77 - Surat Al-Mursalat ()

|

(1) Ninaapa kwa zinazotumwa kwa upole!

(2) Na zinazovuma kwa kasi!

(3) Na zikaeneza maeneo yote!

(4) Na zinazofarikisha zikatawanya!

(5) Na zinazopeleka mawaidha!

(6) Kuwa udhuru au kuonya.

(7) Hakika mnayoahidiwa bila ya shaka yatakuwa!

(8) Wakati nyota zitakapofutwa.

(9) Na mbingu zitakapopasuliwa.

(10) Na milima itakapopeperushwa.

(11) Na Mitume watakapo wekewa wakati wao.

(12) Kwa siku gani hiyo wamewekewa muda huo?

(13) Kwa siku ya kupambanua!

(14) Na nini kitakachokujuulisha siku ya kupambanua ni nini?

(15) Ole wao, siku hiyo hao wanaokanusha!

(16) Kwani hatukuwaangamiza waliotangulia?

(17) Kisha tukawafuatilizia waliofuatia?

(18) Ndio kama hivi tuwatendavyo wakosefu!

(19) Ole wao siku hiyo hao wanaokanusha!

(20) Kwani hatukukuumbeni kwa maji ya kudharauliwa?

(21) Kisha tukayaweka mahali pa utulivu madhubuti?

(22) Mpaka muda maalumu?

(23) Tukakadiria na Sisi ni wabora wa kukadiria.

(24) Ole wao siku hiyo hao wanaokanusha!

(25) Kwani hatukuifanya ardhi yenye kukusanya.

(26) Walio hai na maiti?

(27) Na ndani yake tukaweka milima mirefu yenye kuthibiti, na tunakunywesheni maji matamu?

(28) Ole wao siku hiyo hao wanaokanusha!

(29) Nendeni kwenye adhabu mliyokuwa mkiikanusha!

(30) Nendeni kwenye kivuli chenye mapande matatu!

(31) Hakikingi moto, wala hakiwaepushi na mwako.

(32) Hakika Moto huo unatoa macheche kama majumba!

(33) Kama kwamba ni ngamia wa rangi ya manjano!

(34) Ole wao siku hiyo hao wanaokanusha!

(35) Hii ni siku ambayo hawatatamka kitu.

(36) Wala hawataruhusiwa kutoa udhuru.

(37) Ole wao siku hiyo hao waliokanusha!

(38) Hii ndiyo siku ya kupambanua. Tumekukusanyeni nyinyi na waliotangulia.

(39) Ikiwa mnayo hila, nifanyieni hila Mimi!

(40) Ole wao siku hiyo hao waliokanusha!

(41) Hakika wacha Mungu watakuwa katika vivuli na chemchemI.

(42) Na matunda wanayoyapenda.

(43) Kuleni na kunyweni kwa furaha kwa yale mliyokuwa mkiyatenda.

(44) Hakika ndio kama hivyo tunavyowalipa watendao mema.

(45) Ole wao siku hiyo hao wanaokanusha!

(46) Kuleni na mjifurahishe kidogo tu. Hakika nyinyi ni wakosefu!

(47) Ole wao siku hiyo hao wanaokanusha!

(48) Na wakiambiwa: Inameni! Hawainami.

(49) Ole wao siku hiyo hao wanaokanusha!

(50) Basi maneno gani baada ya haya watayaamini?