71 - Surat Nuh ()

|

(1) Hakika Sisi tulimtuma Nuhu kwa watu wake: uwaonye kaumu yako kabla ya kuwafikia adhabu chungu.

(2) Akasema: Enyi watu wangu! Kwa hakika mimi ni mwonyaji wa dhaahiri kwenu.

(3) Ya kwamba mumuabudu Mwenyezi Mungu, na mumche Yeye, na mumtii.

(4) Atakughufirieni madhambi yenu, na atakuakhirisheni mpaka muda uliowekwa. Hakika muda wa Mwenyezi Mungu utapofika haucheleweshwi. Laiti mngejua!

(5) Akasema: Ee Mola wangu Mlezi! Hakika mimi nimewaita watu wangu usiku na mchana.

(6) Lakini wito wangu haukuwazidisha ila kukimbia.

(7) Na hakika mimi kila nilipowaita ili upate kuwaghufiria, walijiziba masikio yao kwa vidole vyao, na wakajigubika nguo zao, na wakakamia, na wakatakabari vikubwa mno!

(8) Tena niliwaita kwa uwazi.

(9) Kisha nikawatangazia kwa kelele, tena nikasema nao kwa siri.

(10) Nikasema: Ombeni msamaha kwa Mola wenu Mlezi; hakika Yeye ni Mwingi wa kusamehe.

(11) Atakuleteeni mvua inyeshe mfululizo.

(12) Na atakupeni mali na wana, na atakupeni mabustani na atakufanyieni mito.

(13) Mna nini hamweki heshima ya Mwenyezi Mungu?

(14) Na hali Yeye kakuumbeni daraja baada ya daraja?

(15) Kwani hamwoni jinsi Mwenyezi Mungu alivyoziumba mbingu saba kwa matabaka?

(16) Na akaufanya mwezi ndani yake uwe nuru, na akalifanya jua kuwa taa?

(17) Na Mwenyezi Mungu amekuotesheni katika ardhi kama mimea.

(18) Kisha atakurudisheni humo na atakutoeni tena.

(19) Na Mwenyezi Mungu amekukunjulieni ardhi kama busati.

(20) Ili mtembee humo katika njia zilizo pana.

(21) Nuhu akasema: Mola wangu Mlezi! Hakika hao wameniasi, na wamemfuata yule ambaye mali yake na wanawe hawakumzidishia ila khasara.

(22) Na wakapanga vitimbi vikubwa.

(23) Na wakasema: Msiwaache miungu yenu, wala msimwache Wadda wala Suwaa' wala Yaghutha, wala Yau'qa, wala Nasra.

(24) Na hao walikwisha wapoteza wengi, wala usiwazidishie waliodhulumu ila kupotea.

(25) (Basi kwa ajili ya makosa yao waligharikishwa wakaingizwa Motoni, wala hawakuwapata wa kuwanusuru badala ya Mwenyezi Mungu.

(26) Na Nuhu akasema: Mola wangu Mlezi! Usimwache juu ya ardhi mkaazi wake yeyote katika makafiri!

(27) Hakika ukiwaacha watawapoteza waja wako, wala wao hawatazaa ila waovu makafiri.

(28) Mola wangu Mlezi! Nighufirie mimi na wazazi wangu, na kila aliyeingia nyumbani mwangu kuwa ni mwenye kuamini, na Waumini wote wanaume, na Waumini wanawake. Na wala usiwazidishie waliodhulumu ila kupotea.