwa ni miongoni mwa waliopoteza bahati zao katika ulimwengu wao na Akhera yao.» Maneno haya ndiyo yale aliyoyapokea Ādam kutoka kwa Mola wake akayatumia katika kumuomba, ndipo Mola wake Akaikubali toba yake. "Akasema, Aliyetukuka, kumwambia Ādam, Ḥawā’ na Ibilisi, «Shukeni kutoka mbinguni muende ardhini, baadhi yenu mkiwa ni maadui wa wengine. Huko mtakuwa na mahala pa nyinyi kutulia na pa kujiliwaza mpaka muda wenu ukome.» "Mwenyezi Mngu, Aliyetukuka, Akasema kumwambia Ādam, Ḥawā’ na kizazi chao, «Huko ardhini mtaishi, yaani mtapitisha siku za uhai wenu duniani, na huko kitakuwa kifo chenu, na kutoka huko Mola wenu atawatoa na awakusanye mkiwa hai Siku ya Ufufuzi.» "Enyi wanadamu, tumewawekea vazi lenye kusitiri tupu zenu, nalo ni vazi la lazima, na vazi la pambo na kujirembesha, nalo ni vazi la kujikamilisha na kujifurahisha. Na vazi la uchaji Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka, kwa kutekeleza maamrisho na kujiepusha na makatazo, ndilo vazi bora kwa aliyeamini. Hayo Ndiyo ambayo Mwenyezi Mungu Amewaneemesha nayo miongoni mwa alama za umola (ulezi) wa Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka, upweke Wake, wema Wake na rehema Zake kwa waja Wake, ili mpate kuzikumbuka neema hizi na mumshukuru Mwenyezi Mungu juu yake". "Enyi wanadamu! Asiwadanganye Shetani akawapambia maasia, kama alivyowapambia wazazi wenu, Ādam na Ḥawā’, akawatoa Peponi kwa sababu hiyo, akawavua vazi lao ambalo Mwenyezi Mungu Aliwasitiri nalo ili tupu zao zifunuke. Shetani na kizazi chake na viumbe wa jinsi yake wanawaona nyinyi, na nyinyi hamuwaoni, basi jichungeni nao. Hakika sisi tumewafanya Mashetani ni wategemewa wa makafiri ambao hawampwekeshi Mwenyezi Mungu wala hawawaamini Mitume Wake wala hawautumii muongozo Wake". (Suratul Aaraf 19-27)

Na baada ya kuteremka Adamu Ardhini na akaruzukiwa watoto na kizazi alikufa Adamu - juu yake amani- kisha kikaongezeka kizazi chake taifa baada ya taifa na wakapatwa na upotoshaji wa shetani na akawaenezea tabia ya kwenda kinyume na mafundisho na kuabudu makaburi ya watu wema miongoni mwa baba zao na wakabadilishwa kutoka kwenye imani kupelekwa kwenye shirki, basi Mwenyezi Mungu akawapelekea kwao Mtume naye ni (Nuhu Amani iwe juu yake).

 §  C- Nuhu -juu yake Amani.

Kwa hakika ilikuwa tofauti ya miaka kati ya Nuhu na Adamu ni karne kumi, alimtuma Mwenyezi Mungu kwa watu wake baada ya kuwa watu hao wamepotea na wakawa wanaabudu miungu badala ya kumuabudu Mwenyezi Mungu, na wakawa wanaabudu masanamu na mawe na makaburi na katika miungu yao iliyokuwa maarufu zaidi ni Wadda na Suwaa Yaghuutha na Yauuqa na Nasraa,Mwenyezi Mungu akamtuma kwao ili awarudishe kwenye kumuabudu Mwenyezi Mungu peke yake, kama alivyotufahamisha hilo Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa maneno yake: "Hakika tulimtuma Nūḥu kwa watu wake, ili awalinganie kwenye kumpwekesha Mwenyezi Mungu, kutakasika na sifa pungufu ni Kwake, na kumtakasia ibada, akasema, «Enyi watu wangu, muabuduni Mwenyezi Mungu, Peke Yake, na mumnyenyekee kwa kumtii, nyinyi hamna Mola anayestahiki kuabudiwa isipokuwa Yeye, Aliyetukuka na kuwa juu, mtakasieni ibada. Msipofanya na mkasalia katika kuabudu masanamu yenu, hakika mimi nawaogopea msishukiwe na adhabu ya Siku ambayo shida yenu itakuwa kubwa, nayo ni Siku ya Kiyama.» [Al A'raf: 59]. Na akaendelea kuwalingania watu wake wamuabudu Mwenyezi Mungu kwa muda mrefu, na hawakumuamini na Nuhu isipokuwa watu wachache na akamuomba Mola wake kwa kusema: "Nuhu akasema, «Mola wangu! Kwa hakika mimi nimewalingania watu wangu usiku na mchana ili wakuamini wewe na wakutii. Ulinganizi wangu kwao ili waamini, haukuwaongezea kitu isipokuwa ni kukimbia na kuipa mgongo haki. Na mimi kila nikiwalingania wao ili wakuamini wewe, ipate kuwa hiyo ni njia ya wewe kuwasamehe dhambi zao, hutia vidole vyao masikioni mwao, ili wasisikie ulinganizi wa haki, na hujifunika nguo zao wasipate kuniona, na hujikita kwenye ukafiri wao na hufanya kiburi sana cha kutoikubali haki. Kisha mimi nikawalingania wao kwenye Imani waziwazi na sio kwa kujificha. Kisha nikawatangazia wao ulinganizi kwa sauti kubwa wakati mwingine, na nikafanya kwa siri huo ulinganizi kwa sauti ya chini wakati mwingine. Ni kawaambia watu wangu, ‘Muombeni Mola wenu msamaha wa dhambi zenu na tubieni Kwake kutokana na ukafiri wenu, hakika Yeye ni Mwingi wa kusamehe kwa anayetubia miongoni mwa waja wake na akarudia Kwake.’» Mtakapotubia na mkaomba msamaha, Mwenyezi Mungu Atawateremshia mvua nyingi ya mfululizo, Ataiongeza mali yenu na pia watoto wenu, Atawafanya muwe na mabustani ya nyinyi kuneemeka kwa matunda yake na uzuri wake, na Atawajaalia nyinyi muwe na mito ambayo mtaitumia kwa kuipatia maji mimea yenu na pia wanyama wenu. Mnani nyinyi, enyi watu, hamuweki heshima kwa Mwenyezi Mungu? na hali yeye Amewaumbeni namna (hatua) baada ya namna (hatua)?" [Surat Nuuh 5- 14] Na pamoja na juhudi hii endelevu na pupa ya ajabu ya kuwaongoza watu wake, lakini wao walimfanya kuwa muongo na wakamcheza shere na wakampa sifa ya uwendawazimu.

Basi Mwenyezi Mungu akampa wahyi ya kuwa. "Hawatomuamini Mwenyezi Mungu isipokuwa walioamini kabla ya hapo, «basi usisikitike, ewe Nūḥu juu ya yale waliokuwa wakiyafanya". [Surat Huud 36] Na akamuamrisha kutengeneza safina ambayo itabeba ndani yake kila yule aliyeamini pamoja naye. "Na Nuhu akawa anatengeneza jahazi, na kila kundi la wakubwa wa watu wake likimpitia, humcheza shere. Nuhu, aliwaambia, «Iwapo nyinyi mnatucheza shere leo, kwa ujinga wenu wa kutojua ukweli wa ahadi ya Mwenyezi Mungu, basi sisi tutawacheza shere nyinyi kesho wakati wa kuzama kama mnavyotucheza shere". Mtajua hapo, itakapokuja amri ya Mwenyezi Mungu kwa hilo, ni yupi ambaye itamjia, hapa ulimwenguni, adhabu ya Mwenyezi Mungu yenye kumtweza (kumdhalilisha) na itamshukia huko Akhera, adhabu ya daima isiyokatika.» Mpaka ilipokuja amri yetu ya kuwaangamiza wao kama tulivyomuahidi Nuhu kwa hilo, na maji yakachimbuka kwa nguvu kutoka kwenye tanuri, mahala pa kuchomea mikate, ikiwa ni alama ya kuja adhabu, tulimuambia Nuhu, «Beba ndani ya jahazi kila aina, miongoni mwa aina za wanyama wa kiume na wa kike, na uwabebe ndani yake watu wa nyumbani kwako, isipokuwa yule aliyetanguliwa na Neno kuwa ataadhibiwa katika wale wasiomuamini Mwenyezi Mungu kama mtoto wake na mke wake, na ubebe ndani yake aliyeamini pamoja na wewe katika watu wako.» Na hakuna aliyeamini pamoja naye isipokuwa wachache ingawa yeye alikaa nao kwa muda mrefu". Nuhu alisema kuwaambia walioamini pamoja naye, «Pandeni kwenye jahazi kwa jina la Mwenyezi Mungu. Kwa jina la Mwenyezi Mungu itatembea majini, na kwa jina la Mwenyezi Mungu itafika mwisho wa kwenda kwake na kutia nanga kwake. Hakika Mola wangu ni Mwingi wa kusamehe dhambi za mwenye kutubia na kurudi Kwake miongoni mwa waja Wake, ni Mwingi wa huruma kwao kwa kutowaadhibu baada ya kutubia. Nayo ikawa inatembeanao kwenye mawimbi yanayopaa na kwenda juu mpaka yakawa kama majabali kwa urefu wake wa kwenda juu. Hapo Nuhu alimuita mtoto wake wa kiume, ambaye alikuwa yupo mahali kando na amejiepusha na Waumini, akamwambia, «Ewe mwanangu, panda na sisi kwenye jahazi na usiwe pamoja na wenye kumkanusha Mwenyezi Mungu, utakuja kuzama.» Mtoto wa Nuhu akasema, «Nitakimbilia kwenye jabali nijihifadhi na maji na hilo litanizuia na kuzama. Nuhu akamjibu, «Leo hakuna kitu chenye kuzuia amri ya Mwenyezi Mungu na hukumu Yake iliyoteremka kwa viumbe, ya gharika na maangamivu, isipokuwa yule aliyehurumiwa na Mwenyezi Mungu Aliyetukuka, basi amini na upande jahazini pamoja na sisi.» Hapo mawimbi makubwa yalitenganisha baina ya Nuhu na mwanawe na akawa ni miongoni mwa waliogharikishwa wenye kuangamia". "Akasema Mwenyezi Mungu kuiambia ardhi, baada ya watu wa Nuhu kuangamia, «Ewe ardhi! Kunywa maji yako. Na ewe mbingu! Simamisha kunyesha mvua.» Na maji yakapungua na yakanywea, na amri ya Mwenyezi Mungu ikapitishwa ya kuangamia watu wa Nuhu, na jahazi ikaegesha juu jabali la Jūdīy. Na hapo kukasemwa, «Kuwa mbali (na rehema ya Mwenyezi Mungu) ni kwa wale madhalimu waliokiuka mipaka ya Mwenyezi Mungu na wasiamini.» Na Nuhu alimlingania Mola Wake kwa kumuomba na akasema, «Mola wangu, wewe umeniahidi kwamba utaniokoa, mimi na jamaa zangu, tusizame na tusiangamie, na hakika mtoto wangu ni miongoni mwa watu wa nyumbani kwangu, na ahadi yako ndio kweli ambayo haibadiliki, na wewe ndiye hodari zaidi wa wenye kuhukumu na muadilifu wao zaidi.» Mwenyezi Mungu Akasema, «Ewe Nuhu hakika yule mtoto wako aliyeangamia si katika jamaa ambao nilikuahidi kuwa nitawaokoa. Hii ni kwa sababu ya ukafiri wake na kufanya kwake matendo yasiyokuwa mema. Na mimi nakukataza usiniombe jambo usilokuwa na ujuzi nalo. Mimi nakusihi usiwe ni miongoni mwa wajinga kwa kuniomba hilo.» Akasema Nuhu, «Ewe Mola wangu, Mimi najihami kwako na nataka hifadhi kukuomba kitu nisichokuwa na ujuzi nacho, na usiponisamehe dhambi zangu na ukanihurumia kwa rehema zako, nitakuwa ni miongoni mwa wale waliojinyima hadhi zao na wakaangamia". Mwenyezi Mungu Akasema, «Ewe Nuhu Shuka kwenye ardhi kavu kutoka kwenye jahazi, kwa amani na salama zitokazo kwetu, na baraka ikishuka juu yako na juu ya umma katika wale walioko na wewe. Na kuna umma na makundi miongoni mwa watu wa uovu ambao tutawastarehesha katika uhai wa kiulimwengu mpaka ufike muda wao wa kuishi kisha iwapate wao kutoka kwetu adhabu iumizayo Siku ya Kiyama.» [Surat: 38-48].

 §  D- Mtume Huud -Amani iwe juu.

Kisha baada ya muda fulani alituma Mwenyezi Mungu kwenye kabila la Aad katika sehemu iitwayo Ah'qaaf- baada ya kuwa walikuwa wapotofu na wakiabudu asiyekuwa Mwenyezi Mungu- Mwenyezi Mungu aliwatumia mtume miongoni mwao naye ni (Huud) Amani iwe juu yake.

Ametupa habari Mwenyezi Mungu kuhusu hilo kwa kusema: "Hakika tulimtuma, kwenda kwa watu wa kabila la 'Ād, ndugu yao Hūd, walipoabudu masanamu badala ya Mwenyezi Mungu, akawaambia, «Muabuduni Mwenyezi Mungu, Peke Yake, hamna mola anayestahiki kuabudiwa isipokuwa Yeye, Aliyetukuka na kuwa juu, mtakasieni ibada. Je, hamuiogopi adhabu ya Mwenyezi Mungu na hasira Zake kwenu?» Wakasema wale viongozi waliokufuru katika watu wa Hūd, «Sisi tunajua kwamba wewe, kwa kutuita sisi kuacha kuabudu waungu wetu na kumuabudu Mwenyezi Mungu, Peke Yake, ni mpungufu wa akili, na sisi tunaamini kwamba wewe, kwa hayo usemayo, ni katika wale wanaomzulia Mwenyezi Mungu uongo.» Hūd akasema, «Enyi watu wangu, sina upungufu katika akili yangu, isipokuwa mimi ni mjumbe kutoka kwa Mola wa viumbe wote". «Ninawafikishia nyinyi yale ambayo Amenituma nayo Mola wangu kwenu. Na mimi kwenu, katika yale niliyowaita kwayo ya kumpwekesha Mwenyezi Mungu na kuitumia sheria Yake, ni mshauri mwenye imani, ni muaminifu juu ya wahyi wa Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka. Je, imewafanya nyinyi muone ajabu kwamba Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka, Ameteremsha kwenu yale ambayo yanawakumbusha mambo yaliyo na kheri kwenu, kwa ulimi wa mtu katika nyinyi, mnaoujua ukoo wake na ukweli wake, ili awaogopeshe adhabu ya Mwenyezi Mungu? Na kumbukeni neema za Mwenyezi Mungu juu yenu, Alipowafanya nyinyi mshike nafasi ya waliokuwa kabla yenu katika ardhi baada ya kuwaangamiza kaumu ya Nuhu na akawazidishia miili yenu nguvu na ukubwa. Basi kumbukeni neema za Mwenyezi Mungu nyingi juu yenu kwa kutarajia kufanikiwa mafanikio makubwa duniani na Akhera.» ’Ād walisema kumwambia Hūd, amani imshukie, «Je, umetuita tumuabudu Mwenyezi Mungu, Peke Yake, na tuihame ibada ya masanamu ambayo tumeirithi kutoka kwa baba zetu? Basi tuletee adhabu ambayo unatutisha nayo iwapo wewe ni miongoni mwa wakweli katika hayo usemayo.» Hūd alisema kuwaambia watu wake, «Mshashukiwa na adhabu kutoka kwa Mola wenu, Aliyetukuka na kuwa juu, «Mnajadiliana na mimi juu ya masanamu hawa mliowaita waungu, nyinyi na baba zenu? Mwenyezi Mungu Hakuteremsha hoja yoyote wala dalili ya kuwa waabudiwe, kwani wao wameumbwa, Hawadhuru wala hawanufaishi; mwenye kuabudiwa peke yake si mwingine ni Muumba, kutakasika na sifa za upungufu ni Kwake. Basi ngojeni kuteremkiwa na adhabu, kwani mimi, pamoja na nyinyi, nangojea kuteremka kwake. Huu ni upeo wa kuonya na kutisha.» "Mwenyezi Mungu akamuokoa Hūd na walioamini pamojanaye kwa rehema kubwa kutoka kwake, Aliyetukuka. Na akawaangamiza makafiri wote miongoni mwa watu wake, Akawavunjavunja mpaka wa mwisho wao. Na wao hawakuwa ni Waumini kwa kuwa walikusanya baina ya kukanusha aya za Mwenyezi Mungu na kuacha kufanya vitendo vyema". [Suratiul Aaraf 65-72]

Basi Mwenyezi Mungu akawatumia upepo mfululizo kwa siku nane upepo ambao unabomoa kila kitu kwa amri ya Mola wake, na Mwenyezi Mungu akamuokoa Huud na wale walioamini pamoja naye.

 §  E- Mtume Saleh -Amani iwe juu yake.

Kisha ukapita muda kidogo, na likaanza kabila la Thamuud kaskazini mwa bara arabu na wakapotea kwa kuacha njia iliyonyooka na wakashika njia ya upotovu wa waliokuwa kabla yao, hivyo akawatumia Mwenyezi Mungu mtume atokanaye na wao ambaye ni (Swalehe) juu yake amani na akamuunga mkono kwa alama zinazo julisha juu ya ukweli wake, nayo ni Ngamia mkubwa asiyekuwa na wakufanana naye katika viumbe, na akatufahamisha Mwenyezi Mungu Mtukufu habari zake akasema: "Na tulimtuma, kwenda kwa watu wa kabila la Thamūd, ndugu yao Ṣwaleḥ, walipoabudu masanamu badala ya Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka. Ṣāleḥ aliwaambia, «Enyi watu wangu, muabuduni Mwenyezi Mungu, Peke Yake, hamna mola anayestahiki kuabudiwa isipokuwa Yeye, Aliyetukuka na kuwa juu, mtakasieni ibada, nimewajia na hoja juu ya ukweli wa yale ninayowaitia kwayo. Nayo ni kuwa nilimuomba Mwenyezi Mungu mbele yenu, Akawatolea kutoka kwenye jiwe hili ngamia mkubwa kama mlivyoomba, basi muacheni ale kwenye malisho yaliyoko kwenye ardhi ya Mwenyezi Mungu, na msimfanyie lolote la kumdhuru, mkifanya hivyo, mtapatwa na adhabu iumizayo. Na kumbukeni neema ya Mwenyezi Mungu juu yenu, Alipowafanya nyinyi mnashika nafasi za waliokuwa kabla yenu katika ardhi, baada ya kabila la ‘Ād, Akawamakinisha nyinyi katika ardhi nzuri, mkaifanya makao, mkajenga kwenye mabonde yake majumba makubwa na mkayachonga majabali yake ili mfanye majumba mengine. Basi kumbukeni neema za Mwenyezi Mungu juu yenu na msizunguke katika ardhi kwa uharibifu". "Wakasema mabwana na wakubwa wa wale waliokuwa wakijiona kuwa ni wakubwa, miongoni mwa watu wa Ṣāleḥ, kuwaambia wale waliokuwa wakiwafanya wanyonge na kuwadharau, «Kwani mnajua kwamba Ṣāleḥ ametumwa kwetu na Mwenyezi Mungu?» Wale walioamini walisema, «Sisi tunayaamini yale ambayo Mwenyezi Mungu Amemtuma nayo na tunaifuata sheria aliyokuja nayo. Wakasema wale waliojiona, «Sisi ni wenye kuyakanusha hayo mliyoyaamini nyinyi na kuyafuata kuhusu unabii wa Ṣāleḥ.” Wakamchinja ngamia kwa kutojali onyo la Ṣāleḥ, na wakaingiwa na kiburi kilichowafanya wasifuate amri ya Mola wao na wakasema, kwa kejeli na kwa kuona kuwa adhabu iko mbali na wao, «Ewe Ṣāleḥ, tuletee hiyo adhabu ambayo unatuonya nayo, iwapo wewe ni miongoni mwa Mitume wa Mwenyezi Mungu!» "Basi wale waliokufuru walishikwa na tetemeko kali ambalo lilizitoa nyoyo zao, wakawa wameangamia katika mji wao, wamegandamana na ardhi kwa magoti yao na nyuso zao, hakuna yeyote kati yao aliyeponyoka". "Ṣwalehe, amani imshukie, alijiepusha na watu wake, walipomchinja ngamia, na maangamivu yakawa ni yenye kuwashukia, na akasema kuwaambia, «Enyi watu wangu! Nimewafikishia yale Mola wangu Aliyoniamuru niwafikishie, kuhusu maamrisho Yake na makatazo Yake, na nimewafanyia bidii kiasi nilichoweza katika kuwavutia kwenye kheri na kuwakemea shari na kuwa muaminifu, lakini nyinyi hamuwapendi waaminifu kwenu, ndipo mkayakataa maneno yao na mkamtii kila shetani aliyelaaniwa.» [surat Aaraf 73-74].

Na akatuma Mwenyezi Mungu baada ya hapo mitume wengi kwa kila Umma hapa duniani, na hakuna Umma wowote isipokuwa alipita katika umma huo mtume, Mwenyezi Mungu alitupa habari ya baadhi yao na wengine wengi hakutupa habari zao na wote hao mitume wametumwa na ujumbe mmoja nao ni kuwaamrisha watu wamuabudu Mwenyezi Mungu peke yake hana mshirika wake, na kuwacha kumuabudu asiyekuwa Mwenyezi Mungu. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu. "Kwa hakika tulipeleka kwa kila umma uliopita mjumbe wa kuwaamrisha wao kumuabudu Mwenyezi Mungu na kumtii Peke Yake, na kuacha kumuabudu asiyekuwa Yeye miongoni mwa Mashetani, mizimu, wafu na vinginevyo kati ya vile vinavyotegemewa badala ya Mwenyezi Mungu. Basi wakawa miongoni mwao wale ambao Mwenyezi Mungu aliwaongoa wakafuata njia ya Mitume, na kati yao wakapatikana wakaidi waliofuata njia za upotofu, hapo ikapasa kwao upotevu na Mwenyezi Mungu Asiwaafikie (hakuwawezesha kuongoka). Basi tembeeni katika ardhi na mjionee kwa macho yenu vipi yalivyokuwa marejeo ya hawa wakanushaji na maangamivu yaliyowashukia, mpate kuzingatia?" [An Nahli: 36].

 §  J- Mtume Ibrahim -Amani iwe juu yake.

Kisha akamtuma Mwenyezi Mungu baada ya hapo Nabii Ibrahim - juu yake amani- kwa watu wake baada ya kuwa wamepotea na ni wenye kuabudu Sayari na masanamu, Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Kwa hakika, tulimpa Ibrāhīm uongofu wake ambao yeye aliwalingania watu waufuate kabla ya Mūsā na Hārūn. Na sisi tulikuwa tunajua kwamba yeye anastahiki hilo. Pindi aliposema kumwambia baba yake na watu wake, «Ni masanamu gani hawa mliowatengeneza kisha mkakaa kuwaabudu na mkajilazimisha nao.» Wakasema, «Tuliwakuta baba zetu wakiwaabudu, na sisi tunawaabudu kwa kuwaiga wao.» Ibrāhīm akawaambia, «Kwa hakika nyinyi na wazee wenu, kwa kuwaabudu kwenu hawa masanamu, mko mbali waziwazi na haki.» Wakasema, «Je, neno hili ambalo umekuja nalo kwetu ni la usawa na ukweli, au neno lako ni la mtu anayefanya mzaha na shere, hajui analosema?» Ibrāhīm, rehema na amani zimshukie, akasema, «Bali Mola wenu Ambaye ninawalingania mumuabudu Ndiye Mola wa mbingu na ardhi Ambaye Ameziumba, na mimi ni mwenye kulitolea ushahidi hilo. «Na ninaapa kwa Mwenyezi Mungu, nitawachimba masanamu wenu niwavunjevunje baada ya nyinyi kuondoka kwenda zenu na kuwaacha.» "Hapo Ibrāhīm akawavunjavunja masanamu akawafanya vipande- vipande vidogo na akamuacha mkubwa wao, ili watu wake wapate kumrudia kumuuliza, na ili uelemevu wao na upotevu wao upate kujulikana waziwazi, na ili hoja isimame kwao". "Na watu wakarudi na wakawaona masanamu wao wamevunjwa- vunjwa na wametwezwa (wamedhalilishwa). Hapo wakaulizana wao kwa wao, «Ni nani aliyefanya haya kwa waungu wetu? Huyo, kwa kweli, ni dhalimu kwa kuwa na ujasiri juu ya waungu wanaostahiki kuheshimiwa na kutukuzwa.» Hapo wale waliomsikia Ibraim akiapa kwamba atawachimba masanamu wao, «Tulimsikia kijana akiwataja kwa ubaya, anaitwa Ibrāhīm.» Viongozi wao wakasema, «Mleteni Ibrāhīm mbele ya watu aonekane, wapate kushuhudia kukubali kwake makosa ya aliyoyasema, ili iwe ni hoja dhidi yake.» Ibrāhīm akaletwa, na wakamuuliza kwa njia ya kumpinga, «Je, ni wewe uliowavunjavunja waungu wetu?» Wakikusudia masanamu wao. Ibrāhīm akalipata alitakalo la kuonyesha wazi upumbavu wao na huku wakiona, akasema, «Aliyewavunjavunja ni huyu sanamu mkubwa, waulizeni hilo waungu wenu mnaowadai iwapo watasema au watawapa majibu.» "Hapo wakatahayari na ukawafunukia wazi upotevu wao, vipi wanawaabudu na ilhali wao wanashindwa kujitetea wenyewe kitu chochote wala kumjibu mwenye kuwauliza? Na wakakubali wenyewe kuwa wamefanya udhalimu na ushirikina". "Punde si punde ukakamavu wao uliwarudia baada ya kushindwa hoja, wakageuka kurudi kwenye ubatilifu wao na wakatumia hoja dhidi ya Ibrāhīm ambayo ni hoja dhidi yao wakasema, «Vipi tutawauliza na hali wewe unajua kuwa hawa hawasemi?» "Ibrāhīm akasema: «Vipi mnaabudu masanamu wasionufaisha wanapoabudiwa wala kudhuru wanapoachwa? "Ubaya ni wenu na ni wa waungu wenu mnaowaabudu badala ya Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka. Kwani hamtii akili mkajua uovu wa haya mliyonayo?» Ilipoporomoka hoja yao na ukweli ukajitokeza, waliamua kutumia uwezo wao na wakasema, «Mchomeni Ibrāhīm kwa moto mkionyesha hasira kwa ajili ya waungu wenu, iwapo nyinyi ni wenye kuwasaidia basi washeni moto mkubwa na mumtupe ndani yake.» Mwenyezi Mungu Akamsaidia Mtume Wake na Akauambia moto, «Kuwa baridi na salama kwa Ibrāhīm!» Ili asipatwe na udhia wala asifikwe na jambo la kuchukiza. "Na wale watu walimtakia Ibrāhīm maangamivu na Mwenyezi Mungu Akavitengua vitimbi vyao na Akawafanya wao wawe ni wenye kushindwa na kuwa chini". [Surat Al-anbiyaa 50-70]

Kisha akahama Ibrahim -Amani iwe juu yake- na mwanaye baada ya hapo kutoka Palestina mpaka Makkah, na akamuamrisha Mwenyezi Mungu Ibrahim na Mwanaye kujenga Al-kaaba tukufu, na akawaita watu kuja kuhiji katika nyumba hiyo na kumuabudu Mwenyezi Mungu peke yake. "Na tulimuusia Ibrahim na mwanaye Ismail yakuwa waisafishe nyumba yangu kwa wenye kuizunguka na wenye kukaa humo na wenye kurukuu na kusujudu" [Al Baqarah: 125]

 §  F- Mtume Luut -Amani iwe juu yake.

Kisha baada ya hapo alimtuma Mwenyezi Mungu Nabii Luut kwa watu wake na walikuwa ni watu wabaya wanamuabudu asiyekuwa Mwenyezi Mungu na wakifanya machafu wao kwa wao. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na mkumbuke, ewe Mtume, Lūuṭ, amani imshukie, pindi aliposema kuwaambia watu wake, «Je, mnafanya kitendo kibaya kilichofikia upeo wa ubaya? Hakuna yeyote, miongoni mwa viumbe, aliyefanya kitendo hicho kabla yenu. "Nyinyi mnawaendea wanaume kwenye sehemu zao za nyuma, hali ya kuingiwa na matamanio ya kufanya hivyo, bila kujali uovu wake, huku mkiacha kile alichowahalalishia Mwenyezi Mungu kwa wake zenu. Bali nyinyi ni watu mliopita kiasi katika kukiuka mipaka ya Mwenyezi Mungu. Hakika kuwaendea wanaume badala ya wanawake ni miongoni mwa machafu ambayo yalianzishwa na kaumu ya Luut, na hawakutanguliwa na yeyote katika viumbe". Hayakuwa majibu ya watu wa Lūuṭ, alipowapinga kwa kitendo chao kilichofikia upeo wa ubaya, isipokuwa ni kuambiana wao kwa wao, «Mtoeni Lūṭ na wafuasi wake nchini mwenu, kwa kuwa yeye na wanaomfuata ni watu wanaojiepusha na kuwajia wanaume kwenye sehemu zao za nyuma.» [Suratul Aaraf 80-82] Basi Mwenyezi Mungu akamuokoa Nabii Luut na watu wake isipokuwa mke wake alikuwa ni katika makafiri, pale alipomuamrisha Mwenyezi Mungu aondoke kijijini muda wa usiku yeye na watu wake, na ilipokuja adhabu ya Mwenyezi Mungu akakigeuza kijiji juu chini chini juu na akawanyweshelezea mvua ya mawe ya udongo mgumu uliokamatana.

 §  J- Mtume Shuaibu -Amani iwe juu yake.

Kisha akatuma Mwenyezi Mungu baada ya hapo kwa watu wa Madyan ndugu yao Shuaibu baada ya kuwa wamepotea na wakaachana na uongofu, na ikaenea tabia mbovu ya kuwafanyia watu uadui na kupunguza katika kilo na mizani, basi akatuhabarisha Mwenyezi Mungu kuhusu watu hao kwa maneno yake aliposema: "Hakika tulimtuma, kwa watu wa kabila linalokaa Madyan, ndugu yao Shu'ayb, amani imshukie, akasema kuwaambia, «Enyi watu wangu, muabuduni Mwenyezi Mungu, Peke Yake, Asiye na mshirika. Hamna Mola anayestahiki kuabudiwa isipokuwa Yeye, Aliyetukuka na kuwa juu. Mtakasieni ibada. Hakika imewajia nyinyi hoja, kutoka kwa Mola wenu, juu ya ukweli wa yale ninayowaitia. Watekelezeeni watu haki zao kwa kutimiza vipimo na mizani. Na msiwapunguzie haki zao mkawadhulumu. Wala msifanye uharibifu katika ardhi, kwa ukafiri na kudhulumu, baada ya kuwa imetengenezwa kwa sheria za Mitume waliopita, amani iwashukie. Hayo niliyowaitia nyinyi ni bora kwenu katika ulimwengu wenu na Akhera yenu, iwapo nyinyi ni wenye kuniamini katika yale ninayowaitia, ni wenye kuzifuata sheria za Mwenyezi Mungu kivitendo". «Na wala msikae katika kila njia mkiwatisha watu kwa kuwaua wasipowapa mali yao, mkimzuia aliyemuamini Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka na kuwa juu, na akatenda mema asifuate njia iliyonyooka, na mkataka njia ya Mwenyezi Mungu iwe kombo, na mnaipotoa mkifuata matamanio yenu, na mnawafukuza watu wasiifuate. Na kumbukeni neema ya Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka, juu yenu ilipokuwa idadi yenu ni chache Mwenyezi Mungu akawafanya muwe wengi mkawa mna nguvu, wenye enzi. Na angalieni, ulikuwa vipi mwisho wa wale waharibifu katika ardhi na ni yapi yaliyowashukia ya maangamivu na kuvunjikiwa? Na iwapo kundi miongoni mwenu waliyakubali yale Aliyonituma nayo Mwenyezi Mungu na kundi la watu wengine wasiyakubali hayo, basi ngojeni, enyi wakanushaji wa hukumu ya Mwenyezi Mungu inayotoa uamuzi baina yetu na nyinyi, itakapowashukia adhabu Yake ambayo aliwaonya nayo. Na Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka na kuwa juu, ni mbora wa wenye kuhukumu baina ya waja Wake. Walisema watukufu na wakubwa wa watu wa Shu'ayb waliokataa, kwa kiburi, kumuamini Mwenyezi Mungu na kumfuata Mtume Wake Shu'ayb, amani imshukiye, «Tutakutoa, ewe Shu'ayb, wewe na walio pamoja na wewe kutoka kwenye miji yetu, isipokuwa ukiwa utarudi kwenye dini yetu.» Shu'ayb akasema akilipinga na kulionea ajabu neno lao, «Je, tuwafuate nyinyi kwenye dini yenu na mila yenu ya batili hata kama sisi tunaichukia kwa kujua kwetu ubatili wake?» Akasema Shu'ayb kuwaambia watu wake, kwa kuongezea, «Tutakuwa tumemzulia Mwenyezi Mungu uongo tukirudi kwenye dini yenu baada ya Mwenyezi Mungu kutuokoa nayo. Haiwezekani kwetu kugeuka kuifuata dini isiyokuwa ya Mola wetu, isipokuwa iwapo Mwenyezi Mungu, Mola wetu, Ametaka. Hakika Mola wetu Amekiendea kila kitu kwa ujuzi, kwa hivyo Anakijua kinachowafaa waja. Ni kwa Mwenyezi Mungu, Peke Yake, mategemeo yetu ya kupata uongofu na ushindi. Ewe Mola wetu, toa uamuzi wa haki kati yetu na watu wetu, na wewe ndiye mbora wa wenye kutoa uamuzi. Wakasema watukufu na wakubwa wenye kukanusha, wenye kupinga ulinganizi wa Tawhīd (kumpwekesha Mwenyezi Mungu) waliofikia kiwango cha juu katika ujeuri na uasi, wakitahadharisha kwamba Shu'ayb asifuatwe, «Kwa hakika, lau mnamfuata Shu'ayb, nyinyi kwa hivyo mtakuwa wenye kuangamia.» Basi wale waliokufuru walishikwa na tetemeko kali ambalo lilizitoa nyoyo zao, wakawa wameangamia katika mji wao, wamegandama na ardhi kwa magoti yao na nyuso zao, hakuna yeyote kati yao aliyeponyoka. Wale ambao walimkanusha Shu'ayb walikuwa kana kwamba hawakukaa kwenye nyumba zao wala hawakustarehe humo. Kwani walimalizwa, isibaki alama yoyote yao, wakapata hasara na maangamivu duniani na Akhera. Shu'ayb alijiepusha nao, alipokuwa na yakini kwamba adhabu ya Mwenyezi Mungu ni yenye kuwashukia, na akasema, «Enyi watu wangu, ‘Nimewafikishia ujumbe wa Mola wangu na nimewashauri muingie kwenye Dini ya Mwenyezi Mungu na muache hayo mliyonayo; hamkusikia wala hamkutii. Vipi mimi niwasikitikie watu walioukataa upweke wa Mwenyezi Mungu na wakawakanusha Mitume Wake?’» [Suratul Aaraf 85-95]

 §  K- Mtume Mussa -Amani iwe juu yake.

Kisha akazuka katika mji wa Misri mfalme muovu mwenye kiburi, anaitwa Fir'auni anadai uungu na kuwa wamuabudu yeye na anawachinja awatakao na kuwadhulumu awatakao,akatupa habari Mwenyezi Mungu kuhusu Firauni kwa maneno yake: "Hakika Fir’awn alifanya kiburi na akapita mipaka katika nchi, akawafanya watu wake kuwa ni makundi tofauti-tofauti, akawa analinyongesha kundi moja ya hayo, nalo ni lile la Wana wa Isrāīl, akawa anawaua watoto wao wa kiume na anawabakisha wanawake wao kwa kutumika na kudharauliwa, Hakika yeye alikuwa ni miongoni mwa waharibifu katika ardhi. "Na tunataka kuwafadhili wale ambao Fir'awn aliwafanya wanyonge nchini, tuwafanye ni viongozi katika wema na ni wenye kuulingania, na tuwafanye wao wairithi nchi baada ya kuangamia Fir'awn na watu wake". Na tuwape uthabiti katika nchi na tumfanye Fir’awn, Hāmān na askari wao waone, kutoka kundi hili linalonyongeshwa kile walichokuwa wakikiogopa cha kuangamia kwao na kuondoka ufalme wao na kuwatoa wao kwenye nyumba zao kwa mkono wa mzaliwa wa Wana wa Isrāīl. "Na tukampa mawazo mama yake Mūsā alipomzaa na akamuogopea asije Fir'awn akamchinja kama anavyowachinja watoto wa wana wa Isrāeli kwamba «mnyonyeshe ukiwa mtulivu, na pindi uogopapo kujulikana mambo yake, muweke sandukuni na ulitupe kwenye mto wa Nail bila ya kuogopa kwamba fir'awn na watu wake watamuua na bila ya kuwa na masikitiko ya kuwa mbalinaye, hakika sisi tutamrudisha kwako na tutamtumiliza kuwa Mtume.» Hapo akamuweka sandukuni na akalitupa kwenye mto Nail, na wafuasi wa Fir'awn wakalipata na wakalichukua, na mwisho wake ukawa vile Alivyokadiria Mwenyezi Mungu kuwa Mūsā awe ni adui yao kwa kuwa kinyume na dini yao, na awatie kwenye huzuni ya kuzamishwa na kuondokewa na ufalme wao mikononi mwake. Kwa hakika, Fir'awn na Hāmān na wasaidizi wao walikuwa wafanyaji makosa washirikina. Na mke wa Fir'awn alipomuona , Mwenyezi Mungu Alimtia mapenzi moyoni mwake na akasema kumwambia Fir'awn, «Mtoto huyu atakuwa chimbuko la furaha kwangu mimi na wewe, Msimuue kwani huenda tukapata kheri kutoka kwake au tumfanye ni mtoto wetu» na hali Fir'awn na jamaa wa nyumbani kwake hawafahamu kwamba maangamivu yao yatatokea mikononi mwake. Na kifua cha mama yake Mūsā kikawa hakijishughulishi na kitu chochote duniani isipokuwa hamu ya Mūsā na kumtaja, na alikaribia kudhihirisha kuwa yule ni mwanawe lau si sisi kumthibitisha, naye akavumilia asilidhihirishe hilo, ili awe ni miongoni mwa wenye kuamini ahadi ya Mwenyezi Mungu na mwenye kuwa na yakini nayo. Na akasema mama yake Mūsā kumwambia nduguye wa kike alipomtupa mtoni, «Fuata athari za Mūsā uone atafanywa nini? Akafuata athari zake na akamuona kwa mbali na hali watu wa Fir'awn hawajui kwamba yeye ni dada yake na kwamba yeye anafuatilia habari zake. Na tulimzuia Mūsā asinyonye kutoka kwa wanyonyeshaji kabla hatujamrudisha kwa mama yake, hapo dada yake akasema, «Je, ni waonyeshe watu wa nyumba ambao watamlea na kumnyonyesha vizuri na ambao watakuwa na huruma naye? Wakamkubalia hilo. Basi tukamrudisha Mūsā kwa mama yake, ili jicho lake litulie kwake na tukamtekelezea ahadi yetu kwake, kwa kuwa alirudi kwake akiwa amesalimika na kuuawa na Fir'awn, na ili asihuzunike kwa kuepukana naye, na ajue kwamba ahadi ya Mwenyezi Mungu ni kweli, ile Aliyowaahidi kuwa atawarudishia na Amfanye ni miongoni mwa Mitume. Hakika Mwenyezi Mungu Haendi kinyume na ahadi Yake, lakini wengi wa washirikina hawajui kwamba ahadi ya Mwenyezi Mungu ni kweli. Na Alipofikia Mūsā umri wa kuwa na nguvu na ikakamilika akili yake, tulimpa busara na elimu ya kutambua hukumu za Sheria. Na kama tulivyompa Mūsā malipo mema kwa utiifu wake na wema wake, tunampa malipo mema mwenye kufanya wema miongoni mwa waja wetu. Na Mūsā aliingia mjini kwa kujificha wakati ambapo watu wake walikuwa wako katika hali ya kughafilika, akawapata humo watu wawili wanapigana, mmoja wao ni katika wana wa Isrāeli jamaa za Mūsā na mwingine ni katika jamaa za Fir’awn. Basi yule aliyekuwa ni katika jamaa ya Mūsā alitaka msaada dhidi ya yule Aliyekuwa katika maadui zake, hapo Mūsā akampiga ngumi na akafa. Mūsā akasema alipomuua, «Huu ni katika ushawishi wa Shetani aliyenipandisha hasira zangu mpaka nikampiga huyu akafa. Hakika ya Shetani ni adui wa mwanadamu ni mwenye kupoteza njia ya uongofu, ni mwenye uadui wa waziwazi.» Kitendo hiki cha Mūsā kilikuwa kabla ya kupewa unabii. Mūsā akasema, «Mola wangu! Mimi nimejidhulumu nafsi yangu kwa kumuua mtu ambaye hukuniamuru kumuua, basi nisamehe dhambi hilo.» Na Mwenyezi Mungu Akamsamehe. Kwani Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe sana dhambi za waja Wake, ni Mwenye huruma nao sana. Mūsā akasema, «Mola wangu! Kwa vile ulivyonineemesha kwa toba, msamaha na neema nyingi, sitakuwa mwenye kumsaidia yeyote kufanya uasi wake na uhalifu wake. Hivyo basi Mūsā akaingiwa na khofu akiwa kwenye mji wa Fir’awn, anatafuta habari zinazozungumzwa na watu kuhusu yeye na yule mtu aliyemuua, hapo akamuona yule mtu wake wa jana akipigana na Mmisri mwingine na akimtaka amsaidie. Mūsā alimwambia, «Kwa kweli, wewe ni mwingi wa upotofu, ni mpotevu waziwazi.» Basi alipotaka Mūsā kumshika Mmisri kupambana naye, alisema, «Je, unataka kuniua mimi kama ulivyomuua mtu jana? Hutaki isipokuwa kuwa jeuri katika nchi, na hutaki kuwa ni miongoni mwa wale wanaofanya upatanishi kati ya watu.» Na akaja mtu mmoja mbiombio kutoka mwisho wa mji, akasema, «Ewe Mūsā! Kwa hakika wale watukufu wa jamii ya Fir’awn wanafanya njama ya kukuua na wanashauriana juu ya hilo, basi toka. Kwani mimi ni kati ya wale wanaokupa ushauri mzuri na wanaokupendelea wema.» Hapo Mūsā akautoka mji wa Fir'awn akiwa katika hali ya kuogopa, akitazamia kukamatwa na wale wanaomtafuta, na akamuomba Mwenyezi Mungu Amuokoe na watu madhalimu. Na alipokusudia kuelekea nchi ya Madyan, na akatoka nje ya utawala wa Fir'awn, alisema, «Nina matumaini kwamba Mola wangu Ataniongoza njia nzuri ya kuelekea Madyan.» Alipoyafikia maji ya Madyan, alilikuta hapo kundi la watu wanawapa maji wanyama wao, na akawakuta, kando ya kundi hilo, wanawake wawili wamejitenga na watu na wamewazuilia wanyama wao na pale penye maji, kwa kushindwa kwao na udhaifu wao wa kutoweza kubanana na wanaume, na wanangojea mpaka wanyama wa watu waondoke kwenye maji kisha hapo wawapatie wanyama wao maji. Mūsā, amani imshukie, alipowaona aliwaonea huruma, kisha alisema kuwaambia, «Mna nini nyinyi?» wakasema, «Hatuwezi kubanana na wanaume, na hatuchoti maji mpaka watu wamalize kuchota, na baba yetu ni mzee sana hawezi kuwachotea maji wanyama wake kwa udhaifu wake na uzee wake.» Basi Mūsā akawachotea maji wanyama wa wale wanawake wawili, kisha akageuka kwenda kwenye kivuli cha mti kujifunika nacho na akasema, «Mola wangu! Hakika mimi ni muhitaji wa wema wako wowote ule utakaoniletea,» kama vile chakula. Na njaa ilikuwa imemshika sana. Hapo akaja mmoja wa wale wanawake wawili aliowachotea maji akitembea na huku akiona haya akasema, «Baba yangu anakuita ili akupe malipo ya maji uliyotuchotea.» Na Mūsā akaenda naye hadi kwa baba yake. Alipomjia baba yake na akamsimulia habari zake yeye pamoja na Fir’awn na watu wake, yule baba wa mwanamke alisema, «Usiogope! Umeokoka na watu madhalimu, nao ni Fir'awn na watu wake, kwani wao hawana mamlaka yoyote nchini kwetu.» Akasema mmoja wa wanawake wawili kumwambia baba yake, «Ewe baba yangu! Muajiri yeye akuchungie wanyama wako, kwani mtu bora wa wewe kumuajiri kwa kuchunga ni yule aliye na nguvu ya kuwalinda wanyama wako, aliye muaminifu ambaye huchelei kuwa atakufanyia hiana katika amana unayompatia.» Mzee akasema kumwambia Mūsā, «Mimi nataka kukuoza mmoja wa mabinti wangu hawa wawili, kwa sharti uwe muajiriwa wangu wa kuwachunga wanyama wangu kwa kipindi cha miaka minane. Na ukikamilisha miaka kumi, basi hiyo ni hisani yako. Na mimi sitaki kukusumbua kwa kuifanya miaka kumi. Utanikuta mimi, Mwenyezi Mungu Akitaka, ni miongoni mwa watu wema, katika uzuri wa tangamano na utekelezaji wa ahadi ya ninayoyasema. Mūsā akasema, «Hilo ulilolisema lisimame kuwa ndio ahadi baina yangu mimi na wewe, muda wowote wa vipindi viwili nitakaa kazini, nitakuwa nimekutekelezea, na sitatakiwa kuongeza juu yake, na Mwenyezi Mungu, kwa tunayoyasema, ni Mtegemewa, ni Mtunzi, Anatuona na Anakijua kile tulichofanya mapatano juu yake.» Basi Nabii wa Mwenyezi Mungu Mūsā, amani imshukie, alipomtekelezea mwenzake kipindi cha miaka kumi, nao ni muda mkamilifu zaidi wa vile vipindi viwili, na akaenda na watu wa nyumbani kwake kuelekea Misri, aliona moto upande wa jabali la Ṭūr. Mūsā alisema kuwaambia watu wa nyumbani kwake, «Subirini na mngojee. Mimi nimeona moto. Huenda nikawaletea habari kutoka kule, au nikawaletea kijinga cha moto mkapata kuota nacho.» Basi Mūsā alipoujia moto, Mwenyezi Mungu Alimuita kutoka upande wa bonde la mkono wa kulia wa Mūsā, katika ardhi iliyobarikiwa ya upande wa mti kwamba: «Ewe Mūsā! Mimi Ndiye Mwenyezi Mungu, Mola wa viumbe wote,» na kwamba: «itupe fimbo yako!» Na Mūsā akaitupa, ikageuka kuwa nyoka anayetembea kwa haraka. Alipoiona inatetemeka kana kwamba ni nyoka kama walivyo nyoka wengine, aligeuka kumkimbia na hakugeuka kwa kuogopa. Na hapo Mola wake Alimuita, «Ewe Mūsā! Nielekee mimi, na usiogope! Wewe ni miongoni mwa wenye kuaminika na kila lenye kuchukiza. «Tia mkono wako kwenye mfuko wa kanzu yako uliofunguliwa kifuani na uutoe, utatoka ukiwa mweupe, kama barafu, weupe ambao si wa ugonjwa wala mbalanga, na ujikumbatie kwa mikono yako ili usalimike na hofu. Hivi viwili nilivyokuonyesha, ewe Mūsā, vya fimbo kugeuka nyoka na kuufanya mkono wako kuwa mweupe na wenye kung’ara, si kwa ugonjwa wala mbalanga, ni dalili mbili kutoka kwa Mola wako, uende nazo kwa Fir’awn na watukufu wa watu wake.» Hakika Fir’awn na viongozi walio karibu naye walikuwa ni wakanushaji. Mūsā akasema, «Mola wangu! Mimi nimemuua mtu wa jamii ya Fir’awn, basi naogopa wasije wakaniua. Na ndugu yangu, Hārūn, ana ufasaha zaidi wa matamshi kuliko mimi, basi mtume yeye pamoja na mimi awe msaidizi wangu, ataniamini na atawafafanulia wao yale ninayowaambia. Mimi ninachelea wasije wakanikanusha mimi kwa maneno yangu nitakayowaambia kwamba mimi nimetimilizwa kwao.» Mwenyezi Mungu Akamwambia Mūsā, «Tutakupa nguvu kwa ndugu yako, na tutawapa nyinyi wawili hoja juu ya Fir’awn na watu wake wasiweze kuwafikia nyinyi kwa ubaya wowote. Nyinyi wawili na wale wenye kuwaamini nyinyi ndio mtakaopewa ushindi juu ya Fir’awn na watu wake kwa sababu ya aya (miujiza) yetu na ukweli unaoonyeshwa na aya hizo.» [Suratul Qaswasi 4-35]

Basi akaondoka na ndugu yake Haruna kwenda kwa -Mfalme Mwenye kiburi- wakimlingania katika kumuabudu Mwenyezi Mungu Mola wa viumbe wote. Fir’awn akamwambia Mūsā, «Na huyo Mola wa viumbe wote Ambaye unadai kwamba wewe ni mjumbe Wake, ni kitu gani?» Mūsā akasema, «Yeye ni Mmiliki na Mwenye kuiendesha mbingu na ardhi na vilivyoko baina ya viwili hivyo. Iwapo nyinyi mna yakini na hilo, basi aminini.» Fir’awn akasema kuwaambia walioko pembezoni mwake miongoni mwa watukufu wa watu wake, «Je, hamsikii maneno ya Mūsā ya ajabu kwamba kuna mola asiyekuwa mimi?» Mūsā akasema, «Mola Ambaye mimi nawalingania nyinyi Kwake ni Yule Aliyewaumba nyinyi na Aliyewaumba wa mwanzo. Basi vipi nyinyi mnamuabudu ambaye ni kiumbe kama nyinyi na yeye ana mababa waliotoweka kama mababa zenu?» Fir’awn akasema kuwaambia wale watu wake makhsusi akiwapandisha ghadhabu zao, kwa kuwa Mūsā amemkanusha yeye, «Kwa kweli, huyu mjumbe wenu aliyeletwa kwenu ni mwendawazimu , anasema maneno yasiyofahamika.» Mūsā akasema, «Mola wa Mashariki na Magharibi na vilivyoko baina ya viwili hivyo, na vilivyomo ndani yake vya mwangaza na giza. Hili linapelekea kuwa ni lazima kumuamini Yeye Peke Yake, iwapo nyinyi ni miongoni mwa watu wa akili na kuzingatia.» Fir’awn akamwambia Mūsā kwa kumtisha, «Ukichukua mwingine asiyekuwa mimi ukamfanya ni mola nitakufunga jela pamoja na wale niliowafunga.» Mūsā akasema, «Je, utanifanya mimi ni miongoni mwa wafungwa jela, hata nikikuletea hoja ya kukata ambayo kwa hoja hiyo utabainika ukweli wangu?» Fir’awn akasema, «Basi ilete ikiwa wewe ni miongoni mwa wakweli katika madai yako.» Hapo Mūsā aliitupa fimbo yake na ikageuka nyoka mkubwa anayeonekana waziwazi. Na akauvuta mkono wake kutoka kwenye uwazi wa kanzu iliyofunguliwa kifuani au chini ya kwapa lake, na papo hapo ukawa mweupe kama maziwa usio na mbalanga, ukiwa ni alama kwa Fir'awn; akiurejesha unarudi rangi yake ya mwanzo, kama ulivyo mwili wake. Fir’awn akasema kuwaambia watukufu wa watu wake, kwa kuogopa wasije wakaamini, «Kwa kweli Mūsā ni mchawi hodari. Anataka kuwatoa nyinyi, kwa uchawi wake, kwenye ardhi yenu. Basi mnatoa shauri gani kuhusu yeye nipate kuyafuata maoni yenu?» Watu wake wakamwambia, «Msubirishe Mūsā na Hārūn, na utume askari mijini wawakusanye wachawi. Watakujia na kila anayejua uchawi na akawa hodari kuufahamu.» Wakakusanywa wachawi, na wakapangiwa wakati maalumu, nao ni wakati wa mchana wa siku ya Pambo ambayo wanajitenga na shughuli zao, na wanajikusanya na kujipamba, ili wakutane na Mūsā na wawahimize watu kujumuika kwa matarajio kwamba ushindi uwe ni wa wachawi. Sisi tunatarajia ushindi uwe ni wa wachawi ili tujikite kwenye dini yetu. Na wachawi walipomjia Fir’awn walimwambia, ‘Je, sisi tutakuwa na malipo ya mali au heshima ikiwa tutakuwa ni wenye kumshinda Mūsā?» Fir’awn akasema, «Ndio, nyinyi mtapata kwangu malipo mnayoyataka, na nyinyi hapo mtakuwa ni miongoni mwa wenye kusogezwa karibu na mimi.» Mūsā akasema kuwaambia wachawi, akitaka kuutangua uchawi wao na kuonyesha kuwa kile alichokileta si uchawi, «Tupeni mtakavyovitupa vya uchawi.» Basi wakatupa kamba zao na fimbo zao, na zikawadhihirikia watu kwenye akili zao kuwa ni nyoka wanaotembea, na wakaapa kwa enzi ya Fir’awn kwa kusema, «Sisi ni wenye kushinda.» Hapo akaitupa Mūsā fimbo yake, na papo hapo ikawa ni nyoka mkubwa, akawa anavimeza vile vilivyotokana na wao, hao wachawi, vya uzushi wa bandia. Waliposhuhudia hilo na wakajua kuwa halitokani na udanganyifu wa wachawi, walimuamini Mwenyezi Mungu na wakamsujudia. Wakasema, «Tumemuamini Mola wa viumbe wote. «Naye ni Mola wa Mūsā na Hārūn.» Naye ni yule Ambaye lazima ibada ielekezwe Kwake, Peke Yake, si kwa mwingine. Fir’awn akasema kuwaambia wachawi kwa kukataa, «Mmemkubali Mūsā bila ya idhini yangu!» Na akasema akiashiria kuwa kitendo cha Mūsā ni uchawi, «Yeye ni mkubwa wenu aliyewafundisha nyinyi uchawi, basi mtayajua mateso yatakayowafikia. Nitaikata mikono yenu na miguu yenu kwa kuitawanya: kwa kuukata mkono wa kulia na mguu wa kushoto au kinyume chake, na nitawasulubu nyote.» Wachawi walisema kumwambia Fir’awn, «Hakuna madhara ya duniani yatakayotupata, kwa kweli sisi ni wenye kurudi kwa Mola wetu, Atupe neema ya kuendelea. Sisi tunataraji Mola wetu Atusamehe makosa yetu ya ushirikina na mengineyo kwa kuwa sisi ndio Waumini wa mwanzo katika watu wako.» Na Mwenyezi Mungu Akampelekea wahyi Mūsā, amani imshukie, kwamba, «Nenda usiku pamoja na walioamini miongoni mwa Wana wa Isrāeli, ili Fir’awn na askari wake, ambao watawafuata nyinyi, wasije wakawafikia kabla ya kufika kwenu baharini.» Fir’awn akawatuma askari wake, alipopata habari kwamba Wana wa Isrāeli wameondoka usiku, (akawaamrisha) wakusanye jeshi lake kutoka miji ya utawala wake. Fir’awn akasema, «Kwa Hakika, Wana wa Isrāeli waliokimbia pamoja na Mūsā ni pote twevu (ni kundi dhalili) lenye idadi ndogo. Na wao wamevijaza hasira vifua vyetu kwa kuwa wameenda kinyume na dini yetu na wametoka bila ya idhini yetu, na sisi sote tuko macho, tuko tayari nao.» Mwenyezi Mungu Akamtoa Fir’awn na watu wake kwenye ardhi ya Misri yenye mabustani, mabubujiko ya maji, (chemchem) hazina za mali na majumba mazuri. Na kama tulivyowatoa, tuliwapatia nyumba hizo Wana wa Isrāeli baada yao wao. Hivyo basi Fir’awn na askari wake walimfuata Mūsā na waliokuwa pamoja naye wakati wa kuchomoza jua. Yalipoonana makundi mawili, watu wa Mūsā walisema, «Kwa hakika kikosi cha Fir’auni kimetufikia na kitatuangamiza.» Mūsā alisema kuwaambia, «Sivyo! Mambo si kama mlivyosema!. Hamtafikiwa. Kwa hakika Mwenyezi Mungu Yuko na mimi kwa msaada, Ataniongoza njia ya kuokoka mimi na kuokoka nyinyi.» Hapo tukampelekea wahyi Mūsā kwamba, «Piga bahari kwa fimbo yako!» Akapiga. Na bahari ikapasuka njia kumi na mbili kwa idadi ya kabila za Wana wa Isrāeli. Na kila kipande kilichojitenga na bahari ni kama jabali kubwa. Na tulimsogeza karibu Fir’auni na watu wake mpaka wakaingia baharini. Na tukamuokoa Mūsā na waliokuwa pamoja naye wote. Bahari ikaendelea kuachana kwake (kwa ule mpasuko) mpaka wakavuka kwenye nchi kavu. Kisha tukamzamisha Fir’auni na waliokuwa pamoja naye kwa kuifanya bahari iwafunike baada ya wao kuingia ndani wakimfuata Mūsā na watu wake. Kwa hakika, katika hilo lililotokea pana mazingatio ya ajabu yenye kuonyesha dalili ya uweza wa Mwenyezi Mungu. Na wengi wa wafuasi wa Fir’auni hawakuwa ni wenye kuamini, pamoja na alama hii yenye kushinda. Na kwa kweli Mola wako Ndiye Mshindi katika kuwatesa waliomkanusha na wakaenda kinyume na amri Yake, Mwenye rehema kwa waja Wake walioamini". [Suratu Shuarai 23-67]

Basi alipofikwa firauni na Gharika alisema: Nimeamini kuwa yeye Mwenyezi Mungu hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa yule amabaye wamemuamini wana wa Israeli, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Je, sasa hivi, ewe Fir'aun, wakati kifo kimekushukia ndipo, unakubali kuwa wewe ni mja wa Mwenyezi Mungu na hali ulimuasi na ukawa ni miongoni mwa waharibifu wenye kuzuia njia Yake kabla ya adhabu Yake kukushukia! Basi toba haitokunufaisha wakati wa kukata roho na kushuhudia kifo na adhabu". "Basi leo tutakuokoa kwa (kuuweka) mwili wako, akutazame mwenye kukanusha kuangamia kwako, ili uwe ni mazingatio kwa watu wenye kuja baada yako kuwaidhika na wewe. Na hakika wengi zaidi kati ya watu ni wenye kughafilika na hoja zetu na dalili zetu, hawazifikirii wala hawazizingatii".

Na Mwenyezi Mungu akawarithisha watu wa Mussa ambao walikuwa wananyanyaswa, akawarithisha ardhi kuanzia mashariki mpaka magharibi ardhi ambayo aliibariki na vilivyomo ndani yake, na akaangamiza yote aliyoyatengeneza Fir'auni na watu wake na majumba ya kifahari ambayo walikuwa wakiyajenga.

Na akateremsha Mwenyezi Mungu baada ya hapo kwa Mussa kitabu cha Taurati, ndani yake kinaweka wazi halali na haramu ambayo inapasa kwa wana wa Israeli (watu wa Musa) kuifuata.

Kisha Musa akafa -Amani iwe juu yake- na akatuma Mwenyezi Mungu baada yake mitume wengi kwa watu wake -wana wa israeli- wakiwafahamisha njia sahihi kila alipokufa mtume alikuja baada yake Mtume mwingine.

Mwenyezi Mungu alitusimulia visa vya baadhi yao kwa mfano Daudi na Sulaiman na Ayoub na Zakaria, na hakutusimulia sana visa vyao, kisha akamalizia kuwatuma hawa mitume kwa kumtuma Issa mwana wa Maryam juu yake amani, ambaye maisha yake yalikuwa yamejaa alama za utume kuanzia kuzaliwa kwake mpaka kuinuliwa kwake mbinguni.

Baada ya kupita vizazi na vizazi, ilipatwa Taurati aliyoiteremsha Mwenyezi Mungu kwa Mussa mabadiliko na kupindishwa kupitia mikono ya mayahudi ambao wanadai kuwa wao ni wafuasi wa Mussa -juu yake amani- Na Mussa yuko mbali nao, na Taurati iliyoko mikononi mwao haihesabiki kuwa ndiyo taurati ambayo iliteremshwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa kuwa wameingiza humo mambo ambayo hayastahiki kuwa yametoka kwa Mwenyezi Mungu, na wakamsifia Mwenyezi Mungu katika taurati hiyo kwa sifa ambazo zina mapungufu na ujinga na udhaifu- Ametukuka Mwenyezi Mungu kwa hayo wanayoyasema kutukuka kwa hali ya juu kabisa - amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu katika kutaja sifa zao: "Maangamivu na onyo kali kwa wanavyuoni wa shari wa Kiyahudi ambao wanaandika kitabu kwa mikono yao kisha wanasema, “Hiki kinatoka kwa Mwenyezi Mungu.” Nacho kinaenda kinyume na yale ambayo Mwenyezi Mungu Amemteremshia Nabii wake Mūsā rehema na amani zimshukie, ili wapokee, kwa kitendo hicho, manufaa ya ulimwenguni. Basi wao watapata mateso yenye kuangamiza kwa sababu ya kuuandika kwao ubatilifu huu kwa mikono yao, na watapata mateso yenye kuangamiza kwa sababu ya mali ya haramu wanayoichukua kwa shughuli yao hiyo, kama hongo na mfano wake. [Suratul Baqara 79]

 §  H- Mtume Isa Amani iwe juu yake.

Kwa hakika alikuwa Maryamu mwana wa Imrani Bikira aliyekuwa twahara ni mshika ibada miongoni mwa washika ibada na mwenye kufuata amri za Mwenyezi Mungu zilizoteremshwa kwa Mitume baada ya Musa, na alikuwa ni katika familia aliyoichagua Mwenyezi Mungu kwa walimwengu wa wakati huo. kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika Mwenyezi Mungu Amemchagua Ādam, na Nuhu, na jamii ya Ibrāhīm na jamii ya 'Imrān Akawafanya kuwa bora kwa watu wa zama zao". [Al Imran: 33]. Na wakampa habari njema Malaika kwa kuchaguliwa kwake na Mwenyezi Mungu. "Na kumbuka, ewe Mtume, pindi Malaika waliposema, «Ewe Maryam, hakika Mola wako Amekuchagua kwa kumtii na Amekusafisha na tabia duni na Amekuchagua kati ya wanawake wa ulimwengu wote katika zama zako. «Ewe Maryam, Endelea daima kumtii Mola wako, simama kwa utulivu na unyenyekevu na usujudu na urukuu pamoja na wenye kurukuu kwa kumshukuru Mola wako juu ya neema Alizokutunukia.» [Surat Al-imran 42-43].

Kisha akatoa habari Mwenyezi Mungu kutakasika na machafu ni kwake na mtukufu, Namna gani alivyomuumba Issa katika kizazi chake pasi na yakuwa na Baba. Kama ilivyo katika kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na utaje, ewe Mtume, katika Qur’ani hii habari ya Maryam alipojiweka mbali na watu wake, akajifanyia mahali upande wa Mashariki kando na wao. Akaweka kizuizi chenye kumsitiri na jamaa zake na watu wengine, hapo tukampelekea Malaika Jibrili akajitokeza kwake katika sura ya binadamu aliyetimia umbo. Maryam akasema kumwambia, «Mimi najilinda kwa Mwenyezi Mungu aniepushe nawe usinifanyie ubaya, iwapo wewe ni miongoni mwa wanaomcha Mwenyezi Mungu.» Malaika akamwambia, «Kwa hakika, mimi ni mjumbe wa Mola wako, Amenituma kwako nikutunuku mtoto wa kiume aliyesafika na madhambi.» Maryam akamwambia Malaika, «Vipi mimi niwe na mtoto wa kiume, na hakuna binadamu aliyenigusa kwa ndoa ya halali, na mimi sikuwa mzinifu?» Malaika akasema kumwambia, «Mambo ni hivyo kama unavyoeleza kwamba hakuna binadamu aliyekugusa na hukuwa mzinifu, lakini Mola wako Amesema, ‘Jambo hili kwangu ni jepesi, na ili mtoto huyu awe ni alama kwa watu yenye kuonyesha uweza wa Mwenyezi Mungu Aliyetukuka, na awe ni rehema itakayotokana na sisi kwake yeye, kwa mama yake na kwa watu.’» Na kupatikana kwa Īṣsā kwa namna hii lilikuwa ni jambo lililokadiriwa katika Ubao uliohifadhiwa, basi hapana budi lifanyike. Maryam akabeba mimba ya mtoto wa kiume baada ya Jibrili kupuliza kwenye mwanya wa kanzu yake, na pulizo hilo likafika kwenye uzao wake, na kwa sababu hiyo mimba ikaingia, na akaenda nayo mahali pa mbali na watu. Na uchungu wa mimba ukamfanya aende kwenye kigogo cha mtende, hapo akasema, «Natamani kama ningelikufa kabla ya siku ya leo na nikawa kitu kisichojulikana, kisichotajwa na kisichotambulika ‘ni nani mimi?.’» Jibrili au 'Īssā akamwita na kumwambia, «usisikitike, kwani Mola wako amekufanyia chini yako mkondo wa maji. «Na ukitikise kigogo cha mtende, zitakuangukia tende mbivu laini zitokazo mtini. «Basi zile tende hizo mbivu na unywe maji na ujifurahishe kwa huyo mtoto mwenye kuzaliwa. Na umuonapo yeyote miongoni mwa watu, akakuuliza juu ya jambo lako, mwambie, ‘Mimi nimejilazimisha nafsi yangu kwa Mwenyezi Mungu ninyamaze, sitasema na mtu leo.’» Kunyamaza kimya kulikuwa ni ibada katika Sheria yao, na haikuwa hivyo katika Sheria ya Mtume Muhammad, rehema ya Mwenyezi Mungu na amani zimshukie. Hapo Maryam aliwajia watu wake, naye amembeba mtoto wake, akitokea mahali pa mbali. Walipomuona namna hiyo, walisema kumwambia, «Ewe Maryam! Umeleta jambo kubwa ulilolizua. «Ewe dada ya mtu mwema Hārūn! Baba yako hakuwa ni mtu mbaya anayefanya machafu, na mama yako hakuwa ni mwanamke mbaya anayefanya umalaya.» Maryam akaashiria kwa mwanawe Īssā ili wamuulize na waseme naye. Wakasema kwa kumpinga, «Vipi tutasema na ambaye bado yuko mlezini (katika mbeleko) tena mchanga wa kunyonya?» Īssā akasema, naye akiwa katika hali ya uchanga wa kuwa mlezini akinyonya, «Mimi ni mja wa Mwenyezi Mungu, Ameamua kunipatia Kitabu, nacho ni Injili, na amenifanya kuwa Nabii. «Na Amenifanya niwe na wingi wa wema na manufaa popote nipatikanapo, na ameniusia kutunza Swala na kutoa Zaka muda wote nitapokuwa hai. «Na Amenifanya mimi niwe mwenye kumtendea wema mama yangu, na hakunifanya ni mwenye kujiona wala ni mbaya mwenye kumuasi Mola wangu. «Na salamu na amani ziko juu yangu mimi siku niliyozaliwa, siku nitakapokufa na siku nitakapofufuliwa nikiwa hai siku ya Kiyama.» Huyo tuliyokuhadithia, ewe Mtume, sifa zake na habari zake ndiye Īssā mwana wa Maryam pasina shaka, hali ya kuwa yeye ni neno la haki ambalo Mayahudi na Manaswara wanalitia shaka. Haikuwa kwa Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka, wala hainasibiani na Yeye kujichukulia mtoto miongoni mwa waja wake na viumbe vyake, Ameepukana na kutakasika na hilo; Akiamua jambo lolote, miongoni mwa mambo, na Akalitaka liwe, dogo au kubwa, halimkatalii, kwa hakika Yeye huliambia, «Kuwa» na likawa kama alivyolitaka liwe. Na Īssā aliwaambia watu wake, «Na hakika ya Mwenyezi Mungu, Ambaye nawalingania nyinyi Kwake, ni Mola wangu na Mola wenu, basi muabuduni Yeye Peke Yake Asiye na mshirika, kwani mimi na nyinyi tuko sawa katika uja na kumnyenyekea Yeye. Hii ndio njia iliyonyooka". [Surat Maryam 16-36]

Na Issa -Amani iwe juu yake- alipowalingania watu kumuabudu Mwenyezi Mungu, kuna waliomuitikia na kuna wengi walio kataa ulinganiaji wake, na akaendelea na ulinganiaji wake akiwalingania watu kwenye kumuabudu Mwenyezi Mungu lakini wengi walimkufuru na kumfanyia uadui na wakajaribu kumuua! akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu kumwambia Issa: (Ewe Issa hakika mimi nitakutimizia muda wako na nitakunyanyua kukuleta kwangu na nitakutwaharisha kuepukana na wale waliokufuru) [Al-Imran: 55]. Basi Mwenyezi Mungu akauweka mfanano kwa mmoja wa waliokuwa wakimfukuza wakamshika wakidhani kuwa ndiyo Issa bin Maryam -juu yake amani- wakamuuwa na wakamsulubu, na ama Mtume Issa bin Maryam kwa hakika Mwenyezi Mungu alimuinua kumpeleka kwake. Na kabla ya kuihama dunia aliwapa bishara watu wake kuwa Mwenyezi Mungu atamtuma Mtume mwingine jina lake anaitwa Ahmad ataieneza Mwenyezi Mungu dini hiii kupitia kwake. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Wakumbushe ewe Mtume, watu wako pindi Īssā, mwana wa Maryam, alipowaambia watu wake, «Mimi ni Mjumbe wa Mwenyezi Mungu kwenu, ni mwenye kusadikisha Taurati iliyokuja kabla yangu na ni mwenye kushuhudilia ukweli wa Mtume atakayekuja baada yangu, jina lake ni Ahmad, naye ni Muhammad, rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani,na ni mwenye kulingania watu wamuamini, basi alipowajia Muhammad, rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani, kwa aya zilizo wazi walisema, «Huu ni uchawi waziwazi.» [Surat swaffi 6]

Kisha ukapita muda wa miaka kadhaa, katika zama hizo wakagawanyika wafuasi wa Nabii Issa na likatoka kundi miongoni mwao wakapituka mipaka na wakadai yakuwa Issa ni mwana wa Mungu -Ametakasika Mwenyezi Mungu kwa yale wayasemayo kutakasika kuliko kukubwa- walidanganyika kwa hilo kwakuwa walimuona Issa ni mtoto asiyekuwa na baba, basi akatoa habari Mwenyezi Mungu kuhusu hilo kwa kauli yake: "Hakika mfano wa Mwenyezi Mungu kumuumba 'Īssa, bila ya baba, ni kama mfano wa Mwenyezi Mungu kumuumba Adam, bila ya baba wala mama. Mwenyezi Mungu Alimuumba kutokana na mchanga wa ardhi kisha Akamwabia, «kuwa kiumbe», akawa. Basi madai ya uungu wa 'Īssā kwa kuwa aliumbwa bila ya baba, ni madai ya uongo. Ādam, amani imshukie, aliumbwa bila ya baba wala mama, na wote wamekubaliana kwamba yeye ni mja miongoni mwa waja wa Mwenyezi Mungu. [Al Imran: 59]. Wala kuumbwa kwa Issa bila baba si jambo la ajabu sana kuliko kuumbwa kwa Adam pasina kuwa na baba wala mama.

Na kwa ajili hiyo basi Mwenyezi Mungu anawasemesha wana wa Israeli katika Qur'ani ili wajiweke mbali na kukufuru, hii kwa maneno yake Mwenyezi Mungu Mtukufu aliposema: "Enyi watu wa Injili! Msiikiuke itikadi ya haki katika dini yenu, na msiseme kuhusu Mwenyezi Mungu isipokuwa haki. Hivyo basi, msimfanye kuwa Ana mke wala msimfanye kuwa ana mwana; hakika Al-Masīḥ ‘Īssā, mwana wa Maryam, ni mjumbe wa Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu Amemtuma kwa haki na Amemuumba kwa neno ambalo Amemtuma nalo Jibrili alipeleke kwa Maryam, nalo ni neno Lake, «Kuwa!» na ikawa. Nalo ni mvivio (mpulizo) kutoka kwa Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka, aliouvivia Jibrili kwa amri ya Mola Wake. Kwa hivyo , aminini kwamba Mwenyezi Mungu ni Mmoja na mjisalimishe Kwake na muwaamini Mitume Wake katika yale waliowaletea kutoka kwa Mwenyezi Mungu na muyafuate kivitendo. Wala msimfanye ‘Īssā na mama yake kuwa ni washirika wa Mwenyezi Mungu. Komeni na matamshi hayo! Itakuwa bora kwenu kuliko hayo mliyonayo. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mola Mmoja, kutakasika na sifa za upungufu ni Kwake. Vilivyoko mbinguni na ardhini ni miliki Yake. Basi vipi Atakuwa na mke au mtoto kati ya hivyo? Inatosha kuwa Mwenyezi Mungu Ndiye Msimamizi wa kupanga mambo ya viumbe Wake na kuendesha maisha yao. Hivyo basi, mtegemeeni, Yeye Peke Yake, kwani Yeye Ndiye Mwenye kuwatosha". Hatoona unyonge Issa kuwa ni mja wa Mwenyezi Mungu.Vile vile Malaika waliokaribishwa kukubali kuwa wao ni waja wa Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka. Na yeyote mwenye kuona unyonge kufuata kikamilifu na kunyenyekea na akafanya kiburi, Basi hao Mwenyezi Mungu Atawafufua Awakusanye Kwake Siku ya Kiyama, Atoe uamuzi baina yao kwa hukumu Yake ya uadilifu na Amlipe kila mmoja kwa kile anachostahili. Ama wale ambao wamemuamini Mwenyezi Mungu, kiitikadi, kimaneno na kivitendo, wakasimama imara kufuata sheria Zake, basi Yeye Atawalipa thawabu za vitendo vyao na Atawaongeza kutokana na fadhila Zake. Na ama waliokataa kumtii Mwenyezi Mungu na wakafanya kiburi kwa kutojidhalilisha Kwake, Atawaadhibu adhabu iumizayo. Hawatompata wa kuwasimamia atakayewaokoa na adhabu Yake, wala wa kuwanusuru ambaye atawanusuru badala ya Mwenyezi Mungu". [Surat Nisaai 171- 173]

Na atamsemesha Mwenyezi Mungu Nabii Issa siku ya Kiyama kwa kauli yake : Na kumbuka pindi atakaposema Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka, Siku ya Kiyama, «Ewe ‘Īssā mwana wa Maryam! Kwani wewe uliwaambia watu, ‘nifanyeni mimi na mama yangu kuwa ni waabudiwa badala ya Mwenyezi Mungu’?» ‘Īssā atajibu, kwa kumtakasa Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka, na kumuepusha na sifa za upungufu, «Haipasii kwangu kuwaambia watu yasiyokuwa haki. Nikiwa nililisema hili, basi ushalijua. Kwani hakuna chochote kinachofichikana kwako. Wewe unayajua yaliyomo ndani ya nafsi yangu, na mimi siyajui yaliyomo ndani ya nafsi yako. Hakika yako wewe Ndiye Mjuzi wa kila kitu, kilichofichikana au kuwa wazi.» ‘Īssā, amani imshukie, atasema, «Ewe Mola wangu! Sikuwaambia wao isipokuwa yale uliyonitumia wahyi nayo na ukaniamrisha kuyafikisha, ya kukupwekesha wewe tu na kukuabudu. Na mimi nilikuwa nikishuhudia vitendo vyao na maneno yao nilipokuwa nikiishi nao. Na uliponikamilishia muda wangu wa kuishi katika ardhi, ukanipaza mbinguni nikiwa hai, ulikuwa wewe ndiye Mwenye kuzichungulia siri zao, na wewe ni Mwenye kushuhudia kila kitu, hakifichiki kwako chochote chenye kufichika ardhini au mbinguni". "Hakika yako wewe , ewe Mwenyezi Mungu, ukiwa utawaadhibu, basi wao ni waja wako, na wewe ndiye Mjuzi wa hali zao, unawafanya unavyotaka kwa uadilifu wako. Na ukiwa utawasamehe, kwa rehema yako, wale waliofuata njia za kuwafanya wasamehewe, basi wewe ndiye Mshindi Asiyeshindwa, Mwenye hekima katika uendeshaji wa mambo yake na amri Zake". Aya hii inamsifu Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka, kwa hekima Yake, uadilifu Wake na ukamilifu wa ujuzi Wake. Mwenyezi Mungu Atamwambia ‘Īssā Siku ya Kiyama, «Hii ndiyo Siku ya Malipo ambayo kutawafaa wale waliompwekesha Mwenyezi Mungu kule kumpwekesha kwao Mola wao na kufuata kwao sheria Yake, ukweli wa nia zao, maneno yao na matendo yao. Watakuwa na mabustani ya Pepo, inayopita mito chini ya majumba yake ya fahari, hali ya kukaa humo milele. Mwenyezi Mungu Ameridhika nao ndipo Akayakubali mema yao, na wao wameridhika naye kwa malipo mazuri mengi aliyowapa. Kwa Malipo hayo na kuwa Yeye Ameridhika nao huko ndiko kufuzu kukubwa. [Al Maaidah: 116-119].

Kwa hivyo Masihi Issa Mwana wa Mariamu -juu yake amani- yuko mbali na kundi hili la mamilioni ambao wanajiita wenyewe kwa jina la Wakristo na wanaamini kuwa wao ni wafuasi wa Kristo (Masihi).

  3- Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu (Ni Mwisho wa Manabii na Mitume).

Na baada ya kunyanyuliwa Issa -Amani iwe juu yake- kilipita kipindi kirefu takribani karne sita (miaka mia) (600) watu wakazidi kupotoka na kuacha uongofu, na ukawaenea Ukafiri na upotofu na kumwabudu asiyekuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu. Basi Mwenyezi Mungu akamtuma Muhammad - rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- katika mji wa Makka katika ardhi ya Hijjazi kwa uongofu na dini ya haki; ili amuabudu Mwenyezi Mungu mmoja tu, na akamzawadia alama na miujiza mbali mbali yenye kujulisha juu ya utume wake na ujumbe wake na akawa kwa ujumbe huo ni mwisho wa mitume, na akaifanya dini yake kuwa ndiyo mwisho wa dini zote na akaihifadhi na kutobadilishwa na kugeuzwa mpaka mwisho wa maisha ya dunia na kusimama kiama, Basi ni nani huyo Muhammadi? Na, ni akina nani watu wake? Na ni vipi alimtuma? Ni ipi Dalili ya Utume wake? Na ni upi ufafanuzi wa historia yake? Haya ndiyo tutakayojaribu kuyaweka wazi kwa idhini ya Allah katika kurasa hizi za muhutasari.

 §  A- Nasaba (ukoo) wake na Utukufu wake .

Yeye ni Muhammad bin Abdillahi, mtoto wa Abdulmuttwalib mtoto wa Haashim Mtoto wa Abdi Manafi, mtoto wa Qusswayyi, mtoto wa Kilabi, Nasaba yake inafika kwa Ismail Mtoto wa Ibrahim -juu ya wawili hao amani- ni katika kabila la Makuraishi wanaotokana na waarabu, alizaliwa Makkah mwaka 571 tangu kuzaliwa kwa Masiha -Amani iwe juu yake- Alifariki baba yake mzazi hali yakuwa yuko tumboni kwa mama yake na akaishi hali yakuwa ni yatima na akalelewa na Babu yake Mzee Abdulmuttwalib, kisha baada ya kufa babu yake alilelewa na baba yake mdogo aitwae Abuu Twaalib.

 §  B- Sifa zake:

Tumetaja kuwa Mtume mteuliwa anatoka kwa Mwenyezi Mungu ni lazima awe ni katika kilele cha juu kutoka katika nafsi yenye kuheshimika na mwenye maneno ya kweli na tabia njema na vile vile alikuwa Muhammad -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- kwa hakika aliishi hali yakuwa ni mkweli muaminifu mwenye tabia njema mwenye maneno mazuri mwenye ulimi fasaha na mwenye kupendwa na watu wa karibu pia na wa mbali akitukuzwa na watu wake akiheshimiwa kati yao, na walikuwa hawamuiti isipokuwa kwa jina la muamunifu, na walikuwa wakitunza kwake amana zao wakati wanaposafiri.

Na kwa kuongezea uzuri wa tabia zake; kwa hakika alikuwa ni mzuri wa umbile jicho halichoki kumwangalia, mwenye uso mweupe mwenye macho makubwa mwenye nyusi nyingi, mwenye nywele nyeusi, na mabega mapana, hakuwa mrefu sana wala mfupi na alikuwa mwenye kimo cha kati na kati na alikuwa anakaribia urefu. Na anamsifia mmoja kati ya maswahaba zake kwa kusema: "Nilimuona Mtume wa Mwenyezi Mungu -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- akiwa katika pambo (vazi) la kiyemeni sijawahi kumuona mtu mzuri kama yeye" Na alikuwa hawezi kusoma wala kuandika tena akiwa amezungukwa na watu wasiojua kusoma wala kuandika na ni Nadra sana kumpata mmoja wao mwenye kuweza kusoma na kuandika lakini walikuwa ni wajanja na wenye nguvu na kumbukumbu za haraka pasina kufikiria.

 §  C- Makuraish na Waarabu.

Walikuwa ni Watu wa Mtume - Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- na Jamaa zake wa karibu wakiishi katika mji wa Makkah pembeni mwa nyumba tukufu na Al-kaaba tukufu ambayo Mwenyezi Mungu alimuamrisha Ibrahimu- juu yake amani aijenge yeye na mwanaye Ismail.

Lakini baada ya kupita muda mrefu waliachana na dini ya Ibrahim (kumtakasia dini Mwenyezi Mungu) na wakaweka wao- na makabila yaliyokuwa yanawazunguka- masanamu yatokanayo na mawe na miti na dhahabu pembeni mwa Al-kaaba, na wakayatukuza na wakaitakidi kuwa yanauwezo wa kunufaisha na kudhuru na wakaanzisha utaratibu wa kuyaabudu, na masanamu yaliyokuwa maarufu zaidi ni sanamu linaloitwa Hubal, ambalo lilikuwa ni sanamu kubwa na lenye mambo makubwa. Ukiongezea masanamu wengine na miti iliyoko nje ya Makka iliyokuwa ikiabudiwa kinyume na Mwenyezi Mungu, na huzungushiwa mapambo ya utakatifu, na yalikuwa maisha yao yamezungukwa na mazingira ambayo pembezoni mwake kumejaa upingaji haki, ufahari na kiburi na kuwafanyia uadui wengine na vita vikali, japokuwa palikuwepo kati yao wenye tabia nzuri mfano ushujaa na kuwakirimu wageni na ukweli wa maneno na mambo mengine.

 §  Kutumwa kwa Mtume Rehema na amani za Allah ziwe juu yake anasema:

Na alipo fikisha Mtume-Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- miaka arobaini na alikuwa katika pango la Hiraa nje kidogo ya mji wa Makkah, ulimshukia Wahyi wa kwanza kutoka mbinguni kutoka kwa Mwenyezi Mungu basi akamjia Malaika Jibrili, akambana na akamwambia, Soma, akasema : Mimi siyo msomaji kisha akambana mara ya pili mpaka akachoka kwa kubanwa ,akasema kwa kumwambia, soma, akasema Mimi siyo msomaji, kisha akambana mara ya tatu mpaka akachoka zaidi kwa kubanwa kisha akamwambia: Soma, akamuuliza nisome nini, akasema: Soma, ewe Nabii, Qur’ani uliyoteremshiwa ukianza kwa Jina la Mola wako Aliyepwekeka kwa kuumba. Aliyemuumba kila binadamu kwa pande la damu nzito nyekundu. "Soma, ewe Nabii, kile ulichoteremshiwa, na Mola wako ni Mwingi wa wema, Mwingi wa ukarimu". Aliyewafundisha viumbe wake kuandika kwa kalamu. Alimfundisha binadamu vitu ambavyo hakuwa akivijua. Akamtoa kwenye giza la ujinga, Akampeleka kwenye nuru ya elimu. [Surat Al-alaq]

Kisha akaondoka Malaika na akamuacha, basi akarudi Mtume-Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- nyumbani kwake kwa mkewe akiwa na khofu ya hali ya juu, na akamwambia mkewe Khadija nifunike mimi naogopa, mke wake akamwambia, siyo hivyo na hatokufedhehesha Mwenyezi hata mara moja, kwa hakika wewe utaunga udugu na utabeba matatizo na utawasaidia watu katika matatizo makubwa.

Kisha akamjia Jibrili akiwa kwenye sura yake ambayo Mwenyezi Mungu amemuumbia, akiwa amefunika vilivyomo mpaka mwisho mwa upeo wa macho, akasema: ewe Muhammad mimi ni Jibrili na wewe ni Mtume wa Mwenyezi Mungu.

Kisha ukafululiza Wahyi kutoka mbinguni ukimuamrisha Mtume kuwalingania watu wake kwenye kumuabudu Mwenyezi Mungu peke yake na kuwatahadharisha na ushirikina na ukafiri, na akaanza kuwalingania watu wake mmoja mmoja na watu wake wa karibu; ili kuwaingiza katika uislamu na wa kwanza kuuamini ni mke wake Khadija bint ya Khuwailid na Rafiki yake kipenzi Abuu bakar aliye mkweli na mtoto wa baba yake mdogo ambaye ni Ally mtoto wa Abuu twaalib.

Kisha baada ya kujua watu wake kuwa anawalingania walianza kumpiga vita na kumfanyia vitimbi na uadui. Alitoka kwa watu wake asubuhi ya siku moja na akawaita kwa sauti yake ya juu "Waa swabaahaau" Ni neno wanalolisema waarabu wanapotaka kuwakusanya watu, (kama kusema: kumekucha! kumekucha! La mgambo likilia kuna jambo) basi wakamfuata watu wake wakikusanyika ili kusikia wanaambiwa nini, na walipojikusanya akawaambia: "Hivi mnaonaje ikiwa nitawapa habari kuwa maadui wamekuvamieni asubuhi au jioni hivi mtakuwa ni wenye kunisadikisha? wakasema, haijawahi kutokea wewe kusema uongo akasema: basi mimi kwenu nyinyi ni muonyaji wenu kuhusu adhabu kali. Kisha baba yake mdogo Abuu Lahab naye ni mmoja kati ya baba zake wadogo, na yeye na mke wake ndiyo walikwa wenye uadui mkubwa na Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- 'Umepata hasara wewe! hivi umetukusanya kwa jambo hili? basi akateremsha Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake - Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Imehasirika mikono miwili ya Abu Lahab, na yeye mwenyewe ameangamia, kwa kumuudhi Mtume, rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani. Hasara ya Abu Lahab ilithubutu. Haikumfaa mali yake wala alichokichuma Ataingia kwenye Moto wenye miale, yeye na mke wake ambaye alikuwa akibeba miba na kuiweka kwenye njia anayopita Mtume, rehema ya Mwenyezi Mungu na amani zimshukie, ili kumuudhi. Kwenye shingo yake patakuwa na kamba imara gumu ililio kavu, atabebwa nayo kwenye Moto wa Jahanamu, kisha atarushwa nayo mpaka chini. [Surat Al-masad 1-5]

Kisha akaendelea Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- akiwalingania katika uislamu, na akiwaambia semeni Hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu pekee, mkisema hivyo mtafaulu, wakasema, hivi umeifanya miungu kuwa Mungu mmoja hakika hili ni jambo la ajabu mno.

Na zikashuka aya mbali mbali kutoka kwa Mwenyezi Mungu zikiwalingania kwenye uongofu na zikiwatahadharisha na upotovu ambao walikuwa nao, miongoni mwa hizo Aya ni kauli yake Mwenyezi Mungu: "Sema, ewe Mtume, uwaambie washirikina kwa kuwakaripia na kulionea ajabu tendo lao, «Je nyinyi mnamkanusha Mwenyezi Mungu Aliyeumba ardhi kwa siku mbili, mnamfanya kuwa Ana washirika na wanaofanana Naye mkawa mnawaabudu pamoja Naye? Muumbaji Huyo Ndiye Mola wa viumbe wote. «Na Akajaalia Mwenye kutakasika katika ardhi majabali yaliyojikita juu yake, Akaibarikia kwa kuifanya iwe na kheri nyingi kwa watu wake, Akakadiria humo riziki za chakula kwa watu wake na yale yanayowafaa maishani kwa kipindi cha Siku nne: Siku mbili Aliumba ndani yake ardhi na Siku mbili Aliweka katika ardhi majabali yaliyojikita na Akakadiria katika Siku mbili hizo riziki zake zikiwa sawa kwa wenye kuuliza, yaani kwa mwenye kutaka kuliuliza hilo apate kulijua. Kisha Akalingana sawa mbinguni, na ilikuwa moshi hapo kabla, Akasema kuiambia mbingu na ardhi, «Fuateni amri yangu kwa hiari au kwa nguvu!» Nazo zikasema, «Tumekuja tukiwa watiifu kwako. Hatuna matakwa kinyume cha matakwa yako.» Mwenyezi Mungu Akapitisha kuziumba mbingu saba na kuzisawazisha kwa Siku mbili. Na kwa hilo ukatimia uumbaji wa mbingu na ardhi kwa Siku sita kwa hekima Anayoijua Mwenyezi Mungu, pamoja na uweza Wake, kutakasika na sifa za upungufu ni Kwake, wa kuziumba kwa mara moja. Na Akapeleka wahyi katika kila mbingu kwa Analolitaka na kuliamuru. Na tumeipamba mbingu ya karibu kwa nyota zinazong’ara na kwa ajili ya kuuhifadhi na Mashetani wanaosikiliza kwa kuiba. Uumbaji huo mzuri ni makadirio ya Aliye Mshindi katika ufalme Wake, Aliye Mjuzi Ambaye ujuzi Wake umekizunguka kila kitu. Basi wakipuuza wakanushaji hawa baada ya kubainishiwa sifa za Qur’ani zinazotajika vyema, na sifa za Mungu Mkubwa, waambie, «Kwa kweli, ninawaonya nyinyi adhabu yenye kuwamaliza mfano wa adhabu (iliyowashukia watu wa kabila la) 'Ād na Thamud walipomkanusha Mola wao na kuwaasi Mitume wao.» [Surat Fuswilat 9-13]

Lakini aya hizi na kule kulinganiwa hakukuwazidishia isipokuwa kuzidisha maasi na kuwa na kiburi cha kuiacha haki, bali wakazidi kuwaadhibu kila mwenye kuingia katika dini ya uislamu, na haswa wale wanyonge ambao hawana watu wa kuwakingia kifua, basi wakawa wanaweka katika kifua cha mmoja wao jiwe kubwa, wanamkokota kumpitisha masokoni katika wakati wa jua kali na wakimwambia kufuru dini ya Muhammad au ridhika na adhabu hii, mpaka wako miongoni mwao walikufa kutokana na adhabu hii kali.

Ama Mtume wa Mwenyezi Mungu -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- alikuwa kwenye himaya ya baba yake mdogo Abuu twaalib ambaye alikuwa akimpenda na akimuhurumia na alikuwa ni katika wakubwa wa kabila la kikuraishi lenye kuogopwa, isipokuwa hakuingia katika uislamu.

Na wakajaribu Makuraishi kumjadili Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- juu ya Da'wa yake wakamuahidi mali na ufalme na vyenye kudanganya ili aachane na kulingania katika dini hii mpya ambayo inafanya kuonekana wabaya miungu wao ambayo wanaitukuza na kuiabudu kinyume na Mwenyezi Mungu, na ukawa msimamo wa Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- ni mkali wenye kukatisha tamaa, kwa sababu jambo hili ni amri ameamrishwa na Mwenyezi Mungu ili alifikishe kwa watu, na kama ataachana na jambo hili basi atamuadhibu Mwenyezi Mungu. Na akawaambia kuwa mimi nawatakia khere na nyinyi ni watu wangu na jamaa zangu "Na ninamuapa Mwenyezi Mungu lau kama ningewadanganya watu wote basi nisingekudanganyeni nyinyi, na lau kama ningewafanyia hiyana watu wote basi nisingekufanyieni nyinyi".

Na walipoona kuwa juhudi za kujadiliana naye hazikufanikiwa katika kusimamisha Da'awa, uadui wa makuraishi ukazidi dhidi ya Mtume-Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- na wafuasi wake. Na wakataka makuraishi kutoka kwa Abuu twaalib amsalimishe Muhammad -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- ili wamuue, na wampe wakitakacho au aache kuieneza dini yake kati yao, basi Baba yake mdogo akamtaka ajizuie kuilingania dini hii.

Basi akaelezea Mtume -Rehema za mwenyezi mungu ziwe juu yake na amani- na akasema: "Ewe Baba yangu Mdogo, namuapia Mwenyezi Mungu, lau wangeweka jua katika mkono wangu wa kulia na wakaweka Mwezi upande wangu wa kushoto ili niiache dini hii, sitoweza kuiwacha dini hii mpaka Mwenyezi Mungu aidhihirishe dini hii au nife kwa ajili yake .

Basi akasema Baba yake mdogo: Nenda na useme lile utakalo kulisema na hawatakufanya chochote na wakikufanya chochote niko tayari kufa kwa ajili yako, na yalipomfika Abuu twalib mauti na mbele yake kulikuwa na baadhi ya wakubwa wa kikuraishi alimjia Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- akimsisitiza kuingia katika uislamu na akimwambia: Ewe Baba yangu mdogo sema Neno ambalo nitakudhamini kwalo mbele ya Mwenyezi Mungu, sema: 'Laa ilaaha illa llahu' basi wakubwa wakamwambia, hivi unataka kuiacha mila ya Abdul mutwalib (yaani unaiacha dini ya mababa na mababu) basi akaona ni jambo kubwa sana kuiacha dini ya baba zake na kuingia katika dini ya uislamu hivyo akafa hali yakuwa ni mshirikina. Basi akahuzunika Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- huzuni iliyokuwa kubwa kwa kufa Baba yake mdogo katika ushirikina, basi Mwenyezi Mungu akampa habari kwa kauli yake: "Hakika Wewe, ewe Mtume, humuongoi, unayependa aongoke. Lakini hilo liko kwenye mkono wa Mwenyezi Mungu, Anamuongoa Anayemtaka kumuongoa kwenye Imani na kumuafikia aifuate. Na Yeye Ndiye Anayemjua zaidi anayefaa kuongoka, hivyo basi Anamuongoa". [Suratil Qaswas 56]

Na alipata maudhi Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- baada ya kufa Baba yake mdogo Abuu Twaalib na wakawa wanachukua uchafu (kinyesi cha wanyama) na wakimuwekea mgongoni mwake wakati akisali mbele ya Kaaba.

Kisha akatoka Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- kuelekea mji wa Twaif ili awalinganie watu wa Twaaif kuingia katika uislamu, (nao ni mji wenye umbali wa kilo mita 70 kutoka katika mji wa Makkah) wakaipinga Da'awa yake vikali kuliko walivyoipinga watu wa Makkah, na wakawashawishi wale wapuuzi wao kwa kumpiga Mtume mawe -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- na wakamfukuza kutoka Twaif na wakawa wanamfuatilia nyuma wakimrushia mawe mpaka wakamtoa damu kwenye visigino vyake vitukufu.

Basi akaelekea Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- kwa Mola wake akimuomba na kumtaka amnusuru, basi Mwenyezi Mungu akamtumia Malaika akamwambia, "Hakika Mola wako amesikia namna wanavyokusema watu wako, sasa ikiwa utataka nitawabananisha kwa milima miwili- yaani milima miwili mikubwa-" Akasema Mtume: Hapana lakini natarajia kwa Mwenyezi Mungu kuwa atatoa katika migongo yao wenye kumuabudu yeye peke yake na wala hawatomshirikisha na chochote.

Kisha akarudi Makkah Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- na uadui ukaendelea na mashambulizi kutoka kwa watu wake kwa kila aliyemuamini alifanyiwa uadui, kisha likaja kundi kutoka katika mji wa Yathriba - mji ambao baada ya hapo ukaitwa kwa jina la Madinah- wakaja kwa Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- akawalingania katika uislamu nao wakasilimu, na akawatumia mmoja wa maswahaba zake akiitwa Mus'abu mtoto wa Umair akiwafundisha mafundisho ya uislamu, na wakasilimu kwenye mikono yake watu wengi wa Madina.

Na wakaja kwa Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- mwaka uliofuata wakimpa ahadi ya utiifu katika kuingia kwenye uislamu, kisha akawaamrisha maswahaba zake kuhamia Madina na wakahama makundi kwa makundi na mtu mmoja mmoja -na wakapewa jina la Muhaajiriina - (Yaani: Wahamiaji) na wakawapokea watu wa Madina kwa ukarimu na ukaribisho mzuri na kwa kuwakubali na wakawakaribisha katika majumba yao na wakagawana nao mali na majumba yao- na wakaitwa baada ya hapo kuwa ni Answar- (Watetezi)

kisha Makuraishi walipojua kuhama huku wakakubaliana kumuua Mtume -Rehema za mwenyezi mungu ziwe juu yake na amani-, na wakakubaliana waivamie nyumba yake ambayo analala humo, na akitoka wampige na upanga pigo kama la mtu moja, Mwenyezi Mungu akamuepusha nao na akawatoka pasina wao kuhisi chochote, na akakutana na Abuu bakar Swiddiq na akamuamrisha Ally kubakia Makkah ili aweze kurudisha amana za watu zilizohifadhiwa kwa Mtume kwa wenyenazo.

Na akiwa njiani anahama Makuraishi waliweka zawadi yenye thamani kubwa kwa yeyote atakaye mkamata Muhammad -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- sawa awe hai au amekufa, lakini Mwenyezi Mungu akamuokoa nao akafika Madina na swahiba wake Abuubakar wakiwa salama .

Na wakampokea watu wa Madina kwa bashasha na ukaribisho mzuri na furaha ya hali ya juu, na wakatoka wote kwenda kumpokea Mtume wa Mwenyezi Mungu wakisema amekuja Mtume wa Mwenyezi Mungu.

Yalidumu Makazi kwa Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani-, na akaanza kujenga msikiti kwanza ili kusimamshwe humo sala, kisha akawa anawafundisha watu sheria za uislamu na akiwasomea Qur'ani na akiwalea kwa tabia njema, wakakusanyika pembeni mwake maswahaba zake wakijifunza toka kwake uongofu na wakatakasika nafsi zao kutokana na uongofu na tabia zao zikawa za hali ya juu na mapenzi yao ya kumpenda Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- yakawa ni ya ndani na wakaathirika na sifa zake za hali ya juu na mafungamano ya udugu wakiimani yakawa ni yenye nguvu. Na ukawa mji wa Madina ni mji wa Madina kweli kweli wenye kupigiwa mfano, Madina ambayo unaishi katika anga iliyojaa furaha na udugu, hakuna tofauti kati ya tajiri wala masikini wala mweupe na mweusi wala hakuna tofauti kati ya mwarabu na asiyekuwa mwarabu wala hawajioni bora baadhi yao kwa wengine isipokuwa kwa imani na uchamungu, na likatengenezeka kwa watu hawa wateule Taifa bora na la ukweli lililokuwa na likajulikana kihistoria.

Na baada ya mwaka mmoja kuanzia alipohama Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- yalianza mashambulizi na vita kati ya Mtume na maswahaba zake dhidi ya kabila la kikuraishi, na kila aliyekwenda pamoja na kabila hilo katika kuifanyia uadui dini ya uislamu.

Na vikatokea vita vya kwanza kati yao, navyo ni vita vya Badri vikubwa katika bonde lililopo kati ya Makkah na Madina, akawapa Mwenyezi Mungu msaada waislamu, na walikuwa idadi yao ni wapiganaji 314 wakipigana na Makuraishi ambao idadi ya wapiganaji wao walikuwa 1000, na waislamu wakapata ushindi wa kutosha, na wakauliwa Makuraishi sabini na wengi wao ni wakubwa na viongozi wa Makuraishi, na waliobakia wakakimbia.

Kisha zikaja vita vingine kati ya Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- na Makuraishi, aliweza Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- katika mwisho wake (Baada ya kurudi kwake toka Makkah kwa miaka minane) kulipeleka jeshi ambalo nguvu yake ilikuwa ni wapiganaji 10,000 miongoni mwao ni katika walioingia katika uislamu walipokuwa Makka tukufu ili kuwapiga vita Makuraishi nyumbani kwao na waingie mji wa Makkah kwa nguvu na waweze kuwashinda ushindi wenye nguvu, na kulishinda kabila lake ambalo lilitaka kumuua na kuwaadhibu maswahaba zake na likazuia watu kuingia katika dini ambayo amekuja nayo kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Basi akawakusanya baada ya ushindi uliokuwa mashuhuri na akasema kuwaambia: Enyi kundi la Kikuraishi Hivi mnadhani kuwa mimi nitawafanya nini?wakasema: Ndugu mkarimu na mtoto wa ndugu yetu mkarimu, akasema: Basi ondokeni kwani nyie mko huru, akawasamehe na akawapa uhuru wa kujiiunga na dini ya uislamu".

Na ikawa hii ni sababu ya kuingia watu katika dini ya uislamu makundi kwa makundi, na likasilimu bara arabu lote na wakaingia katika dini ya uislamu.

Na wala haukupita muda mrefu akawa amehiji Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- na wakahiji pamoja naye watu 144,000 katika wale wapya waliongia katika dini ya uislamu.

Na akasimama akiwahutubia katika siku ya Hijja kubwa na akiwabainishia hukumu za dini na sheria za uislamu kisha akawaambia: "Huenda mimi na nyie tusikutane tena baada ya mwaka huu, basi fahamuni kuwa inatakiwa amfikishie aliyekuwepo yule asiyekuwepo". Kisha akawaangalia na akasema: "je nimefikisha?" Watu wakasema: ndiyo, akasema: "Ewe Mola wangu wa haki shuhudia". Akasema: "Tambueni kuwa nimefikisha" Watu wakasema: 'ndiyo' Akasema: "Ewe Mola wangu shuhudia kuwa nimefikisha".

Kisha akarudi Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- katika mji wa Madina baada ya Hijja, na akawahutubia watu siku moja na akawaambia; "Hakika mja amepewa hiyari na Mwenyezi Mungu kati ya kubakia duniani au kuchagua yaliyoko kwa Mwenyezi Mungu basi mja akachagua yaliyoko kwa Mwenyezi Mungu", wakalia maswahaba na wakawa wamejua kuwa yeye anakusudia nafsi yake na kuwa yeye yuko karibu kufariki na kuiacha dunia, na katika siku ya juma tatu ya tarehe kumi na mbili mwezi wa tatu Hijiria katika mwaka wa kumi na moja tangu kuhama Mtume, yalizidi maradhi ya bwana Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- na kikamuanza kilevi cha mauti, akawatazama maswahaba wake mtazamo wa kuwaaga na akawausia kuzihifadhi sala na akaisalimisha roho yake tukufu na akahama kuelekea kwa kipenzi aliye juu.

Walipata pigo maswahaba -Radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yao- na wakapata huzuni na masikitiko makubwa na msiba ukawaathiri mpaka ikafikia hatua mmoja wao ambaye ni Omari bin khatwab -Radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake- alisimama akiwa amechomoa upanga wake kutokana na mfadhaiko mkubwa na akasema: sitosikia yeyote anasema kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu amekufa isipokuwa nitamuua.

Basi akasimama Abuu bakar swiddiq akiwakumbusha kwa maneno ya Mwenyezi Mungu Mtukufu. "Hakuwa Muhammad , rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani, ni kiumbe aina nyingine, isipokuwa yeye ni Mtume wa jinsi ya Mitume wengine waliokuweko kabla yake, anafikisha ujumbe wa Mola wake. Basi iwapo atakufa, kwa kumalizika muda wake, au atauawa, kama walivyoeneza uvumi maadui, kwani mtarudi nyuma na kuacha dini yenu na kuyaacha aliyowaletea Mtume wenu? Basi yeyote miongoni mwenu atakayerudi nyuma akaiacha dini yake, yeye hatamdhuru Mwenyezi Mungu chochote, bali ataidhuru nafsi yake madhara makubwa. Ama atakayekuwa na msimamo imara juu ya Imani yake na akamshukuru Mola wake juu ya neema ya Uislamu, hakika Mwenyezi Mungu Atamlipa malipo mazuri kabisa". [Al-Imran: 144]. Basi aliposikia Omar aya hizi hakuvumilia isipokuwa alianguka na akazimia.

Huyu ndiye Muhammad Mtume wa Mwenyezi Mungu, na mwisho wa manabii na mitume alimtuma Mwenyezi Mungu kwa watu wote akiwapa bishara njema na kuwaonya na akafikisha ujumbe na akatekeleza amana na akaupa umma nasaha .

Alimpa nguvu Mwenyezi Mungu kwa Qur'ani tukufu iliyoteremshwa kutoka mbinguni, Qur'ani ambayo "Batili haikifikii kutoka upande wowote katika pande Zake, na hakuna kitu chenye kuibatilisha, kwani hiyo imetunzwa isipunguzwe wala isizidishwe. Ni uteremsho kutoka kwa Mwingi wa hekima katika kuendesha mambo ya waja Wake, Mwenye kushukuriwa kwa sifa za ukamilifu Alizonazo". [Surat Fuswilat 42] Qur'ani ambayo kama wangekusanyika wanadamu kuanzia wa mwanzo ilipoumbwa dunia mpaka wa mwisho ili wapate kuleta mfano wake, hawataweza kuleta mfano wake hata kama wao kwa wao wangekuwa ni wenyekusaidiana.

Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Enyi watu Muabuduni Mwenyezi Mungu Ambaye kakuumbeni nyinyi na Akawaumba waliokuwa kabla yenu, ili muwe ni miongoni mwa wenye kumcha Mwenyezi Mungu". Mola wenu ni Yule Aliyewafanyia ardhi iwe ni tandiko, ili maisha yenu yawe mepesi juu yake, na mbingu ziwe zimejengeka madhubuti, na Akateremsha mvua kutoka mawinguni, Akatoa kwa mvua hiyo matunda na mimea aina mbali mbali ili iwe ni riziki kwenu. Basi, msimuwekee Mwenyezi Mungu washirika katika ibada, hali nyinyi mnajua kuwa Mwenyezi Mungu Amepwekeka katika kuumba, kuruzuku na kustahiki kuabudiwa. Na mkiwa, enyi makafiri, mna shaka juu ya Qurani tuliyomteremshia mja wetu Muhammad, Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani, na mkadai kuwa haitoki kwa Mwenyezi Mungu, basi leteni sura moja inayofanana na sura ya Qurani, na takeni msaada kutoka kwa yeyote mnayemuweza ili awasaidie, iwapo nyinyi ni wakweli katika madai yenu. Mkiwa hamuwezi sasa, na hamtaweza wakati unaokuja kabisa, basi uogopeni Moto, kwa kumuamini Nabii, Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani, na kumtii Mwenyezi Mungu Aliyetukuka. Moto ambao kuni zake ni watu na mawe, umeandaliwa kwa wenye kumkanusha Mwenyezi Mungu na Mitume Wake. Waambie, ewe Mtume, watu wa Imani na amali nzuri, habari yenye kuwajaza furaha, kuwa wao huko Akhera watakuwa na Mabustani ya ajabu, ambayo inapita mito chini ya majumba yake makubwa na miti yake yenye vivuli. Kila Anapowaruzuku Mwenyezi Mungu humo aina yoyote ya matunda yenye ladha, watasema, “Mwenyezi Mungu Alituruzuku aina hii ya matunda kipindi cha nyuma.” Watakapoionja wataikuta ladha yake ni tofauti na ladha yake (yaani: na ile ladha ya duniani), ingawa inafanana na aina iliyopita kwa rangi, sura na jina. Na katika hayo Mabustani ya Peponi watakuwa na wake waliosafishika na kila aina ya uchafu, wa nje, kama mkojo na damu ya hedhi, na wandani, kama kusema uongo na kuwa na tabia mbaya. Na wao, katika Pepo na starehe zake, watakaa milele, hawafi humo wala hawatoki". [Al Baqara: 21-25].

Na hii Qur'ani imejengeka kwa sura mia moja na kumi na Nne (114), ndani yake kuna aya elfu sita, Mwenyezi Mungu anawapa changamoto wanadamu kwa zama zote zilizopita kuwa walete sura moja tu mfano wa hii Qur'ani, na sura fupi zaidi katika Qur'ani zimejengeka kwa aya tatu tu.

Basi ikiwa wataweza kufanya hivyo (kuleta mfano wa Qur'ani) basi nawajue kuwa hii Qur'ani haitoki kwa Mwenyezi Mungu. Na huu ni muujiza mkubwa ambao Mwenyezi Mungu amempa msaada Mtume wake -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- kama alivyo mpa msaada Mwenyezi Mungu kwa miujiza mingine isiyo ya kawaida, miongoni mwayo:

 §  E- Kupewa Msaada Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- kwa miujiza mbali mbali:

1- Alikuwa anamuomba Mwenyezi Mungu na anaweka mkono wake katika chombo yanatibuka maji kutoka katika vidole vyake na wanakunywa wanajeshi maji hayo, idadi yao ni zaidi ya elfu moja .

2- Na alikuwa akimuomba Mola wake na anaweka mkono wake katika chakula na chakula kinaongezeka katika sahani mpaka kinatosha kuliwa na maswahaba Elfu moja na mia tano.

3- Na alikuwa akiinua mikono yake mbinguni akimuomba Mwenyezi Mungu kuteremsha mvua, basi alikuwa haondoki sehemu ile aliyoombea mpaka yabubujike maji kutoka usoni kwake Mtukufu kutokana na athari ya mvua na miujiza mingine mingi.

Na akampa Mwenyezi Mungu msaada wa kumuhifadhi na wala hawezi yeyote kumfikia kwa yule atakaye kumuuwa na atakaye kuificha nuru ambayo amekuja nayo kutoka kwa Mwenyezi Mungu, kama ilivyo katika kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu. "Ewe Mtume, fikisha wahyi wa Mwenyezi Mungu uliyoteremshwa kwako kutoka kwa Mola wako. Na iwapo utapunguza bidii katika kuufikisha, ukaficha chochote katika wahyi huo, basi utakuwa hukuufikisha ujumbe wa Mola wako. Na kwa hakika, Mtume , rehema ya Mwenyezi Mungu na amani zimshukie, alifikisha ujumbe wa Mola wake kikamilifu. Basi yeyote atakayedai kuwa yeye alificha chochote, katika yale aliyoteremshiwa, atakuwa amemzulia Mwenyezi Mungu na Mtume Wake uongo mkubwa. Na Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka, ni Mwenye kukulinda na kukuokoa na maadui zako. Si juu yako lolote isipokuwa ni kufikisha. Kwa hakika Mwenyezi Mungu hamuelekezi kwenye uongofu aliyepotea njia ya haki na akayapinga uliyokuja nayo kutoka kwa Mwenyezi Mungu". [Al Maaida: 67].

Hakika alikuwa Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- pamoja na kupewa msaada na Mwenyezi Mungu -ni kiigizo chema katika matendo yake yote na kauli zake,na alikuwa wa mwanzo kutekeleza amri za Mwenyezi Mungu zinazoteremka juu yake kutoka kwa Mwenyezi Mungu, na alikuwa ni miongoni mwa wenye pupa ya kufanya ibada na utiifu, na ni mkarimu, hakibakii kitu mikononi mwake katika mali isipokuwa ataitoa katika njia ya Mwenyezi Mungu kwa kuwapa maskini na mafukara na wenye kuhitaji, bali hata urithi aliwaambia maswahaba wake kuwa: "Sisi jopo la Manabii haturithiwi, chochote tulichokiacha ni sadaka"

Ama kuhusu tabia zake hakuna awezaye kuzifikia, hakuandamana na yeyote isipokuwa alimpenda toka ndani ya moyo wake, hivyo basi anakuwa Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- ndiye kipenzi mkubwa kwake yeye kuliko watoto wake na mzazi wake na watu wote.

Anasema Anas bin Maalik mtumishi wa bwana Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- "sikuwahi kugusa kiganja kizuri na kilaini wala chenye kunukia zaidi kuliko kiganja cha Mtume wa Mwenyezi Mungu, na kwa hakika nilimuhudumia miaka kumi na wala hakuwahi kuniambia kwa kitu nilichokifanya kwanini umekifanya, wala sijawahi kuacha kufanya kitu akaniambia kwanini hukufanya "[1].

Huyo ndiye Muhammad Mtume wa Mwenyezi Mungu ambaye Mwenyezi Mungu ameiinua heshima yake na akuinua utajo wake kwa walimwengu wote, na wala hatajwi mwanadamu katika huu ulimwengu leo hii na kabla ya leo kama anavyotajwa yeye, tangu mwaka Elfu moja na mia Nne, mamilioni ya vipaza sauti katika pande zote za ulimwengu vinamtangaza kila siku mara tano kwa kusema: "Nashuhudia kuwa Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu " mamilioni ya wenye kusali wanarudia rudia kila siku mara kumi kwa kusema "Nashuhudia kuwa Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu".

 §  F- Maswahaba watukufu :

Waliibeba Maswahaba watukufu Da'wa ya uislamu baada ya kufa kwa bwana Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- na wakaenda nayo mashariki mwa ardhi na magharibi yake, na walikuwa kiukweli ni walinganiaji bora wa dini hii, na walikuwa kwa hakika ni watu wakweli katika kuongea kwao na wenye uadilifu mkubwa na wingi wa kutunza Amana, na wenye pupa ya kuwaongoa watu na kuwaenezea kheri.

Walijipamba na sifa za mitume na wakawaiga kwa sifa zao, na ikawa kwa tabia hizi athari yake ni ya wazi katika kukubalika kwa dini hii kwa mataifa ya duniani, watu wakaingia mfululizo katika dini ya Mwenyezi Mungu makundi kutoka Afrika magharibi mpaka mashariki ya Asia na mpaka katikati mwa bara la ulaya kwa kuuipenda dini hii bila kulazimwishwa wala kutenzwa nguvu.

Hakika hao ni Maswahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu ambao ni watu bora baada ya manabii, na walio Maarufu kati yao ni makhalifa wanne ambao walihukumu dola ya kiislamu baada ya kufa kwa bwana Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- na wao ni :

1- Abubakari Swidiiq.

2- Omar bin khattwab.

3- Othman bin Affaan.

4- Ally bin Abii Twaalib.

Waislamu wanawatambua maswahaba hawa kwa kina na wanawaheshimu, na wanajikurubisha kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa kumpenda Mtume wake na kuwapenda Maswahaba wa Mtume wake wote, wake kwa waume na wanawatukuza na wanawaheshimu na kuwaweka katika nafasi zao wanazostahiki.

Wala hakuna mwenye kuwachukia na kuwavunjia heshima yao isipokuwa yule mwenye kuikufuru dini ya uislamu hata kama atadai kuwa yeye ni muislamu, Mwenyezi Mungu amewasifia kwa kauli yake. {Mmekuwa Umma bora mlioteuliwa kwa ajili ya watu mnaamrisha mema na mnakataza mabaya na mnamuamini Mwenyezi Mungu} [Al-Imran: 110]

Na alithibitisha Radhi zake kwao pale walipompa Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- kiapo cha utiifu Akasema: Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mwenyezi Mungu Ameridhika na Waumini pale walipokupa mkono wa ahadi, ewe Mtume, chini ya mti (Hii ndio hiyo Bay 'ah al-Ridwān ya hapo Ḥudaybiyah). Mwenyezi Mungu Alijua yaliyomo ndani ya nyoyo za Waumini hawa ya Imani, ukweli na utekelezaji ahadi, basi Mwenyezi Mungu Akawateremshia utulivu, Akaziimarisha nyoyo zao na Akawapa, badala ya kile kilichowapita katika mapatano ya Ḥudaybiyah, ufunguzi wa karibu, nao ni ufunguzi wa kuiteka Khaybar. (Suratil fat-hi 18)

  4- Nguzo za Uislamu :

Uislamu una nguzo tano za msingi, kwa uwazi wake nikuwa ni wajibu wa muislamu kulazimiana na nguzo hizo mpaka isadikike kwake kuwa na sifa ya kuitwa muislamu.

 §  1- Ni kushuhudia kuwa hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu peke yake na muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu.

Na ni neno la kwanza ambalo anapaswa aliseme mwenye kuingia katika uislamu, na atasema: (Ash-hadu anlaa ilaaha illa llaahu, wa ash-hadu anna Muhammadan rasuulullah)- Nashuhudia kuwa hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu na kuwa Muhammadi ni Mtume wa Mwenyezi Mungu-aseme maneno hayo akiamini maana zake zote, kama tulivyo fafanua huko nyuma.

Basi anaitakidi kuwa Mwenyezi Mungu ni Mola mmoja wa pekee ambaye hakuzaa wala hakuzaliwa, wala hana yeyote mwenye kufanana naye, na yeye ndiye muumba na asiye kuwa yeye basi huyo ni kiumbe, na yeye peke yake ndiye Mwenyezi Mungu anayestahiki kuabudiwa, hakuna mola mwingine asiyekuwa yeye, na anaitakidi kuwa Muhammad ni mja wa Mwenyezi Mungu na ni Mtume wake aliyeteremshiwa wahyi kutoka mbinguni na mfikishaji kwa ajili ya Mwenyezi Mungu wa maamrisho yake na makatazo yake ni wajibu kumsadikisha katika yale aliyoyatolea habari na kumtii katika yale aliyoyamrisha na kujiepusha na yale aliyoyakataza na kuyakemea.

 §  B- Nguzo ya pili: Kusimamisha swala.

Na katika Sala kuna dhihiri alama za unyenyekevu kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu, na mja husimama hali yakuwa mnyenyekevu anasoma aya za Qur'ani na kumtukuza Mwenyezi Mungu kwa aina tofauti za Dhikri na sifa, akirukuu kwa ajili yake na akaporomoka hali ya kusujudu, akimnong'oneza na kumuomba na kumtaka kutokana na fadhila zake tukufu na hayo ni kiunganishi kati ya mja na Mola wake ambaye amemuumba na anajua mambo yake ya siri na dhahiri na kumuelekea Mwenyezi Mungu mja wake wakati wa kusujudu, kufanya hivyo ni sababu ya kumpenda Mwenyezi Mungu mja wake na kuwa karibu naye na kumridhia, na mwenye kuacha ibada kwa kiburi cha kuacha kumwabudia Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu humkasirikia na humlaani na hutoka mtu huyo katika uislamu.

Na wajibu ni kusali sala tano kwa kila siku ikikusanya ndani yake kisimamo na kusoma suratil faatiha: Naanza kusoma Qur’ani kwa jina la Mwenyezi Mungu nikiomba msaada Wake. «Allah» ni jina la Mwenyezi Mungu, Mwingi wa baraka Mwenye kutukuka, Anayestahiki kuabudiwa na sio mwingine. Nalo ni jina mahsusi zaidi miongoni mwa majina ya Mwenyezi Mungu Aliyetukuka, na haitwi kwa jina hili yeyote isipokuwa Yeye Aliyetakasika na sifa za upungufu. «Al-Raḥmān» Mwenye rehema nyingi Ambaye rehema Zake zimewaenea viumbe vyote. «Al-Raḥīm» mwenye kuwarehemu Waumini. Na majina mawili haya, kati ya majina ya Mwenyezi Mungu Aliyetukuka, yanakusanya uthibitishaji wa sifa ya urehemevu kwa Mwenyezi Mungu Aliyetukuka kama inavyonasibiana na haiba Yake. Shukrani zote njema ni za Mwenyezi Mungu, Mwingi wa rehema mwenye kurehemu Mwingi wa rehema na mwenye kurehemu. Na Yeye, kutakasika ni Kwake, Peke Yake Ndiye Mwenye mamlaka ya Siku ya Kiyama, nayo ni Siku ya Malipo kwa matendo yaliyofanywa na waja. Muislamu anapoisoma aya hii katika kila rakaa, inamkumbusha siku ya Akhera na inamhimiza ajitayarishe kufanya matendo mema na kujiepusha na maasia na mabaya. Wewe tu ndiye tunayekuabudu na wewe tu ndiye tunayekuomba msaada. Tuongoze njia iliyonyooka. Njia ya wale uliowaneemesha. Na siyo ya wale waliokasirikiwa, wala ya waliopotea Suratul- Faatiha 1-7 Na kusoma chochote chepesi katika Qur'ani na ikijumuisha kurukuu na kusujudu na kumuomba Mwenyezi Mungu na kumtukuza kwa kusema:- Allahu Ak-bar- (Mwenyezi Mungu ni Mkubwa) na kwenye kurukuu kwa kusema :- Sub-hana rabbiyal Adhwiim- (Ametakasika Mola wangu Mtukufu) na kwenye kusujudu kwa kusema (Sub-haana rabbiyal Aala) ametakasika Mola wangu aliye juu.

Na kabla ya kutekeleza ibada ya sala ni lazima kwa mwenye kusali awe amejitwaharisha kutokana na najisi (haja ndogo na haja kubwa) katika mwili wake na mavazi yake na sehemu yake ya kusalia, awe ametawadha kwa maji na huko kutawadha kuna kuwa kwa kuosha uso wake na mikono yake na kupaka kichwa chake maji kisha kuosha miguu yake miwili.

Na kama atakuwa ni mwenye janaba (kwa kuingiliana na mke wake) basi ni wajibu juu yake kuoga kwa kuuosha mwili wake wote.

 §  C- Nguzo ya Tatu: ZAKAH.

Nacho ni kiwango fulani cha rasilimali amekifaradhisha Mwenyezi Mungu kwa matajiri kuwapa mafukara na masikini na wenye kuhitajia miongoni mwa watu katika jamii ili kukidhi mahitajio yao na idadi yake kifedha ni asilimia mbili na nusu katika mia moja, kutoka katika rasilimali, na hugawiwa kwa mwenye kustahiki Zakah.

Na nguzo hii ni sababu ya kuenea misaada ya kijamii kati ya mtu mmoja mmoja katika jamii pamoja na kuzidisha mapenzi na kuzoeana na kusaidizana baina yao na kuondosha chuki na vifundo kutoka katika tabaka la masikini kwenda kwenye tabaka la matajiri na waliofanyiwa wepesi, na ni sababu kuu ya kukuwa kwa uchumi na kuendelea kwa mzunguko wa mali kwa mfumo sahihi na kufika kwenye tabaka zote za jamii. Na hizi Zakkah ni wajibu katika mali kwa aina zote za mali, kuanzia pesa na wanyama na matunda na nafaka na mali iliyoandaliwa kwa ajili ya kuuzwa na zisizokuwa hizo kwa viwango tofauti kutokana na rasilimali ya kila aina katika aina za mali.

 §  D- Nguzo ya Nne : Kufunga Mwezi wa Ramadhani

Swaumu: Kufunga ni kujizuilia na kula na kunywa na kuwaendea wake, kwa nia ya kumuabudu Mwenyezi Mungu, kujizuia kuanzia kuchomoza Alfajiri mpaka kuzama jua.

Na Mwezi mtukufu wa Ramadhani ambao Mwenyezi Mungu amefaradhisha kufunga katika mwezi huo, ni Mwezi wa Tisa katika miezi ya miandamo, nao ni mwezi ambao ilianza kushuka Qur'ani kwa Mtume-Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani-

Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: {Mwezi mtukufu wa Ramadhani ambao imeshuka ndani yake Qur'ani hali ya kuwa ni muongozo wa watu na wenye kutenganisha kati ya haki na batili, basi yeyote atakaye kuwepo wakati mwezi huo unaandama basi na afunge mwezi huo} [Al Baqara: 185].

Na miongoni mwa faida kubwa za funga nikujizoesha kusubiri na kuongeza nguvu ya uwezo wa uchamungu na imani katika moyo, na hivyo ni kuwa swaumu ni siri kati ya mja na Mola wake kwani mwandamu anaweza kujitenga akakaa sehemu akala na akanywa na wala asijue mtu yeyote kufunga kwake, basi ikiwa ataacha kufanya hivyo kwa ajili ya kumuabudu Mwenyezi Mungu na kutii amri zake peke yake asiye na mshirika na yeye akijuwa kuwa hakuna yeyote anayeweza kuiona ibada yake hii isipokuwa Mwenyezi Mungu, inakuwa hiyo ni sababu ya kumzidishia imani na ucha mungu wake, na kwa hivyo ndiyo ikawa malipo ya wenye kufunga ni makubwa kwa Mwenyezi Mungu, bali wana mlango maalumu peponi uitwao mlango wa Rayyan. Na muislamu anatakiwa kufunga swaumu za hiyari kwa ajili kujiweka karibu na Mwenyezi Mungu, zisizokuwa za Mwezi wa Ramadhani siku zote za mwaka mzima isipokuwa siku mbili za Eid ulfitri na Eidul adh-ha.

 §  E- Nguzo ya Tano: Ni kuhiji nyumba tukufu.

Na ni lazima kwa muislamu kuitekeleza mara moja katika umri wake wote, na kama atazidisha zaidi ya mara moja basi itakuwa ni kujikurubisha zaidi kwa Mwenyezi Mungu. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu. "Na Mwenyezi Mungu amewawajibishia watu wafanye hijja kwenye nyumba hiyo tukufu kwa mwenye kuweza kufunga safari ya kwenda huko". [Al-Imran: 97]. Basi atasafiri muislamu kwenda katika viwanja vya ibada katika mji Mtukufu wa Makka katika mwezi wa Hijja nao ni mwezi wa mwisho katika miezi ya Hijriya mwezi mwandamo, na kabla ya kuingia Makkah atavua muislamu nguo zake na atavaa vazi la Ihraam nazo ni shuka mbili nyeupe.

Kisha atafanya matendo mbali mbali ya Hijja ikiwemo kutufu nyumba tukufu Alkaaba na kufanya Saayi -kukimbia- baina ya Mlima Swafaa na Mar-waa na kusimama Arafa na Kulala Muzdalifah na kufanya matendo mengine.

Na Hijja ni mkusanyiko mkubwa wa waislamu Duniani unawafunika udugu na kuhurumiana na pamoja na kupeana nasaha, vazi lao ni moja na kiwanja chao ni kimoja hakuna yeyote kati yao anayekuwa mbora isipokuwa kwa uchamungu, na malipo ya Hijja ni makubwa, amesema Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani: {Yeyote atakaye Hijji na akawa hakuzungumza upuuzi wala kufanya machafu, ataondoka kwenye madhambi nakuwa kama siku alivyozaliwa na mama yake} [2]

  5- Nguzo za Imani.

Na ikifahamika kuwa nguzo za uislamu kuwa ni alama za wazi ambazo anazitekeleza muislamu na kuwa utekelezaji wake unajulisha juu ya kushikamana na uislamu wake, basi kuna nguzo zingine ndani ya moyo ambazo inapasa kwa muislamu kuziamini ili uislamu wake uwe sahihi, na nguzo hizo huitwa nguzo za imani, kila kinapozidi kiwango chake katika moyo wake ndivyo anavyozidi kupanda daraja la imani na anastahiki kuingia katika waja wa Mwenyezi Mungu walioamini, na daraja hili ni daraja kubwa sana kwa waislamu, kwani kila Muumini ni muislamu lakini si kila muislamu ni muumini ambaye kaifikia daraja ya waumini.

Ni jambo la hakika kuwa ana asili ya imani lakini yawezekana asiwe na imani iliyokamilika.

Na nguzo za Imani ni sita

Ni kumuamini Mwenyezi Mungu na Malaika wake na vitabu vyake na Mitume wake na siku ya mwisho na kuamini Qadari kheri yake na shari yake.

Basi nguzo ya kwanza: Ni kumwamini Mwenyezi Mungu, na kunaujaza moyo kumpenda Mwenyezi Mungu na kumtukuza na kujidhalilisha kwake na kuonyesha unyonge mbele yake na kutii maamrisho yake yeye peke yake hana mshirika wake, kama unavyoujaza moyo hofu ya kumuogopa Mwenyezi Mungu, na kutarajia yaliyoko kwake, ili mtu awe ni katika waja wa Mwenyezi Mungu wachamungu na wenye kufuata njia iliyonyooka.

Nguzo ya pili: Ni kuwaamini Malaika na kuwa wao ni waja wa Mwenyezi Mungu wameumbwa kwa nuru na idadi yao hakuna aijuaye kutokana na wingi wao mbinguni na ardhini isipokuwa Mwenyezi Mungu, wameletwa kwa ajili ya ibada na kumtaja Mwenyezi Mungu na kumtakasa ,"Wanamtakasa usiku na mchana wala hawachoki", "Hawamuasi Mwenyezi Mungu kwa yale aliyowaamrisha na wanafanya yale walioamrishwa" {Surat Tahriim 6} Na kila mmoja wao anakazi yake ambayo Mwenyezi Mungu amemfanyia wepesi, miongoni mwao kuna wenye kuibeba Ar-shi (Napo ni mahali alipotulizana Mwenyezi Mungu),na wengine wamewakilishwa kutoa roho, na wengine huteremka na wahyi kutoka mbinguni naye ni Jibrili -juu yake amani- na ndiye mbora wao, na wengine ni walinzi wa peponi na kuna walinzi wa motoni na wengine wasiokuwa hao katika Malaika wema wanao wapenda waumini wa kibinadamu, na wanazidisha kuwatakia msamaha kwa Mwenyezi Mungu na kuwaaombea dua.

Nguzo ya Tatu; Kuviamini vitabu vilivyoteremshwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Basi Muislamu huamini kuwa Mwenyezi Mungu ameteremsha vitabu kwa amtakaye katika Mitume wake vitabu ambavyo vimekusanya kheri na ukweli na mambo ya uadilifu kutoka kwake Mtukufu, na akateremsha kwa nabii Mussa Taurati na kwa Issa Injili na kwa Daudi Zaburi na kwa Ibrahim Swahifa, na hivi vitabu havizingatiwi uwepo wake kama alivyoviteremsha Mwenyezi Mungu Mtukufu, kama anavyoamini kuwa Mwenyezi Mungu ameiteremsha Qur'ani kwa Mtume wa mwisho wa Mitume naye ni Muhammad -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- na kuwa yeye ameteremsha Aya kwa utaratibu wa kufuatana kwa muda wote wa miaka ishirini na tatu na akazihifadhi Mwenyezi Mungu zisibadilishwe wala kugeuzwa. "Hakika sisi tumeiteremsha Qur’ani kwa Nabii Muhammad, rehema na amani zimshukie, na hakika sisi tunachukua ahadi kuitunza isiongezwe, isipunguzwe wala sehemu yoyote katika hiyo isipotee". [A Hijri: 9].

Nguzo ya Nne : Kuwaamini Mitume.

Na yametangulia maneno kuhusu hao mitume kwa ufafanuzi zaidi na kuwa umma zote zilizotangulia katika Historia nzima hakika aliwatumia mitume na dini yao ni moja, na Mola wao ni mmoja na wanawalingania wanadamu kumpwekesha Mwenyezi Mungu na kumuabudu yeye na wakiwatahadharisha kutokana na ukafiri na ushirikina na maasi. "Na hakuna umma wowote uliopita isipokuwa alipita kwao muonyaji" {Surat Faatir 24} Nao hao Mitume ni wanadamu kama wanadamu wengine aliwachagua Mwenyezi Mungu ili kufikisha ujumbe wake: {Hakika sisi tumekuletea wahyi, ewe Mtume, ili ufikishe ujumbe kama tulivyomletea wahyi Nuhu na Manabii wengine baada yake. Na tumewapelekea wahyi Ibrāhīm, Ismā’īl, Is-ḥāq, Ya‘qūb na Kizazi chake, nao ni Manabii waliokuwa katika makabila kumi na mbili ya wana wa Isrāeli wanaotokana na kizazi cha Ya’qūb, na pia ‘Īsā, Ayyūb, Yūnus, Hārūn na Sulaimān na tukampa Dāwūd Zaburi, nacho ni kitabu na kurasa zilizoandikwa}. Na tumewatuma Mitume ambao tumekuelezea habari zao katika Qur’ani, kabla ya aya hii, na Mitume wengine ambao hatukukuelezea habari zao kwa hekima tuliyoikusudia. Na Mwenyezi Mungu Alisema na Mūsā waziwazi ili kumtukuza kwa sifa hii. Katika aya hii tukufu kuna uthibitisho wa sifa ya Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka, ya kusema kama inavyolingana na utukufu Wake, na kwamba Yeye Mwenyezi Mungu Alisema na Nabii Wake Mūsā, amani imshukie, kikweli bila ya mtu wa kati (baina yao). Nimewatuma wajumbe kwa viumbe wangu wakatoe habari njema ya malipo yangu mema na waonye juu ya adhabu yangu, ili wanadamu wasiwe na hoja watakayoifanya ni kisingizio cha udhuru baada ya kuwatuma Mitume. Na daima Mwenyezi Mungu ni Mshindi katika mamlaka Yake, ni Mwingi wa hekima katika uendeshaji wake wa mambo". {An-nissa 163-165} Muislamu anawaamini hao Mitume wote na anawapenda wote na anawanusuru wote, na wala hawatofautishi kati yao, na mwenye kumkufuru yeyote kati ya hao Mitume au akamtukana na akamuudhi kwa hakika anakuwa amewakufuru wote.

Na mbora wao na mtukufu wao kwa cheo mbele ya Mwenyezi Mungu ni Mwisho wa Manabii ambaye ni Muhammad -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani.

Nguzo ya Tano: Kuamini siku ya mwisho.

Na kuwa Mwenyezi Mungu atawafufua waja kutoka kwenye makaburi yao na atawafufua siku ya kiyama wote ili awahesabu kutokana na matendo yao ya maisha ya hapa duniani. "Na malipizo ya Mwenyezi Mungu ya kuwatesa maadui Wake Siku ya Kiyama yatakuwa kwenye siku ambayo itabadilishwa ardhi hii kwa ardhi nyingine nyeupe iliyotakata kama fedha, na vile vile zitabadilishwa mbingu kwa nyingine, na watatoka viumbe makaburini mwao wakiwa hai wakiwa wamejitokeza kukutana na Mwenyezi Mungu Aliye Mmoja, Mwenye kutenza nguvu, Aliyepwekeka kwa utukufu Wake, majina Yake, sifa Zake na matendo Yake na kulazimisha Kwake kila kitu". {Surat Ibrahiim 48}

"Pindi mbingu zitakapopasuka na ukaharibika mpango wake. Na pindi nyota zitakapoangukiana. Na pindi Mwenyezi Mungu Atakapozifanya bahari kulipuka na maji yake kutoweka. Na pindi makaburi yatakapogeuzwa kwa kufufuliwa waliomo ndani yake. Wakati huo itajua kila nafsi na vitendo vyake vyote ilivyovifanya, vilivyotangulia na vilivyoahirika na italipwa kwa vitendo hivyo". {Suratul infitaar 1-5}

"Kwani haoni mwanadamu anayekanusha kufufuliwa vile umbo lake lilivyoanza akapata kuchukua dalili ya kuwa atarudishwa kuwa hai, kwamba sisi tumemuumba kwa tone la manii lililopitia hatua tofauti mpaka akawa mkubwa, na ghafla anageuka kuwa ni mwingi wa utesi aliyejitolea wazi kwa kujadiliana? Na mkanushaji Kufufuliwa alitupigia mfano usiofaa kupigwa, nao ni kulinganisha uweza wa Muumba na ule wa muumbwa, na akasahau kulianzaje kule kuumbwa kwake. Alisema, «Ni nani mwenye kuhuisha mifupa iliyochakaa na kumumunyuka? Mwambie, «Atakaye ihuisha ni Yule Aliyeiumba mara ya kwanza, na Yeye kwa viumbe vyake vyote ni Mjuzi, hakifichikani Kwake yeye kitu chochote. «Ambaye Amewatolea, kwenye mti wa kijani ulio mbichi, moto unaochoma, ambao kwa mti huo mnawasha moto.» Yeye Ndiye Anayeweza kutoa, kwenye kitu, kinyume chake. Katika hayo pana dalili ya upweke wa Mwenyezi Mungu na ukamilifu wa uweza Wake, na miongoni mwa uweza huo ni kuwatoa wafu kutoka makaburini mwao wakiwa hai. Je, kwani hakuwa yule aliyeumba mbingu na ardhi na vilivyomo ndani yake ni Mwenye uweza wa kuumba mfano wao, Akawarudisha kama Alivyowaanzisha? Ndio, kwa kweli Yeye Analiweza hilo. Na Yeye ni Mwenye sifa kamilifu za uumbaji viumbe vyote , Aliye Mjuzi wa kila Alichokiumba na Atakachokiumba, hakuna kinachofichikana kwake. Hakika amri Yake Anapotaka kitu kiwe ni kukiambia, «Kuwa!» Na kikawa. Na kati ya hizo ni kufisha, kuhuisha, kufufua na kukusanya. Ameepukana Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka na kutakasika, na uelemevu na kuwa na mshirika. Yeye Ndiye Mwenye kumiliki kila kitu, Mwenye kuendesha mambo ya viumbe Vyake bila ya kuwa na mshindani au mpinzani. Na zimejitokeza dalili za uweza Wake na ukamilifu wa neema Zake. Na Kwake Yeye mtarejea ili muhesabiwe na mlipwe." {Surat Yasiin 73-77}

"Na Mwenyezi Mungu Ataiweka Mizani ya uadilifu kwa ajili ya Hesabu katika siku ya Kiyama. Hawatodhulumiwa hawa wala wengine kitu chochote, hata kama ni kitendo, kizuri au kibaya, cha kadiri ya mdudu chungu mdogo, kitazingatiwa katika hesabu ya mwenyewe. Na inatosha kuwa Mwenyezi Mungu ni Mwenye kuyadhibiti matendo ya waja Wake na ni Mwenye kuwalipa kwayo". [Al Anbiyaai: 47].

{Basi anaye tenda chembe ndogo ya wema, atauona! Na anaye tenda chembe ndogo ya uovu atauona!} ((278)). [Azzalzalat: 7-8]. Na hufunguliwa milango ya moto kwa yule anayestahiki ghadhabu za Mwenyezi Mungu na hasira zake na adhabu zake zenye kuumiza, na hufunguliwa milango ya pepo kwa waumini ambao wanatenda yaliyo mema. {Na watawapokea Malaika na kuwaambia hii ndiyo siku yenu ambayo mlikuwa mkiahidiwa} {suratil An-biyaai 103} "Na waongozwe wale waliomkanusha Mwenyezi Mungu na Mitume Wake kuelekezwa upande wa Jahanamu makundi kwa makundi, na watakapoifikia itafunguliwa milango yake saba na wale washika hazina wake waliowakilishwa kuisimamia hiyo Jahanamu. Na hao washika hazina watawakaripia kwa kusema, «Vipi nyinyi mlimuasi Mwenyezi Mungu na mkakataa kuwa Yeye ni Mola wa haki Peke Yake.? Kwani hamkutumiwa Mitume miongoni mwenu wanaowasomea aya za Mola wenu na kuwaonya na misukosuko ya Siku ya Leo?» Watasema wakikubali makosa yao, «Ndio, walitujia na ukweli Mitume wa Mola wetu na wakatuonya na Siku ya Leo, lakini lishathibiti neno la Mwenyezi Mungu kwamba adhabu Yake itawafikia wenye kumkanusha Yeye.» Na wataongozwa wale waliomcha Mola wao, kwa kumpwekesha na kufanya vitendo vya utiifu Kwake, wapelekwe Peponi, makundi kwa makundi. Na watakapoifikia na waombewe kuingia, milango yake itafunguliwa, na Malaika waliowakilishwa kuisimamia Pepo watawakongowea (watawapongeza) na watawaamkia kwa ucheshi na furaha kwa kuwa wamesafishika na athari za maasia na watawaambia, «Amani iwe juu yenu! Mmesalimika na kila baya. Hali zenu ni nzuri. Basi ingieni Peponi mkae milele humo.» Na hapo Waumini watasema, «Shukrani zote ni za Mwenyezi Mungu Aliyetuhakikishia ukweli wa ahadi Yake Aliyotuahidi kupitia kwa ndimi za Mitume Wake, na Akaturithisha ardhi ya Pepo tukawa tunashukia kwenye ardhi hiyo popote pale tunapotaka. Ni mazuri yaliyoje malipo ya watu wema waliojitahidi kumtii Mola wao.» {Surat Zumar 71-75}

Hii ndiyo pepo ambayo ndani yake kuna Neema ambazo jicho halijawahi kuona wala sikio halikuwahi kusikia wala moyo wa mwanadamu haukuwahi kufikiria. "Hakuna nafsi yoyote inayoyajua yale aliyowawekea Mwenyezi Mungu hawa Waumini ya kutuliza macho na kufurahisha moyo, yakiwa ni malipo yao kwa matendo yao mema. Je, Yule Aliyekuwa mtiifu kwa Mwenyezi Mungu na Mtume Wake, mwenye kuamini agizo lake la kuwalipa mema wema wenye kufanya mema na kuwalipa ubaya wenye kufanya mabaya, ni kama yule aliyemkanusha Mwenyezi Mungu na Mitume wake na akaikanusha Siku ya Kiyama? Hawalingani mbele ya Mwenyezi Mungu. Ama wale waliomuamini Mwenyezi Mungu na wakayafanya yale waliyoamrishwa kwayo, basi malipo yao ni mabustani ya Pepo watashukia huko na watakaa kwenye starehe zake wakiandaliwa, yakiwa malipo yao kwa yale waliokuwa wakiyafanya ulimwenguni ya utiifu Kwake. Na ama wale waliotoka nje ya utiifu kwa Mwenyezi Mungu na wakafanya matendo ya kumuasi, basi mahali pao pa kutulia ni moto wa Jahanamu, kila wakitaka kutoka wanarudishwa ndani. Na wataambiwa, kwa kulaumiwa na kukaripiwa, «Onjeni adhabu ya Moto ambayo mlikuwa mkiikanusha ulimwenguni.» {Surat Sajidah 17-20}

"Sifa ya Pepo ambayo Mwenyezi Mungu Amewaahidi wachamungu: ndani yake kuna mito mikubwa ya maji yasiyobadilika, na mito ya maziwa yasiyogeuka utamu wake, na mito ya shizi (pombe) ambayo wanaionea ladha wenye kuinywa, na mito ya asali iliyosafishwa isiyo na taka. Na wachamungu hawa watapata ndani ya hiyo pepo matunda yote ya aina tofauti na mengineyo. Na kubwa kuliko hayo ni kule kusitiriwa na kusamehewa dhambi zao. Basi je, wale watakaokuwa ndani ya Pepo hiyo ni kama wale watakaokaa Motoni bila kutoka humo na wakanyweshwa maji yaliyo moto sana hadi ya mwisho yakawakata tumbo zao?" {Surat Muhammad 15} "Hakika wachamungu watakuwa kwenye mabustani ya Pepo na neema kubwa. Watajistarehesha kwa vile Alivyowapa Mwenyezi Mungu vya neema miongoni mwa aina mbalimbali za ladha na starehe, na Atawaokoa Mwenyezi Mungu kutokana na adhabu ya Moto. Kuleni chakula kwa furaha, na mnywe kinywaji chenye ladha, yakiwa ni malipo ya matendo mema mliyoyafanya duniani Nao watakuwa wameegemea, wako juu ya vitanda vinavyoelekeana, na tutawaoza wanawake weupe wenye macho mapana yaliyo mazuri. (Surat Tuur 17- 20)

Atujaalie Mwenyezi Mungu tuwe ni katika watu wa peponi.

Nguzo ya sita: Kuamini Qadar kheri zake na shari zake.

Na kuwa kila harakati hapa ulimwenguni ni makadirio yaliyoandikwa toka kwa Mwenyezi Mungu aliyetukuka jambo lake "Hampatwi na msiba wowote, enyi watu, kwenye ardhi wala ndani ya nafsi zenu, utokanao na magonjwa, njaa na ndwele (maradhi), isipokuwa umeandikwa kwenye Ubao Uliyohifadhiwa kabla ya kuumbwa viumbe. Hakika hilo, kwa Mwenyezi Mungu, ni jambo sahali (jepesi)". Suratil Hadid 22

"Hakika sisi kila kitu tumekiumba kwa kipimo tulichokikadiria na kukipitisha, na ilitangulia elimu yetu ya kukijua kitu hicho na kukiandika kwenye Ubao Uliohifadhiwa". (Al- qamar 49) "Je, hujui, ewe Mtume, kwamba Mwenyezi Mungu anavijua vilivyomo mbinguni na ardhini ujuzi kamili Aliouthibitisha katika Ubao Uliohifadhiwa? Ujuzi huo ni jambo sahali kwa Mwenyezi Mungu Ambaye hakuna kitu kinachomshinda". Al-hajj 70

Hizi nguzo sita atakaye zikamilisha na akaziamini kiukweli anakuwa ni katika waja wa Mwenyezi Mungu walioamini, na viumbe wote wanatofautiana katika daraja za imani wanazidiana baadhi yao wao kwa wao, na daraja la juu kabisa la imani ni daraja la Ihsan (wema) nalo nikufikia katika nafasi ya "Kumuabudu Mwenyezi Mungu kana kwamba unamuona na kama haumuoni basi yeye anakuona" [3] Na hawa ndiyo viumbe bora watakaofaulu kwa kupata Daraja la juu peponi katika makazi ya Firdausi.

  6- Mafundisho ya Uislamu na Tabia zake

 §  A- Maamrisho.

Hizi ni Baadhi ya Tabia za uislamu na Adabu zake ambazo zinapupia juu ya kuifunza tabia njema jamii ya kiislamu, na tutazitaja kwa ufupi kwa kuzingatia uchambuzi wa tabia hizi, na tabia hizi zinatokana na misingi mikuu ya uislamu, ambayo ni Kitabu cha Mwenyezi Mungu( Qur'ani tukufu) na Hadithi za Bwana Mtume -Rehema za mwenyezi mungu ziwe juu yake na Amani -

 Kwanza: Ukweli katika mazungumzo:

Uislamu unawalazimisha wafuasi wake wenye kujinasibisha kwake kuwa wakweli wakati wa mazungumzo, na unawawekea kuwa ni alama ya kudumu nayo ambayo haifai kwa hali yoyote kuepukana nayo, na unawatahadharisha kwa tahadhari kubwa juu ya uongo, na unawakataza kwa ibara za hali ya juu sana kwa kuwakataza, na kwa sifa iliyowazi ya katazo hilo. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Enyi mliomuamini Mwenyezi Mungu na Mtume Wake na mkaitumia sheria Yake! Fuateni maamrisho ya Mwenyezi Mungu na epukeni makatazo Yake katika kila kitu mnachokitenda na mnachokiacha, na kuweni pamoja na wakweli katika Imani zao na ahadi zao na katika kila jambo miongoni mwa mambo yao. [Surat Taubah 119] Na Amesema Mtume wa Allah rehema na amani za Allah ziwe juu yake: Kutoka kwa Abdillah bin Mas'udi -Radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake- Amesema: Amesema Mtume -Rehema za mwenyezi mungu ziwe juu yake na Amani -: "Shikamaneni na ukweli, kwani ukweli hupelekea katika wema, na hakika wema hupelekea katika pepo, na hatoacha mtu kuwa mkweli na akishughulika na ukweli mpaka ataandikwa kwa Mwenyezi Mungu kuwa ni mkweli, na tahadharini na uongo, kwani uongo unapelekea katika uovu, na hakika uovu hupelekea katika moto, na hatoacha mtu kuendelea kuwa muongo, na akishughulika na uongo mpaka ataandikwa mbele ya Mwenyezi Mungu kuwa ni muongo".

Na uongo si katika sifa za waumini bali ni sifa za wanafiki [4] Amesema Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani-: "Alama za Mnafiki ni tatu: Anapozungumza husema uongo, na anapoahidi huenda kinyume, na akiaminiwa hufanya hiyana".[5]

Hivyo wanasifika maswahaba watukufu na sifa za ukweli mpaka akasema mmoja wao: hatukuwa tukiujua uongo katika zama za Mtume -Rehema za mwenyezi mungu ziwe juu yake na Amani.

 Ya pili: Kutekeleza amana na kutimiza makubaliano na mikataba, na kufanya uadilifu kwa watu.

Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: {Hakika Mwenyezi Mungu anakuamrisheni mzifikishe amana kwa watu wake na pindi mnapo wahukumu watu basi muwahukumu kwa uadilifu} [An Nisaai: 58]. Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: {Na tekelezeni Ahadi Kwa hakika ahadi ni yenye kuulizwa} "Na timizeni kipimo wala msikipunguze mnapowapimia wasiokuwa nyinyi, na mfanye mizani ya sawa, kwani kufanya uadilifu katika upimaji wa vibaba na mizani ni bora kwenu nyinyi ulimwenguni na kuna mwisho mwema mbele ya Mwenyezi Mungu kesho Akhera". [Surat Israa 34-35]

Na akawasifu waumini kwa kauli yake. "Wale wanaotekeleza ahadi ya Mwenyezi Mungu Ambayo Aliwaamrisha kwayo na hawaitengui ahadi ya mkazo ambayo walimuahidi nayo Mwenyezi Mungu". [Ar Ra'di: 20].

 Ya tatu: Unyenyekevu na kutokuwa na Kiburi.

Na kwa hakika alikuwa Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- ni mnyenyekevu mno kuliko watu wengine, akikaa na maswahaba wake anakuwa kama mmoja wao, alikuwa hapendi kusimamiwa na watu anapofika mahala na kwa hakika ilikuwa akijiwa na mtu mwenye Haja humshika mkono na kuondoka naye na hamrudishi mpaka amtimizie haja zake, na kwa hakika aliwaamrisha waislamu kuwa ni wanyenyekevu na akasema: (Hakika Mwenyezi Mungu alinifunulia wahyi kuwa tunyenyekeane mpaka asiweze kujifaharisha mmoja kwa mwingine, wala asimfanyie yeyote uadui mwingine)

 Ya Nne: Ukarimu na utoaji katika njia za kheri.

Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na mali yoyote mnayoitoa, nafuu yake itawarudia nyinyi wenyewe kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Na Waumini hawatoi isipokuwa kwa kutafuta radhi ya Mwenyezi Mungu. Na mali yoyote mnayoitoa, kwa kumtakasia Mwenyezi Mungu, mtapewa kikamilifu thawabu zake na hamtapunguziwa chochote katika hizo. Katika aya hii pana kuthibitisha sifa ya Uso kwa Mwenyezi Mungu Aliyetakata na kila sifa pungufu (waj-hu Allah) kwa namna inayonasibiana na Yeye. [Baqarat 272] Na kwa hakika amewasifu Mwenyezi Mungu Waumini kwa kauli yake: "Na wanalisha chakula, pamoja na kuwa wanakipenda na kukihitajia, kumpa fukara asiyeweza kuchuma, asiyemiliki chochote katika vitu vya kiulimwengu, na kumpa mtu aliyetekwa vitani miongoni mwa washirikina na wengineo", [Al- insaan 8] Ukarimu na moyo mzuri ni sifa za Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- na ni sifa za waumini wenye kumfuata, hakubakii kwake chochote katika mali isipokuwa hukitoa katika njia ya kheri. Amesema Jabir radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu-ni mmoja kati ya maswahaba wa Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- "Hakuwahi kuombwa Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani - kitu chochote akasema hapana". Na amehimiza juu ya kumkirimu mgeni na akasema: "Yeyote mwenye kumuamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho basi asimuudhi jirani yake, Na Yeyote mwenye kumuamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho basi na amkirimu mgeni wake, Na Yeyote mwenye kumuamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho basi na aseme la kheri au anyamaze."

 Ya Tano: Subira na kuvumilia matatizo:

Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: {Na subiri kwa yote yatakayo kupata hakika hayo ni katika mambo yanayostahiki kuazimiwa (na kila mtu) [Luqman 17] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Enyi Mlioamini, takeni msaada kutoka kwa Mwenyezi Mungu katika mambo yenu yote, kwa kusubiri juu ya mikasa na misiba, na kuacha maasia na madhambi na kusubiri juu ya kufanya mambo ya utiifu na yale yanayomkurubisha mtu kwa Mola wake, na kwa Swala ambayo kwayo nafsi inapata utulivu na ambayo inakataza machafu na maovu. Hakika Mwenyezi Mungu Yuko pamoja na wenye kusubiri". [Al-baqara 153] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: {Na hakika tutawalipa wale waliosubiri malipo yao kwa mazuri zaidi kuliko yale waliyokuwa wakiyafanya} [An-nahli 96] Na kwa hakika Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- alikuwa ni miongoni mwa watu wenye subira ya hali ya juu, na pia mvumilivu katika maudhi na alikuwa halipizi ubaya kwa ubaya, watu wake walimuudhi naye akiwalingania kuingia katika uislamu na walimpiga mpaka wakamtoa damu usoni kwake akawa anafuta damu usoni huku akisema: "Ewe Mola wangu wa haki wasamehe watu wangu kwani kwa hakika hawajui walifanyalo" [6]

 Ya Sita: Haya (Aibu):

Muislamu halisi hujizuia na machafu na huwa mwenye haya, na haya ni sehemu katika imani, na haya humsukuma mtu katika kila tabia njema, na inamzuia kuwa na kauli chafu na kufanya machafu yawe maneno au matendo, Na amesema Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani-: "Haya (Aibu) haiji ila kwa kheri"

 Ya Saba: Kuwatendea Wema wazazi wawili:

Kuwatendea wema wazazi wawili na kuamiliana nao vizuri na kujishusha kwa ajili yao ni katika wajibu wa msingi katika dini ya uislamu, na uwajibu huu huzidishiwa mkazo zaidi kila wanavyozidi wazazi wawili kuzeeka na kuwahitaji wazazi wawili, na kwa hakika ameamrisha Mwenyezi Mungu Mtukufu kuwafanyia wema katika Kitabu chake kitukufu na akatilia mkazo utukufu wa haki zao na akasema Mwenyezi Mungu - kutakasika na machafu ni kwake: {Na amehukumu Mola wako yakuwa msimuabudu isipokuwa yeye na wazazi wawili kuwatendea wema, na ikiwa mmoja wao atafikia uzee naye yu pamoja nawe au wote wawili basi usiwaambie hata 'Aah!' wala usiwakemee, na sema nao maneno yaliyokuwa mazuri} Na uwe, kwa mama yako na baba yako, mdhalilifu na mnyenyekevu kwa kuwahurumia, na umuombe Mola wako awarehemu kwa rehema Zake kunjufu wakiwa hai na wakiwa wamekufa, kama walivyovumilia juu ya kukulea ulipokuwa mdogo usiokuwa na uwezo wala nguvu". [Al-israa].

Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na tumemuusia mwanadamu kuwatendea wema wazazi wake wawili na kuwafanyia hisani, Mama yake alimbeba tumboni, shida juu ya shida, na mimba yake na kumaliza kunyonya kwake ni ndani ya kipindi cha miaka miwili, na tukamwambia, «Mshukuru Mwenyezi Mungu kisha uwashukuru wazazi wako, kwangu mimi ndio marejeo nipate kumlipa kila mmoja kwa anachostahili". [Luqman: 14].

Na alimuuliza mtu mmoja Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- (Ni nani ambaye ana haki zaidi ya kuishi naye vizuri) Akasema: ("Mama yako", akasema, kisha nani, akasema: "Mama yako" ,akasema kisha nani, akasema: "Mama yako," akasema: kisha nani? akasema "Baba yako" [7]

Na kwa hivyo basi uislamu unamlazimisha muislamu kuwatii wazazi wake wawili katika kila wanalomuamrisha kulifanya isipokuwa itakapokuwa ni katika kumuasi Mwenyezi Mungu wakati huo hairuhusiwi kumtii kiumbe katika kumuasi Mwenyezi Mungu, Amesema Mwenyezi Mtukufu: {Na ikiwa wazazi wako watakushurutisha kunishirikisha mimi kwa jambo ambalo huna ujuzi nalo basi usiwatii lakini kaa nao hapa duniani kwa wema} [Luqman: 15]. Kama ambavyo ni wajibu kuwafanyia upole na kujishusha kwa ajili yao na kuwakirimu kwa maneno na vitendo na kuwafanyia wema wa kila aina kwa kadiri ya uwezo wake kama kuwalisha na kuwavisha na kuwatibu maradhi yao na kuwakinga na mabaya na kuwaombea dua na kuwatakia msamaha na kutekeleza ahadi zao na kuwakirimu marafiki zao.

 Ya Nane: Kuamiliana kwa Tabia njema na watu wengine:

Amesema Mtume rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani: (Muumini aliyekamilika kiimani zaidi ni yule mwenye tabia njema zaidi kuliko wengine)[8]

Amesema Mtume Rehema za mwenyezi mungu ziwe juu yake na amani: (Hakika miongoni mwa wenye kupendeza zaidi kwangu mimi na watakao kaa karibu yangu zaidi siku ya kiyama ni wale wazuri wenu wa tabia) [9]

Na akamsifia Mtume wake -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- kwa kauli yake: "Na hakika wewe, ewe Mtume, ni mwenye tabia njema". [Al Qalam: 4]. Na Amesema Mtume Rehema za mwenyezi mungu ziwe juu yake na na amani: "Kwa hakika nilitumwa ili kukamilisha tabia njema"[10] Kwa hivyo yapasa kwa muislamu kuwa na tabia njema kwa wazazi wake hali ya kuwafanyia wema kama tulivyokwisha sema, kuwa na tabia nzuri kwa watoto kwa kuwalea malezi mema na kuwafundisha uislamu na kuwaweka mbali na kila linalowadhuru hapa Duniani na akhera, awape matumizi kutoka katika mali yake mpaka watakapofikia umri wa kuweza kujitegemea wenyewe na kuwa na uwezo wa kujitafutia. na vile vile anatakiwa awe na tabia njema kwa mke wake na ndugu zake na dada zake na ndugu zake wa karibu na majirani zake na watu wote, awapendelee ndugu zake kama anavyojipendelea yeye nafsi yake na awe ni mwenyekuunga udugu na majirani zake ,na awaheshimu wakubwa wao na kuwaonea huruma wadogo zao na awatembelee na kuwaliwaza waliopata matatizo kwa kuifanyia kazi kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na wafanyieni Ihsani (wema) wazazi wawili na jamaa na Mayatima na Masikini na Majirani na jirani walio karibu na majirani walio mbali na marafiki walio ubavuni na msafiri aliyeharibikiwa". [An Nisaai: 36]. Na kauli ya Mtume Rehema za mwenyezi mungu ziwe juu yake na amani: (Yeyote mwenye kumuamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho basi na asimuudhi jirani yake)[11]

 Ya Tisa: Kupigana Jihadi Katika Njia ya Mwenyezi Mungu Mtukufu ili kumnusuru aliyedhulumiwa na kuisadikisha haki na kusambaza uadilifu.

Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na piganeni, enyi Waumini, ili kuinusuru dini ya Mwenyezi Mungu, na wale wanaopigana nanyi, wala msifanye yaliyokatazwa ya kukatakata viungo, kufanya hiyana (ya kuchukua kitu katika ngawira kabla ya kugawanywa), kumuua asiyefaa kuuawa miongoni mwa wanawake, watoto, wazee na wanaoingia kwenye hukumu yao. Hakika Mwenyezi Mungu Hawapendi wale wanaokiuka mipaka Yake na kuyahalalisha yalioharamishwa na Mwenyezi Mungu na Mtume Wake". [Al-baqara 190] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na ni lipi linalowazuia, enyi Waumini, kupigana jihadi katika njia ya kuitetea dini ya Mwenyezi Mungu na kuwatetea waja Wake wanaodhalilishwa, miongoni mwa wanaume na wanawake na watoto waliodhulumiwa, na ambao hawana ujanja wala njia ya kufanya isipokuwa ni kumtaka Mola wao Awanusuru wakimuomba kwa kusema, «Mola wetu, tutoe kwenye mji huu (Makkah) ambao watu wake wamejidhulumu nafsi zao kwa kukufuru na wamewadhulumu Waumini kwa kuwakera, na utuletee kutoka Kwako msimamizi wa kusimamia mambo yetu na mtetezi wa kututetea dhidi ya madhalimu»? [An-saai75]

Lengo la jihadi katika uislamu ni kuithibitisha haki, na kueneza uadilifu kwa watu na kuwapiga vita wale wote wenye kuwadhulumu waja na wanawafukuza na kuwazuia kufanya ibada ya Mwenyezi Mungu na pia kuwazuia wasiingie katika uislamu, na Jihadi kwa upande mwingine inakataza fikira za kuwalazimisha watu kwa nguvu kuingia katika dini ya uislamu. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: {Hakuna kulazimishwa katika dini} [Albaqarat 256]

Na wakati wa vita haifai kwa muislamu kumuua mwanamke wala mtoto mdogo wala mzee aliyezeeka bali huuliwa Madhalimu wenye kupigana.

Na yeyote atakaye uliwa katika njia ya Mwenyezi Mungu basi mtu huyo ni shahidi na ana cheo na malipo na thawabu kwa Mwenyezi Mungu, Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Wala usidhani, ewe Mtume, kwamba wale waliouawa katika njia ya Mwenyezi Mungu ni wafu hawahisi chochote. Bali wao wako hai uhai wa barzakh (Akhera) kwenye ujirani wa Mola wao Ambaye walipigana jihadi kwa ajili Yake na wakafa katika njia Yake, inawapitia riziki yao huko Peponi na wananeemeshwa". {Wanafurahia aliyowapa Mwenyezi Mungu kwa fadhila zake na wanawashangilia walioko nyuma yao ya kwamba haitokuwa hofu juu yao wala hawatahuzunika} [Al-Imran: 169،170].

 Ya Kumi: Kuomba Dua Na kumtaja Mwenyezi Mungu na kusoma Qur'ani:

Kila inavyozidi Imani ya Muumini ndivyo unavyozidi mshikamano wake na Mwenyezi Mungu Mtukufu na kumuomba yeye na kunyenyekea mbele yake katika kumkidhia haja zake hapa duniani na kumsamehe madhambi yake na makosa yake na kumuinua daraja siku ya mwisho, na Mwenyezi Mungu ni mkarimu anapenda kuombwa na waombaji. Amesema - kutakata na machafu ni kwake- {Na ikiwa watakuuliza waja wangu kuhusu mimi, basi mimi niko karibu na jibu maombi ya mwenye kuniomba pindi atakaponiomba} [Al Baqarah: 186]. Hivyo Mwenyezi Mungu anajibu dua atakapo kuwa mja ameomba kheri, na humlipa mja thawabu kwa maombi haya.

Na hivyo katika sifa za waumini ni kukithirisha kumtaja Mwenyezi Mungu Mtukufu usiku na mchana kwa siri na kwa wazi basi na amtukuze Mwenyezi Mungu kwa kila aina ya kutukuza na kumtaja kwa mfano kusema: Sub-hanallah, Alhamdulillah, Walaa ilaaha illa llah, Wallahu Ak-baru, na dhikri nyingine katika matamshi ya kumtaja Mwenyezi Mungu Mtukufu, na kwa hakika amezipangia hizo dhikri ujira mkubwa na thawabu nyingi kutoka kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu: Amesema Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- (Wametangulia wapweke, wakasema maswahaba ni kina nani hao wapweke ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu Akasema: "Ni wale wenye kumtaja Mwenyezi Mungu sana wake kwa waume) Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Enyi mliomuamini Mwenyezi Mungu na Mtume Wake na mkafuata sheria Zake kwa vitendo, mtajeni Mwenyezi Mungu kwa nyoyo zenu, ndimi zenu na viungo vyenu utajo mwingi sana". {Na mumtakase asubuhi na jioni} Ahzaab: 41,42 na Amesema- kutakasika na machafu nikwake- {Basi nikumbukeni kwa kunitaja nami nitawakumbuka na mnishukuru mimi na wala msinikufuru} [Al-baqra 152] Na miongoni mwa Dhikri ni kusoma kitabu cha Mwenyezi Mungu - Qurani tukufu- kila anavyozidisha mja kusoma Qur'ani na kuizingatia cheo chake kinazidi kuwa juu kwa Mwenyezi Mungu.

Ataambiwa msomaji wa Qur'an tukufu siku ya kiyama: {Soma na upande kama ulivyokuwa ukisoma ulimwenguni kwa upandishwaji wako daraja utaishia mwisho wa aya ambayo utakayoisoma) [12]

 Ya Kumi na moja: Kujifunza elimu ya kisheria na kuwafundisha watu na kuwalingania kutafuta elimu.

Amesema Mtume Rehema na amani za Allah ziwe juu yake: "Yeyote atakaye fuata njia kwa nia ya kutafuta elimu, Allah humfanyia wepesi mtu huyo njia ya kwenda peponi, na kwa hakika Malaika wanawainamishia mbawa zao kwa kuridhia kwa anachokifanya- kutafuta elimu-[13]

Amesema Mtume Rehema za mwenyezi mungu ziwe juu yake na amani: "Mbora wenu ni yule aliyejifunza Qur'ani na akaifundisha" Amesema Mtume rehema za mwenyezi mungu ziwe juu yake na amani: "Hakika Malaika wanamswalia mwenye kuwafundisha watu kheri" [14] Amesema Mtume rehema za mwenyezi mungu ziwe juu yake na amani: "Mwenye kulingania katika uongofu atapata malipo mfano wa malipo ya mwenye kuufanyia kazi na uongofu na haipunguzi katika ujira wake kitu chochote [15][16]

Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakuna yeyote aliye na kauli nzuri zaidi kuliko yule anayelingania kupwekeshwa Mwenyezi Mungu na kuabudiwa Yeye Peke Yake, na anayesema, «Mimi ni katika Waislamu wanaofuata amri Ya Mwenyezi Mungu na Sheria Yake.» Katika aya hii kuna kusisitiza kulingania kwa Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kueleza utukufu wa wanavyuoni wenye kulingania Kwake kwa ujuzi, kulingana na yale yaliyokuja kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani zimshukie. [Fuswilat 33]

 Ya kumi na mbili: Kuridhia Hukumu ya Mwenyezi Mungu na Mtume wake:

Kutopinga jambo ambalo Mwenyezi Mungu amelifanya kuwa ni sheria, kwani Mwenyezi Mungu -kutakasika na machafu ni kwake- ndiye hakimu wa mahakimu wote, na ni mwenye huruma kuliko yeyote hakifichikani chochote kilichopo mbinguni wala ardhini, wala haziathiriki hukumu zake kwa matamanio ya waja na tamaa za wenye mamlaka , na miongoni mwa rehema zake ni kuwawekea sheria waja wake sheria ambazo zina maslahi kwao duniani na akhera, na kutowalazimisha katika sheria hizo jambo wasiloliweza. Na katika mambo yanayopelekea kumuabudu yeye, ni kuhukumiana katika sheria zake katika kila jambo, hilo liambatane na kuridhia toka moyoni.

Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mwenyezi Mungu Aliyetukuka Anaapa kwa nafsi Yake tukufu, kwamba hawa hawataamini kweli kweli mpaka wakufanye wewe ni hakimu kwenye ugomvi unaotokea baina yao katika uhai wako na watake uamuzi wa Sunnah yako baada ya kufa kwako, kisha wasiingiwe na dhiki katika nafsi zao kwa matokeo ya hukumu yako, na washikamane na wewe, pamoja na hivyo, kwa kukufuata kikamilifu. Kutoa uamuzi kulingana na aliyokuja nayo Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani, kutoka kwenye Qur’ani na Sunnah katika kila jambo katika mambo ya kimaisha, pamoja na kuridhika na kusalimu amri, ni miongoni mwa uthabiti Imani". [An- nisaa: 65] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Je, wanataka Mayahudi hawa uhukumu kati yao kwa yale ya upotevu na ujinga waliyoyazoea washirikina wanaoabudu masanamu? Hayo hayawi wala hayafai kabisa. Na ni nani aliye muadilifu zaidi kuliko Mwenyezi Mungu katika hukumu Yake kwa aliyezifahamu sheria za Mwenyezi Mungu, akamuamini na akawa na yakini kwamba hukumu ya Mwenyezi Mungu ndiyo ya haki?" [Al-maida 50]

 §  B- Mambo yaliyo haramu na yaliyokatazwa.

 Jambo la Kwanza: Shirki; Kuelekeza aina yoyote katika aina za ibada kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu)

Kama mwenye kumsujudia asiyekuwa Mwenyezi Mungu au kumuomba asiyekuwa Mwenyezi Mungu, na kumtaka amkidhie haja zake au achinje kikurubisho kwa ajili ya asiyekuwa Mwenyezi Mungu, sawa sawa awe huyu anayeombwa yuko hai au amekufa au kaburi au sanamu au jiwe au mti au Malaika au walii au mnyama au visivyokuwa hivyo vilivyotajwa, yote hayo ni shirki ambayo Mwenyezi Mungu hamsamehe mja isipokuwa akitubia na akaingia katika uislamu upya.

Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika Mwenyezi Mungu, Hamsamehe aliyemshirikisha Yeye na yeyote miongoni mwa viumbe Wake au akamkufuru kwa aina yoyote ya ukafiri mkubwa. Lakini Anayasamehe na kuyafuta madhambi yaliyo chini ya ushirikina kwa Anayemtaka miongoni mwa waja Wake. Na yeyote anayemshirikisha Mwenyezi Mungu na mwingine, hakika amefanya dhambi kubwa". [Al- nisaa :48] Hivyo Muislamu hamuabudu isipokuwa Mwenyezi Mungu -kutakasika na machafu ni kwake- na wala hamuombi isipokuwa Mwenyezi Mungu na wala hamnyenyekei isipokuwa Mwenyezi Mungu amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: Sema, «Hakika Swala yangu na kuchinja kwangu wanyama, na uzima wangu na kufa kwangu vyote ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu muumba wa walimwengu wote". «Asiye na mshirika katika uungu Wake wala katika umola Wake wala katika majina Yake na sifa Zake. Kumpwekesha huko Mwenyezi Mungu kulikosafishika ndiko Alikoniamrisha mimi Mola wangu, Aliyetukuka na kuwa juu. Na mimi ni wa kwanza kumfuata Mwenyezi Mungu kikamilifu katika umma huu.» [Surat An-aam 162-163]

Na miongoni mwa shirki vilevile: ni kuitakidi kuwa Mwenyezi Mungu ana mke au mtoto -ametukuka Mwenyezi Mungu na kaepukana na hayo kutukuka kukubwa- au kuitakidi kuwa kuna mungu mwingine asiyekuwa Mwenyezi Mungu ambaye anaendesha ulimwengu huu. «Lau mbinguni na ardhini kungekuwa na waungu wasiokuwa Mwenyezi Mungu, kutakata na sifa za upungufu ni Kwake na kutukuka ni Kwake, wenye kuyaendesha mambo yake, ungeliharibika mpango wake. Basi Mwenyezi Mungu, Bwana wa 'Arshi, Ameepukana na sifa za upungufu na Ametakasika na kila sifa ambayo wakanushaji makafiri wanamsifu nayo ya uongo, uzushi na kila aibu". [Al-anbiyau 22]

 Jambo la pili: Uchawi, Ukuhani, na kudai kujua mambo yaliyofichikana:

Uchawi na ukuhani ni Kufuru, na wala mchawi hawezi kuwa mchawi isipokuwa kwa kuwa na mawasiliano na mashetani, na kuwaabudu kinyume na Mwenyezi Mungu, hivyo basi haifai kwa muislamu kwenda kwa mchawi na wala haifai kuwasadikisha katika uongo wao wa kudai kujua mambo yaliyofichikana, na katika mambo ambayo wanayatolea habari katika matukio na habari ambazo wanadai kuwa zitatokea baadaye.

Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sema, ewe Mtume, kuwaambia wao, «Hakuna yeyote ajuwaye, mbinguni wala ardhini, jambo lolote lililofichikana ambalo Mwenyezi Mungu Amejihusisha Mwenyewe kulijua. Na wao hawajui ni lini watafufuliwa kutoka makaburini mwao wakati wa Kiyama kusimama.» [An-namlu 65] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na Yeye, kutakasika na sifa za upungufu ni Kwake, ni mjuzi wa kisichoonekana na macho. Hatakitoa wazi hicho kisichoonekana kwa yeyote miongoni mwa viumbe Wake". Isipokuwa kwa yule Aliyemchagua Mwenyezi Mungu na kumpendelea kwa kumpa utume, kwani Yeye huwajuza baadhi ya yale yaliyofichika yasionekane. Na Anatuma, mbele ya huyo Mtume na nyuma yake, Malaika wenye kumhifadhi na majini, ili wasiisikilize kwa kuiba jambo hilo la ghaibu, kisha wakaambiana kwa siri kisha wakawadokeza makuhani". [Al Jinni: 26-27].

 Jambo la Tatu: Dhulma:

Na Dhulma ni mlango mpana, yanaingia humo matendo mengi mabaya na sifa mbaya ambazo zinamuathiri mtu mmoja mmoja, inaingia ndani yake mtu kujidhulumu yeye mwenyewe nafsi yake na kumdhulumu aliye pembezoni mwake, na kuidhulumu jamii yake, bali na kuwadhulumu maadui wake. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: {Wala kuchukiana na watu kusikupelekeeni kutokuwafanyia uadilifu fanyeni uadilifu huko ndiko kunako mkurubisha mtu na uchamungu} [Al Maaida: 8]. Na kwa hakika ametueleza Mwenyezi Mungu kuwa yeye hawapendi madhalimu. Amesema Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- (Enyi waja wangu hakika mimi nimeharamisha Dhulma katika nafsi yangu na nimeifanya kuwa haramu baina yenu hivyo msidhulumiane) [17]. Amesema Mtume rehema za mwenyezi mungu ziwe juu yake na amani: "Msaidie ndugu yako akiwa amedhulumu au kudhulumiwa", Akasema mtu mmoja: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, unaonaje ikiwa ndugu yangu kadhulumu, vipi nitamsaidia? Akasema: "Unamuhama au unamzuia asifanye Dhulma, kwa kufanya hivyo ndiyo kumnusuru" [18]

 Jambo la Nne: Kuua Nafsi ambayo Mwenyezi Mungu ameharamisha kuiua isipokuwa kwa haki:

Nalo ni kosa kubwa sana katika dini ya uislamu, na Mwenyezi Mungu ameahidi adhabu kali kwa atakaye fanya kosa hilo na akaliwekea adhabu kali duniani nayo ni kuuliwa mwenye kuuwa, isipokuwa atakaposamehe ndugu wa aliyeuliwa. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: {kwa sababu hiyo tuliwafaradhishia wana wa Israeli, yakwamba yeyote atakayeua nafsi bila ya hatia au akafanya ufisadi katika ardhi, atakuwa ni kama amewauwa watu wote, na atakayeihuisha basi atakuwa ni kama amewahuisha watu wote}. [Al Maaidah: 32]. Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na mwenye kumfanyia uadui Muumini akamuua kwa kusudi pasi na haki, mwisho wake atakaoishia ni Jahanamu, hali ya kukaa milele humo, pamoja na kukasirikiwa na Mwenyezi Mungu Aliyetukuka na kufukuzwa kwenye rehema Yake, iwapo Mwenyezi Mungu Atamlipa kwa kosa lake. Na Mwenyezi Mungu Amemuandalia adhabu kali zaidi kwa uhalifu huu mkubwa aliyoufanya. Lakini Mwenyezi Mungu, Aliyetakasika na kila sifa ya upungufu, Atawasamehe na kuwafadhili wenye Imani kwa kutowapa malipo ya kukaa milele ndani ya Jahanamu". [An-nisaa 93]

 Jambo la Tano: Kuwavamia watu katika mali zao:

Sawa iwe kwa wizi au kupokonya au kwa Rushwa au kwa utapeli au kwa njia nyingine zisizokuwa hizo. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na mwizi wa kiume na mwizi wa kike, wakateni, enyi watawala, mikono yao kuambatana na Sheria. Hayo yakiwa ni malipo yao kwa kuchukua kwao mali ya watu pasi na haki, na ni mateso ambayo kwayo Mwenyezi Mungu Anawazuia wengineo kufanya mfano wa kitendo chao. Na Mwenyezi Mungu ni Mshindi katika mamlaka Yake, ni Mwenye hekima katika amri Zake na makatazo Yake". [Al-maaida 38] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: {Na wala msile mali zenu baina yenu kwa Batili} [Al-baqara 188] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Wale wanaozifuja mali za mayatima wakawa wanazichukua pasi na haki, hakika wanakula Moto utakaowaka matumboni mwao Siku ya Kiyama; watauingia Moto ambao watalisikia joto lake". [An Nisaa: 10].

Hivyo uislamu unapiga vita kwa nguvu uadui wa mali za watu wengine, na umetilia mkazo sana jambo hilo, na umempangia mwenye kufanya uadui wa mali za watu adhabu nzito ambayo ni kemeo kwake na watu mfano wake wenye kuvunja nidhamu na amani katika jamii.

 Jambo la sita: Kughushi na kusaliti na kufanya hiyana:

Katika miamala yote kuanzia kuuza na kununua na makubaliano na mambo mengine, nazo ni sifa mbaya ambazo uislamu umezikataza na kuzitahadharisha sifa hizo.

Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Adhabu kali ni ya wale wanaopunja vipimo vya vibaba na mizani". Ambao wakinunua kwa watu cha kupimwa kwa vibaba au kwa mizani hujikamilishia wao wenyewe. Na wakiwauzia watu kinachouzwa kwa vibaba au mizani wanapunguza vipimo. Hivi hawadhanii kuwa wao watafufuliwa? katika Siku kubwa? Siku watakaposimama watu mbele ya Mweyezi Mungu ili Awahesabu kwa machache na mengi waliyoyatenda. [Al Mutwaffifiin: 1-5]. Amesema Mtume rehma na amani za Allah ziwe juu yake: {Yeyote atakaye tufanyia ghushi (udanganyifu) huyo si katika sisi} Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: {Hakika Mwenyezi Mungu hampendi yeyote yule mwenye sifa ya hiyana mwenye madhambi} [An- nisaa 107]

 Jambo la saba: Kuwashambulia watu:

Kuwashambulia katika heshima zao kwa kuwatukana na kuwasengenya na kuwafitinisha na kuwahusudu na kuwadhania vibaya na kuwapeleleza, na kuwadharau, na mengine yasiyokuwa hayo, unachunga sana uislamu kujenga jamii iliyosafi na twahara inayogubikwa na upendo na udugu na uaminifu na kusaidiana, na ndiyo sababu uislamu unapiga vita kwa nguvu maradhi yote ya kijamii ambayo yanapelekea mpasuko katika jamii na kueneza chuki na ugomvi na umimi kati ya watu wake.

Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Enyi mliomuamini Mwenyezi Mungu na Mtume Wake na mkafuata Sheria Zake kwa vitendo, wasitoke wanaume Waumini wakawacheza shere wanaume Waumini wengine, huenda akawa yule anayechezwa shere katika wao ni bora kuliko wale wenye kucheza shere, na wasitoke wanawake Waumini wakawacheza shere wanawake Waumini wengine, kwani huenda yule anayechezwa shere miongoni mwao ni bora kuliko wale wenye kucheza shere. Wala msitiane dosari nyinyi kwa nyinyi, wala msiitane majina ambayo yanachukiwa na wenye kuitwa nayo, kwani ubaya wa sifa na jina ni utokaji nje wa maadili ya Dini, nao ni kucheza shere kwa njia ya dharau, kuaibisha kwa maneno au ishara na kupeana majina mabaya, baada ya kuwa mmeingia kwenye Uislamu na mmeufahamu. Na Asiyetubia na huku kuchezeana shere, kutiana dosari, na kuitana majina mabaya na utokaji nje wa maadili ya Dini, basi hao ndio watu waliozidhulumu nafsi zao kwa kuyatenda mambo haya yaliyokatazwa". "Enyi mliomuamini Mwenyezi Mungu na Mtume Wake na mkafuata Sheria Zake kivitendo, Jiepusheni na dhana mbaya nyingi kwa Waumini, kwani dhana nyingine ni dhambi. Wala msipekue aibu za Waislamu, wala msisemane nyinyi kwa nyinyi maneno yenye kuchukiwa na wenye kusemwa na hali wao hawapo. Je, anapenda mmoja wenu kula nyama ya ndugu yake akiwa amekufa? Nyinyi mnalichukia hilo, basi lichukieni lile la kumsengenya. Na muogopeni Mwenyezi Mungu katika yale Aliyowaamrisha nyinyi na kuwakataza. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa kukubali toba za waja Wake Waumini, ni Mwingi wa rehema kwao". [Al-hujuraat 11-12]

Kama ambavyo uislamu unapiga vita kwa nguvu kubwa kufarakana na matabaka na kujipambanua kitabaka kati ya watu wa jamii moja kwa watu wote, kila mtu kwa mtazamo wa uislamu ni sawa, hakuna ubora kwa mwarabu na asiyekuwa mwarabu wala ubora wa mweupe kwa mweusi isipokuwa ubora unakuwa kwa kile mtu alichokibeba katika moyo wake katika mambo ya dini na uchamungu, watu wote hushindana kwa mipaka iliyosawa katika matendo mema. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Enyi watu! Sisi tumewaumba nyinyi kutokana na baba mmoja, naye ni Ādam, na mama mmoja, naye ni Ḥawā’, hivyo basi hakuna kufadhilishana baina yenu kinasaba, na tumewafanya nyinyi kwa kuzaana kuwa mataifa na makabila mbalimbali ili mjuane nyinyi kwa nyinyi, hakika mtukufu wenu zaidi mbele ya Mwenyezi Mungu ni yule anayemcha Yeye zaidi. Hakika Mwenyezi Mungu Anawajua sana wachamungu na Anawatambua". [Alhujuraat 13[Al Hujrati: 13].

 Jambo la Nane: Kucheza Kamari na kunywa pombe na kutumia madawa ya kulevya:

Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Enyi mlioamini Hakika pombe na kamari na kuabudiwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu na kutazamia kwa mishale ya kupiga ramli ni uchafu na ni katika kazi za shetani basi jiepusheni navyo ili mpate kufaulu } Hakika Shetani anataka, kwa kuwapambia madhambi, kuweka baina yenu chenye kuleta uadui na chuki, kwa sababu ya kunywa pombe na kucheza kamari, na kuwaepusha na kumtaja Mwenyezi Mungu na kuswali, kwa kutokuwa na akili katika unywaji pombe na kujishughulisha na pumbao la uchezaji kamari. Basi komekeni na hayo. [Al Maida: 90-91].

 Jambo la tisa: Ni kula nyamafu, na damu na nyama ya nguruwe:

Na vitu vyote vichafu ambavyo vina madhara kwa mwanadamu, na vilevile vichinjwa vinavyokurubishwa siyo kwa ajili ya Mwenyezi Mungu. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Enyi Waumini, kuleni katika vyakula mnavyovipenda vilivyo halali ambavyo tumewaruzuku, wala msiwe kama makafiri ambao wanaviharamisha vizuri na kuvihalalisha viovu na mumshukurie Mwenyezi Mungu neema Zake kubwa kwenu kwa nyoyo zenu, ndimi zenu na viungo vyenu, iwapo kwa kweli nyinyi mnafuata amri Yake, ni wenye kusikia na kumtii Yeye, mnamuabudu Yeye Peke Yake Asiyekuwa na mshirika". "Hakika Mwenyezi Mungu Amewaharamishia nyinyi kinachowadhuru, kama mfu ambaye hakuchinjwa kwa njia ya kisheria, na damu inayotiririka, na nyama ya nguruwe, na vichinjwa ambavyo vilikusudiwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu. Na katika wema wa Mwenyezi Mungu na usahilishaji Wake kwenu ni kwamba Amewahalalishia nyinyi kuvila vitu hivi vilivyoharamishwa wakati wa dharura. Hivyo basi, yeyote ambaye dharura itampelekea kula kitu katika hivyo, pasi na kuwa ni mwenye kudhulumu katika kula kwake kwa kupitisha kipimo cha haja yake, wala kuikiuka mipaka ya Mwenyezi Mungu katika yale aliyohalalishiwa, basi huyo hana dhambi kwa hilo. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa kusamehe waja Wake, ni Mwenye huruma kwao". [Al-baqara 172-173]

 Jambo la kumi: Kufanya zinaa na Tendo la watu wa Nabii Luti (kuingiliana nyuma):

Uzinifu ni katika kitendo kichafu chenye kuharibu tabia na jamii na husababisha mchanganyiko katika nasaba na kupoteza familia, na kukosa malezi sahihi, na watoto wa zinaa ndiyo wanaohisi uchungu wa uovu na kuichukia jamii. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Wala msikaribie uzinifu na mambo yanayopelekea huko ili msiingie ndani yake, hakika hilo ni tendo baya sana, na njia mbaya zaidi ni njia ya tendo hilo". [Al-israa 32]

Na hiyo zinaa ni sababu ya kuenea magonjwa ya jinsia yenye kuangamiza nguvu kazi ya jamii. Amesema Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- {Hautaenea uchafu kwa watu mpaka kufikia hatua ya kuutangaza uchafu huo, isipokuwa malipo yake yatakuwa ni kuenea maradhi ya milipuko na maradhi mengine ambayo hayakuwepo kwa waliotangulia kabla yao}[19]

Na kwa hivyo basi ameamrisha Mwenyezi Mungu kuziba mianya yote yenye kupelekea kufanya zinaa, basi akawaamrisha waislamu kuinamisha macho yao kwa sababu kutazama haramu ndiyo chanzo cha kupelekea kwenye uzinifu, na akawaamrisha wanawake kujisitiri na kuvaa Hijabu na kujilinda na uzinzi, ili kuilinda jamii kutokana na uchafu wa zinaa, na kwa upande mwingine uislamu ukaamrisha kuoa na kuhimiza kuoa na kupendezesha kuoa bali umeahidi malipo makubwa na thawabu hata kwa kustarehe kwa tendo la ndoa ambalo wanalifanya mume na mke, hayo yote ili kuanzisha familia yenye heshima na yenye kujihifadhi na kutofanya machafu, ili iwe ni kitovu cha malezi yenye mafanikio katika kumlea mtoto wa leo ambaye atakuwa kijana wa kesho.

 Jambo la kumi na moja: Kula Riba :

Riba ni maangamizi ya uchumi na kuchukua fursa ya mwenye kuhitajia mali, sawa sawa awe mfanya biashara katika biashara yake au fakiri mwenye kuhitajia, na riba ni kukopesha mali mpaka ufikie muda fulani kwa kutoa badala yake ziada fulani wakati wa kuilipa ile mali, hivyo basi mkopeshaji anatumia fursa ya kuhitajia mali kwa fakiri, na anabeba mzigo mkubwa wa madeni yaliyolimbikizana zaidi ya alichopewa.

Na mtoa riba anatumia fursa ya uhitaji wa mfanya biashara au viwanda au wakulima au wengine wasiokuwa hao miongoni mwa wenye kuendesha uchumi.

Anatumia fursa ya uhitaji wao wa lazima kuwaelekeza kwenye mtiririko wa pesa, na kuwawekea kiwango cha ziada ya faida katika kile walichokikopa, bila wao (wakopeshaji) kuhusika katika kile kitakachotokea miongoni mwa hatari kama kufilisika au kupata hasara.

Na akipata hasara huyu mfanya biashara hulimbikizana madeni na humtupia deni hilo mtoa riba, wakati ambapo wangekuwa ni wenyekushirikiana katika faida na hasara, huyu angeshiriki kwa juhudi zake na huyu kwa mali zake kama ulivyoamrisha uislamu, lingezunguka gurudumu la uchumi endelevu kwa maslahi ya wote.

Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Enyi mliomuamini Mwenyezi Mungu na mkamfuata Mtume Wake, muogopeni Mwenyezi Mungu na muache kutaka ziada iliyosalia juu ya rasilimali zenu, ambayo mlistahiki kupata kabla riba haijaharamishwa, iwapo imani yenu ni ya dhati kimaneno na kivitendo". Msipokomeka na hilo mlilokatazwa na Mwenyezi Mungu, basi kuweni na yakini ya vita kutoka kwa Mwenyezi Mungu na Mtume Wake, na mkirudi kwa Mola wenu na mkaacha kula riba, ni haki yenu mchukue madeni yenu bila ya nyongeza, msimdhulumu yeyote kwa kuchukua zaidi ya rasilimali zenu wala msidhulumiwe na yeyote kwa kupunguza kiwango cha pesa mlichokopesha". Na iwapo mdaiwa hawezi kulipa, mpeni muhula mpaka Mwenyezi Mungu Atakapomfanyia sahali (wepesi) riziki na kuwarudishia mali yenu. Na mkiacha rasilimali yote au baadhi yake mkamuondolea mdaiwa, hilo ni bora zaidi kwenu, mkiwa mnajua fadhila yake ya kuwa hilo ni bora kwenu katika ulimwengu na Akhera". [Al Baqara: 278-279].

 Jambo la kumi na mbili: uchoyo na ubahili:

Nao ni dalili ya umimi na kujipendelea mwenyewe, na kwa ubahili huu anakuwa ni mwenye kulimbikiza mali na kukataa kuitolea zakah kwa ajili ya kuwapa mafukara na maskini, na anapingana na jamii yake kwa kukataa vyanzo vya kusaidiana na kujenga udugu ambao ameuamrisha Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na Wala wasidhani wale wanaozifanyia ubahili neema za Mwenyezi Mungu Alizowaneemesha kwa kuwafadhili kwamba ubahili huo ni bora kwao. Bali hiyo ni shari kwao. Kwani mali hiyo waliyoikusanya itakuwa ni kitanzi cha moto kitakachowekwa shingoni mwao Siku ya Kiyama. Na Mwenyezi Mungu, Aliyetakasika na kutukuka, Ndiye Mwenye kumiliki ufalme; na Yeye Ndiye Atakayesalia baada ya kutoweka viumbe Wake wote. Yeye Ndiye Mtambuzi wa matendo yenu yote, na Atamlipa kila mtu kwa kadiri anavyostahiki. [Al-Imran: 180].

 Jambo la kumi na tatu: Uongo na kutoa ushahidi wa uongo:

Na kwa hakika tulitanguliza kauli ya Mtume Rehema za Allah ziwe juu yake na amani "Na Tahadharini sana na uongo! kwani uongo unapelekea katika uovu, na hakika uovu unampelekea mtu kuingia Motoni, na hatoacha mtu kuendelea kusema uongo, na kuutafuta uongo mpaka ataandikwa mbele ya Mwenyezi Mungu kuwa ni muongo".

Na miongoni mwa uongo wenye kuchukiza ni ule ambao unakuwa wakati wa kutoa ushuhuda wa uongo, na kwa hakika alitilia mkazo Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani - katika kuwaweka mbali watu na kushuhudia uongo na akatahadharisha kwakuwa mwisho wake ni mbaya, na akainua sauti yake kwa kuwaambia maswahaba zake: "Hivi nisikufahamisheni dhambi kubwa zaidi, ni kumshirikisha Mwenyezi Mungu, na kutowatendea wema wazazi wawili", na alikuwa ameegemea akakaa na akasema: "Eleweni vyema pia na kuzungumza uongo, eleweni vyema pia na kutoa ushuhuda wa uongo". [20] Na hakuacha kurudiarudia kwa kutahadharisha umma usijekuangukia katika kusema na kushuhudia uongo.

 Jambo la kumi na Nne: Kiburi na kudanganyika, kujisikia na majivuno:

Kiburi na kudanganyika na majivuno, ni sifa mbaya na dharau zenye kuchukiwa katika dini ya uislamu, na kwa hakika ametuhabarisha Mwenyezi Mungu Mtukufu kuwa yeye hawapendi wenye viburi, na akasema kuhusu wao huko akhera. {Hivi haikuwa jahanamu ndiyo mafikio ya wenye kufanya kiburi} [Azzumar 60] Basi mwenye kiburi mwenye kujidanganya mwenyewe anachukiwa na Mwenyezi Mungu kutokana na tabia zake.

 §  C- Kutubia kutokana na kufanya yaliyoharamishwa:

Haya madhambi makubwa na yaliyoharamishwa ambayo tumeyataja, ni wajibu kwa kila muislamu ajiepushe nayo na kuchukua tahadhari kubwa ya kudumbukia humo, kwani kila tendo analolifanya mwanadamu atalipwa kwa kitendo hicho siku ya kiyama, ikiwa ni kheri atalipwa kheri na ikiwa ni shari atalipwa kwa shari yake.

Na akitumbukia muislamu katika chochote katika mambo ya haramu, basi anafanya haraka moja kwa moja kutubia kutokana na makosa hayo, na kukimbilia kwa Mwenyezi Mungu na kutaka msamaha kwake, na ni wajibu juu yake kujiondoa katika dhambi hizo ambazo ametumbukia humo, na ajute kwa yale aliyoyafanya na aazimie kuwa hatorudia makosa hayo, na ikiwa imetokea kumdhulumu yeyote basi na arudishe alichodhulumu au atake kusuluhishana, wakati huo itakuwa ni toba ya kweli na Mwenyezi Mungu atamsamehe na wala hatomuadhibu kwa kosa ambalo ametubia, na mwenye kutubia kutokana na dhambi anakuwa kama ambaye hakufanya dhambi.

Na ni wajibu juu yake amtake Mwenyezi Mungu msamaha sana, bali ni wajibu kwa kila Muislamu azidishe kuomba msamaha kwa yale yanayomuhusu katika makosa madogo au makubwa. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Ni kawaambia watu wangu, ‘Muombeni Mola wenu msamaha wa dhambi zenu na tubieni Kwake kutokana na ukafiri wenu, hakika Yeye ni Mwingi wa kusamehe kwa anayetubia miongoni mwa waja Wake na akarudi Kwake.’» [Nuuh 10] Na wingi wa kuomba msamaha na kukimbilia kwa Mwenyezi Mungu ni sifa ya waumini wanyenyekevu. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sema, ewe Mtume, kuwaambia waja wangu waliojidhulumu nafsi zao kwa kuyajia madhambi ambayo nafsi zao zinawaitia, «Msikate tamaa na rehema ya Mwenyezi Mungu, kwa wingi wa madhambi yenu, kwani Mwenyezi Mungu Anasamehe dhambi zote kwa mwenye kutubia kutokana nayo na akayaacha namna yatakavyokuwa. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa kusamehe madhambi ya wenye kutubia miongoni mwa waja Wake, ni Mwenye kuwarehemu". «Na rudini kwa Mola wenu, enyi watu, kwa kutii na kutubia, na mnyenyekeeni yeye kabla hayajawashukia mateso Yake, kisha hakuna yeyote Atakayewanusuru badala ya Mwenyezi Mungu". [Azzumar 53,54]

 §  D- Waislamu kutilia umuhimu misingi sahihi ya kuchukua dini hii:

ilivyo kuwa maneno na matendo na kukiri kwake Mtume wa Mwenyezi Mungu -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- kumejengwa kwa maneno ya Mwenyezi Mungu Mtukufu, maneno yenye kuchambua amri zake na makatazo yake katika dini ya uislamu, Waislamu wameyatilia umuhimu mkubwa maneno hayo kutokana na usahihi ulionukuliwa kupitia hadithi zilizopokelewa kutoka kwa Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- na wakatoa jitihada kubwa katika kuzisafisha nukuu kutokana na ziada ambayo si katika maneno ya Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani-, na katika kubainisha kauli alizosingiziwa Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- wameweka kwa ajili hiyo kanuni madhubuti ambayo inapaswa kuchungwa katika kunakili hadithi hizi kutoka katika zama moja kwenda zama nyingine.

Na tutazungumzia kwa ufupi sana kuhusu (Elimu ya Hadithi) ili jambo hilo liwe wazi kwa msomaji, jambo hilo ambalo limeutofautisha umma wa kiislamu na mila na dini zingine, kwa kuufanyia wepesi umma wa kiislamu katika kuihifadhi dini yake na kuwa safi isiyochanganyika na uongo na uzushi katika zama zote zilizopita.

Kwa hakika dini ya uislamu imetegemea katika kunukuu maneno ya Mwenyezi Mungu Mtukufu na ya Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- Juu ya mambo mawili makubwa:

1- Kuhifadhi moyoni, na kuandika katika kurasa, na waislamu wa mwanzo ni katika umma huu walikuwa na uwezo mkubwa kuliko umma nyingi zilizopita katika kuhifadhi na kuelewa kiundani na kwa upana kwa kule kusifika kwao na sifa ya akili safi na kumbukumbu yenye nguvu, na hili linajulikana na liko wazi kwa mwenye kuisoma historia yao na wakajua habari zao, na kwa hakika alikuwa swahaba anasikia hadithi kutoka katika kinywa cha Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- na anayahifadhi vizuri na kuyanukuu kwa wakati wake, na baada yake Taabiy (mwanafunzi wa swahaba) ambaye anaihifadhi hadithi hiyo, kisha anaifikisha kwa yule aliye baada yake, na hivyo ndivyo inaendelea cheni ya hadithi mpaka kufikia kwa mmoja kati ya wasomi wa hadithi ambaye huziandika hadithi hizi na kuzihifadhi moyoni na kuzikusanya katika kitabu na kuwasomea wanafunzi wake kitabu hiki nao wanazihifadhi hizi hadithi na kuziandika kisha nao wanawasomea wanafunzi wao, na kwa mpangilio huu wakafuata na mpaka vinafika vitabu hivi katika mataifa yote wanavipata kwa njia hii na utaratibu huu.

Na kwa namna hii haikubaliki hata kidogo hadithi kutoka kwa Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- pasina kujua cheni ya wapokezi ambao imenukuliwa hadithi hii toka kwao kuja kwetu.

Na huendana na jambo hili vilevile elimu nyingine ambayo inautofautisha umma wa kiislamu na umma zingine, nayo ni elimu ya wapokezi au elimu ya Jar-hi na Taadiil.

Nayo ni elimu inayotilia umuhimu wa kujua hali za hawa wapokezi ambao wananukuu hadithi za bwana Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani - hivyo hutilia umuhimu historia yao wenyewe, kwa kujua tarehe ya kuzaliwa kwao na kufa kwao, kujua mashekhe (walimu) wao na wanafunzi wao na kuthibitishwa na wasomi wa sasa, na kujua upeo wa udhibiti wao kuwa na hifdhi nzuri, na yanayowazunguka miongoni mwa uaminifu na ukweli wa mazungumzo, na yasiyokuwa hayo katika mambo ambayo ni muhimu kwa mwanachuoni wa Hadithi ili ahakiki ukweli wa hadithi iliyopokelewa kutoka katika mlolongo wa wapokezi.

kwa hakika hiyo ni elimu ya kipekee katika umma huu kwa kuipupia juu ya usahihi wa maneno yaliyo egemezwa kwa Mtume wa umma huu, na wala haipatikani katika Historia nzima kuanzia mwanzo mpaka leo juhudi kama hii kubwa ya kutilia umuhimu maneno ya mtu yeyote kama yalivyotiliwa umuhimu maneno ya Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani -.

Hakika hiyo ni elimu kubwa iliyonukuliwa katika vitabu vilivyotilia umuhimu uliotimia katika kupokea hadithi, na imetaja historia binafsi kwa mchanganuo kwa maelfu ya wapokezi, siyo kwa ajili ya chochote isipokuwa ni kwa sababu wao walikuwa ni kiunganishi katika kuhamisha hadihi za Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani - kuzipeleka kwenye zama zinazofuata, na katika elimu hii hapakuwa na kupakana mafuta kwa mgongo wa chupa kwa mtu yeyote, bali elimu hiyo ilikuwa kama mizani kina cha ukosoaji, muongo huambiwa kuwa ni muongo, na mkweli huitwa mkweli na mwenye hifdhi mbaya huambiwa na mwenye hifdhi imara huambiwa vilevile, kwa hivyo, na wakaiwekea elimu hiyo ya Jarhi wa Taadiil misingi kabambe ambayo wanaijua watu wa fani hii.

Na wala haiwi hadithi sahihi kwao isipokuwa itakapoungana cheni ya wapokezi walioipokea wao kwa wao, na ukatimia uadilifu wa hawa wapokezi na ukweli wa maneno pamoja na nguvu ya hifdhi na udhibiti.

 Jambo jingine katika elimu ya hadithi.

Ni katika ongezeko la mlolongo wa cheni wa hadithi moja, pale ambapo inafikia hadithi iliyopokelewa kutoka kwa Mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani- kuwa na njia nyingi na milolongo ya wapokezi, hivyo basi inakuwa hadithi moja ina cheni mbili au tatu au Nne na wakati mwingine inakuwa na cheni kumi na wakati mwingine zaidi ya hapo.

Na kila unavyo ongezeka mlolongo wa cheni ya mapokezi ya hadithi ndivyo inavyokuwa hadithi ina nguvu zaidi, na kuzidi kuwa madhubuti katika tabaka zake zote na ikiwa hivyo huitwa Hadithi Mutawaatir (Mfululizo) nayo ni aina ya juu zaidi ya nukuu kwa waislamu, na kila ambavyo jambo linakuwa muhimu zaidi katika dini ya uislamu kama kuweka wazi nguzo za uislamu basi huwa Hadithi mutawaari zinakuwa nyingi katika kuelezea jambo hilo, na huongezeka cheni zake za upokeaji, na kila inapokuwa jambo ni la matawi na mambo yenye kupendeza zinakuwa chache cheni za mapokezi yake na utiliwaji muhimu wake unakuwa ni hafifu.

Na Daraja la juu zaidi ambalo waislamu walilipa kipaumbele katika usahihi wa kunukuu ni kunukuu Qur'ani Tukufu pale ambapo ilipata kutiliwa umuhimu wa hali ya juu kwa kuandikwa katika makaratasi na kuhifadhiwa vifuani, na kuyaboresha matamshi yake na matokeo ya herufi zake na njia za usomaji wake, na kwa hakika waislamu waliinukuu kwa mlomlongo wa maelfu ya mapokezi kupitia vizazi na vizazi, hivyo haikuwezekana kuingiliwa na mkono wa upotoshaji na ubadilishaji kwa miaka yote iliyopita, na msahafu ambao unasomwa Magharibi ndiyo msahafu unaosomwa mashariki. Ndiyo msahafu uliopo katika sehemu mbalimbali za ardhi, kwa kusadikisha maneno ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika sisi tumeiteremsha Qur’ani na hakika sisi tunachukua ahadi kuihifadhi". [Al Hijri: 9].

 §  E- Na baada ya hayo:

Basi hii ndiyo Dini ya uislamu ambayo inatangaza kumpwekesha Mwenyezi Mungu kwa Uungu, Nembo yake ni (Laa ilaaha illa llahu), hii ndiyo dini ya uislamu Ambayo ameridhia Mwenyezi Mungu kwa waja wake kuwa ndiyo dini sahihi na ya kweli.

"Leo hii nimekukamilishieni Dini yenu na nimekutimizieni neema zangu, na nimekuridhieni kuwa Uislamu ndiyo Dini yenu". [Al Maida: 3]

Hii ndiyo dini ya uislamu, dini Ambayo hamkubalii Mwenyezi Mungu mtu yeyote atakayefuata dini isiyokuwa ya uislamu. "Na Mwenye kutafuta dini isiyokuwa dini ya Kiislamu, ambayo ni kujisalimisha kwa Mwenyezi Mungu kwa kumpwekesha na kumfuata kwa kumtii na kumdhalilikia, na kwa Mtume wake aliye Nabii wa mwisho Muhammad, rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani, kwa kumuamini na kumfuata na kumpenda kwa dhahiri na kwa siri, basi hiyo haitakubaliwa kwake, na yeye Akhera atakuwa ni miongoni mwa wenye kupata hasara ambao walizifanyia ubahili nafsi zao kwa kuzinyima mambo yenye kuzinufaisha". [Al-Imran: 85].

Hii ndiyo dini ya uislamu ambayo atakayeamini dini hii na akafanya mema anakuwa ni katika waliofaulu kuingia katika pepo yenye neema. "Hakika wale walioniamini, wakawakubali Mitume wangu na wakafanya mema watapata Pepo ya juu kabisa, ya kati na kati na yenye mashukio bora kabisa". Hali ya kukaa milele humo, hawatotaka kuepukana nayo kwa kuwa na hamu nayo na kuipenda. [Al -kahaf 107,108]

Hii ndiyo dini ya uislamu haina ukiritimba na kundi lolote la watu, na siyo maalumu kwa jinsia fulani ya watu, bali atakaye amini na kuwaita watu katika uislamu basi mtu huyo anakuwa katika watu bora katika uislamu, na anakuwa yeye ni mwema kwa Mwenyezi Mungu. "Hakika mbora wenu kwa Mwenyezi Mungu ni mchamungu zaidi". [Al Hujrati: 13].

Na ni wajibu juu yetu kumkumbusha msomaji kuhusu mambo muhimu ambayo vizuizi kwa watu kati yao na kuingia katika dini na vinawazuia kuingia katika dini hii:

Jambo la kwanza: Kutokuijua Dini ya Uislamu kiitikadi na kisheria na kiadabu,- Na kwa kawaida watu huwa ni maadui kwa lile wasilolijua- kwa mwenye kutilia umuhimu wa kuijua dini ya uislamu asome kisha na asome tena kisha asome tena, mpaka aijue dini hii kutoka katika vyanzo vyake vya asili, na kuwe kusoma kwake ni kwa moyo mmoja wa uadilifu akitafuta haki bila kuegemea upande wowote.

Jambo la pili: Ubaguzi wa dini mazoea na utamaduni ambayo mtu amekulia humo bila kufikiria kwa kina na kutazama usahihi wa dini ambayo amekulia, na unaendelea ubaguzi wa kitaifa mpaka kufikia hatua ya kukataa kila dini isiyokuwa ya baba zake na babu zake, na ubaguzi huyafumba macho na kuyaziba masikio na huzifunga akili, basi mtu anakuwa hawezi kufikiria kwa uhuru upande wowote na wala kutofautisha kati ya giza na mwangaza.

Jambo la Tatu: Matamanio ya nafsi na mahitajio yake na kutamani kwake, haya huzitawala fikira na maamuzi pia, na huzipeleka kule yatakapo, na humuangamiza mtu -pale anapoyaendekeza- bila yeye kujua, na humzuia kwa nguvu zote kuikubali haki na kuifuata.

Jambo la Nne: kuwa na baadhi ya makosa na kukengeuka kwa baadhi ya waislamu na kuuegemeza uongo na uzushi katika uislamu, na uislamu uko mbali na hayo, na wakumbuke watu wote kuwa dini ya Mwenyezi Mungu haihusishwi na makosa ya watu.

Na kwa hakika njia rahisi ya kuujua ukweli na uongofu, ni mtu kuelekeza moyo wake kwa Mwenyezi Mungu kwa unyenyekevu, akimuomba amuongoze katika njia iliyonyooka na dini iliyo simama sawa ambayo anaipenda Mwenyezi Mungu na kuiridhia na kupata mja maisha mazuri na furaha ya kudumu ambayo hatopata tabu baada hapo, na ajue kuwa Mwenyezi Mungu hujibu dua ya muombaji anapomuomba. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na watakapo kuuliza, ewe Nabii, waja Wangu kuhusu Mimi, «Mimi Niko karibu nao, Nasikia maombi ya muombaji yeyote anaponiomba. Basi, ni wanitii Mimi katika Niliyowaamrisha nayo na Niliyowakataza nayo na waniamini Mimi, wapate kuongokewa kwenye maslahi yao ya dini yao na dunia yao. Katika aya hii pana utoaji habari kutoka Kwa Mwenyezi Mungu, Aliyetakasika na kila sifa ya upungufu, kuhusu ukaribu Wake kwa waja Wake, ukaribu unaolingana na utukufu Wake. [Al Baqarah: 186].

Kimetimia kwa sifa njema za Mwenyezi Mungu.



[1] Ameitoa hadithi hii Imamu Bukhariy (4/230)

[2] Hadithi hii ameitoa Imamu Bukhariy na Muslimu(2/164) Kitabu cha Hijja ,mlango wa ubora wa hijaa iliyotimia.

[3] ametoa hadithi hii Al-bukhaariy4777

[4] Mnafiki ni yule mtu ambaye anajidhihirisha kuwa ni muislamu lakini kiuhalisia itikadi yake moyoni haiamini dini ya uislamu.

[5] Hadithi amaeitoa Bukhariy katika kitabu cha Imani ,Mlango wa alama za wanafiki(1/15)

[6] Hadithi ameitoa Bukhariy katika kitabu cha wenye kuritadi mlango(5) (9/20)

[7] Hadithi hii ameitoa Bukhariy katika Kitabu cha adabu mlango wa nani mwenye haki zaidi wakuamiliana nae vizuri(8/2)

[8] Hadithi ameitoa Abuu Daudi katika kitabu cha Sunnah mlango wa kuzidi imani na kupungua(5/6),na Tirmidhiy katika kitabu cha unyonyeshaji mlango ulikujakuelezea haki za mwanamke kwa mume wake (3/457)na kasema Tirmidhiy: hadithi hii ni nzuri na sahihi amesema albaniy: angalia sahihi ya Abii Daudi(3/886)

[9] {15} Hadithi ameitoa Bukhariy: Kitabul manaaqib ,mlango,wa sifa za mtume -Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani(4/230) kwa tamko (Hakika katika wabora wenu ni wale wazuri wenu wa tabia)

[10] Hadithi ameitoa Imamu Ahmad katika (17/80) na amesema Ahmad Shaakir kuwa isnad yake ni sahihi,na ameitoa Bukhariy fil adabu ,na Baihaqiy katika mlango wa imani na Haakim katika Mustadrak.

[11] Hadithi ameitoa Bukhariy katika mlango wa Adabu,mlango wa mwenye kumuamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho basi na asimuudhi jirani (8/13).

[12] Ameitoa Abuu Daud (1464) na tamko ni lake,na Tirmidhiiy (2914).An-nasai katika (sunanul kubraa)( 8056) na Ahmad(6799 )

[13] hadithi ameitoa Tirmidhiy Mlango wa elimu mlango wa fadhila za ibada(4/153),na Abuu Daud: kitabu cha elimu mlango wa kuhimiza juu ya kutafuta elimu(45857),na ibnu maajah katika muqaddimat (1/81)na ameisahihisha Albaniy(swahihul jaamiy(5/302)

[14] Hadithi ameitoa Bukhariy katika kitabu cha fadhila ,Mlango wa mbora wenu ni yule mwenye kujifunza Qur'an na akifundisha (6/236)

[15] hadithi ameitoa Tirmidhiy katika kitabu cha elimu,mlango wa uliokuja kuzungumzia fadhila ufahamu wa ibada(5/50kwa matamshi marefu.)

[16] Ameitoa muslim katika kitabu cha elimu mlango mwenye kufufua sunnah nzuri au mbaya(227/16)

[17] ameitoa muslim: Kitabu cha wema na kuunga udugu,mlango wa kuharamisha Dhulma(16/132)

[18] Ameitoa Bukhariy katika kitabu cha Dhulma na hasira ,mlango unaohusu kumnusuru ndugu yako dhalimu au mdhulumiwa: (3/168)

[19] Hadithi ameitoa ibnu majjah :kitabu cha fitina mlango wa makosa (2/1333)na amesema Al-baniy kuhusu hadithi hiyo kuwa ni hasan(swahhi ibnu majjah(2/370)

[20] hadithi ameitoa bukhari kitabu cha ushuhuda ,mlango wa uliosemwa katika kushuhudia uongo(3/225)