(1) Ninaapa kwa wanaojipanga kwa safu.
(2) Na kwa wenye kukataza mabaya.
(3) Na kwa wenye kusoma Ukumbusho.
(4) Hakika mungu wenu bila ya shaka ni Mmoja.
(5) Mola Mlezi wa mbingu na ardhi, na yaliyomo kati yao, na ni Mola Mlezi wa mashariki zote.
(6) Hakika Sisi tumeipamba mbingu ya karibu kwa pambo la nyota.
(7) Na kulinda na kila shetani muasi.
(8) Wasiweze kuwasikiliza viumbe watukufu. Na wanafukuzwa huko kila upande.
(9) Wakifurushwa. Na wanayo adhabu ya kudumu.
(10) Isipokuwa anayenyakua kitu kidogo, na mara humfwatia kimondo kinachong'ara.
(11) Hebu waulize: Je! Wao ni wenye umbo gumu zaidi au hao wengine tuliowaumba. Hakika Sisi tuliwaumba wao kwa udongo unaonata.
(12) Bali unastaajabu, na wao wanafanya masihara.
(13) Na wanapokumbushwa, hawakumbuki.
(14) Na wanapoona Ishara, wanafanya masihara.
(15) Na husema: Haya si chochote isipokuwa ni uchawi tu ulio dhahiri.
(16) Ati tukishakufa na tukawa udongo na mifupa ndio kweli tutafufuliwa?
(17) Hata baba zetu wa zamani?
(18) Sema: Naam! Hali nanyi ni madhalili.
(19) Huko utapigwa ukelele mmoja tu! Na hapo ndipo wataona!
(20) Watasema: Ole wetu! Hii ndiyo Siku ya Malipo.
(21) Hii ndiyo Siku ya Hukumu mliyokuwa mkiikadhibisha.
(22) Wakusanyeni wale waliodhulumu, na wake zao, na hao ambao wao waliokuwa wakiwaabudu.
(23) Badala ya Mwenyezi Mungu. Waongozeni njia ya Jahannamu!
(24) Na wasimamisheni. Hakika hao wataulizwa:
(25) Mna nini? Mbona hamsaidiani?
(26) Bali hii leo, watasalimu amri.
(27) Wataelekeana wao kwa wao kuulizana.
(28) Watasema: Kwa hakika nyinyi mlikuwa mkitujia upande wa kulia.
(29) Watasema (wakubwa): Bali nyinyi wenyewe hamkuwa Waumini.
(30) Sisi hatukuwa na mamlaka juu yenu, bali nyinyi wenyewe mlikuwa wapotovu.
(31) Basi hukumu ya Mola wetu Mlezi imekwisha tuthibitikia. Hakika bila ya shaka tutaonja tu adhabu.
(32) Tulikupotezeni kwa sababu sisi wenyewe tulikuwa wapotovu.
(33) Basi wao kwa hakika siku hiyo watashirikiana katika adhabu pamoja.
(34) Hivyo ndivyo tutakavyowafanyia wahalifu.
(35) Wao walipokuwa wakiambiwa La ilaha illa 'Llahu (Hapana mungu ila Mwenyezi Mungu tu), wanajivuna.
(36) Na wakisema: Hivyo sisi tuiache miungu yetu kwa ajili ya huyu mtunga mashairi mwendawazimu?
(37) Bali huyu amekuja kwa haki, na amewasadikisha Mitume.
(38) Hakika nyinyi bila ya shaka mtaionja adhabu chungu.
(39) Wala hamlipwi isipokuwa hayo mliyokuwa mkiyafanya.
(40) Isipokuwa waja wa Mwenyezi Mungu waliohitariwa.
(41) Hao ndio watakaopata riziki maalumu.
(42) Matunda, nao wataheshimiwa.
(43) Katika Bustani za neema.
(44) Wako juu ya viti wameelekeana.
(45) Wanazungushiwa kikombe chenye kinywaji cha chemchemi.
(46) Kinywaji cheupe, kitamu kwa wanywao.
(47) Hakina madhara, wala hakiwaleweshi.
(48) Na watakuwa nao wanawake wenye macho ya staha, mazuri.
(49) Hao wanawake kama mayai yaliyohifadhika.
(50) Basi wakaelekeeana kuulizana wenyewe kwa wenyewe.
(51) Aseme msemaji mmoja miongoni mwao: Hakika mimi nilikuwa na rafiki.
(52) Aliyekuwa akinambia: Hivyo wewe ni katika wanaosadiki.
(53) Ati tukishakufa tukawa udongo na mafupa, ndiyo tutalipwa na kufanyiwa hesabu?
(54) Atasema: Je, nyie mnawaona?
(55) Basi atachungulia amwone katikati ya Jahannamu.
(56) Atasema: Wallahi! (Naapa kwa jina la Mwenyezi Mungu) Ulikaribia sana kunipoteza.
(57) Na lau kuwa si neema ya Mola wangu Mlezi, bila ya shaka ningelikuwa miongoni mwa waliohudhurishwa.
(58) Je, Sisi hatutakufa?
(59) Isipokuwa kifo chetu cha kwanza? Wala sisi hatutaadhibiwa.
(60) Hakika huku bila ya shaka ndiko kufuzu kukubwa.
(61) Kwa mfano wa haya na watende watendao.
(62) Je, kukaribishwa hivi si ndiyo bora, au mti wa Zaqqum?
(63) Hakika Sisi tumeufanya huo kuwa ni mateso kwa waliodhulumu.
(64) Hakika huo ni mti unaotoka katikati ya Jahannamu.
(65) Mashada ya matunda yake kama kwamba ni vichwa vya mashetani.
(66) Basi hakika bila ya shaka hao watayala hayo, na wajaze matumbo kwayo.
(67) Kisha juu yake wanyweshwe mchanganyo wa maji ya moto yaliyochemka.
(68) Kisha hakika marejeo yao bila ya shaka yatakuwa kwenye Jahannamu.
(69) Hakika waliwakuta baba zao wamepotea.
(70) Na wao wakafanya haraka kufuata nyayo zao.
(71) Na bila ya shaka walikwisha potea kabla yao wengi wa watu wa zamani.
(72) Na Sisi hakika tuliwapelekea waonyaji.
(73) Basi hebu angalia ulikuwaje mwisho wa walioonywa.
(74) Isipokuwa waja wa Mwenyezi Mungu waliohitariwa.
(75) Na hakika Nuhu alituita, na Sisi ni bora wa waitikiaji.
(76) Na tulimwokoa yeye na ahali zake kutokana na msiba mkubwa.
(77) Na tuliwajaalia dhuria zake ndio wenye kubakia.
(78) Na tukamwachia (sifa njema) kwa waliokuja baadaye.
(79) Iwe salama kwa Nuhu ulimwenguni kote!
(80) Kwa hakika hivi ndivyo tunavyowalipa wanaofanya mema.
(81) Hakika yeye ni katika waja wetu walioamini.
(82) Kisha tukawazamisha wale wengine.
(83) Na hakika Ibrahim alikuwa katika kundi lake.
(84) Alipomjia Mola wake Mlezi kwa moyo mzima.
(85) Alimwambia baba yake na watu wake: Mnaabudu nini?
(86) Kwa kuzua tu mnataka miungu mingine badala ya Mwenyezi Mungu?
(87) Mnamdhania nini Mola Mlezi wa walimwengu wote?
(88) Kisha akapiga jicho kutazama nyota.
(89) Akasema: Hakika mimi ni mgonjwa!
(90) Nao wakamwacha, wakampa kisogo.
(91) Basi akaiendea miungu yao kwa siri, akaiambia: Mbona hamli?
(92) Mna nini hata hamsemi?
(93) Kisha akaigeukia kuipiga kwa mkono wa kulia.
(94) Basi wakamjia upesi upesi.
(95) Akasema: Hivyo mnaviabudu vitu mnavyovichonga wenyewe?
(96) Na hali Mwenyezi Mungu ndiye aliyekuumbeni nyinyi na hivyo mnavyovifanya!
(97) Wakasema: Mjengeeni jengo, na kisha mtupeni motoni humo!
(98) Basi walitaka kumfanyia vitimbi, lakini tukawafanya wao ndio wa chini zaidi.
(99) Na akasema: Hakika mimi nahama, nakwenda kwa Mola wangu Mlezi; Yeye ataniongoa.
(100) Ewe Mola wangu Mlezi! Nitunukie aliye miongoni mwa watenda mema.
(101) Basi tukambashiria mwana aliye mpole.
(102) Basi alipofika makamo ya kwenda na kurudi pamoja naye, alimwambia: Ewe mwanangu! Hakika mimi nimeona usingizini kuwa ninakuchinja. Basi angalia wewe, waonaje? Akasema: Ewe baba yangu! Tenda unavyoamrishwa, utanikuta mimi, Insha Allah (Mwenyezi Mungu akipenda), katika wanaosubiri.
(103) Basi wote wawili walipojisalimisha, na akamlaza juu ya kipaji.
(104) Tulimwita: Ewe Ibrahim!
(105) Umekwisha itimiliza ndoto. Hakika hivi ndivyo tunavyowalipa wanaotenda mema.
(106) Hakika haya ni majaribio yaliyo dhahiri.
(107) Basi tukamtolea fidia kwa dhabihu mtukufu.
(108) Na tukamwachia (sifa njema) kwa watu waliokuja baadaye.
(109) Iwe salama kwa Ibrahim!
(110) Hivi ndivyo tunavyowalipa wanaofanya mema.
(111) Hakika yeye ni katika waja wetu walioamini.
(112) Na tukambashiria kuzaliwa Is-haqa, naye ni Nabii miongoni mwa watu wema.
(113) Na tukambarikia yeye na Is-haqa. Na miongoni mwa dhuria zao walitokea wema na wenye kudhulumu nafsi zao waziwazi.
(114) Na kwa hakika tuliwafanyia hisani Musa na Haruni.
(115) Na tukawaokoa wao na watu wao kutokana na dhiki kubwa.
(116) Na tukawanusuru; na wakawa wao ndio wenye kushinda.
(117) Na tukawapa wawili hao Kitabu kinachobainisha.
(118) Na tukawaongoa kwenye njia iliyonyooka.
(119) Na tukawaachia (sifa njema) katika watu waliokuja baadaye.
(120) Iwe salama kwa Musa na Haruni!
(121) Hakika hivyo ndivyo tunavyowalipa walio wema.
(122) Hakika wawili hao ni katika waja wetu walioamini.
(123) Na hakika Ilyas bila ya shaka alikuwa miongoni mwa Mitume.
(124) Alipowaambia watu wake: Hamumchi Mungu?
(125) Mnamwomba Baa'li na mnamwacha Mbora wa waumbaji.
(126) Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wenu na Mola Mlezi wa baba zenu wa zamani?
(127) Wakamkadhibisha. Basi kwa hakika watahudhurishwa.
(128) Isipokuwa waja wa Mwenyezi Mungu waliosafishwa.
(129) Na tumemwachia (sifa nzuri) kwa waliokuja baadaye.
(130) Iwe salama kwa Ilyas.
(131) Hakika hivyo ndivyo tunavyowalipa walio wema.
(132) Hakika yeye ni katika waja wetu walioamini.
(133) Na hakika Lut'i bila ya shaka ni miongoni mwa Mitume.
(134) Tulipomwokoa yeye na ahali zake wote.
(135) Isipokuwa mwanamke mkongwe katika wale waliobakia nyuma.
(136) Kisha tukawaangamiza wale wengineo.
(137) Na hakika nyinyi mnawapitia wakati wa asubuhi.
(138) Na usiku. Basi je, hamyatii akilini?
(139) Na hakika Yunus alikuwa miongoni mwa Mitume.
(140) Alipokimbia akenda katika jahazi lililosheheni.
(141) Akaingia katika kupigiwa kura, na akawa katika walioshindwa.
(142) Samaki akammeza hali ya kuwa ni mwenye kulaumiwa.
(143) Na ingelikuwa hakuwa katika wanaomtakasa Mwenyezi Mungu.
(144) Bila ya shaka angelikaa ndani yake mpaka siku ya kufufuliwa.
(145) Lakini tulimtupa ufukweni patupu, hali yu mgonjwa.
(146) Na tukauotesha juu yake mmea wa aina ya mung'unye.
(147) Na tulimtuma kwa watu laki moja au zaidi.
(148) Basi wakaamini, na tukawastarehesha kwa muda.
(149) Basi waulize: Ati Mola wako Mlezi ndiye mwenye watoto wa kike, na wao wanao watoto wa kiume?
(150) Au tumewaumba Malaika kuwa ni wanawake, na wao wakashuhudia?
(151) Ati ni kwa uzushi wao ndio wanasema.
(152) Mwenyezi Mungu amezaa! Ama hakika bila ya shaka hao ni waongo!
(153) Ati amehiari watoto wa kike kuliko wanaume?
(154) Mna nini? Mnahukumu vipi nyinyi?
(155) Hamkumbuki?
(156) Au mnayo hoja iliyo wazi?
(157) Basi leteni Kitabu chenu kama nyinyi ni wakweli.
(158) Na wameweka mahusiano ya nasaba baina yake na majini; na majini wamekwisha jua bila ya shaka kuwa wao watahudhurishwa.
(159) Ametakasika Mwenyezi Mungu mbali na hayo wanayomsingizia.
(160) Isipokuwa waja wa Mwenyezi Mungu waliosafishwa.
(161) Basi hakika nyinyi na mnaowaabudu.
(162) Hamwezi kuwapoteza.
(163) Isipokuwa yule atakayeingia Motoni.
(164) Na hapana katika sisi ila anapo mahali pake maalumu.
(165) Na hakika bila ya shaka sisi ndio wajipangao safu.
(166) Na hakika sisi ndio wenye kusabihi kutakasa.
(167) Na walikuwapo waliokuwa wakisema.
(168) Tungelikuwa na Ukumbusho kama wa watu wa zamani.
(169) Bila ya shaka tungelikuwa ni waja wa Mwenyezi Mungu wenye kumkusudia Yeye tu.
(170) Lakini waliukufuru. Basi watakuja jua.
(171) Na bila ya shaka neno letu lilikwisha tangulia kwa waja wetu waliotumwa.
(172) Ya kuwa wao bila ya shaka ndio watakaonusuriwa.
(173) Na kwamba jeshi letu ndilo litakaloshinda.
(174) Basi waachilie mbali kwa muda.
(175) Na watazame, nao wataona.
(176) Je, wanaiharakishia adhabu yetu?
(177) Basi itakaposhuka uwanjani kwao, itakuwa asubuhi mbaya kwa walioonywa.
(178) Na waache kwa muda.
(179) Na tazama, na wao wataona.
(180) Ametakasika Mola wako Mlezi Mwenye utukufu mbali na yale wanayomzulia.
(181) Na Salamu juu ya Mitume.
(182) Na sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu Mola Mlezi wa walimwengu wote.