(1) Kaf Ha Ya 'Ayn Swad.
(2) Huu ni ukumbusho wa rehema ya Mola wako Mlezi kwa mja wake, Zakariya.
(3) Alipomwita Mola wake Mlezi kwa siri.
(4) Akasema: Mola wangu Mlezi! Hakika mimi, mifupa yangu imedhoofika, na kichwa kinametameta kwa mvi; wala, Mola wangu Mlezi, sikuwa mwenye bahati mbaya kwa kukuomba Wewe.
(5) Na hakika mimi ninawahofia wasimamizi wa baada yangu. Na mke wangu ni tasa. Basi nitunuku mrithi kutoka kwako.
(6) Anirithi na awarithi ukoo wa Yaaqub. Na umjaalie ewe Mola wangu Mlezi awe mwenye kuridhisha.
(7) (Akaambiwa): Ewe Zakariya! Hakika Sisi tunakubashiria mwana; jina lake ni Yahya. Hatujapata kumpa jina hilo yeyote kabla yake.
(8) Akasema: Ewe Mola wangu Mlezi! Vipi nitakuwa na mwana na ilhali mke wangu ni tasa, na mimi nimeshafikia ukongwe katika uzee?
(9) Akasema: Hivyo ndivyo alivyosema Mola wako Mlezi: Haya ni mepesi kwangu. Na hakika Mimi nilikwisha kuumba wewe zamani na wala hukuwa kitu.
(10) Akasema: Mola wangu Mlezi nijaalie Ishara. Akasema: Ishara yako ni kuwa hutasema na watu kwa usiku tatu, na ilhali u mzima sawasawa.
(11) Basi akawatokea kaumu yake kutoka mihirabuni. Akawaashiria kwamba: Msabihini Mwenyezi Mungu asubuhi na jioni.
(12) Ewe Yahya! Kishike Kitabu kwa nguvu! Nasi tulimpa hekima angali mtoto.
(13) Na tukampa huruma itokayo kwetu, na utakaso, na akawa mchamungu.
(14) Na akawa mwema kwa wazazi wake, wala hakuwa jabari muasi.
(15) Na salama iwe juu yake siku ya kuzaliwa, na siku ya kufa, na siku ya kufufuliwa.
(16) Na mtaje Maryamu katika Kitabu, pale alipojitenga na jamaa zake mahali upande wa mashariki.
(17) Na akaweka pazia kujikinga nao. Basi tukamtumia Roho wetu, naye akajifananisha kwake sawa sawa na mtu.
(18) (Maryamu) akasema: Hakika mimi ninajikinga kwa Mwingi wa rehema aniepushe nawe, ikiwa wewe ni mchamungu.
(19) (Malaika huyo) akasema: Hakika mimi ni mtume tu kutoka kwa Mola wako Mlezi ili nikutunuku mwana aliyetakasika.
(20) Akasema: Nitampataje mwana ilhali mtu yeyote hajawahi nigusa, wala sikuwahi kuwa kahaba?
(21) (Malaika) akasema: Hivyo ndiyo alivyosema Mola wako Mlezi: Haya ni mepesi kwangu! Na ili tumfanye kuwa ni Ishara kwa watu, na rehema kutoka kwetu, na hilo ni jambo lililokwisha hukumiwa.
(22) Basi akachukua mimba yake, na akaondoka nayo mpaka mahali pa mbali.
(23) Kisha uchungu ukampeleka kwenye shina la mtende; akasema: Laiti ningelikufa kabla ya haya, na nikawa niliyesahaulika kabisa!
(24) Kwa hivyo, akamnadi kutokea chini yake: Usihuzunike! Hakika Mola wako Mlezi ameshajaalia chini yako kijito kidogo cha maji!
(25) Na litikise kwako hilo shina la mtende, utakuangushia tende nzuri zilizo mbivu.
(26) Basi kula, na kunywa, na litulizie jicho lako. Na pindi ukimwona mtu yeyote, basi sema: Hakika mimi nimeweka nadhiri kwa Mwingi wa rehema, ya kufunga; kwa hivyo leo sitasema na mtu yeyote.
(27) Basi akaenda naye (mwanawe) kwa jamaa zake amembeba. Wakasema: Ewe Maryamu! Hakika umeleta kitu cha ajabu sana!
(28) Ewe dada yake Harun! Baba yako hakuwa mtu mbaya, wala mama yako hakuwa kahaba.
(29) Kwa hivyo, akamuashiria (mtoto). Wakasema: Vipi tumsemeshe aliye bado mtoto mdogo yumo katika mlezi?
(30) (Mtoto huyo) akasema: Hakika mimi ni mja wa Mwenyezi Mungu. Amenipa Kitabu, na amenifanya Nabii.
(31) Na amenijaalia ni mwenye kubarikiwa popote pale niwapo. Na ameniusia Swala na Zaka maadamu ni hai.
(32) Na nimtendee wema mama yangu. Wala hakunifanya niwe jeuri, mwovu.
(33) Na amani iko juu yangu siku niliyozaliwa, na siku nitakayokufa, na siku nitakayofufuliwa kuwa hai.
(34) Huyo ndiye Isa mwana wa Maryamu. Ndiyo kauli ya haki ambayo wanaifanyia shaka.
(35) Haiwi kwa Mwenyezi Mungu kujifanyia mwana, Subhanahu (Yeye ametakasika)! Anapolihukumia jambo, basi hakika huliambia tu: Kuwa! Na linakuwa.
(36) Na hakika Mwenyezi Mungu ndiye Mola wangu Mlezi, na Mola wenu Mlezi. Basi muabuduni Yeye. Hii ndiyo Njia iliyonyooka.
(37) Lakini makundi yakahitilafiana wao kwa wao. Basi ole wao hao waliokufuru kwa kuhudhuria Siku iliyo kuu!
(38) Watasikia na wataona vizuri vilivyoje Siku watakayotujia! Lakini madhalimu sasa wamo katika upotovu ulio dhahiri.
(39) Na waonye siku ya majuto makubwa itapokatwa amri. Nao wamo katika ghafla, wala hawaamini.
(40) Hakika Sisi ndio tutairithi ardhi na wale walio juu yake. Na kwetu watarejeshwa.
(41) Hakika yeye alikuwa mkweli mno, na Nabii.
(42) Alipomwambia baba yake: Ewe baba yangu! Kwa nini unaabudu visivyosikia, na visivyoona, na visivyokufaa chochote?
(43) Ewe baba yangu! Kwa yakini imenifikia elimu ambayo haikukujia wewe. Basi nifuate mimi, nami nitakuongoza Njia iliyo sawa.
(44) Ewe baba yangu! Usimuabudu Shetani. Hakika Shetani ni mwenye kumuasi sana Mwingi wa rehema.
(45) Ewe baba yangu! Hakika mimi ninahofu ije kupata adhabu inayotoka kwa Mwingi wa Rehema, ukaja kuwa mwenziwe Shetani.
(46) (Baba) akasema: Je huitaki miungu yangu, ewe Ibrahim? Kama huachi, basi lazima nitakupiga mawe. Na niondokee mbali kwa muda!
(47) (Ibrahim) akasema: Salamun 'alaika (Amani iwe juu yako)! Mimi nitakuombea msamaha kwa Mola wangu Mlezi. Hakika Yeye ananihurumia sana.
(48) Nami ninajitenga mbali nanyi na hayo mnayoyaabudu badala ya Mwenyezi Mungu. Na ninamwomba Mola wangu Mlezi; asaa nisiwe mwenye kukosa bahati kwa kumwomba Mola wangu Mlezi.
(49) Basi alipojitenga mbali nao na yale waliyokuwa wakiyaabudu badala ya Mwenyezi Mungu, tukamtunuku Is-haq na Yaaqub, na kila mmoja wao tukamfanya Nabii.
(50) Na tukawatunuku katika rehema zetu na tukawajaalia kupewa sifa za kweli tukufu.
(51) Na mtaje Musa katika Kitabu. Hakika yeye alikuwa ni mwenye kuchaguliwa, na alikuwa Mtume, Nabii.
(52) Na tulimwita upande wa kulia wa mlima na tukamsogeza kunong'ona naye.
(53) Nasi kwa rehema zetu tukamtunuku kakaye, Harun, awe Nabii.
(54) Na mtaje katika Kitabu Ismail. Bila ya shaka yeye alikuwa ni mkweli wa ahadi, na alikuwa Mtume, Nabii.
(55) Na alikuwa akiwaamrisha ahali zake Swala na Zaka, na alikuwa mbele ya Mola wake Mlezi mwenye kuridhiwa.
(56) Na mtaje katika Kitabu Idris. Hakika yeye alikuwa ni mkweli mno, Nabii.
(57) Na tulimuinua mahali pa juu.
(58) Hao ndio aliowaneemesha Mwenyezi Mungu miongoni mwa Manabii katika uzao wa Adam, na katika uzao wa wale tuliowabeba pamoja na Nuhu, na katika uzao wa Ibrahim na Israil, na katika wale tuliowaongoa na tukawateua. Wanaposomewa Aya za Mwingi wa rehema, huanguka kusujudu na kulia.
(59) Lakini wakaja baada yao wafuatizi waliipoteza Swala, na wakafuata matamanio. Basi watakuja kuta malipo ya ubaya.
(60) Isipokuwa mwenye kutubu, akaamini, na akatenda mema. Hao basi, wataingia Peponi wala hawatadhulumiwa chochote.
(61) Bustani za milele ambazo aliwaahidi Rahmani (Mwingi wa Rehema) waja wake katika ghaibu. Hakika Yeye ahadi yake hakuna shaka itafika.
(62) Humo hawatasikia upuuzi wowote, isipokuwa Salama tu. Na watapata humo riziki zao asubuhi na jioni.
(63) Hiyo ndiyo Pepo tutayowarithisha katika waja wetu wale waliokuwa wachamungu.
(64) (Nao watasema:) Wala hatuteremki isipokuwa kwa amri ya Mola wako Mlezi. Ni yake Yeye yaliyoko mbele yetu na yaliyoko nyuma yetu, na yaliyomo katikati ya hayo. Na Mola wako Mlezi si mwenye kusahau.
(65) Mola Mlezi wa mbingu na ardhi na vilivyo baina yake. Basi muabudu Yeye tu, na usubiri katika kumuabudu. Je, unajua chochote kilicho sawa naye?
(66) Na mwanadamu husema: Hivyo, nitakapokufa, ni kweli nitafufuliwa niwe hai tena?
(67) Je, hakumbuki mwanadamu ya kwamba hakika tulimuumba kabla, na wala hakuwa chochote?
(68) Basi ninaapa kwa Mola wako Mlezi! Kwa yakini tutawakusanya wao pamoja na mashetani. Kisha tutawahudhurisha kuizunguka Jahannamu huku wamepiga magoti!
(69) Kisha kwa yakini tutaondoa kutoka katika kila kundi wale miongoni mwao waliozidi kumuasi Arrahmani (Mwingi wa Rehema).
(70) Tena hakika Sisi tunawajua vyema zaidi wanaostahiki kuunguzwa humo.
(71) Wala hapana yeyote katika nyinyi isipokuwa ataifikia. Hiyo ni hukumu ya Mola wako Mlezi ambayo lazima itimizwe.
(72) Kisha tutawaokoa sawasawa wale waliomcha Mungu; na tutawaacha madhalimu humo huku wamepiga magoti.
(73) Na wanaposomewa Aya zetu zilizo wazi, wale waliokufuru huwaambia wale walioamini: Ni lipi katika makundi mawili haya lenye cheo kizuri na lilio zuri zaidi barazani?
(74) Na kaumu ngapi tuliziangamiza zilizokuwa na mapambo mazuri zaidi na wazuri zaidi katika muonekano!
(75) Sema: Yule aliye katika upotofu, basi Arrahmani (Mwingi wa rahema) na amuongezee (muda, mali na mengineyo) mpaka atakapoona yale waliyoahidiwa - ima ni adhabu au ni Saa, hapo ndipo watakapojua ni nani mwenye makao maovu zaidi na mwenye jeshi dhaifu zaidi.
(76) Na Mwenyezi Mungu huwazidishia wale walioongoka uwongofu. Na mema yenye kubakia ni bora katika malipo mbele ya Mola wako Mlezi na yana marejeo mema.
(77) Je, umemwona aliyezikufuru Ishara zetu na akasema: Kwa hakika mimi nitapewa mali na wana!
(78) Kwani yeye amepata habari za ghaibu, au amechukua ahadi kwa Arrahmani (Mwingi wa Rehema)?
(79) Hasha! Tutaandika anayoyasema, na tutamuongezea sawasawa katika adhabu.
(80) Na tutamrithi hayo anayoyasema, na atatujia mtupu peke yake!
(81) Na walichukua miungu mingine badala ya Mwenyezi Mungu ili ati iwape nguvu.
(82) Sivyo kabisa! Wataikataa hiyo ibada yao, na watakuwa ndio dhidi yao.
(83) Kwani huoni ya kwamba tumewatuma mashetani kwa makafiri wawachochee sawasawa?
(84) Basi usiwafanyie haraka. Sisi tunawahisabia idadi ya siku zao.
(85) Siku tutakayowakusanya wachamungu kuwapeleka kwa Arrahmani (Mwingi wa rehema) kuwa ni wageni wake.
(86) Na tukawaswaga wahalifu kwenda katika Jahannamu hali ya kuwa wana kiu.
(87) Hawatakuwa na mamlaka ya uombezi isipokuwa yule aliyechukua ahadi kwa Arrahmani (Mwingi wa rehema).
(88) Na wao ati walisema kuwa Arrahmani (Mwingi wa rehema) alijifanyia mwana!
(89) Hakika mmeleta jambo la kuchusha mno!
(90) Zinakaribia mbingu kulipuka kwa hilo, na ardhi kupasuka, na milima kuanguka vipande vipande.
(91) Kwa kudai kwao kuwa Arrahmani (Mwingi wa rehema) ana mwana.
(92) Wala Arrahmani (Mwingi wa rehema) hafailii kujichukulia mwana.
(93) Hapana yeyote aliyemo mbinguni na ardhini isipokuwa atamjia Arrahmani (Mwingi wa rehema) kuwa ni mja wake.
(94) Yeye hakika amewadhibiti na amewahesabu sawasawa.
(95) Na kila mmoja wao atamjia Siku ya Qiyama peke yake.
(96) Hakika wale walioamini na wakatenda mema, Arrahmani (Mwingi wa rehema) atawajaalia mapenzi.
(97) Na hakika tumeifanya nyepesi (Qur'ani) kwa ulimi wako, ili uwabashirie kwayo wachamungu, na uwaonye kwayo kaumu wagumu mno.
(98) Na kaumu ngapi tuliziangamiza kabla yao. Je, unawaona hata mmoja katika wao au unasikia hata mnong'ono wao?