27 - Surat An-Naml ()

|

(1) T'aa Siin. Hizi ni Aya za Qur-ani na Kitabu kinachobainisha.

(2) Uwongofu na bishara kwa Waumini.

(3) Ambao wanashika Swala, na wanatoa Zaka, na Akhera wana yakini nayo.

(4) wa hakika wale wasioiamini Akhera tumewapambia vitendo vyao, kwa hivyo wanatangatanga ovyo.

(5) ao ndio watapata adhabu mbaya kabisa, na hao katika Akhera ndiyo watapata hasara zaidi.

(6) Na hakika wewe unafundishwa Qur-ani inayotokana kwake Mwenye hekima, Mwenye kujua zaidi.

(7) (Kumbuka) Musa alipowaambia ahali zake: Hakika nimeona moto, nitakwenda niwaletee habari kutoka huko, au nitawaletea kijinga kinacho waka ili mpate kuota moto.

(8) Basi alipoufikia, ilinadiwa: Amebarikiwa aliyemo katika moto huu na walioko pembezoni mwake. Na ametakasika Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote.

(9) Ewe Musa! Hakika Mimi ndiye Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, Mwenye hekima.

(10) Na itupe fimbo yako! Alipoiona ikitikisika kama nyoka, aligeuka nyuma wala hakungoja. Ewe Musa! Usihofu! Hakika hawahofu mbele yangu Mitume.

(11) Lakini aliyedhulumu, kisha akabadilisha wema baada ya ubaya, basi Mimi hakika ni Mwingi wa kusamehe, Mwingi wa kurehemu.

(12) Na ingiza mkono wako katika mfuko wako, utatoka mweupe bila ya maradhi. Ni katika Ishara tisa za kumpelekea Firauni na kaumu yake. Hakika hao walikuwa kaumu waovu.

(13) Basi zilipowafikia Ishara zetu hizo zenye kuonyesha, wakasema: Huu ni uchawi dhahiri.

(14) Na wakazikataa kwa dhuluma na kujivuna, na hali ya kuwa nafsi zao zina yakini nazo. Basi angalia ulikuwaje mwisho wa waharibifu!

(15) Na hakika tuliwapa Daudi na Suleiman elimu, na wakasema: Alhamdu Lillahi (Kuhimidiwa kote ni kwa Mwenyezi Mungu) aliyetufadhilisha kuliko wengi katika waja wake Waumini.

(16) Na Suleiman alimrithi Daudi, na akasema: Enyi watu! Tumefunzwa usemi wa ndege, na tumepewa katika kila kitu. Hakika hii ni fadhila iliyo dhahiri.

(17) Na alikusanyiwa Suleiman majeshi yake ya majini, na watu, na ndege; nayo yakapangwa kwa nidhamu.

(18) Mpaka walipofika kwenye bonde la wadudu chungu, alisema mdudu chungu mmoja: Enyi wadudu chungu! Ingieni majumbani mwenu, asiwapondeni Suleiman na majeshi yake bila ya wao kutambua.

(19) Basi (Suleiman) akatabasamu akacheka kwa neno hili, na akasema: Ewe Mola wangu Mlezi! Nizindue niishukuru neema yako uliyonineemesha mimi na wazazi wangu, na nipate kutenda mema uyapendayo, na uniingize kwa rehema yako katika waja wako wema.

(20) Na akawakagua ndege, na akasema: Imekuwaje, mbona simwoni Hud-hud, au amekuwa miongoni mwa wasiokuwepo?

(21) Kwa yakini nitamuadhibu kwa adhabu kali, au nitamchinja, au aniletee hoja ya kutosha.

(22) Basi (Hud-hud) akakaa si mbali na akasema: Nimegundua usilogundua wewe, na ninakujia hivi kutoka nchi ya Sabai, na nakuletea habari za yakini.

(23) Hakika mimi nimemkuta mwanamke anawatawala, naye amepewa kila kitu, na anacho kiti cha enzi kikubwa.

(24) Nimemkuta yeye na watu wake wanalisujudia jua badala ya Mwenyezi Mungu; na Shetani amewapambia vitendo vyao na akawazuilia Njia. Kwa hivyo hawakuongoka.

(25) Na hawamsujudii Mwenyezi Mungu ambaye huyatoa yaliyofichikana katika mbingu na ardhi, na anayajua mnayoyaficha na mnayoyadhihirisha.

(26) Mwenyezi Mungu - hapana mungu isipokuwa Yeye, Mola Mlezi wa 'Arshi tukufu

(27) Akasema (Suleiman): Tutatazama iwapo umesema ukweli au wewe ni miongoni mwa waongo.

(28) Nenda na barua yangu hii na uwafikishie, kisha waache na utazame watarejesha nini.

(29) (Malkia) akasema: Enyi waheshimiwa! Hakika nimeletewa barua tukufu.

(30) Kwa hakika, imetoka kwa Suleiman nayo hakika ni: Kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mwingi wa rehema, Mwingi wa kurehemu.

(31) Msinifanyie jeuri, na fikeni kwangu nanyi mmekwisha kuwa wenye kusalimu amri.

(32) Akasema: Enyi waheshimiwa! Nipeni shauri katika jambo langu hili, kwani mimi sikati shauri yoyote mpaka mhudhurie

(33) Wakasema: Sisi ni wenye nguvu na wakali kwa vita; na amri iko kwako, basi tazama ni nini unaamrisha.

(34) Akasema: Hakika wafalme wanapouingia mji, wanauharibu, na wanawafanya wale watukufu wake kuwa wanyonge. Na hivyo ndivyo watendavyo.

(35) Lakini mimi nitawatumia zawadi, nami nitangoja watakayorudi nayo wajumbe.

(36) Basi alipofika (mjumbe) kwa Suleiman, alisema (Suleiman): Hivyo ndivyo nyinyi mnanisaidia kwa mali? Aliyonipa Mwenyezi Mungu ni bora zaidi kuliko aliyowapa nyinyi. Lakini nyinyi mnafurahia hii zawadi yenu.

(37) Rejea kwao! Kwa yakini sisi tutawajia kwa majeshi wasioyaweza kuyakabili. Na hakika tutawatoa humo na hali wao wamekuwa madhalili na wanyonge.

(38) Akasema: Enyi waheshimiwa! Ni nani kati yenu atakayeniletea kiti chake cha enzi kabla hawajanijia, nao wamekwisha salimu amri?

(39) Akasema Afriti mmoja katika majini: Mimi nitakuletea kabla hujainuka pahala pako hapo. Na mimi kwa hakika katika hilo nina nguvu na muaminifu.

(40) Akasema mwenye elimu ya Kitabu: Mimi nitakuletea kabla ya kupepesa jicho lako. Basi alipokiona kimewekwa kimetulia mbele yake, akasema: Haya ni katika fadhila zake Mola wangu Mlezi, ili anijaribu nitashukuru au nitakufuru. Na mwenye kushukuru, kwa hakika, anashukuru kwa manufaa ya nafsi yake. Na anayekufuru, kwa hakika Mola wangu Mlezi ni Mkwasi na Karimu.

(41) Akasema: Mgeuzieni kiti chake cha enzi hiki, tuone ataongoka, au atakuwa miongoni mwa wasioongoka.

(42) Basi (Malkia) alipofika akaambiwa: Je, kiti chako cha enzi ni kama hiki? Akasema: Kama kwamba ndicho hiki. (Suleiman na watu wake wakasema): Na sisi tumepewa elimu kabla yake (Malkia), na tukawa Waislamu.

(43) Na yale aliyokuwa akiyaabudu badala ya Mwenyezi Mungu yalimzuilia. Hakika yeye (Malkia) alikuwa katika kaumu ya makafiri.

(44) Akaambiwa: Liingie behewa la hili jumba. Alipoliona, alidhani ni maji, na akapandisha nguo mpaka kwenye miundi yake. (Suleiman) akasema: Hakika hilo ni behewa liliosakafiwa kwa vioo! Akasema (Malkia): Mola wangu Mlezi! Mimi nimejidhulumu, na sasa ninanyenyekea pamoja na Suleiman kwa Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote.

(45) Na kwa kina Thamud tulimtuma ndugu yao Saleh kuwaambia: Muabuduni Mwenyezi Mungu. Basi wakawa makundi mawili yanayogombana.

(46) Akasema: Enyi kaumu yangu! Kwa nini mnauhimiza wovu kabla ya wema? Kwa nini hamuombi msamaha kwa Mwenyezi Mungu ili mrehemewe?

(47) Wakasema: Tuna kisirani nawe na wale walio pamoja nawe. Yeye akasema: Uaguzi wa ukorofi wenu uko kwa Mwenyezi Mungu; lakini nyinyi ni watu mnaojaribiwa.

(48) Na walikuwamo mjini watu tisa wakifanya uharibifu katika nchi wala hawafanyi mambo kutengenea.

(49) Wakasema: Apishaneni kwa Mwenyezi Mungu tutamshambulia usiku yeye na ahali zake; kisha tutamwambia mrithi wake: Sisi hatukuona maangamizo ya watu wake, na sisi bila ya shaka tunasema ukweli.

(50) Basi wakapanga mipango yao, na Sisi tukapanga mipango yetu, na wao hawatambui.

(51) Basi angalia ulivyokuwa mwisho wa mipango yao, ya kwamba tuliwaangamiza wao pamoja na watu wao wote.

(52) Basi hizo nyumba zao ni tupu kwa sababu ya walivyodhulumu. Hakika bila ya shaka katika hayo ipo Ishara kwa watu wanaojua.

(53) Na tukawaokoa wale walioamini na waliokuwa wanamcha Mungu.

(54) Na Luti alipowaambia watu wake, "Je, mnafanya uchafu nanyi mnaona?

(55) Hakika nyinyi mnawaingilia wanaume kwa matamanio badala ya wanawake? Hakika nyinyi ni kaumu mnaofanya ujinga kabisa!

(56) Basi haikuwa jawabu ya kaumu yake isipokuwa ni walisema, "Wafukuzeni wafwasi wa Luti kutoka katika mji wenu. Hakika wao ni watu wanaojitia usafi."

(57) Basi tukamwokoa yeye na ahali zake, isipokuwa mkewe; tukamkadiria katika waliobaki nyuma.

(58) Na tukawanyeshea mvua. Basi ni ovu mno mvua hiyo ya wale waliokwisha onywa.

(59) Sema: Alhamdu Lillahi (Kuhimidiwa ni kwa Mwenyezi Mungu!) Na amani ishuke juu ya waja wake aliowateua. Je, Mwenyezi Mungu ndiye bora, au wale wanaowashirikisha naye?

(60) Au ni nani yule aliyeziumba mbingu na ardhi, na akawateremshia maji kutoka mbinguni, na kwa hayo tukaziotesha bustani zenye kupendeza? Nyinyi hamkuwa na uwezo wa kuiotesha miti yake. Je, yupo mungu pamoja na Mwenyezi Mungu? Bali hao ni kaumu waliopotoka.

(61) Au nani yule aliyeifanya ardhi mahali pa kutua, na akajaalia ndani yake mito, na akaweka milima? Na akaweka baina ya bahari mbili kizuizi? Je, yupo mungu pamoja na Mwenyezi Mungu? Bali wengi wao hawajui.

(62) Au ni nani yule anayemjibu mwenye shida kubwa pale anapomwomba, na akaiondoa dhiki, na akawafanya warithi wa ardhi? Je, yupo mungu pamoja na Mwenyezi Mungu? Ni machache mnayoyazingatia.

(63) Au ni nani yule anayewaongoa katika giza la bara na bahari, na akazipeleka pepo kuleta bishara kabla ya rehema zake? Je, yupo mungu pamoja na Mwenyezi Mungu? Ametukuka Mwenyezi Mungu juu ya hao wanaomshirikisha naye.

(64) Au ni nani anayeuanzisha uumbaji, kisha akaurejesha? Na ni nani anayewaruzuku kutoka mbinguni na kwenye ardhi? Je, yupo mungu pamoja na Mwenyezi Mungu? Sema: Leteni hoja zenu kama nyinyi ni wakweli.

(65) Sema: Hapana katika mbingu na ardhi ajuaye ya ghaibu isipokuwa Mwenyezi Mungu. Wala wao hawajui lini watafufuliwa.

(66) Kwani huo ujuzi wao umefikilia kuijua Akhera? Bali wao wamo katika shaka nayo tu, bali wao ni vipofu nayo.

(67) Na wakasema wale waliokufuru: Je, tutakapokuwa mchanga, sisi na baba zetu, hivyo kweli tutakuja tolewa?

(68) Hakika ni haya haya tu tuliahidiwa sisi na baba zetu zamani. Hayakuwa haya isipokuwa ni hadithi za uongo za watu wa kale.

(69) Sema: Nendeni katika ardhi, na tazameni ulikuwaje mwisho wa wahalifu.

(70) Wala usiwahuzunikie wala usiwe katika dhiki kwa sababu ya hila zao wanazozifanya.

(71) Na wanasema: Ahadi hii itatokea lini, ikiwa nyinyi ni wakweli?

(72) Sema: Huenda yako karibu kuwafikia sehemu ya yale mnayoyahimiza.

(73) Na hakika Mola wako Mlezi ni Mwenye fadhila kwa watu, lakini wengi wao hawashukuru.

(74) Na hakika Mola wako Mlezi anayajua yanayoficha vifua vyao na wanayoyaweka hadharani.

(75) Na hakuna siri katika mbingu na ardhi isipokuwa imo katika Kitabu kinachobainisha.

(76) Hakika Qur-ani hii inawasimulia Wana wa Israili mengi ya yale wanayohitalifiana ndani yake.

(77) Nayo hakika ni uwongofu na rehema kwa Waumini.

(78) Hakika Mola wako Mlezi atawahukumu kwa hukumu yake, naye ni Mwenye nguvu, ajuaye zaidi.

(79) Basi mtegemee Mweneyezi Mungu; hakika wewe uko juu ya Haki iliyo wazi.

(80) Kwa hakika wewe huwezi kuwafanya maiti wasikie, wala kuwafanya viziwi wasikie wito, wanapokwisha geuka kwenda zao.

(81) Wala huwezi kuwaongoa vipofu waache upotovu wao. Huwezi kuwafanya wasikie isipokuwa wenye kuziamini Ishara zetu; basi hao ndio Waislamu.

(82) Na itakapowaangukia kauli juu yao, tutawatolea mnyama katika ardhi atakayewasemesha, ya kuwa watu walikuwa hawana yakini na Ishara zetu.

(83) Na Siku tutakapokusanya kutoka katika kila umma kundi miongoni mwa wale wanaokadhibisha Ishara zetu, nao watagawanywa mafungu mafungu.

(84) Hata watakapofika, (Mwenyezi Mungu) atasema: Je, nyinyi si mlizikanusha Ishara zangu pasipo kuzijua vyema? Au mlikuwa mkifanya nini?

(85) Na kauli itawaangukia juu yao kwa vile walivyodhulumu. Basi hao hawatatamka lolote.

(86) Je, hawaoni kwamba sisi tumeufanya usiku ili watulie, na mchana wa kuonea. Hakika katika hayo, zipo Ishara kwa watu wanaoamini.

(87) Na Siku litakapopulizwa baragumu, watahangaika waliomo mbinguni na katika ardhi, isipokuwa amtakaye Mwenyezi Mungu. Na wote watamfikia huku ni wanyonge.

(88) Na utaiona milima utaidhania imetulia; ilhali inakwenda kama mwendo wa mawingu. Huo ndio ufundi wa Mwenyezi Mungu aliyetengeneza sawasawa vilivyo kila kitu. Hakika Yeye anazo habari za yote myatendayo.

(89) Mwenye kuja na uzuri, atapata bora kuliko huo. Nao watasalimika kutokana na mahangaiko ya Siku hiyo.

(90) Na atakayekuja na ubaya, basi zitasunukishwa nyuso zao Motoni. Je, kwani mnalipwa isipokuwa mliyokuwa mkiyatenda?

(91) Ama mimi, nimeamrishwa nimuabudu Mola Mlezi wa mji huu aliyeufanya ni mtakatifu; na ni vyake Yeye tu vitu vyote. Na nimeamrishwa niwe miongoni mwa Waislamu (wenye kunyenyekea).

(92) Na niisome Qur-ani. Na mwenye kuongoka, basi ameongoka kwa faida ya nafsi yake. Na mwenye kupotea, basi sema, "Hakika mimi ni miongoni mwa waonyaji."

(93) Na sema, "Alhamdu Lillahi (Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu). Yeye atawaonyesha Ishara zake, na mtazijua. Na Mola wako Mlezi si mwenye kughafilika mbali na hayo myatendayo.