(1) Hii ni Sura tuliyoiteremsha na tukailazimisha; na tukateremsha ndani yake Aya zilizo wazi ili mkumbuke.
(2) Mzinifu mwanamke na mzinifu mwanamume, mtandikeni kila mmoja katika wao bakora mia. Wala isiwashike huruma kwa ajili yao katika hukumu ya Mwenyezi Mungu, ikiwa nyinyi mnamuamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho. Na lishuhudie adhabu yao kundi la Waumini.
(3) Mwanamume mzinifu hamwoi ila mwanamke mzinifu au mwanamke mshirikina. Na mwanamke mzinifu haolewi ila na mwanamume mzinifu au mshirikina. Na hayo yameharamishwa kwa waumini.
(4) Na wanaowasingizia wanawake mahashumu, kisha wasilete mashahidi wanne, basi watandikeni bakora themanini, na msiwakubalie ushahidi wao tena. Na hao ndio wapotovu.
(5) Isipokuwa wale waliotubu baada ya hayo na wakatengenea; kwani bila ya shaka Mwenyezi Mungu ni Msamehevu, Mwenye kurehemu.
(6) Na wale wanaowasingizia wake zao na hawana mashahidi ila nafsi zao, basi ushahidi wa mmoja wao utakuwa kushuhudilia mara nne kwa kiapo cha Mwenyezi Mungu, ya kwamba hakika yeye ni katika wasema kweli.
(7) Na mara ya tano kwamba laana ya Mwenyezi Mungu iwe juu yake ikiwa ni miongoni mwa waongo.
(8) Na mke itamwondokea adhabu kwa kutoa shahada mara nne kwa kiapo cha Mwenyezi Mungu, ya kwamba huyu mume ni miongoni mwa waongo.
(9) Na mara ya tano ya kwamba ghadhabu ya Mwenyezi Mungu iwe juu yake, kama mumewe yu miongoni mwa wanaosema kweli.
(10) Na lau kuwa si fadhila ya Mwenyezi Mungu juu yenu na rehema yake, na ya kuwa Mwenyezi Mungu ni Mpokeaji toba na Mwenye hekima.
(11) Hakika wale walioleta uongo ni kundi miongoni mwenu. Msifikiri ni shari kwenu, bali hiyo ni kheri kwenu. Kila mtu katika wao atapata aliyoyachuma katika madhambi. Na yule aliyejitwika sehemu yake kubwa miongoni mwao, atapata adhabu kubwa.
(12) Kwa nini mlipo ikia habari hii, wanaume Waumini na wanawake Waumini hawakuwadhania wenzao mema, na kusema: Huu ni uzushi dhahiri?
(13) Kwa nini hawakuleta mashahidi wanne? Na ilivyokuwa hawakuleta mashahidi wanne, basi hao mbele ya Mwenyezi Mungu ni waongo.
(14) Na lau kuwa si fadhila ya Mwenyezi Mungu juu yenu na rehema yake katika dunia na Akhera, bila ya shaka ingeliwapata adhabu kubwa kwa sababu ya yale mliyojiingiza.
(15) Mlipoyapokea kwa ndimi zenu na mkasema kwa vinywa vyenu msiyoyajua, na mlifikiri ni jambo dogo, kumbe mbele ya Mwenyezi Mungu ni kubwa.
(16) Na kwa nini mlipoyasikia msiseme: Haitufalii kuzungumza haya. Subhanak! (Umetakasika!) Huu ni uzushi mkubwa!
(17) Mwenyezi Mungu anawaonya msirejee tena kufanya kama haya kabisa, ikiwa nyinyi ni Waumini!
(18) Na Mwenyezi Mungu anawabainishia Aya. Na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi Mwenye hekima.
(19) Kwa hakika wale wanaopenda uenee uchafu kwa walioamini, watapata adhabu chungu katika dunia na Akhera. Na Mwenyezi Mungu anajua na nyinyi hamjui.
(20) Na lau kuwa si fadhila ya Mwenyezi Mungu juu yenu na rehema yake, na kuwa hakika Mwenyezi Mungu ni Mpole, Mwenye kurehemu.
(21) Enyi mlioamini, msizifuate nyayo za Shetani. Na atakayefuata nyayo za Shetani basi yeye huamrisha machafu na maovu. Na lau kuwa si fadhila ya Mwenyezi Mungu na rehema yake juu yenu, asingelitakasika miongoni mwenu kabisa hata mmoja. Lakini Mwenyezi Mungu humtakasa amtakaye, na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia, Mwenye kujua.
(22) Na wale katika nyinyi wenye fadhila na wasaa wasiape kutowapa jamaa zao, na masikini na waliohama kwa Njia ya Mwenyezi Mungu. Na wasamehe, na waachilie mbali. Je, nyinyi hampendi Mwenyezi Mungu awasamehe? Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe Mwenye kurehemu.
(23) Hakika wanaowasingizia wanawake, wanaojiheshimu, walioghafilika, Waumini; wamelaaniwa duniani na Akhera, nao watapata adhabu kubwa.
(24) Siku ambayo zitawashuhudia ndimi zao na mikono yao na miguu yao kwa waliyokuwa wakiyatenda.
(25) Siku hiyo Mwenyezi Mungu atawapa sawa sawa malipo yao ya haki, na watajua kwamba hakika Mwenyezi Mungu ndiye Haki Iliyo Wazi.
(26) Wanawake waovu ni wa wanaume waovu, na wanaume waovu ni wa wanawake waovu. Na wanawake wema ni wa wanaume wema, na wanaume wema ni wa wanawake wema. Hao wameepushwa na hayo wanayoyasema; wao watapata msamaha na riziki ya ukarimu.
(27) Enyi mlioamini! Msiingie nyumba zisizo nyumba zenu mpaka mwombe ruhusa, na mwatolee salamu wenyewe. Hayo ni bora kwenu mpate kukumbuka.
(28) Na msipomkuta mtu humo basi msiingie mpaka mruhusiwe. Na mkiambiwa: Rudini! Basi rudini. Hivi ni usafi zaidi kwenu. Na Mwenyezi Mungu anayajua mnayoyatenda.
(29) Si vibaya kwenu kuingia nyumba zisiokaliwa ambazo ndani yake yamo manufaa yenu. Na Mwenyezi Mungu anajua mnayoyadhihirisha na mnayoyaficha.
(30) Waambie Waumini wanaume wainamishe macho yao, na wazilinde tupu zao. Hili ni takaso bora kwao. Hakika Mwenyezi Mungu anazo habari za wanayoyafanya.
(31) Na waambie Waumini wanawake wainamishe macho yao, na wazilinde tupu zao, wala wasionyeshe uzuri wao isipokuwa unaodhihirika. Na waangushe shungi zao juu ya vifua vyao, wala wasionyeshe uzuri wao ila kwa waume zao, au baba zao, au baba wa waume zao, au watoto wao, au watoto wa waume zao, au kaka zao, au wana wa kaka zao, au wana wa dada zao, au wanawake wenzao, au iliyowamiliki mikono yao ya kuume, au wafwasi wanaume wasio na matamanio, au watoto ambao hawajajua mambo ya kuhusu uke. Wala wasipige chini miguu yao ili yajulikane mapambo waliyoyaficha. Na tubuni nyote kwa Mwenyezi Mungu, enyi Waumini, ili mpate kufanikiwa.
(32) Na waozeni wajane miongoni mwenu na wema katika watumwa wenu na wajakazi wenu. Wakiwa mafakiri Mwenyezi Mungu atawatajirisha kwa fadhila yake. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye wasaa Mwenye kujua.
(33) Na wajizuilie na machafu wale wasiopata cha kuolea, mpaka Mwenyezi Mungu awatajirishe kwa fadhila yake. Na wanaotaka kuandikiwa uhuru katika wale ambao mikono yenu ya kulia imewamiliki, basi waandikieni kama mkiona wema kwao. Na wapeni katika mali ya Mwenyezi Mungu aliyowapa. Wala msiwashurutishe vijakazi vyenu kufanya zina kwa ajili ya kutafuta pato la maisha ya dunia, ilhali wao wanataka kujiheshimu. Na atakayewalazimisha basi Mwenyezi Mungu baada ya kulazimishwa kwao huko, atawasamehe, kwani Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu.
(34) "Na kwa yakini tumewateremshia Ishara zilizo wazi, na mifano kutokana na waliotangulia kabla yenu na mawaidha kwa wachamngu.''
(35) "Mwenyezi Mungu ni Nuru ya Mbingu na Ardhi. Mfano wa Nuru yake ni kama shubaka lenye kuwekwa ndani yake taa. Taa ile imo katika tungi. Tungi lile ni kama nyota inayomeremeta, inayowashwa kwa mafuta yanayotoka katika mti uliobarikiwa, mzaituni. Si wa mashariki wala magharibi. Yanakaribia mafuta yake kung'aa wenyewe ingawa moto haujayagusa, - Nuru juu ya Nuru. Mwenyezi Mungu humwongoa kwenye Nuru yake amtakaye. Na Mwenyezi Mungu huwapigia watu mifano. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujua kila kitu."
(36) Katika Nyumba ambazo Mwenyezi Mungu ameamrisha zitukuzwe, na humo litajwe jina lake, wanamtakasa humo asubuhi na jioni
(37) Watu ambao biashara wala kuuza hakuwashughulishi na kumdhukuru Mwenyezi Mungu, na kushika Sala, na kutoa Zaka. Wanaihofu Siku ambayo nyoyo na macho yatageuka.
(38) Ili Mwenyezi Mungu awalipe bora ya waliyoyatenda, na awazidishie katika fadhila zake. Na Mwenyezi Mungu humruzuku amtakaye bila ya hisabu.
(39) Na waliokufuru vitendo vyao ni kama sarabi (mazigazi) uwandani. Mwenye kiu huyadhania ni maji. Hata akiyaendea hapati chochote. Na atamkuta Mwenyezi Mungu hapo naye amlipe hisabu yake sawa sawa. Na Mwenyezi Mungu ni Mwepesi wa kuhisabu.
(40) Au ni kama giza katika bahari kuu, iliyofunikwa na mawimbi juu ya mawimbi, na juu yake yapo mawingu. Giza juu ya giza. Akiutoa mtu mkono wake anakaribia asiuone. Na ambaye Mwenyezi Mungu hakumjalia kuwa na nuru hawi na nuru.
(41) Je, huoni kwamba Mwenyezi Mungu vinamtakasa vilivyomo katika mbingu na ardhi, na ndege wakikunjua mbawa zao? Kila mmoja amekwisha jua Swala yake na namna ya kumtakasa kwake. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kuyajua wayatendayo.'
(42) Na ni wa Mwenyezi Mungu ufalme wa mbingu na ardhi, na kwa Mwenyezi Mungu ndiyo marejeo ya wote.
(43) Je, huoni ya kwamba Mwenyezi Mungu huyasukuma mawingu, kisha huyaambatisha, kisha huyafanya mirundi? Basi utaona mvua ikitoka kati yake. Na huteremsha kutoka juu kwenye milima ya mawingu mvua ya mawe, akamsibu nayo amtakaye na akamuepusha nayo amtakaye. Hukurubia mmetuko wa umeme wake kupofua macho.
(44) Mwenyezi Mungu hubadilisha usiku na mchana. Hakika katika hayo yapo mazingatio kwa wenye kuona.
(45) Na Mwenyezi Mungu ameumba kila kinyama kutokana na maji. Wengine katika wao huenda kwa matumbo yao, na wengine huenda kwa miguu miwili, na wengine huenda kwa miguu minne. Mwenyezi Mungu huumba ayatakayo. Hakika Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kila kitu.
(46) Kwa yakini tumeteremsha Ishara zinazobainisha. Na Mwenyezi Mungu humwongoa amtakaye kwenye Njia Iliyonyooka.
(47) Na wanasema: Tumemuamini Mwenyezi Mungu na Mtume, na tumetii. Kisha kikundi katika hao hugeuka baada ya hayo. Wala hao si wenye kuamini.
(48) Na wanapoitwa kumuendea Mwenyezi Mungu na Mtume wake ili ahukumu baina yao, kipo kikundi katika wao kinakataa.
(49) Na ikiwa haki ni yao, wanamjia kwa kutii.
(50) Je, wana maradhi katika nyoyo zao, au wanaona shaka, au wanaogopa ya kuwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake watawadhulumu? Bali hao ndio madhalimu.
(51) Haiwi kauli ya Waumini wanapoitwa kwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake ili ahukumu baina yao, ila ni kusema: Tumesikia, na tumetii! Na hao ndio wenye kufanikiwa.
(52) Na wenye kumtii Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na wakamwogopa Mwenyezi Mungu na wakamcha, basi hao ndio wenye kufuzu.
(53) Na wanaapa kwa Mwenyezi Mungu ukomo wa kiapo chao ya kwamba ukiwaamrisha kwa yakini watatoka. Sema: Msiape! Utiifu unajuulikana. Hakika Mwenyezi Mungu anazo habari za mnayoyatenda.
(54) Sema: Mtiini Mwenyezi Mungu, na mtiini Mtume. Na mkigeuka, basi yaliyo juu yake ni yale aliyobebeshwa, na yaliyo juu yenu ni yale mliyobebshwa nyinyi. Na mkimtii yeye, mtaongoka. Na hapana juu ya Mtume ila kufikisha Ujumbe wazi wazi.
(55) Wawe wananiabudu Mimi, wala wasinishirikishe na chochote. Na watakaokufuru baada ya hayo, basi hao ndio wapotovu.
(56) Na shikeni Swala, na toeni Zaka, na mtiini Mtume, ili mpate kurehemewa.
(57) Msiwadhanie waliokufuru kwamba watashinda katika nchi. Na makaazi yao ni Motoni, na hakika ni maovu kweli marejeo yao.
(58) Enyi mlioamini, nawakukitakeni idhini wale iliyowamiliki mikono yenu ya kulia na walio bado kubaleghe miongoni mwenu mara tatu - kabla ya Swala ya alfajiri, na wakati mnapovua nguo zenu adhuhuri, na baada ya Sala ya isha. Hizi ni nyakati tatu za faragha kwenu. Si vibaya kwenu wala kwao baada ya nyakati hizi, kuzungukiana nyinyi kwa nyinyi. Hivyo ndivyo Mwenyezi Mungu anavyowaelezeni Aya zake, na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi Mwenye hekima.
(59) Na watoto wanapofikilia umri wa kubaleghe basi nawatake ruhusa, kama walivyotaka ruhusa wa kabla yao. Hivyo ndivyo anavyowabainishia Mwenyezi Mungu Aya zake, na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi Mwenye hekima.
(60) Na wanawake wazee wasiotaraji kuolewa, si vibaya kwao kupunguza nguo zao, bila ya kujishaua kwa mapambo. Na wakijiheshimu ni bora kwao. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia, Mwenye kujua.
(61) Si vibaya kwa kipofu, wala si vibaya kwa kiguru, wala si vibaya kwa mgonjwa, wala kwenu nyinyi, mkila katika nyumba zenu, au nyumba za baba zenu, au nyumba za mama zenu, au nyumba za kaka zenu, au nyumba za dada zenu, au nyumba za ami zenu, au nyumba za shangazi zenu, au nyumba za wajomba zenu, au nyumba za dada za mama zenu, au za mliowashikia funguo zao, au rafiki yenu. Si vibaya kwenu mkila pamoja au mbali mbali. Na mkiingia katika nyumba, toleaneni salamu, kuwa ni maamkio yanayotoka kwa Mwenyezi Mungu, yenye baraka na mema. Hivyo ndivyo Mwenyezi Mungu anavyo kubainishieni Aya zake ili mpate kuelewa.
(62) Hakika Waumini wa kweli ni wale waliomuamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake; na wanapokuwa pamoja naye kwa jambo la kuwakhusu wote hawaondoki mpaka wamtake ruhusa. Kwa hakika wale wanaokuomba ruhusa, hao ndio wanaomuamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Na wakikuomba ruhusa kwa baadhi ya kazi zao, mruhusu umtakaye miongoni mwao, uwaombee msamaha kwa Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu.
(63) Msifanye wito wa Mtume baina yenu kama wito wa nyinyi kwa nyinyi. Hakika Mwenyezi Mungu anawajua miongoni mwenu wanaoondoka kwa uficho. Basi na watahadhari wanaohalifu amri yake, usije ukawapata msiba au ikawapata adhabu chungu.
(64) Jueni kuwa hakika ni vya Mwenyezi Mungu vilivyomo mbinguni na ardhini. Hakika Yeye anajua mliyo nayo. Na siku mtakaporudishwa kwake atawaeleza waliyoyafanya. Na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa kila kitu.