38 - Surat Sad ()

|

(1) Swad. Naapa kwa Qur-ani yenye mawaidha.

(2) Lakini waliokufuru wamo katika majivuno na upinzani.

(3) Mataifa mangapi tumeyaangamiza kabla yao, na wakapiga kelele, lakini wakati wa kuokoka ulikwisha pita.

(4) Na walistaajabu kuwajia mwonyaji anayetokana nao wenyewe, na makafiri wakasema: Huyu ni mchawi, mwongo.

(5) Amewafanya miungu wote kuwa ni mungu mmoja tu? Hakika hili ni jambo la ajabu.

(6) Na wakaondoka wakubwa wao wakiwaambia: Nendeni zenu na dumuni na miungu yenu, kwani hili ni jambo lililopangwa.

(7) Sisi hatukusikia haya katika mila hii ya mwisho. Haya si chochote ila ni uzushi tu.

(8) Ati yeye tu ndiye aliye teremshiwa mawaidha peke yake katika sisi? Lakini hao wana shaka na mawaidha yangu, bali hawajaionja adhabu yangu.

(9) Au wanazo wao hazina za rehema za Mola wako Mlezi, Mwenye nguvu, Mpaji?

(10) Au wao wana ufalme wa mbingu na ardhi na vilivyomo kati yavyo? Basi na wazipande njia za kwendea huko!

(11) Hao ni askari watakaoshindwa miongoni mwa makundi yatakayoshindwa.

(12) Walikanusha kabla yao kaumu ya Nuhu, na kina A'adi na Firauni mwenye majengo.

(13) Na Thamud na kaumu Luti na watu wa Machakani. Hayo ndiyo makundi.

(14) Hao wote waliwakadhibisha Mitume; basi wakastahiki adhabu yangu.

(15) Na hawa hawangojei ila ukelele mmoja tu usio na muda.

(16) Na walisema: ‘Mola wetu Mlezi! Tuletee upesi sehemu yetu ya adhabu kabla ya Siku ya Hesabu.’

(17) Subiri kwa hayo wayasemayo, na umkumbuke mja wetu Daudi, mwenye nguvu. Hakika yeye alikuwa mwingi wa kutubia.

(18) Hakika tuliidhalilisha milima pamoja naye ikisabihi jioni na asubuhi pamoja naye.

(19) Na pia ndege waliokusanywa makundi kwa makundi; wote walikuwa wanyenyekevu kwake.

(20) Na tukautia nguvu ufalme wake, na tukampa hekima, na kukata hukumu.

(21) Na je, imekufikia habari ya wagombanao walipopindukia ukuta kuingia chumbani?

(22) Walipomuingilia Daudi, naye akawaogopa. Wakasema: Usiogope! Sisi ni wagombanao wawili, mmoja wetu amemdhulumu mwenziwe. Basi tuhukumu kwa haki, wala usipendelee. Na utuongoe kwenye njia iliyo sawa.

(23) Hakika huyu ndugu yangu ana kondoo wa kike tisini na tisa; na mimi ninaye kondoo mke mmoja. Akasema: Nipe huyo nikufugie! na amenishinda kwa maneno.

(24) Akasema: Kweli amekudhulumu kwa kumtaka kondoo wako mmoja kuongezea kwenye kondoo wake. Na hakika washirika wengi hudhulumiana wao kwa wao, isipokuwa walioamini na wakatenda mema. Na hao ni wachache. Na Daudi akajua kuwa tumemfanyia mtihani. Basi akamwomba msamaha Mola wake Mlezi, na akaanguka kusujudu na kutubia.

(25) Basi tukamsamehe kwa hayo. Naye kwa hakika anao mkaribisho mkubwa na marejeo mazuri kwetu.

(26) Ewe Daudi! Hakika Sisi tumekufanya wewe uwe Khalifa katika nchi. Basi wahukumu watu kwa haki, wala usifuate matamanio yakakupoteza kwenye Njia ya Mwenyezi Mungu. Hakika wanaoipotea Njia ya Mwenyezi Mungu wakaiacha, watapata adhabu kali kwa sababu ya kusahau kwao Siku ya Hisabu.

(27) Na hatukuziumba mbingu na ardhi na vilivyomo ndani yavyo bure. Hiyo ni dhana ya waliokufuru. Ole wao waliokufuru kwa Moto utakaowapata.

(28) Je, tuwafanye walioamini na wakatenda mema kama wafanyao uharibifu katika nchi? Au tuwafanye wacha Mungu kama waovu?

(29) Na hiki Kitabu, tumekuteremshia wewe, kimebarikiwa, ili wazizingatie Aya zake, na wawaidhike wenye akili.

(30) Na Daudi tukamtunukia Suleiman. Alikuwa mja mwema. Na hakika alikuwa mwingi wa kutubia.

(31) Alipopelekewa jioni farasi wasimamao kidete, tayari kutoka shoti.

(32) Basi akasema: Navipenda vitu vizuri kwa kumkumbuka Mola wangu Mlezi. Kisha wakafichikana nyuma ya boma.

(33) (Akasema:) Nirudishieni! Akaanza kuwapapasa miguu na shingo.

(34) Na tulimtia mtihanini Suleiman, na tukauweka mwili juu ya kiti chake, kisha akarejea kwa kutubu.

(35) Akasema: Mola wangu Mlezi! Nisamehe na unipe ufalme usiomwelekea yeyote baada yangu. Hakika Wewe ndiye Mpaji.

(36) Basi tukaufanya upepo umtumikie, ukenda kwa amri yake, popote alipotaka kufika.

(37) Na tukayafanya mashetani yamtumikie, wote wajenzi na wapiga mbizi.

(38) Na wengine wafungwao kwa minyororo.

(39) Hichi ndicho kipawa chetu. Basi toa au zuia, bila ya hisabu.

(40) Na hakika yeye kwetu Sisi ana cheo cha kukaribishwa kwetu, na pahala pazuri pa kurejea.

(41) Na mkumbuke mja wetu Ayubu alipomwita Mola wake Mlezi akasema: Kwa hakika Shetani amenifikishia udhia na adhabu.

(42) (Akaambiwa:) Piga-piga ardhi kwa mguu wako! Basi haya maji baridi ya kuogea na ya kunywa.

(43) Na tukampa ahali zake na wengine kama wao pamoja nao, kuwa ni rehema itokayo kwetu, na iwe kumbusho kwa watu wenye akili.

(44) Na shika kicha cha vijiti tu mkononi mwako, kisha ndio upigie nacho, wala usivunje kiapo. Hakika tulimkuta mwenye subira, mbora wa waja, kwa hakika alikuwa mwingi wa kutubu.

(45) Na wakumbuke waja wetu, Ibrahim na Is-haqa na Yaa'qubu waliokuwa na nguvu na busara.

(46) Sisi tumewahusisha wao kwa sifa ya ukumbusho wa Akhera.

(47) Na hakika wao kwetu sisi ni wateuliwa walio bora.

(48) Na mtaje Ismail na Alyasaa na Dhulkifli, na wote hao ni katika walio bora.

(49) Huu ni ukumbusho. Na hakika wacha Mungu wana marudio mazuri.

(50) Bustani za milele zitakazofunguliwa milango yao kwa ajili yao.

(51) Humo wataegemea matakia, wawe wanaagiza humo matunda mengi na vinywaji.

(52) Na pamoja nao wake zao wenye kutuliza macho, hirimu zao.

(53) Haya ndiyo mliyoahidiwa kwa Siku ya Hisabu.

(54) Hakika hii ndiyo riziki yetu isiyomalizika.

(55) Ndiyo hivi! Na hakika wenye kuasi bila ya shaka watapata marudio maovu kabisa;

(56) Nayo ni Jahannamu! Wataingia humo. Nacho hicho ni kitanda kiovu mno cha kulalia.

(57) Ndiyo hivi! Basi na wayaonje maji ya moto na ya usaha!

(58) Na adhabu nyenginezo za namna hii.

(59) Hili ndilo kundi litakalo ingia pamoja nanyi. Hapana makaribisho mema kwao. Hakika hao wanaingia Motoni.

(60) Waseme: Lakini nyinyi! Hamna mapokezi mazuri! Nyinyi ndio mliotusabibisha haya, napo ni pahala paovu kabisa!

(61) Waseme: Mola wetu Mlezi aliyetusabibisha haya, mzidishie adhabu mara mbili Motoni.

(62) Watasema: Tuna nini hata hatuwaoni wale watu ambao tukiwahisabu ndio katika waovu?

(63) Tulikosea tulipowafanyia masihara, au macho yetu tu hayawaoni?

(64) Hakika hayo bila ya shaka ndiyo mahasimiano ya watu wa Motoni.

(65) Sema: Hakika mimi ni mwonyaji tu; na hapana mungu ila Mwenyezi Mungu Mmoja, Mtenda nguvu.

(66) Mola Mlezi wa mbingu na ardhi na viliomo baina yake, Mwenye nguvu, Mwenye kusamehe.

(67) Sema: Hii ni habari kubwa kabisa.

(68) Ambayo nyinyi mnaipuuza.

(69) Sikuwa na elimu ya mambo ya viumbe wakuu watukufu walipokuwa wakishindana.

(70) Haikufunuliwa kwangu isipokuwa ya kwamba hakika mimi ni mwonyaji dhahiri.

(71) Mola wako Mlezi alipowaambia Malaika: Hakika Mimi nitaumba mtu kutokana na udongo.

(72) Na nitakapomkamilisha na kumpulizia roho inayotokana nami, basi muangukieni kwa kumtii.

(73) Basi wakasujudu Malaika wote pamoja.

(74) Isipokuwa Iblisi; alijivuna na akawa katika makafiri.

(75) Mwenyezi Mungu akamwambia: Ewe Iblisi! Kipi kilicho kuzuia kumtii yule niliyemuumba kwa mikono yangu? Je, umejiona mkubwa, au umekuwa katika wakuu kweli?

(76) Akasema: Mimi ni bora kuliko yeye. Umeniumba kwa moto, na yeye umemuumba kwa udongo.

(77) Akasema: Basi toka humo, kwani hakika wewe umelaanika.

(78) Na hakika laana yangu itakuwa juu yako mpaka Siku ya Malipo.

(79) Akasema: Mola wangu Mlezi! Nipe muhula mpaka siku watakayofufuliwa viumbe.

(80) Mwenyezi Mungu akasema: Basi umekwisha kuwa miongoni mwa waliopewa muhula.

(81) Mpaka siku ya wakati maalumu.

(82) Akasema (Iblisi): Naapa kwa utukufu wako, bila ya shaka nitawapoteza wote.

(83) Isipokuwa wale waja wako miongoni mwao waliohitariwa.

(84) Akasema: Haki! Na haki ninaisema.

(85) Bila ya shaka nitaijaza Jahannamu kwa wewe na kwa hao wote wenye kukufuata miongoni mwao.

(86) Sema (Ewe Mtume): Sikuombeni ujira juu ya haya, wala mimi si katika wadanganyifu.

(87) Hayakuwa haya ila ni mawaidha kwa walimwengu wote.

(88) Na bila ya shaka mtajua habari zake baada ya muda.