47 - Surat Muhammad ()

|

(1) Wale waliokufuru na wakazuilia njia ya Mwenyezi Mungu, Yeye atavipotoa vitendo vyao.

(2) Na wale walioamini, na wakatenda mema, na wakaamini yale aliyoteremshiwa Muhammad - nayo ni Haki iliyotoka kwa Mola wao Mlezi - atawafutia makosa yao na ataitengeneza hali yao.

(3) Hayo ni kwa sababu wale waliokufuru wamefuata upotovu, na wale walioamini wamefuata Haki iliyotoka kwa Mola wao Mlezi. Hivyo ndivyo Mwenyezi Mungu anavyowapigia watu mifano yao.

(4) Basi mnapowakuta wale waliokufuru, wapigeni shingoni mwao, mpaka mkiwadhoofisha, wafungeni pingu. Tena waachilieni kwa hisani au wajikomboe, mpaka vita vipoe. Ndivyo hivyo. Na lau angelitaka Mwenyezi Mungu, angeliwashinda mwenyewe, lakini haya ni kwa sababu awatie mitihani nyinyi kwa nyinyi. Na wale waliouliwa katika njia ya Mwenyezi Mungu, hatayapoteza matendo yao.

(5) Atawaongoza na awatengezee hali yao.

(6) Na atawaingiza katika Pepo aliyowajuulisha.

(7) Enyi mlioamini! Mkimnusuru Mwenyezi Mungu, naye atawanusuruni na ataiimarisha miguu yenu.

(8) Na wale waliokufuru, basi kwao ni maangamizo, na atavipoteza vitendo vyao.

(9) Hayo ni kwa sababu waliyachukia yale aliyoyateremsha Mwenyezi Mungu, basi akaviangusha vitendo vyao.

(10) Kwani hawakutembea katika ardhi wakaona ulikuwaje mwisho wa wale waliokuwa kabla yao? Mwenyezi Mungu aliwaangamiza, na kwa makafiri hawa itakuwa mifano ya hayo.

(11) Hayo ni kwa sababu Mwenyezi Mungu ni Mlinzi wa wale walioamini. Na makafiri hawana mlinzi.

(12) Hakika Mwenyezi Mungu atawaingiza wale walioamini na wakatenda mema katika Bustani za mbinguni zipitiwazo na mito kati yake. Na wale waliokufuru hujifurahisha na hula kama walavyo wanyama, na Moto ndio makazi yao.

(13) Na ni miji mingapi iliyokuwa na nguvu zaidi kuliko mji wako huu uliokutoa? Tuliwateketeza na wala hawakuwa na yeyote wa kuwanusuru.

(14) Je, yule aliye kwenye ubainifu kutoka kwa Mola wake Mlezi ni kama yule aliyepambiwa uovu wa vitendo vyake, na wakafuata matamanio yao?

(15) Mfano wa Bustani ya mbinguni waliyoahidiwa wachamngu, ina mito ya maji yasiyovunda, na mito ya maziwa yasiyoharibika ladha yake, na mito ya mvinyo wenye ladha kwa wanywao, na mito ya asali iliyosafishwa. Na wao humo watakuwa na kila namna ya matunda, na maghfira kutoka kwa Mola wao Mlezi. Basi hao ni kama watakaodumu Motoni na wakinyweshwa maji yanayochemka ya kuwakatakata matumbo yao?

(16) Na wapo miongoni mwao wanaokusikiliza, mpaka wakiondoka kwako, huwauliza waliopewa elimu: 'Amesema nini sasa hivi?' Hao ndio ambao Mwenyezi Mungu ameziba nyoyo zao, na wakafuata matamanio yao.

(17) Na wale walioongoka anawazidishia uongofu na anawapa uchamungu wao.

(18) Kwani wanangojea jengine isipokuwa iwafikie Saa (ya Kiyama) kwa ghafla? Na hakika alama zake zimekwishakuja. Na itakapowajia, kutawafaa nini kukumbuka kwao?

(19) Basi jua ya kwamba hapana mungu ila Mwenyezi Mungu, na omba maghufira kwa dhambi zako na za Waumini wanaume na Waumini wanawake. Na Mwenyezi Mungu anajua mahali penu pa kwenda na kurudi, na mahali penu pa kukaa.

(20) Na Waumini wanasema: 'Kwa nini haiteremshwi Sura?' Na inapoteremshwa Sura madhubuti na ikatajwa ndani yake habari ya vita, utawaona wenye maradhi katika nyoyo zao wanakutazama mtazamo wa anayezimia kwa sababu ya mauti. Basi ni bora kwao.

(21) Utiifu na kauli njema. Na jambo likishaazimiwa, basi wakiwa ni wakweli kwa Mwenyezi Mungu, bila ya shaka itakuwa ni heri kwao.

(22) Basi mnatarajia kwamba mkigeuka mkaenda zenu kwamba ndio mtafanya uharibifu katika nchi na muwatupe jamaa zenu?

(23) Hao ndio aliowalaani Mwenyezi Mungu, na akawatia uziwi, na akawapofua macho yao.

(24) Je, hawaizingatii hii Qur-ani? Au kwenye nyoyo (zao) zipo kufuli zake?

(25) Kwa hakika wale wanaorudi nyuma baada ya uwongofu kwisha wabainikia, Shetani huyo amewashawishi na amewaghuri.

(26) Hayo ni kwa sababu waliwaambia wale waliochukia yale aliyoyateremsha Mwenyezi Mungu: 'Tutakutiini katika baadhi ya mambo.' Na Mwenyezi Mungu anajua siri zao.

(27) Basi itakuwaje Malaika watakapowafisha wakawa wanawapiga nyuso zao na migongo yao!

(28) Hayo ni kwa sababu wao waliyafuata yale yaliyomchukiza Mwenyezi Mungu na wakachukia yanayomridhisha, basi akaviangusha vitendo vyao.

(29) Je, wenye maradhi nyoyoni mwao wanadhani kwamba Mwenyezi Mungu hatazidhihirisha chuki zao?

(30) Na tungelipenda, tungelikuonyesha hao na ungeliwatambua kwa alama zao. Lakini bila ya shaka utawajua kwa namna ya msemo wao. Na Mwenyezi Mungu anavijua vitendo vyenu.

(31) Na bila ya shaka tutawajaribu mpaka tuwajue wapignao Jihadi katika nyinyi na wanaosubiri. Nasi tutazifanyia mtihani habari zenu.

(32) Kwa hakika wale waliokufuru na wakazuilia njia ya Mwenyezi Mungu na wakapinzana na Mtume baada ya uwongofu kwishawabainikia, hao hawatamdhuru Mwenyezi Mungu kwa lolote. Naye ataviangusha vitendo vyao.

(33) Enyi mlioamini! Mtiini Mwenyezi Mungu, na mtiini Mtume, wala msiviharibu vitendo vyenu.

(34) Hakika wale waliokufuru na wakazuilia njia ya Mwenyezi Mungu, kisha wakafa na hali ni makafiri, Mwenyezi Mungu hatawasamehe makosa yao.

(35) Basi msilegee na mkataka suluhu, maana nyinyi ndio mtakaoshinda. Na Mwenyezi Mungu yu pamoja nanyi, wala hatawanyima malipo ya vitendo vyenu.

(36) Hakika uhai wa duniani ni mchezo na pumbao. Na mkiamini na mkamcha Mungu, Mwenyezi Mungu atakupeni ujira wenu, wala hatakutakeni mali zenu.

(37) Na akikutakeni hizo na kukushikilieni, mtafanya ubahili, na atatoa undani wa chuki zenu.

(38) Angalieni! Nyinyi hawa mnaitwa mtumie mali katika njia ya Mwenyezi Mungu, na wapo katika nyinyi wanaofanya ubahili. Na anayefanya ubahili, basi anajifanyia ubahili mwenyewe. Na Mwenyezi Mungu si mhitaji, na nyinyi ndio wahitaji. Na mkigeuka, atawaleta watu wengine badala yenu, nao hawatakuwa kama nyinyi.