(1) Ha Mim
(2) Uteremsho huu umetoka kwa Mwingi wa rehema, Mwingi wa kurehemu.
(3) Hiki ni Kitabu kilichopambanuliwa Aya zake, cha kusomwa kwa Kiarabu kwa watu wanaojua.
(4) Kitoacho habari njema, na chenye kuonya. Lakini wengi katika wao wamepuuza; kwa hivyo hawasikii.
(5) Na wakasema: Nyoyo zetu zimo katika vifuniko kwa hayo unayotuitia, na masikio yetu yana uziwi, na baina yetu na wewe lipo pazia. Basi wewe tenda, nasi hakika tunatenda.
(6) Sema: Hakika mimi ni mtu kama nyinyi; inafunuliwa kwangu ya kwamba Mungu wenu ni Mungu Mmoja tu. Basi nyookeni sawa kumwendea Yeye, na mumtake msamaha, na ole wao wanaomshirikisha.
(7) Ambao hawatoi Zaka na wanaikataa Akhera.
(8) Hakika wale walioamini na wakatenda mema, watakuwa na ujira usio na ukomo.
(9) Sema: Hivyo nyinyi mnamkataa yule aliyeumba ardhi katika siku mbili, na mnamfanyia washirika? Huyu ndiye Mola Mlezi wa walimwengu wote.
(10) Na akaweka humo milima juu yake, na akabarikia humo na akakadiria humo chakula chake katika siku nne. Haya ni sawa kabisa kwa wanaouliza.
(11) Kisha akazielekea mbingu, na zilikuwa moshi, akaziambia hizo na ardhi: Njooni, kwa hiari au kwa nguvu! Vyote viwili vikasema: Tumekuja nasi ni watiifu.
(12) Basi akazifanya mbingu saba kwa siku mbili, na akazipangia kila mbingu mambo yake. Na tukaipamba mbingu ya chini kwa mataa na kwa ulinzi. Hiki ndicho kipimo cha Mwenye Nguvu, ajuaye zaidi.
(13) Basi wakipuuza wewe sema: Nakuhadharisheni adhabu mfano wa adhabu ya 'Adi na Thamudi.
(14) Walipowajia Mitume mbele yao na nyuma yao wakawaambia: Msimuabudu ila Mwenyezi Mungu! Wakasema: Angelitaka Mola wetu Mlezi, bila ya shaka angeliwateremsha Malaika. Basi sisi hakika tunayakataa hayo mliyotumwa nayo.
(15) Ama kina 'Adi, hao walijivuna katika nchi bila ya haki, na wakasema: Ni nani mwenye nguvu kushinda sisi? Kwani wao hawakuona kwamba Mwenyezi Mungu aliyewaumba ni Mwenye nguvu kushinda wao? Na wao wakawa wanazikataa Ishara zetu!
(16) Basi tukawatumia upepo wa kimbunga katika siku za misiba, ili tuwaonjeshe adhabu ya kuwahizi katika uhai wa duniani, na bila ya shaka adhabu ya Akhera ina hizaya zaidi, na wala wao hawatanusuriwa.
(17) Na ama Thamudi, hao tuliwaongoza, lakini walipenda upofu kuliko uwongofu. Basi ukawachukua moto wa adhabu ya kuwafedhehesha kwa sababu ya yale waliyokuwa wakiyachuma.
(18) Na tukawaokoa wale walioamini na wakawa wanamcha Mungu.
(19) Na siku watakapokusanywa maadui wa Mwenyezi Mungu kwenye Moto, nao wakigawanywa kwa makundi.
(20) Hata watakapoufikia Moto, yatawashuhudia masikio yao, na macho yao na ngozi zao kwa yale waliyokuwa wakiyatenda.
(21) Na wao wataziambia ngozi zao: Kwa nini mmetushuhudilia? Nazo zitasema: Ametutamkisha Mwenyezi Mungu ambaye alitamkisha kila kitu! Na Yeye ndiye aliyewaumba mara ya kwanza, na kwake Yeye tu mtarejeshwa.
(22) Na hamkuwa wenye kujificha hata masikio yenu, na macho yenu, na ngozi zenu, zisikushuhudilieni. Lakini mlidhani kwamba Mwenyezi Mungu hayajui mengi katika yale mliyokuwa mkiyatenda.
(23) Basi hiyo dhana yenu mliyokuwa mkimdhania Mola wenu Mlezi, imekuangamizeni; na mmekuwa miongoni mwa waliohasiri.
(24) Basi wakisubiri, Moto ndio maskani yao. Na wakiomba radhi, hawakubaliwi.
(25) Na tukawawekea marafiki, na wakawapambia yaliyo mbele yao na nyuma yao. Basi ikawathibitikia kauli wawe pamoja na mataifa yaliyopita kabla yao, miongoni mwa majini na watu. Hakika hao wamekuwa ni wenye kuhasirika.
(26) Na wale waliokufuru walisema: Msiisikilize Qur-ani hii, na timueni zogo ndani yake, huenda mkashinda.
(27) Basi hapana shaka tutawaonjesha hao waliokufuru adhabu kali, na hapana shaka tutawalipa malipo mabaya zaidi kwa yale waliyokuwa wakiyafanya.
(28) Hayo ndiyo malipo ya Maadui wa Mwenyezi Mungu - Moto! Humo watakuwa na maskani ya kudumu, ndiyo malipo yao kwa sababu walikuwa wakizikataa Ishara zetu.
(29) Na wale waliokufuru watasema: Mola wetu Mlezi! Tuonyeshe wale waliotupoteza miongoni mwa majini na watu ili tuwaweke chini ya miguu yetu, wapate kuwa miongoni wa walio chini kabisa.
(30) Hakika wale waliosema: Mola wetu Mlezi ni Mwenyezi Mungu! Kisha wakanyooka sawa, hao huwateremkia Malaika wakawaambia: Msiogope, wala msihuzunike; nanyi furahini kwa Pepo mliyokuwa mkiahidiwa.
(31) Sisi ni vipenzi vyenu katika maisha ya dunia na katika Akhera, na humo mtapata kinachotamaniwa na nafsi zenu, na humo mtapata mtakavyovitaka.
(32) Ni takrima itokayo kwa Mwenye kusamehe, Mwingi wa kurehemu.
(33) Na ni nani mbora zaidi wa kusema kuliko aitaye kwa Mwenyezi Mungu na akatenda mema, na akasema: Hakika mimi ni katika Waislamu?
(34) Mema na maovu hayalingani. Pinga uovu kwa lililo jema zaidi. Hapo yule ambaye baina yako naye pana uadui atakuwa kama rafiki jamaa wa kukuonea uchungu.
(35) Lakini hawapewi wema huu ila wanaosubiri, wala hawapewi ila wenye bahati kubwa.
(36) Na Shetani akikuchochea kwa uchochezi, wewe jikinge kwa Mwenyezi Mungu. Hakika Yeye ni Mwenye kusikia, ajuaye zaidi.
(37) Na katika Ishara zake ni usiku na mchana, na jua na mwezi. Basi msilisujudie jua wala mwezi, bali msujudieni Mwenyezi Mungu aliyeviumba, ikiwa nyinyi mnamuabudu Yeye tu.
(38) Na ikiwa watajivuna, basi hao walioko kwa Mola wako Mlezi wanamtakasa Yeye usiku na mchana, na wao hawachoki.
(39) Na katika Ishara zake ni kwamba unaiona ardhi nyonge, lakini tunapoiteremshia maji, mara unaiona inataharaki na kuumuka. Bila ya shaka yule aliyeihuisha ardhi ndiye atakayehuisha wafu. Hakika Yeye ni Muweza mno wa kila kitu.
(40) Hakika wale wanaopindukia mipaka katika Ishara zetu, hawafichikani kwetu. Je, atakayetupwa Motoni ni bora au atakayekuja kwa amani Siku ya Kiyama? Tendeni mpendavyo, kwa hakika Yeye anayaona vyema mnayoyatenda.
(41) Kwa hakika wale walioyakufuru mawaidha haya yanapowajia (wataangamia), na haya bila ya shaka ni Kitabu chenye nguvu na utukufu.
(42) Haukifikii upotovu mbele yake wala nyuma yake. Kimeteremshwa na Mwenye hekima, Msifiwa mno.
(43) Huambiwi ila yale yale waliyoambiwa Mitume wa kabla yako. Hakika Mola wako Mlezi bila ya shaka ni Mwenye maghfira, na ni Mwenye adhabu chungu.
(44) Na lau tungeliifanya Qur-ani kwa lugha ya kigeni, wangelisema: Kwa nini Aya zake hazikupambanuliwa? Yawaje lugha ya kigeni na Mtume Mwaarabu? Sema: Hii Qur-ani ni uwongofu na ponya kwa wenye kuamini. Na wale wasioamini umo uziwi katika masikio yao, nayo kwao imezibwa hawaioni. Hao wanaitwa nao wako pahala mbali.
(45) Na hakika tulimpa Musa Kitabu, lakini pakatokea tofauti juu yake. Na lau kuwa halikwishatangulia neno la Mola wako Mlezi, wangelihukumiwa. Na hakika wao wamo katika shaka yenye kuwatia wasiwasi juu yake.
(46) Anayetenda mema, basi anajitendea mwenyewe nafsi yake. Na mwenye kutenda uovu, basi ni juu ya nafsi yake vile vile; wala Mola wako Mlezi si mwenye kuwadhulumu waja.
(47) Ujuzi wa kuijua Saa ya Kiyama unarudishwa kwake tu Mwenyezi Mungu. Na matunda hayatoki katika mafumba yake, wala cha kike hakichukui mimba, wala hakizai, ila kwa kujua kwake. Na siku atakayowaita, akawaambia: 'Wako wapi washirika wangu?' Hapo watasema: 'Tunakiri kwako ya kwamba hapana miongoni mwetu anayeshuhudia hayo.'
(48) Na wakawapotea wale waliokuwa wakiwaomba hapo kwanza, na wakawa na yakini kuwa hawana pa kukimbilia.
(49) Mwanadamu hachoki kuomba dua za heri, na inapompata shari, mara huvunjika moyo muno akakata tamaa sana.
(50) Na pindi tukimwonjesha rehema itokayo kwetu baada ya dhara kumgusa, bila ya shaka husema: 'Haya nayastahiki mimi, wala sidhani kuwa Kiyama kitakuja. Na hata nikirudishwa kwa Mola wangu Mlezi, bila ya shaka nina mema yangu kwake!' Basi kwa yakini tutawaelezea wale waliokufuru hayo waliyoyatenda, na kwa yakini tutawaonjesha adhabu ngumu.
(51) Na tukimneemesha mwanadamu, hugeuka na kujitenga upande, na inapomgusa shari, huwa na madua marefu marefu.
(52) Sema: 'Mnaonaje! Ikiwa haya yanatoka kwa Mwenyezi Mungu, nanyi ikawa ndio mmeyakataa, ni nani aliyepotea zaidi kuliko aliye katika upinzani wa mbali?'
(53) Tutawaonyesha Ishara zetu katika upeo wa mbali na katika nafsi zao wenyewe mpaka iwabainikie kwamba haya ni kweli. Je, haikutoshi kwamba Mola wako Mlezi kuwa Yeye ni Shahidi bora wa kila kitu?
(54) Tanabahi, hakika wao wamo katika shaka ya kukutana na Mola wao Mlezi! Tanabahi, hakika Yeye amekizunguka kila kitu.