43 - Surat Az-Zukhruf ()

|

(1) Ha Mim

(2) Ninaapa kwa Kitabu kinachobainisha.

(3) Hakika Sisi tumeifanya Qur-ani kwa Kiarabu ili mfahamu.

(4) Na hakika hiyo imo katika Asili ya Maandiko yaliyoko kwetu, ni tukufu na yenye hekima.

(5) Je, tuache kuwakumbusha kabisa kwa kuwa nyinyi ni watu mliopita mipaka kwa ukafiri?

(6) Na Manabii wangapi tuliwatuma kwa watu wa zamani!

(7) Na hawajii Nabii yeyote ila walikuwa wakimkejeli.

(8) Na tuliwaangamiza waliokuwa na nguvu kushinda wao. Na mfano wa watu wa zamani umekwisha pita.

(9) Na ukiwauliza: 'Nani aliyeziumba mbingu na ardhi?' Bila ya shaka watasema: 'Kaziumba Mwenye nguvu, ajuaye zaidi.'

(10) Ambaye amewafanyieni ardhi kama tandiko, na akawafanyieni ndani yake njia mpate kuongoka.

(11) Na ambaye ndiye aliyeteremsha kutoka mbinguni maji kwa kiasi, na kwa hayo tukaifufua nchi iliyokufa. Na namna hivi ndivyo mtakavyo tolewa.

(12) Na ambaye ndiye aliyeumba katika kila kitu jike na dume, na akawafanyieni merikebu na wanyama mnaowapanda.

(13) Ili mkae vizuri migongoni mwao, kisha mkumbuke neema za Mola wenu Mlezi mnapokaa sawa sawa juu yao, na mseme: 'Ametakasika aliyemfanya huyu atutumikie, na tusingeliweza kufanya haya wenyewe.'

(14) Na hakika sisi tutarudi kwa Mola wetu Mlezi.

(15) Na wanamfanyia katika waja wake fungu. Kwa hakika mwanadamu ni mtovu wa fadhila aliye dhahiri.

(16) Au amejichukulia watoto wanawake katika vile alivyoviumba, na akakuteulieni nyinyi watoto wanaume?

(17) Na anapobashiriwa mmoja wao kwa yale aliyompigia mfano Mwenyezi Mungu, uso wake husawijika na hujaa hasira.

(18) Ati aliyelelewa katika mapambo na katika mabishano hawezi kusema kwa bayana?

(19) Na wakawafanya Malaika, ambao ni waja wa Mwingi wa Rehema, ni wanawake! Kwani wameshuhudia kuumbwa kwao? Ushahidi wao utaandikwa na wao watahojiwa!

(20) Nao husema: 'Angelipenda Mwingi wa Rehema tusingeliwaabudu sisi.' Hawana ujuzi wowote wa hayo! Hawana ila kusema uwongo tu!

(21) Kwani tuliwapa Kitabu kabla ya hiki, na ikawa wao wanakishikilia hicho.

(22) Bali wanasema: 'Hakika sisi tuliwakuta baba zetu wanashika dini mahsusi, basi na sisi tunaongoza nyayo zao.'

(23) Na kadhaalika hatukumtuma mwonyaji kwenye mji wowote ila watu wake waliodeka kwa starehe walisema: 'Hakika sisi tuliwakuta baba zetu wanashika dini mahsusi, na sisi tunafuata nyayo zao.'

(24) Akasema (Mwonyaji): 'Hata nikiwaletea yenye uwongofu bora kuliko mliowakuta nao baba zenu?' Wakasema: 'Sisi tunayakataa tu hayo mliyotumwa nayo.'

(25) Kwa hivyo, tukawalipizia. Basi angalia ulikuwaje mwisho wa waliokadhibisha!

(26) Na pale Ibrahim alipomwambia baba yake na kaumu yake: 'Hakika mimi ninajitenga mbali na hayo mnayoyaabudu.'

(27) Isipokuwa yule aliyeniumba, kwani Yeye ataniongoa.'

(28) Na akalifanya hili liwe neno lenye kubaki katika vizazi vyake ili warejee.

(29) Bali tuliwastarehesha hawa na baba zao mpaka ikawafikia Haki na Mtume aliyebainisha.

(30) Na ilipowafikia Haki wakasema: 'Huu ni uchawi, na sisi hakika tunaukataa.'

(31) Na walisema: 'Kwa nini Qur-ani hii haikuteremshwa kwa mtu mkubwa katika miji miwili hii?'

(32) Kwani wao ndio wanaogawa rehema za Mola wako Mlezi? Sisi tumewagawanyia baina yao maisha yao katika uhai wa duniani, na tukawanyanyua baadhi yao juu ya wengine kwa daraja nyingi; kwa hivyo baadhi yao wanawafanya wenginewe wawatumikie. Na rehema za Mwenyezi Mungu ni bora kuliko hayo wanayoyakusanya.

(33) Na lau isingekuwa watu watakuwa kundi moja, tungeliwajaalia wanaomkufuru Rahmani nyumba zao kuwa na dari ya fedha, na ngazi zao pia wanazopandia

(34) Na milango ya nyumba zao na vitanda wanavyoegemea juu yake.

(35) Na mapambo. Lakini hayo si chochote ila ni starehe ya maisha ya dunia tu, na Akhera iliyoko kwa Mola wako Mlezi ni ya wenye kumcha Mungu.

(36) Anayeyafanyia upofu maneno ya Rahmani tunamwekea Shetani kuwa ndiye rafiki yake.

(37) Na hakika wao wanawazuilia Njia na wenyewe wanadhani kuwa wameongoka.

(38) Hata atakapotujia atasema: 'Laiti ungelikuweko baina yangu na wewe kama umbali baina ya mashariki na magharibi. Rafiki mwovu mno wewe!'

(39) Na kwa kuwa mlidhulumu, haitakufaeni kitu leo kwamba nyinyi mnashirikiana katika adhabu.

(40) Je, unaweza kuwasikilizisha viziwi, au unaweza kuwaongoa vipofu na waliomo katika upotofu ulio wazi?

(41) Na hata tukikuondoa, Sisi tutalipiza kisasi chetu kwao.

(42) Au tutakuonyesha tuliyowaahidi. Nasi bila ya shaka tuna uweza juu yao.

(43) Basi wewe yashike yaliyofunuliwa kwako. Hakika wewe uko kwenye Njia Iliyonyooka.

(44) Na hakika haya ni ukumbusho kwako na kwa kaumu yako. Na mtakuja ulizwa.

(45) Na waulize Mitume wetu tuliowatuma kabla yako: 'Je, tulifanya miungu mingine iabudiwe badala ya Rahmani?'

(46) Na bila ya shaka tulimtuma Musa kwa Ishara zetu aende kwa Firauni na waheshimiwa wake, na akasema: 'Hakika mimi ni Mtume wa Mola Mlezi wa walimwengu wote!'

(47) Lakini alipowajia na Ishara zetu, wakaingia kuzicheka.

(48) Na hatukuwaonyesha Ishara yoyote ila hiyo ilikuwa kubwa zaidi kuliko nyingineye. Na tukawakamata kwa adhabu ili warejee.

(49) Na wakasema: 'Ewe mchawi! Tuombee kwa Mola wako Mlezi kwa ile ahadi aliyokuahidi; hakika sisi tutakuwa wenye kuongoka.'

(50) Basi tulipowaondolea adhabu hiyo, mara wakaingia kuvunja ahadi.

(51) Na Firauni alitangaza kwa watu wake akisema: 'Enyi watu wangu! Kwani mimi si ninao huu ufalme wa Misri, na hii mito inapita chini yangu. Je, hamwoni?

(52) Au mimi si bora kuliko huyu aliye mnyonge, wala hawezi kusema waziwazi?

(53) Basi mbona hakuvikwa vikuku vya dhahabu au hawakuja Malaika pamoja naye wakamwandama?'

(54) Basi aliwachezea watu wake na wakamtii. Kwa hakika hao walikuwa watu wapotovu.

(55) Walipotukasirisha, tuliwapatiliza tukawazamisha wote!

(56) Kisha tukawafanya kuwa watangulizi na mfano kwa wa baadaye.

(57) Na alipopigiwa mfano Mwana wa Mariamu, watu wako waliupiga ukelele.

(58) Wakasema: 'Miungu yetu kwani si bora kuliko huyu?' Hawakukupigia mfano huo ila kwa ubishi tu. Bali hao ni watu wagomvi!

(59) Hakuwa yeye (Isa) ila ni Mtumwa tuliyemneemesha na tukamfanya ni mfano kwa Wana wa Israili.

(60) Na tungelipenda, tungeliwafanyia miongoni mwenu Malaika katika ardhi wakifuatana.

(61) Na kwa hakika yeye ni alama ya Saa ya Kiyama. Basi usiitilie shaka, na nifuateni. Hii ndiyo Njia Iliyonyooka.

(62) Wala asiwazuilie Shetani. Hakika yeye ni adui yenu wa dhahiri.

(63) Na alipokuja Isa na dalili zilizo wazi, alisema: 'Nimewajia na hekima na ili niwaeleze baadhi ya yale mliyokhitalifiana. Basi mcheni Mwenyezi Mungu, na mnitii mimi.

(64) Kwa hakika Mwenyezi Mungu ni Mola wangu Mlezi, na ni Mola wenu Mlezi. Basi muabuduni Yeye tu. Hii ndiyo Njia Iliyonyooka.'

(65) Lakini makundi kwa makundi yao yalikhitalifiana wao kwa wao. Ole wao waliodhulumu kwa adhabu ya siku chungu.

(66) Je, nini wanangojea ila Saa iwajie kwa ghafla na wala wao hawatambui?

(67) Siku hiyo marafiki watakuwa ni maadui wao kwa wao, isipokuwa wacha Mungu.

(68) Enyi waja wangu! Hamtakuwa na khofu siku hiyo, wala hamtahuzunika.

(69) Ambao waliziamini Ishara zangu na walikuwa Waislamu.

(70) Ingieni Peponi, nyinyi na wake zenu; mtafurahishwa humo.

(71) Watakuwa wanapitishiwa sahani za dhahabu na vikombe, na vitakuwemo ambavyo nafsi zinavipenda na macho yanavifurahia, na nyinyi mtakaa humo milele.

(72) Na hiyo ni Pepo mliyorithishwa kwa hayo mliyokuwa mkiyafanya.

(73) Mnayo humo matunda mengi mtakayoyala.

(74) Kwa hakika wakosefu watakaa katika adhabu ya Jahannamu.

(75) Hawatapumzishwa nayo, na humo watakata tamaa.

(76) Wala Sisi hatukuwadhulumu, bali wao ndio waliokuwa madhalimu.

(77) Nao watapiga kelele waseme: 'Ewe Malik! Na atufishe Mola wako Mlezi!' Naye aseme: 'Hakika nyinyi mtakaa humo humo!'

(78) Kwa yakini tulikuleteeni Haki, lakini wengi katika nyinyi mlikuwa mnaichukia Haki.

(79) Au waliweza kupitisha amri yao? Bali ni Sisi ndio tunaopitisha.

(80) Au wanadhani kwamba hatusikii siri zao na minong'ono yao? Wapi! Na wajumbe wetu wapo karibu nao, wanayaandika.

(81) Sema: 'Ingelikuwa Rahmani (Mwingi wa Rehema) ana mwana, basi mimi ningelikuwa wa kwanza kumuabudu.'

(82) Ametakasika Mola Mlezi wa mbingu na ardhi, Mola Mlezi wa A'rshi, na hayo wanayomsifia.

(83) Basi waache wapige porojo wakicheza mpaka wakutwe na hiyo siku yao waliyoahidiwa.

(84) Na Yeye ndiye Mungu mbinguni, na ndiye Mungu katika ardhi. Naye ndiye Mwenye hekima, Mwenye ujuzi.

(85) Na ametukuka Mwenye ufalme wa mbingu na ardhi na vilivyomo ndani yake. Na uko kwake ujuzi wa Saa ya Kiyama, na kwake Yeye mtarudishwa.

(86) Wala hao mnaowaomba badala yake Yeye hawana uweza wa kumwombea mtu, isipokuwa anayeshuhudia kwa haki, na wao wanajua.

(87) Na ukiwauliza ni nani aliyewaumba. Bila ya shaka watasema ni Mwenyezi Mungu! Basi ni wapi wanakogeuziwa?

(88) Na usemi wake (Mtume) ni: 'Ewe Mola wangu Mlezi! Hakika hawa ni watu wasioamini.

(89) Basi wasamehe, na uwaambie maneno ya salama. Watakuja jua.'