51 - Surat Adh-Dhariyat ()

|

(1) Ninaapa kwa pepo zinazotawanya.

(2) Na zinazobeba mizigo.

(3) Na zinazokwenda kwa wepesi.

(4) Na zinazogawanya kwa amri.

(5) Hakika mnayoahidiwa bila ya shaka ni kweli.

(6) Na kwa hakika malipo bila ya shaka yatatokea.

(7) Ninaapa kwa mbingu zenye njia.

(8) Hakika nyinyi bila ya shaka mmo katika kauli inayohitalifiana.

(9) Anageuzwa kutokana na haki mwenye kugeuzwa.

(10) Wazushi wameangamizwa.

(11) Ambao wameghafilika katika ujinga.

(12) Wanauliza: 'Ni lini hiyo siku ya malipo?'

(13) Hiyo ni siku watakayoadhibiwa Motoni.

(14) Onjeni adhabu yenu! Haya ndiyo mliyokuwa mkiyafanyia haraka.

(15) Hakika wacha Mungu watakuwa katika Mabustani ya mbinguni na chemchemi.

(16) Wanapokea yale aliyowapa Mola wao Mlezi. Kwa hakika hao walikuwa kabla ya haya wakifanya mema.

(17) Walikuwa wakilala kidogo tu usiku.

(18) Na kabla ya alfajiri wakiomba maghfira.

(19) Na katika mali yao ipo haki ya mwenye kuomba na asiyeomba.

(20) Na katika ardhi zipo Ishara kwa wenye yakini.

(21) Na pia katika nafsi zenu - Je, hamwoni?

(22) Na katika mbingu ziko riziki zenu na yale mnayoahidiwa.

(23) Basi ninaapa kwa Mola Mlezi wa mbingu na ardhi, hakika haya ni kweli kama ilivyo kweli kuwa nyinyi mnasema.

(24) Je, imekufikia hadithi ya wageni wa Ibrahim wanaoheshimiwa?

(25) Walipoingia kwake na wakasema: 'Salama!' Na yeye akasema: 'Salama! Nyinyi ni watu nisiowajua.'

(26) Basi akaenda kwa ahali yake na akaja na ndama aliyenona.

(27) Akawakaribishia, akasema: 'Mbona hamli?'

(28) Kwa hivyo, akahisi kuwaogopa katika nafsi yake. Wakasema: 'Usiwe na hofu.' Basi wakambashiria kupata kijana mwenye elimu.

(29) Ndipo mkewe akawaelekea, na huku anasema na akijipiga usoni kwa mastaajabu, na kusema: Mimi ni kikongwe na tasa!

(30) Wakasema: Ndivyo vivyo hivyo alivyosema Mola wako Mlezi. Hakika Yeye ni Mwenye hekima, Mwenye kujua.

(31) Akasema: 'Basi ujumbe wenu ni nini, enyi mliotumwa?'

(32) Wakasema: 'Hakika sisi tumetumwa kwa watu wakosefu.'

(33) Tuwatupie mawe ya udongo.

(34) Yaliyotiwa alama kutoka kwa Mola wako Mlezi kwa ajili ya wanaopindukia mipaka.

(35) Kwa hivyo tutawatoa katika hao wale walioamini.

(36) Lakini hatukupata humo ila nyumba moja tu yenye Waislamu!

(37) Na tukaacha humo Ishara kwa ajili ya wanaoiogopa adhabu chungu.

(38) Na katika habari za Musa, tulipomtuma kwa Firauni na hoja wazi.

(39) Lakini alipuuza kwa sababu ya nguvu zake na akasema: 'Huyu ni mchawi au mwendawazimu!'

(40) Basi tukamkamata yeye na majeshi yake na tukawatupa baharini, na yeye ndiye wa kulaumiwa.

(41) Na katika habari za 'Adi tulipowatumia upepo wa kukata uzazi.

(42) Haukuacha chochote ulichokifikia ila ulikifanya kama kilichonyambuka.

(43) Na katika habari za Thamudi walipoambiwa: 'Jifurahisheni kwa muda mdogo tu.'

(44) Wakaasi amri ya Mola wao Mlezi. Basi ukawanyakua moto wa radi nao wanaona.

(45) Basi hawakuweza kusimama wala hawakuwa wenye kujitetea.

(46) Na kaumu ya Nuhu hapo mbele. Hakika hao walikuwa watu wapotovu.

(47) Na mbingu tumezifanya kwa nguvu na uwezo na hakika Sisi bila ya shaka ndio wenye uwezo wa kuzitanua.

(48) Na ardhi tumeitandaza; basi watandazaji wazuri namna gani Sisi!

(49) Na katika kila kitu tumeumba kwa jozi ili mzingatie.

(50) Basi kimbilieni kwa Mwenyezi Mungu, hakika mimi ni mwonyaji kwenu wa kubainisha nitokae kwake.

(51) Wala msifanye kuwa kuna mungu mwengine pamoja na Mwenyezi Mungu. Hakika mimi ni mwonyaji kwenu wa kubainisha nitokae kwake.

(52) Basi ndio hivyo hivyo, hakuwajia kabla yao Mtume ila walisema: 'Huyu ni mchawi au mwendawazimu.'

(53) Je, wameambizana kwa haya? Bali hawa ni watu waasi.

(54) Basi waachilie mbali, nawe hulaumiwi.

(55) Na kumbusha, kwani ukumbusho huwafaa Waumini.

(56) Nami sikuwaumba majini na watu ila waniabudu Mimi.

(57) Na sitaki kwao riziki, wala sitaki wanilishe.

(58) Hakika Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kuruzuku, Mwenye nguvu, Madhubuti.

(59) Hakika wale waliodhulumu wana fungu lao la adhabu kama fungu la wenzao. Basi wasiniharakishe.

(60) Basi ole wao wale walioikanusha siku yao waliyoahidiwa.