(1) Wanaulizana kuhusu nini?
(2) Kuhusu Ile habari kuu.
(3) Ambayo kwayo wanahitalifiana.
(4) La! Karibu watakuja jua.
(5) Tena la! Karibu watakuja jua.
(6) Kwani hatukuifanya ardhi kama tandiko?
(7) Na milima kama vigingi?
(8) Na tukakuumbeni kwa jozi?
(9) Na tukakufanya kulala kwenu ni mapumziko?
(10) Na tukaufanya usiku ni nguo?
(11) Na tukaufanya mchana ni wa kuchumia maisha?
(12) Na tukajenga juu yenu saba zenye nguvu?
(13) Na tukaifanya taa yenye mwanga na joto.
(14) Na tukateremsha maji yanayoanguka kwa kasi kutoka mawinguni.
(15) Ili tutoe kwayo nafaka na mimea.
(16) Na mabustani yenye miti iliyokamatana.
(17) Hakika siku ya uamuzi imewekewa wakati wake.
(18) Siku litakapopulizwa barugumu, nanyi mtakuja kwa makundi.
(19) Na mbingu zitafunguliwa, ziwe milango.
(20) Na milima itaondolewa na itakuwa kama sarabi.
(21) Hakika Jahannamu inangojea!
(22) Kwa walioasi ndio makazi yao.
(23) Wakae humo karne baada ya karne.
(24) Hawataonja humo chochote kibaridi wala kinywaji.
(25) Ila maji ya moto sana na usaha.
(26) Ndio malipo mwafaka.
(27) Hakika hao hawakuwa wakitaraji kuwa kuna hesabu (juu ya matendo yao).
(28) Na wakakanusha Aya zetu kwa nguvu.
(29) Na kila kitu Sisi tumekidhibiti kwa kukiandika.
(30) Basi onjeni! Nasi hatutakuzidishieni ila adhabu!
(31) Hakika wacha Mungu wanastahiki kufuzu.
(32) Mabustani na mizabibu.
(33) Na wake wazuri waliolingana nao.
(34) Na bilauri zilizojaa.
(35) Hawatasikia humo upuuzi wala uongo.
(36) Malipo kutoka kwa Mola wako Mlezi, kipawa cha kutosha.
(37) Mola Mlezi wa mbingu na ardhi na vilivyo baina yake, Arrahman (Mwingi wa rehema); hawamiliki usemi mbele yake!
(38) Siku atakaposimama Roho na Malaika kwa safu. Hawatasema ila yule ambaye Mwingi wa rehema atamruhusu, na atasema yaliyo sawa tu.
(39) Hiyo ndiyo Siku ya haki. Basi anayetaka, na ashike njia arejee kwa Mola wake Mlezi.
(40) Hakika tumekuhadharisheni adhabu iliyo karibu kufika; Siku ambayo mtu ataona yale yaliyotangulizwa na mikono yake; na kafiri atasema: Laiti ningelikuwa udongo!