(1) Nuun. Ninaapa kwa kalamu na yale wayaandikayo.
(2) Kwa neema ya Mola wako Mlezi wewe si mwendawazimu.
(3) Na kwa hakika wewe una malipo yasiyokatika.
(4) Na hakika wewe una tabia tukufu.
(5) Karibu utaona, na wao wataona.
(6) Ni nani kati yenu aliyepandwa na wazimu.
(7) Hakika Mola wako Mlezi ndiye Yeye ajuaye zaidi nani aliyeipotea Njia yake, na Yeye ndiye anayewajua zaidi walioongoka.
(8) Basi usiwatii wanaokadhibisha.
(9) Wanatamani lau ungelainisha ili nao wakulainishie.
(10) Wala usimtii kila mwingi wa kuapa wa kudharauliwa.
(11) Mtapitapi, apitaye akifitini.
(12) Mwenye kuzuia mno heri, dhalimu, mwingi wa madhambi.
(13) Mkavu, na juu ya hayo, mshari, amejipachika tu.
(14) Ati kwa kuwa ana mali na watoto!
(15) Anaposomewa Aya zetu, husema: Hizi ni simulizi za uongo za watu wa zamani!
(16) Tutamtia kovu juu ya pua yake.
(17) Hakika tumewajaribu hawa kama tulivyowajaribu wale wenye shamba, walipoapa kwamba watayavuna mazao yake itakapokuwa asubuhi.
(18) Wala hawakusema: Mungu akipenda!
(19) Basi lilitokea tukio juu yake kutoka kwa Mola wako Mlezi, nao wamelala!
(20) Likawa kama usiku wa giza.
(21) Asubuhi wakaitana.
(22) Ya kwamba nendeni kondeni mwenu ikiwa mnataka kuvuna.
(23) Basi walikwenda na huku wakinong'onezana.
(24) Ya kuwa leo hata masikini mmoja asikuingilieni.
(25) Na walikwenda asubuhi, nao wameshikilia azimio hilo.
(26) Basi walipoliona, wakasema: Hakika tumepotea!
(27) Bali tumenyimwa!
(28) Mbora wao akasema: Sikukwambieni, kwa nini hamumtakasi Mwenyezi Mungu?
(29) Wakasema: Ametakasika Mola wetu Mlezi! Hakika sisi tulikuwa wenye kudhulumu.
(30) Basi wakakabiliana kulaumiana wao kwa wao.
(31) Wakasema: Ole wetu! Tulikuwa tumeikiuka mipaka!
(32) Asaa Mola wetu Mlezi akatubadilishia lililo bora kuliko hili. Hakika sisi ni wenye kurejea kwa Mola wetu Mlezi.
(33) Namna hivi yanakuwa mateso, na bila ya shaka mateso ya Akhera ni makubwa zaidi, laiti wangeli jua!
(34) Hakika wacha Mungu watakuwa na Bustani za neema kwa Mola wao Mlezi.
(35) Kwani tutawafanya Waislamu kama wakosefu?
(36) Mna nini? Mnahukumu vipi?
(37) Au mnacho kitabu ambacho ndani yake mnasoma?
(38) Kuwa mtapata humo mnayoyapenda?
(39) Au mnazo ahadi za viapo juu yetu za kufika Siku ya Kiyama ya kuwa hakika mtapata kila mnayojihukumia?
(40) Waulize: Ni nani miongoni mwao dhamini wa haya?
(41) Au wanao washirika? Basi wawalete washirika wao wakiwa wanasema kweli.
(42) Siku utakapowekwa wazi muundi, na wataitwa kusujudu, lakini hawataweza
(43) Macho yao yatainama chini, fedheha itawafunika. Na hakika walikuwa wakiitwa wasujudu walipokuwa wazima.
(44) Basi niache na wanaokadhibisha maneno haya! Tutawavutia kidogo kidogo kutokea mahali wasipopajua.
(45) Na ninawapururia muhula; hakika hila zangu ni imara.
(46) Au unawaomba ujira, na wao wanaemewa na gharama hiyo?
(47) Au iko kwao siri, basi wao wanaiandika?
(48) Basi ingojee hukumu ya Mola wako Mlezi, wala usiwe kama mmezwa na samaki, alipo nadi naye kazongwa.
(49) Kama isingelimfikia neema kutoka kwa Mola wake Mlezi, bila ya shaka angelitupwa ufukweni naye ni mwenye kulaumiwa.
(50) Lakini Mola wake Mlezi alimteua na akamfanya miongoni mwa watu wema.
(51) Na waliokufuru hukaribia kukutelezesha kwa macho yao, wanaposikia mawaidha, na wanasema: Hakika yeye ni mwendawazimu.
(52) Na hayakuwa haya, ila ni ukumbusho kwa walimwengu wote.