40 - Surat Ghafir ()

|

(1) Ha, Mim.

(2) Uteremsho wa Kitabu umetoka kwa Mwenyezi Mungu Mwenye nguvu, Mwenye kujua vyema.

(3) Anayesamehe dhambi na anayepokea toba, Mkali wa kuadhibu, Mwenye ukarimu, hakuna mungu ila Yeye; marejeo ni kwake.

(4) Hawazibishi Ishara za Mwenyezi Mungu ila wale waliokufuru; basi kusikughuri wewe kutangatanga kwao katika nchi.

(5) Kabla yao walikadhibisha kaumu ya Nuhu na makundi mengine baada yao. Na kila taifa lilikuwa na hamu juu ya Mtume wao wamkamate. Na walibishana kwa upotovu ili kuipindua haki. Kwa hivyo niliwakamata. Basi ilikuwaje adhabu yangu!

(6) Namna hivi limewathibitikia makafiri neno la Mola wako Mlezi ya kwamba wao ni watu wa Motoni.

(7) Wale wanaobeba 'Arshi, na wale walio pembezoni mwake, wanamsabihi na kumhimidi Mola wao Mlezi, na wanamuamini, na wanawaombea msamaha walioamini kwa kusema: Mola wetu Mlezi! Umekienea kila kitu kwa rehema na ujuzi. Basi wasamehe wale waliotubu na wakaifuata Njia yako, na waepushe na adhabu ya Jahanamu.

(8) Mola wetu Mlezi! Na waingize katika Bustani za Milele ulizowaahidi. Na uwape haya pia wale waliofanya mema miongoni mwa wazee wao na wake zao na dhuriya zao. Hakika Wewe ni Mwenye nguvu, Mwenye hekima.

(9) Na waepushe na maovu; kwani umwepushaye maovu siku hiyo, hakika umemrehemu; na huko ndiko kufuzu kukubwa.

(10) Kwa hakika wale waliokufuru watanadiwa: Bila ya shaka kukuchukieni Mwenyezi Mungu ni kukubwa kuliko kujichukia nyinyi nafsi zenu, mlipokuwa mnaitwa kwenye Imani nanyi mkakataa.

(11) Watasema: Mola wetu Mlezi! Umetufisha mara mbili, na umetuhuisha mara mbili! Basi tunakiri madhambi yetu. Basi je, ipo njia ya kutoka?

(12) Hayo ni hivyo kwa sababu mlikuwa akiombwa Mwenyezi Mungu peke yake mnakataa. Na akishirikishwa mnaamini. Basi hukumu ni ya Mwenyezi Mungu Mtukufu Mkuu.

(13) Yeye ndiye anayekuonyesheni Ishara zake, na anakuteremshieni kutoka mbinguni riziki. Na hapana anayekumbuka ila anayerejea.

(14) Basi mwombeni Mwenyezi Mungu mkimsafia Dini Yeye tu, na wangalichukia makafiri.

(15) Yeye ndiye Mwenye vyeo vya juu, Mwenye 'Arshi. Hutuma Roho kwa amri yake juu ya amtakaye katika waja wake, ili kuonya kwa Siku ya Mkutano.

(16) Siku watakayodhihiri wao. Hapana kitakachofichikana chochote chao kwa Mwenyezi Mungu. Ufalme ni wa nani leo? Ni wa Mwenyezi Mungu, Mmoja, Mshindi.

(17) Leo kila nafsi italipwa kwa yale iliyochuma. Hapana dhuluma leo. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwepesi wa kufanya hesabu.

(18) Na waonye siku inayokurubia, wakati nyoyo zitakapofika kooni, nao wamejaa huzuni. Madhaalimu hawatakuwa na rafiki, wala mwombezi wa kuitikiwa.

(19) (Mwenyezi Mungu) anajua hiyana ya macho na yale ambayo vifua vinayaficha.

(20) Na Mwenyezi Mungu huhukumu kwa haki; lakini hao ambao wao wanawaomba badala yake hawahukumu chochote. Hakika Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kusikia, Mwenye kuona.

(21) Kwani hawatembei katika ardhi wakaona jinsi ulivyokuwa mwisho wa wale waliokuwa kabla yao? Hao walikuwa wamewazidi hawa kwa nguvu na athari katika nchi. Na Mwenyezi Mungu aliwatia mkononi kwa sababu ya madhambi yao. Na wala hapakuwa wa kuwalinda na Mwenyezi Mungu.

(22) Hayo ni kwa sababu walikuwa Mitume wao walikuwa wanawajia kwa hoja zilizo wazi, lakini wakawakataa, ndipo Mwenyezi Mungu akawakamata. Bila ya shaka Yeye ni Mwenye nguvu, Mkali wa kuadhibu.

(23) Na kwa yakini tulimtuma Musa pamoja na Ishara zetu na uthibitisho ulio wazi.

(24) Kumwendea Firauni na Hamana na Qaruni, wakasema: Huyu ni mchawi, mwongo mkubwa.

(25) Basi alipowaletea Haki inayotoka kwetu, walisema: Waueni watoto wanaume wa wale waliomuamini na wawacheni hai wanawake wao. Na haviwi vitimbi vya makafiri ila katika upotovu.

(26) Na Firauni akasema: Niachieni nimuue Musa, naye amwite Mola wake Mlezi! Mimi nachelea asije kubadilishieni dini yenu, au akadhihirisha uharibifu katika nchi.

(27) Na Musa akasema: Mimi najikinga kwa Mola wangu Mlezi na Mola wenu Mlezi anilinde na kila mwenye jeuri asiyeiamini Siku ya Hesabu.

(28) Na akasema mwanamume mmoja Muumini, aliyekuwa mmoja katika watu wa Firauni aliyeficha Imani yake: Mtamuuwa mtu kwa sababu anasema Mola wangu Mlezi ni Mwenyezi Mungu? Na hali naye amekujieni na hoja zilizo wazi? Na akiwa yeye mwongo, basi uongo wake ni juu yake mwenyewe. Na akiwa mkweli, yatakufikieni baadhi ya hayo anayokuahidini. Hakika Mwenyezi Mungu hamwongoi apindukiaye mipaka, mwongo mkubwa.

(29) Enyi watu wangu! Leo mna ufalme, mmeshinda katika nchi; basi ni nani atakayenisaidia kutuokoa na adhabu ya Mwenyezi Mungu kama ikitufikia? Firauni akasema: Sikupeni shauri ila ile niliyoiona, wala siwaongozi ila kwenye njia ya uwongofu.

(30) Na akasema yule aliyeamini: Enyi watu wangu! Hakika mimi nawahofia mfano wa siku za makundi.

(31) Mfano wa hali ya watu wa Nuhu na 'Adi na Thamudi na wale wa baada yao. Na Mwenyezi Mungu hataki kuwadhulumu waja.

(32) Na enyi watu wangu! Hakika mimi nawahofia Siku ya mayowe.

(33) Siku mtakapogeuka kurudi nyuma. Hamtakuwa na wa kukulindeni kwa Mwenyezi Mungu. Na mwenye kuhukumiwa na Mwenyezi Mungu kupotea, basi huyo hana wa kumwongoa.

(34) Na alikwishawajieni Yusuf zamani kwa dalili zilizo wazi, lakini nyinyi mliendelea katika shaka kwa yale aliyokuleteeni; mpaka alipokufa, mkasema: Mwenyezi Mungu hataleta kabisa Mtume baada yake. Kama hivyo Mwenyezi Mungu humwacha kupotea anayepindukia mipaka katika maasi anayejitia shaka.

(35) Hao ambao wanajadiliana katika Ishara za Mwenyezi Mungu pasipo ushahidi wowote uliowafikia, ni chukizo kubwa mbele ya Mwenyezi Mungu na mbele ya wale walioamini. Hivi ndivyo Mwenyezi Mungu azibavyo kila moyo wa jeuri anayejivuna.

(36) Na Firauni akasema: Ewe Hamana! Nijengee mnara ili nipate kuzifikia njia.

(37) Njia za mbinguni ili nikamwone Mungu wa Musa. Na kwa hakika mimi bila ya shaka namjua kuwa ni mwongo tu. Na hivi ndivyo Firauni alivyopambiwa ubaya wa vitendo vyake, na akazuiliwa Njia. Na vitimbi vya Firauni havikuwa ila katika kuangamia tu.

(38) Na yule aliyeamini alisema: Enyi watu wangu! Nifuateni mimi, nitakuongozeni njia ya uwongozi mwema.

(39) Enyi watu wangu! Hakika haya maisha ya dunia ni starehe ipitayo tu, na hakika Akhera ndiyo nyumba ya daima.

(40) Mwenye kutenda uovu, hatalipwa ila sawa na huo uwovu wake. Na anayetenda wema, akiwa mwanamume au mwanamke, naye ni Muumini, basi hao wataingia Peponi, waruzukiwe humo bila ya hesabu.

(41) Na enyi watu wangu! Kwa nini mimi nakuiteni kwenye uwokofu, nanyi mnaniita kwenye Moto?

(42) Mnaniita nimkufuru Mwenyezi Mungu na nimshirikishe na yule ambaye simjui, nami nakuiteni kwa Mwenye nguvu Mwenye kusamehe mno?

(43) Bila ya shaka mnayeniitia kumuabudu hastahiki wito duniani wala Akhera. Na hakika marejeo yetu ni kwa Mwenyezi Mungu. Na wanaopindukia mipaka ndio watu wa Motoni!

(44) Basi mtayakumbuka ninayokuambieni. Nami namkabidhi Mwenyezi Mungu mambo yangu. Hakika Mwenyezi Mungu anawaona vyema waja wake.

(45) Basi Mwenyezi Mungu akamlinda na ubaya wa hila walizozifanya. Na adhabu mbaya itawazunguka watu wa Firauni.

(46) Wanaonyeshwa Moto asubuhi na jioni. Na itapofika Saa ya Kiyama patasemwa: Waingizeni watu wa Firauni katika adhabu kali kabisa!

(47) Na watapohojiana huko Motoni, wanyonge watawaambia wale waliojitukuza: Hakika sisi tulikuwa wafuasi wenu, basi je, hamtuondolei sehemu ya huu Moto?

(48) Watasema wale waliojitukuza: Hakika sote sisi tumo humo humo! Kwani Mwenyezi Mungu ameshahukumu baina ya waja!

(49) Na wale walio Motoni watawaambia walinzi wa Jahannamu: Mwombeni Mola wenu Mlezi atupunguzie walau siku moja ya adhabu.

(50) Nao watasema: Je, hawakuwa wakikufikieni Mitume wenu kwa hoja zilizo wazi? Watasema: Kwani? Watasema: Basi ombeni! Na maombi ya makafiri hayawi ila ni kupotea bure.

(51) Hakika bila ya shaka Sisi tunawanusuru Mitume wetu na wale walioamini katika uhai wa duniani na siku watakaposimama Mashahidi.

(52) Siku ambayo hautawafaa madhalimu udhuru wao, nao watapata laana, na watapata makazi mabaya kabisa.

(53) Na kwa hakika tulimpa Musa uwongofu, na tukawarithisha Wana wa Israili Kitabu.

(54) Ambacho ni Uwongofu na Ukumbusho kwa wenye akili.

(55) Basi subiri. Hakika ahadi ya Mwenyezi Mungu ni kweli. Na omba msamaha kwa dhambi zako, na umtakase Mola wako Mlezi kwa kumhimidi jioni na asubuhi.

(56) Hakika hao wanaobishana katika Ishara za Mwenyezi Mungu bila ya uthibitisho wowote uliowajia, hawana vifuani mwao ila kutaka ukubwa tu, na wala huo hawaufikilii. Basi jikinge kwa Mwenyezi Mungu. Hakika Yeye ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona.

(57) Bila ya shaka kuumba mbingu na ardhi ni kukubwa zaidi kuliko kuwaumba watu. Lakini watu wengi hawajui.

(58) Na kipofu na mwenye kuona hawalingani; na wale walioamini na wakatenda mema hawalingani na muovu. Ni machache mnayoyakumbuka.

(59) Hakika Saa (ya Kiyama) itafika, nayo haina shaka. Lakini watu wengi hawaamini.

(60) Na Mola wenu Mlezi anasema: Niombeni nitakuitikieni. Kwa hakika wale ambao wanajivuna na kuniabudu Mimi wataingia Jahanamu wadhalilike.

(61) Mwenyezi Mungu ndiye aliyewafanyia usiku ili mpate kutulia humo, na mchana wa kuonea. Hakika Mwenyezi Mungu bila ya shaka ni Mwenye fadhila juu ya watu, lakini watu wengi hawashukuru.

(62) Huyo ndiye Mwenyezi Mungu Mola wenu Mlezi, Muumba wa kila kitu. Hapana mungu ila Yeye; basi mnageuzwa wapi?

(63) Namna hivi ndivyo walivyogeuzwa wale waliokuwa wakizikataa Ishara za Mwenyezi Mungu.

(64) Ni Mwenyezi Mungu aliyekufanyieni ardhi kuwa ni pahala pa kukaa, na mbingu kuwa dari. Na akawatia sura, na akazifanya nzuri sura zenu, na akawaruzuku vitu vizuri. Huyo ndiye Mwenyezi Mungu Mola wenu Mlezi. Basi ametukuka Mwenyezi Mungu Mola Mlezi wa walimwengu wote.

(65) Yeye ndiye aliye Hai - hapana mungu isipokuwa Yeye. Basi muabuduni Yeye mkimsafishia Dini Yeye. Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote.

(66) Sema: Mimi nimekatazwa kuwaabudu hao mnaowaomba badala ya Mwenyezi Mungu, ziliponijia hoja zilizo dhahiri kutokana na Mola wangu Mlezi. Na nimeamrishwa nisilimu kwa Mola wa walimwengu wote.

(67) Yeye ndiye aliyewaumba kwa udongo, kisha kwa tone la manii, kisha kwa pande la damu, kisha akawatoa katika hali ya mtoto mchanga, kisha mpate kufikilia utu uzima, kisha mpate kuwa wazee. Na kati yenu wapo wanaokufa kabla, na ili mfikie muda uliokwisha wekwa, na ili mpate kufahamu.

(68) Yeye ndiye anayehuisha na anayefisha. Akihukumu jambo liwe, basi huliambia: Kuwa! Likawa.

(69) Je, huwaoni wale wanaobishana katika Ishara za Mwenyezi Mungu? Wanageuziwa wapi?

(70) Ambao wamekanusha Kitabu na yale tuliyowatuma Mitume wetu. Basi watakuja jua.

(71) Zitakapokuwa pingu shingoni mwao na minyororo, huku wanabururwa

(72) Katika maji ya moto, kisha wanaunguzwa Motoni.

(73) Tena wataambiwa: Wako wapi wale mliokuwa mkiwashirikisha.

(74) Badala ya Mwenyezi Mungu? Watasema: Wametupotea, bali tangu zamani hatukuwa tukiomba kitu! Hivyo ndivyo Mwenyezi Mungu anawaachia makafiri wapotelee mbali.

(75) Haya ni kwa sababu mlikuwa mkijitapa katika ardhi pasipo haki, na kwa sababu mlikuwa mkijishaua.

(76) Ingieni kwenye milango ya Jahanamu, mdumu humo milele. Basi ni maovu yaliyoje makazi ya wanaotakabari!

(77) Basi subiri, hakika ahadi ya Mwenyezi Mungu ni ya kweli. Na ama tukikuonyesha baadhi ya yale tuliyowaahidi au tukikufisha, lakini wao watarudishwa kwetu tu.

(78) Na bila ya shaka tuliwatuma Mitume kabla yako. Wengine katika hao tumekusimulia habari zao, na wengine hatukukusimulia. Na haiwi Mtume alete Ishara yoyote ila kwa idhini ya Mwenyezi Mungu. Basi ikija amri ya Mwenyezi Mungu, huhukumiwa kwa Haki, na hapo wapotofu watahasiri.

(79) Mwenyezi Mungu aliyewajaalia nyama hoa, mifugo, ili muwapande baadhi yao, na muwale baadhi yao.

(80) Na katika hao mnayo manufaa kadhaa wa kadhaa, na mnapata kwao haja zilizomo vifuani mwenu; na mnachukuliwa juu yao, na juu ya merikebu.

(81) Naye anawaonyesha Ishara zake. Basi Ishara gani za Mwenyezi Mungu mnazozikataa?

(82) Kwani hawatembei katika ardhi wakaona namna ulivyokuwa mwisho wa wale waliokuwa kabla yao? Wao walikuwa wengi kuliko hawa, na wamewashinda kwa nguvu na athari katika nchi. Wala hayakuwafaa hayo waliyokuwa wakiyachuma.

(83) Walipowajia Mitume wao kwa hoja zilizo wazi, walijitapa kwa elimu waliyokuwa nayo. Basi yakawazunguka yale waliyokuwa wakiyafanyia masihara.

(84) Walipoiona adhabu yetu, walisema: Tumemuamini Mwenyezi Mungu kuwa ni wa pekee, na tunaikataa miungu tuliyokuwa tukiishirikisha naye.

(85) Lakini imani yao haikuwa yenye kuwafaa kitu wakati ambao wamekwishaiona adhabu yetu. Huu ndio mwendo wa Mwenyezi Mungu uliokuwa kwa waja wake. Na hapo waliokufuru walihasiri.