(1) Ametakasika yule aliyempeleka mja wake usiku mmoja kutoka katika Msikiti Mtakatifu mpaka Msikiti wa Al-Aqswa, ambao tumebariki kandoni mwake, ili tumuonyeshe katika Ishara zetu. Hakika Yeye ndiye Mwenye kusikia zaidi, Mwenye kuona zaidi.
(2) Na tulimpa Musa Kitabu na tukakifanya kuwa ni uwongofu kwa Wana wa Israili. (Tukawambia) kwamba msimfanye yeyote asiyekuwa mimi kuwa mtegemewa wenu.
(3) Kizazi cha wale tuliowabeba pamoja na Nuhu. Hakika yeye alikuwa mja wa kushukuru sana.
(4) Na tukawahukumia Wana wa Israili katika kitabu kwamba hakika mtafanya uharibifu katika ardhi mara mbili, na hakika mtapanda kiburi, kiburi kikubwa.
(5) Na itakapokuja ahadi ya kwanza yake, tutawatumia waja wetu wenye nguvu kubwa. Watawaingilia ndani ya majumba. Na hii ilikuwa ahadi iliyotimizwa.
(6) Kisha tukawarudishia nguvu zenu dhidi yao, na tukawasaidia kwa mali na wana, na tukawajalia mkawa wengi zaidi.
(7) Mkifanya wema, mnafanyia wema nafsi zenu. Na mkifanya ubaya, basi mnajifanyia wenyewe. Na ikifika ahadi ya mwisho ili waziharibu nyuso zenu na waingie msikitini kama walivyoingia mara ya kwanza na waharibu kila walichokiteka kwa uharibifu mkubwa.
(8) Huenda Mola wenu Mlezi akawarehemu, na mkirudia, na sisi tutarudia. Na tumeifanya Jahannam kuwa ni gereza kwa ajili ya makafiri.
(9) Hakika hii Qur-ani inaongoa kwenye yale yaliyonyooka kabisa, na inawabashiria Waumini ambao wanatenda mema ya kwamba wana malipo makubwa.
(10) Na ya kwamba wale wasioiamini Akhera tumewaandalia adhabu chungu.
(11) Na mtu huomba maovu kama vile aombavyo heri, kwani mtu ni mwenye pupa mno.
(12) Na tumefanya usiku na mchana kuwa ishara mbili. Tena tukaifuta ishara ya usiku, na tukaifanya ishara ya mchana ni yenye mwangaza ili mtafute fadhila itokayo kwa Mola wenu Mlezi, na ili mpate kujua idadi ya miaka na hesabu. Na kila kitu tumekifafanua kwa kina waziwazi.
(13) Na kila mtu tumemfungia matendo yake shingoni mwake. Na Siku ya Qiyama tutamtolea kitabu atakachokikuta ki wazi kimekunjuliwa.
(14) Ataambiwa: Soma kitabu chako! Nafsi yako inakutosha leo kukuhesabu.
(15) Anayeongoka, basi anaongoka kwa ajili ya nafsi yake. Na anayepotea, basi anapotea kwa hasara yake mwenyewe. Wala habebi mbebaji mzigo wa mwengine. Wala Sisi hatuadhibu mpaka tumtume Mtume.
(16) Na pindi tukitaka kuuteketeza mji, tunawaamrisha wale wana starehe na taanusi wake, lakini wao wakaendelea kutenda maovu humo. Basi hapo kauli ikathibiti juu ya mji huo, nasi tukauangamiza kwa maangamizo makubwa.
(17) Na kaumu ngapi tumeziangamiza baada ya Nuhu! Na Mola wako Mlezi anatosha kabisa kuwa ni Mwenye kuzijua na kuziona dhambi za waja wake.
(18) Anayetaka yapitayo upesi upesi, tutafanya haraka kumletea hapa hapa tunayoyataka kwa tumtakaye. Kisha tumemwekea Jahannamu, ataingia humo hali ya kuwa ni mwenye kulaumiwa na kufurushwa.
(19) Na anayeitaka Akhera, na akaifanyia juhudi ipasavyo ilhali ni Muumini, basi hao juhudi zao zitakuwa ni za kushukuriwa.
(20) Wote hao tunawakunjulia, hawa na hao, katika vipawa vya Mola wako Mlezi. Wala vipawa vya Mola wako Mlezi havizuiliki.
(21) Angalia vipi tulivyowafadhilisha baadhi yao kuliko wengine wao. Na hakika Akhera ni yenye daraja kubwa zaidi na fadhila kubwa zaidi.
(22) Usimfanye mungu mwengine pamoja na Mwenyezi Mungu, ukaja ukawa wa kulaumiwa uliyetupika.
(23) Na Mola wako Mlezi ameamrisha kuwa msimuabudu yeyote ila Yeye tu, na wazazi wawili muwatendee wema. Mmoja wao akifikia uzee, naye yuko kwako, au wote wawili, basi usimwambie hata, Ah! Wala usiwakemee. Na uwaambie maneno ya heshima.
(24) Na uwainamishie bawa la unyenyekevu kwa kuwaonea rehema. Na useme: Mola wangu Mlezi! Warehemu kama walivyonilea utotoni.
(25) Mola wenu Mlezi anajua kabisa yaliyo nyoyoni mwenu. Ikiwa nyinyi mtakuwa wema, basi hakika Yeye ni Mwenye kuwaghufiria wanaorudi sana kwake.
(26) Na mpe aliye jamaa yako haki yake, na masikini, na msafiri; wala usitumie ovyo kwa fujo.
(27) Hakika wabadhirifu ni ndugu wa Mashetani. Na Shetani ni mwenye kumkufuru mno Mola wake Mlezi.
(28) Na ikiwa ukiwapa mgongo sawasawa, nawe unatafuta rehema kutoka kwa Mola wako Mlezi unayoitaraji, basi sema nao maneno laini.
(29) Wala usiufanye mkono wako kama uliofungwa shingoni mwako, wala usiukunjue wote kabisa, ukabaki ukilaumiwa muflisi.
(30) Hakika Mola wako Mlezi humkunjulia riziki amtakaye, na humpimia amtakaye. Hakika Yeye kwa waja wake ni Mwenye kuwajua na kuwaona vyema.
(31) Wala msiwaue wana wenu kwa kuogopa umasikini. Sisi tunawaruzuku wao na nyinyi. Hakika kuwaua hao kulikuwa ni kosa kubwa.
(32) Wala msikaribie uzinzi. Hakika huo ni uchafu na njia mbaya.
(33) Wala msiuwe nafsi ambayo Mwenyezi Mungu amekataza isipokuwa kwa haki. Na aliyeuliwa kwa kudhulumiwa, basi hakika tumempa msimamizi wake mamlaka. Lakini asipitilize kiasi katika kuua. Kwani yeye anasaidiwa.
(34) Wala msiyakaribie mali ya yatima, isipokuwa kwa njia iliyo nzuri zaidi, mpaka afike utu uzimani. Na timizeni ahadi. Kwa hakika ahadi itaulizwa.
(35) Na timizeni kipimo mnapopima. Na pimeni kwa mizani zilizo sawa. Hayo ni heri na yenye mwisho bora.
(36) Wala usiyafuate usiyo na elimu nayo. Hakika kusikia, na kuona, na moyo hivyo vyote itaulizwa juu yake.
(37) Wala usitembee katika ardhi kwa maringo. Hakika wewe huwezi kuipasua ardhi na kamwe huwezi kufikia urefu wa milima.
(38) Hayo yote ubaya wake ni wenye kuchukiza kwa Mola wako Mlezi.
(39) Hayo ni katika hekima alizokufunulia Mola wako Mlezi. Wala usimweke pamoja na Mwenyezi Mungu mungu mwengine, ukaja ukatupwa katika Jahannamu ukilaumiwa na kufurushwa.
(40) Je, Mola wenu Mlezi amewateulia nyinyi wavulana, na Yeye akawafanya Malaika ni banati zake? Kwa hakika nyinyi mnasema kauli kubwa.
(41) Na tumekwisha bainisha katika Qur'ani hii ili wapate kukumbuka. Lakini haikuwazidisha ila kuwa mbali nayo.
(42) Sema: Lau kuwa wangelikuwa pamoja naye miungu mingine kama wasemavyo, basi wangelitafuta njia ya kumfikia Mwenye Kiti cha Enzi.
(43) Subhanahu Wa Taa'la, (Ametakasika na Ametukuka juu) kabisa na hayo wanayoyasema.
(44) Zinamtakasa zote mbingu saba na ardhi na vyote vilivyomo ndani yake. Na hapana kitu ila kinamtakasa kwa sifa zake. Lakini nyinyi hamfahamu kutakasa kwake. Hakika Yeye ni Mpole na Mwenye maghfira.
(45) Na unaposoma Qur-ani, tunaweka baina yako na wale wasioiamini Akhera pazia linalowafunika.
(46) Na tunaweka vifuniko juu ya nyoyo zao wasije wakaifahamu, na tunaweka kwenye masikio yao uziwi. Na unapomtaja katika Qur-ani Mola wako Mlezi peke yake, basi wao hugeuka nyuma wakaenda zao.
(47) Sisi tunajua vyema kabisa sababu wanayosikilizia wanapokusikiliza, na wanaponong'ona. Wanaposema hao madhalimu: Nyinyi hamumfuati isipokuwa mwanamume aliyerogwa.
(48) Tazama jinsi walivyokupigia mifano. Basi wakapotea. Kwa hivyo hawawezi kuipata njia.
(49) Na walisema: Je! Tutakapokuwa mifupa na mapande yaliyovurugika, tutafufuliwa kwa umbo jipya?
(50) Sema: Kuweni hata mawe na chuma.
(51) Au umbo lolote mnaloliona kubwa katika vifua vyenu. Watasema: Nani atakayeturudisha tena? Sema: Yule yule aliyewaumba mara ya kwanza! Watakutikisia vichwa vyao, na watasema: Ni lini hayo? Sema: Labda huenda itakuwa hivi karibuni!
(52) Siku atakapowaita, nanyi mtamuitikia kwa kumsifu, na mtaadhani kuwa hamkukaa isipokuwa muda mdogo tu.
(53) Waambie waja wangu waseme maneno mazuri, kwa maana hakika Shetani huchochea ugomvi baina yao. Hakika Shetani ni adui aliye dhahiri kwa mwanadamu.
(54) Mola wenu Mlezi anawajua vilivyo. Akitaka, atawarehemu, na akitaka, atawaadhibu. Na hatukukutuma ili uwe msimamizi wao.
(55) Na Mola wako Mlezi anawajua vilivyo waliomo mbinguni na katika ardhi. Na hakika tumewafadhilisha baadhi ya Manabii kuliko wengine, na Daudi tulimpa Zaburi.
(56) Sema: Waombeni hao mnaowadai badala yake Yeye. Hawawezi kuwaondolea madhara, wala kuyaweka pengine.
(57) Hao ambao wao wanaowaomba, wao wenyewe wanatafuta njia ya kwendea kwa Mola wao Mlezi hata miongoni mwao walio karibu mno, na wanataraji rehema zake, na wanaihofu adhabu yake. Hakika adhabu ya Mola wako Mlezi yafaa kutahadhariwa.
(58) Na hapana mji wowote ila Sisi tutauteketeza kabla ya Siku ya Kiyama, au tutaupa adhabu kali. Haya yamekwisha andikwa katika Kitabu.
(59) Na hapana kinachotuzuia kupeleka miujiza ila ni kuwa watu wa zamani waliikanusha. Na tuliwapa Wathamudi ngamia jike kuwa ni Ishara iliyo dhaahiri, lakini walidhulumu kwaye. Nasi hatutumii Ishara isipokuwa kwa ajili ya kuhofisha.
(60) Na tulipokwambia: Hakika Mola wako Mlezi amekwisha wazunguka hao watu. Na hatukuifanya ndoto tuliyokuonyesha isipokuwa ni kuwajaribu watu, na mti uliolaaniwa katika Qur-ani. Na tunawahofisha, lakini haiwazidishii isipokuwa uasi mkubwa.
(61) Na pale tulipowaambia Malaika, "Msujudieni Adam." Wakamsujudia isipokuwa Iblisi. Akasema, "Je, nimsujudie uliyemuumba kwa udongo?"
(62) Akasema, "Hebu unamuona huyu uliyemtukuza zaidi yangu, ukiniahirisha mpaka Siku ya Qiyama, hapana shaka nitawaangamiza dhuria zake isipokuwa wachache tu."
(63) Akasema Mwenyezi Mungu, "Nenda! Na atakayekufuata katika wao, basi hakika Jahannamu itakuwa ndiyo malipo yenu, malipo yaliyo mengi."
(64) Na wachochee uwawezao katika wao kwa sauti yako, na wakusanyie jeshi lako la wapandao farasi na waendao kwa miguu. Na shirikiana nao katika mali na wana, na waahidi. Na Shetani hawapi ahadi isipokuwa ya udanganyifu.
(65) Hakika wewe huna mamlaka yoyote juu ya waja wangu. Na Mola wako Mlezi anatosha kuwa ni Mtegemewa.
(66) Mola wenu Mlezi ndiye anayewaendeshea marikebu katika bahari ili mtafute katika fadhila zake. Hakika Yeye ni Mwingi kuwarehemu nyinyi.
(67) Na inapowakuta taabu katika bahari, hao mnaowaomba wanapotea, isipokuwa Yeye tu. Na anapowaokoa mkafika nchi kavu, mnageuka. Ama mwanadamu ni mwingi wa kukufuru.
(68) Je, mna amani ya kuwa hatawadidimiza katika upande wowote katika nchi kavu, au kwamba hatawatumia tufani la kokoto? Kisha msipate yeyote wa kumtegemea.
(69) Au mna amani ya kuwa hatawarudisha humo mara nyingine na akawatumia kimbunga cha upepo akawazamisha kwa mlivyokufuru, na kisha msipate wa kuwanusuru kutokana nasi.
(70) Na hakika tumewatukuza wanadamu, na tukawabeba katika nchi kavu na baharini, na tukawaruzuku katika vitu vizuri vizuri, na tukawafadhilisha kwa fadhila kubwa kuliko wengi miongoni mwa wale tuliowaumba.
(71) Siku tutakapowaita kila kikundi cha watu kwa mujibu wa wakifuatacho, basi atakayepewa kitabu chake kwa mkono wake wa kulia, basi hao watasoma kitabu chao wala hawatadhulumiwa hata chembe.
(72) Na yule ambaye ni kipofu hapa, basi atakuwa kipofu Akhera, na atakuwa ndiye mpotovu zaidi wa Njia.
(73) Na hakika walikaribia kukushawishi uache hayo tuliyokufunulia ili utuzulie mengineyo. Na hapo, ndipo wangelikufanya mwandani.
(74) Na lau kuwa hatukukuweka imara, ungelikaribia kuwaegemea kidogo.
(75) Hapo basi bila ya shaka, tungelikuonjesha adhabu maradufu ya uhai, na adhabu maradufu ya kifo. Kisha usingepata yeyote wa kukunusuru kutokana nasi.
(76) Na walitaka kukukera ili wakutoe nchini. Na hapo, wao wasingelibakia humo isipokuwa kwa muda mchache tu.
(77) Hiyo ndiyo desturi ya Mitume tuliowatuma kabla yako. Wala hutapata mabadiliko katika desturi yetu.
(78) Simamisha Swala jua linapopinduka mpaka giza la usiku, na Qur-ani ya alfajiri. Hakika Qur-ani ya alfajiri inashuhudiwa daima.
(79) Na amka usiku kwa ibada, ni ziada ya sunna hasa kwako wewe. Huenda Mola wako Mlezi akakunyanyua cheo kinachosifika.
(80) Na sema, "Mola wangu Mlezi! Niingize muingizo mwema, na unitoe kutoka kwema. Na unipe nguvu zinazotoka kwako zinisaidie."
(81) Na sema, "Haki imefika, na batili imetoweka. Hakika batili lazima itoweke!"
(82) Na tunateremsha katika Qur-ani yale ambayo ni uponyaji na rehema kwa Waumini. Wala hayawazidishii madhalimu isipokuwa hasara.
(83) Na tunapomneemesha mtu, hugeuka na kujitenga kando. Na yanapomgusa maovu, hukata tamaa.
(84) Sema, "Kila mmoja anafanya kwa namna yake. Na Mola wenu Mlezi ndiye anayejua zaidi yule aliyeongoka katika njia."
(85) Na wanakuuliza habari za Roho. Sema, "Roho ni katika mambo ya Mola wangu Mlezi. Nanyi hamkupewa katika elimu isipokuwa kidogo tu."
(86) Na tungelipenda, tungeliyaondoa yale tuliyokufunulia. Kisha usingelipata mwakilishi wa kukupigania kwetu kwa haya.
(87) Isipokuwa iwe rehema itokayo kwa Mola wako Mlezi. Hakika fadhila yake kwako ni kubwa.
(88) Sema: Wangelikusanyika watu na majini ili walete mfano wa Qur-ani hii, basi hawawezi kuleta mfano wake, hata kama wakisaidiana wao kwa wao.
(89) Na hakika tumewaeleza watu katika Qur-ani hii kwa kila mfano. Lakini wengi wa watu wakakataa isipokuwa kukufuru tu.
(90) Na walisema, "Hatutakuamini mpaka ututimbulie chemchemi katika ardhi hii."
(91) Au uwe na bustani ya mitende na mizabibu, na utupitishie mito kati yake ikimiminika.
(92) Au utuangushie mbingu vipande vipande kama ulivyodai, au utuletee Mwenyezi Mungu na Malaika uso kwa uso.
(93) Au uwe na nyumba iliyopambwa, au upae mbinguni. Wala hatutaamini kupaa kwako huko mpaka ututeremshie kitabu tukisome. Sema, "Subhana Rabbi (Ametakasika Mola wangu Mlezi)! Kwani mimi ni nani isipokuwa ni mtu tu na Mtume?
(94) Na hakikuwazuilia watu kuamini ulipowajia uwongofu isipokuwa ni kwamba walisema, "Je, mwenyezi Mungu alimtuma mtu kuwa ni Mtume?"
(95) Sema, "Ingelikuwa katika ardhi wapo Malaika wanatembea kwa utulivu wao, basi bila ya shaka tungeliwateremshia Malaika kuwa ni Mtume wao."
(96) Sema, "Mwenyezi Mungu anatosha kuwa Shahidi baina yangu na nyinyi. Hakika Yeye ana habari zote za waja wake na anawaona vyema."
(97) Na yule ambaye Mwenyezi Mungu anamuongoa, basi huyo ndiye aliyeongoka. Na yule ambaye anampotoa, basi hutawapatia walinzi wowote badala yake. Na tutawakusanya Siku ya Qiyama hali ya kuwa wanakokotwa juu ya nyuso zao, huku ni vipofu, mabubu, na viziwi. Na makazi yao ni Jahannamu. Kila ukifanya kuzimika, tutazidi kuuchochea uwake kwa nguvu.
(98) Hayo ni malipo yao kwa sababu walizikataa ishara zetu, na wakasema: Hivyo tukisha kuwa mifupa na mapande yaliyovurugika tutafufuliwa kwa umbo jipya?
(99) Kwani hawakuona ya kwamba Mwenyezi Mungu aliyeumba mbingu na ardhi ni Mwenye kuweza kuumba mfano wao? Na Yeye amewawekea muda usio na shaka yoyote. Lakini madhalimu walikataa isipokuwa kukufuru tu.
(100) Sema, "Lau kuwa nyinyi mnazimiliki hazina za rehema za Mola wangu Mlezi, basi hapana shaka mngelizuia kwa sababu ya kuhofu kuzitumia. Na mtu tangu hapo tabia yake ni mchoyo mno!
(101) Na kwa yakini tulimpa Musa ishara tisa zilizo wazi. Basi waulize Wana wa Israili alipowafikia, na Firauni akamwaambia, "Hakika mimi ninakuona wewe Musa umerogwa!"
(102) Musa akasema, "Wewe unajua bila ya shaka kuwa haya hakuyateremsha isipokuwa Mola Mlezi wa mbingu na ardhi ili kuwa ni ushahidi wa kuonekana. Na hakika mimi bila ya shaka nakuona wewe, Firauni, kuwa utaangamizwa."
(103) Basi Firauni akataka kuwafukuza katika nchi. Kwa hivyo tukamzamisha yeye na wale waliokuwa pamoja naye wote.
(104) Na tukawaambia baada yake Wana wa Israili, "Kaeni katika nchi. Na itapokuja ahadi ya Akhera, tutawaleta nyote pamoja."
(105) Na kwa Haki tumeiteremsha, na kwa Haki imeteremka. Na hatukukutuma isipokuwa uwe mbashiri na mwonyaji.
(106) Na Qur-ani tumeigawanya sehemu mbalimbali ili uwasomee watu kwa kituo, na tumeiteremsha kidogo kidogo.
(107) Sema, "Iaminini au msiiamini. Hakika wale waliopewa elimu kabla yake, wanaposomewa hii, huanguka kifudifudi wanasujudu.
(108) "Na wanasema, 'Subhana Rabbina (Ametakasika Mola wetu Mlezi)! Hakika ahadi ya Mola wetu Mlezi lazima itimizwe!'
(109) "Na huanguka kifudifudi na huku wanalia, na inawazidisha unyenyekevu."
(110) Sema, "Mwombeni Allah (Mwenyezi Mungu), au mwombeni Ar-Rahman (Mwingi wa rehema), kwa jina lolote mnalomwita. Hakika, Yeye ana majina mazuri zaidi. Wala usiswali Swala yako kwa sauti kubwa sana, wala usiifiche kwa sauti ndogo sana, bali shika njia ya kati na kati ya hizo."
(111) Na sema, "Alhamdulillah (sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu) ambaye hakujifanyia mwana yeyote, wala hana mshirika yeyote katika ufalme, wala hana mlinzi yeyote wa kumsaidia kwa sababu ya udhaifu wake. Na mtukuze kwa utukufu mkubwa.