36 - Surat Yasin ()

|

(1) Ya-Sin

(2) Kwa Haki ya Qur-ani yenye hekima!

(3) Hakika wewe ni miongoni mwa waliotumwa.

(4) Juu ya njia iliyonyooka.

(5) Uteremsho wa Mwenye nguvu, Mwingi wa kurehemu.

(6) Ili uwaonye watu ambao baba zao hawakuonywa, basi wao wamekuwa wenye kughafilika.

(7) Bila ya shaka kauli imekwisha thibiti juu ya wengi katika wao, kwa hivyo hawaamini.

(8) Tumeweka makongwa shingoni mwao, yakawafika videvuni. Kwa hivyo vichwa vyao viko juu tu.

(9) Tumeweka kizuizi mbele yao, na kizuizi nyuma yao. Na tumewafunika macho yao, kwa hivyo hawaoni.

(10) Ni sawa sawa kwao ukiwaonya au usiwaonye, hawataamini.

(11) Hakika wewe unamwonya mwenye kufuata ukumbusho, na akamcha Arrahman (Mwingi wa rehema), kwa ghaibu. Basi mbashirie huyo msamaha na ujira mwema.

(12) Hakika Sisi tunawafufua wafu na tunayaandika wanayoyatanguliza, na wanayoyaacha nyuma. Na kila kitu tumekihifadhi katika daftari la asili lenye kubainisha.

(13) Na wapigie mfano wa wakazi wa mji walipojiwa na Mitume.

(14) Tulipowatumia wawili, wakawakanusha. Basi tukawazidishia nguvu kwa mwingine wa tatu. Wakasema: "Hakika sisi tumetumwa kwenu."

(15) Wakasema: "Nyinyi si chochote ila ni watu kama sisi. Na Mwingi wa Rehema hakuteremsha kitu. Nyinyi mnasema uongo tu."

(16) Wakasema: "Mola wetu Mlezi anajua kwamba hakika sisi tumetumwa kwenu."

(17) Wala si juu yetu ila kufikisha ujumbe ulio wazi.

(18) Wakasema: "Sisi tumeamua kuwa nyinyi ni wakorofi. Ikiwa hamtaacha basi kwa yakini tutakupigeni mawe, na mtapata adhabu chungu kutoka kwetu."

(19) Wakasema: "Ukorofi wenu mnao wenyewe! Je! Ni kwa kuwa mnakumbushwa? Ama nyinyi ni watu waliopindukia mipaka."

(20) Na akaja mtu mbio kutokea upande wa mbali wa mjini, akasema: "Enyi watu wangu! Wafuateni hawa waliotumwa."

(21) Wafuateni ambao hawakutakini ujira, hali ya kuwa wenyewe wameongoka.

(22) Na kwa nini nisimuabudu yule aliyeniumba na kwake nitarejeshwa?

(23) Je, niishike miungu mingine badala yake? Arrahmani (Mwingi wa Rehema) akinitakia madhara uombezi wa hao hautanifaa kitu, wala hawataniokoa.

(24) Basi hakika mimi hapo nitakuwa katika upotovu ulio dhahiri.

(25) Hakika mimi nimemuamini Mola wenu Mlezi, basi nisikilizeni!

(26) Akaambiwa: "Ingia Peponi!" Akasema: "Laiti kuwa watu wangu wangelijua.

(27) Jinsi Mola wangu Mlezi alivyonisamehe, na akanifanya miongoni mwa walioheshimiwa.

(28) Na hatukuwateremshia kaumu yake baada yake jeshi kutoka mbinguni, wala si wenye kuteremsha.

(29) Hakukuwa ila ukelele mmoja tu, na mara walizimwa!

(30) Nawasikitikia waja wangu. Hawajii Mtume ila wao humkejeli.

(31) Je, hawaoni umma ngapi tulizoziangamiza kabla yao? Hakika hao hawarejei tena kwao.

(32) Na hapana mmoja ila wote watakusanywa waletwe mbele yetu.

(33) Na Ishara hiyo kwao ni ardhi iliyokufa, nasi tukaifufua, na tukatoa ndani yake nafaka, wakawa wanakula katika hizo!

(34) Na tukafanya ndani yake mabustani ya mitende na mizabibu, na tukatimbua chemichemi ndani yake.

(35) Ili wale katika matunda yake, na hayo hayakufanywa na mikono yao! Basi je, hawashukuru?

(36) Ametakasika yule aliyeumba dume na jike vyote katika vinavyomea katika ardhi na katika nafsi zao, na katika wasivyovijua.

(37) Na usiku ni Ishara kwao. Tunauvua humo mchana, mara wao wanakuwa gizani.

(38) Na jua linakwenda kwa kiwango chake. Hayo ni makadirio ya Mwenye nguvu, Mwenye kujua vyema.

(39) Na mwezi tumeupimia vituo, mpaka unakuwa kama karara kongwe.

(40) Haliwi jua kuufikia mwezi, wala usiku kuupita mchana. Na vyote vinaogelea katika njia zao.

(41) Na ni Ishara kwao kwamba Sisi tuliwapakia dhuria zao katika jahazi lililosheheni.

(42) Na tukawaumbia kutoka mfano wake wanavyovipanda.

(43) Na tukitaka, tunawazamisha, wala hapana wa kuwasaidia, wala hawaokolewi.

(44) Isipokuwa kwa rehema zitokazo kwetu na starehe kwa muda.

(45) Na wanapoambiwa: Jilindeni kutokana na yaliyoko mbele yenu na yaliyoko nyuma yenu, ili mpate kurehemewa...

(46) Na haiwafikii Ishara yoyote katika Ishara za Mola wao Mlezi isipokuwa wao huwa ni wenye kuipa mgongo.

(47) Na wanapoambiwa: Toeni katika aliyokupeni Mwenyezi Mungu, wale waliokufuru huwaambia wale walioamini: Je, tuwalishe wale ambao Mwenyezi Mungu angependa angeliwalisha mwenyewe? Nyinyi hammo isipokuwa katika upotofu ulio dhahiri.

(48) Na wanasema: Ahadi hii itatokea lini, ikiwa nyinyi ni wakweli?

(49) Hawangojei isipokuwa ukelele mmoja tu utakaowachukua nao wamo kuzozana.

(50) Basi hawataweza kuusia, wala kwa watu wao hawarejei.

(51) Na litapulizwa barugumu, mara watatoka makaburini wakikimbilia kwa Mola wao Mlezi.

(52) Watasema: Ole wetu! Ni nani aliyetufufua kwenye malazi yetu? Haya ndiyo aliyoyaahidi Mwingi wa Rehema na wakasema kweli Mitume.

(53) Haitakuwa isipokuwa ukelele mmoja tu, mara wote watahudhurishwa mbele yetu.

(54) Basi leo nafsi yoyote haitadhulumiwa kitu, wala hamtalipwa isipokuwa yale mliyokuwa mkiyatenda.

(55) Hakika watu wa Peponi leo wamo shughulini, wamefurahi.

(56) Wao na wake zao wamo katika vivuli wameegemea juu ya viti vya kifahari.

(57) Watapata humo kila namna ya matunda na watapata kila watakachokitaka.

(58) "Salama!" Hiyo ndiyo kauli itokayo kwa Mola Mlezi Mwenye kurehemu.

(59) Na enyi wakosefu! Jitengeni leo!

(60) Je, sikuagana nanyi, enyi wanadamu, kuwa msimuabudu Shetani? Hakika yeye ni adui dhahiri kwenu.

(61) Na ya kwamba mniabudu Mimi? Hii ndiyo njia iliyonyooka.

(62) Na bila ya shaka yeye amekwishalipoteza kundi kubwa miongoni mwenu. Je, hamkuwa mkifikiri?

(63) Hii basi ndiyo Jahannamu mliyokuwa mkiahidiwa.

(64) Ingieni humo leo kwa vile mlivyokuwa mkikufuru.

(65) Leo tunaviziba vinywa vyao, na iseme nasi mikono yao, na itoe ushahidi miguu yao kwa waliyokuwa wakiyachuma.

(66) Na tungelipenda, tungeliyafutilia mbali macho yao, wakawa wanaiwania njia. Lakini wangeionaje?

(67) Na tungelitaka, tungewageuza sura hapo hapo walipo, basi wasingeweza kwenda wala kurudi.

(68) Na tunayemzeesha, tunamrudisha nyuma katika umbo. Basi je! hawazingatii?

(69) Wala hatukumfundisha (Muhammad) mashairi, wala hayatakikani kwake hayo. Haukuwa huu isipokuwa ni ukumbusho na Qur-ani inayobainisha.

(70) Ili imwonye aliye hai, na neno litimie juu ya makafiri.

(71) Je! Hawaoni kwamba tumewaumbia kutokana na iliyofanya mikono yetu wanyama wa mifugo, na wao wakawa wenye kuwamiliki.

(72) Na Sisi tukawadhalilishia. Basi baadhi yao wako wanaowapanda, na baadhi yao wanawala.

(73) Na wao wanapata kwao manufaa na vinywaji. Basi je, hawashukuru?

(74) Na wameishika miungu mingine badala ya Mwenyezi Mungu ili ati wapate kusaidiwa!

(75) Hawataweza kuwasaidia. Bali hao ndio watakuwa askari wao watakaohudhurishwa.

(76) Basi maneno yao yasikuhuzunishe. Hakika Sisi tunayajua wanayoyaweka siri na wanayoyadhihirisha.

(77) Kwani mwanadamu haoni ya kwamba Sisi tumemuumba yeye kutokana na tone la manii? Kisha sasa yeye ndiyo amekuwa ndiye mgomvi wa dhahiri!

(78) Na akatupigia mfano, na akasahau kuumbwa kwake, akasema: Ni nani huyo atakayeihuisha mifupa nayo imekwisha mung'unyika?

(79) Sema: Ataihuisha huyo huyo aliyeiumba hapo mara ya mwanzo. Na Yeye ni Mjuzi wa kila kuumba.

(80) Aliyekujaalieni kupata moto kutokana na mti wa kijani nanyi mkawa kwa huo mnawasha.

(81) Kwani aliyeziumba mbingu na ardhi hawezi kuwaumba mfano wao? Kwani! Naye ndiye Muumbaji Mkuu, Mjuzi mno.

(82) Hakika amri yake anapotaka kitu ni kukiambia tu: Kuwa! Na kikawa.

(83) Basi ametakasika yule ambaye mkononi mwake umo Ufalme wa kila kitu; na kwake Yeye mtarejeshwa.