(1) Ewe Nabii! Mtakapowapa talaka wanawake, basi wapeni talaka katika wakati wa eda zao. Na fanyeni hisabu ya eda. Na mcheni Mwenyezi Mungu, Mola wenu Mlezi. Msiwatoe katika nyumba zao, wala wasitoke wenyewe, ila wakifanya jambo la uchafu ulio wazi. Hiyo ndiyo mipaka ya Mwenyezi Mungu, msiikiuke. Na mwenye kuikiuka mipaka ya Mwenyezi Mungu, basi hakika amejidhulumu nafsi yake. Hujui; labda Mwenyezi Mungu ataleta jambo jingine baada ya haya.
(2) asi wanapofikia muda wao, ima warejeeni muwaweke kwa wema, au farikianeni nao kwa wema. Na mshuhudishe mashahidi wawili waadilifu miongoni mwenu. Na simamisheni ushahidi kwa ajili ya Mwenyezi Mungu. Hayo anaaidhiwa kwayo anayemuamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho. Na anayemcha Mwenyezi Mungu, humtengezea njia ya kutokea.
(3) Na humruzuku kutokea asipotazamia. Na anayemtegemea Mwenyezi Mungu, Yeye humtosha. Hakika Mwenyezi Mungu anatimiza amri yake. Mwenyezi Mungu kajaalia kila kitu na kipimo chake.
(4) Na wale waliosita hedhi miongoni mwa wanawake wenu, ikiwa mnayo shaka, basi muda wa eda yao ni miezi mitatu, pamoja na ambao hawapati hedhi. Na wenye mimba, eda yao mpaka watakapozaa. Na anayemcha Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu humfanyia mambo yake kuwa mepesi.
(5) Hiyo ni amri ya Mwenyezi Mungu amekuteremshieni. Na anayemcha Mwenyezi Mungu, atamfutia maovu yake, na atampa ujira mkubwa.
(6) Wawekeni humo humo mnamokaa nyinyi kwa kiasi cha pato lenu, wala msiwaletee madhara kwa kuwapa dhiki. Na wakiwa wana mimba, wagharimieni mpaka wajifungue. Na wakikunyonyesheeni, basi wapeni ujira wao, na shaurianeni kwa wema. Na mkiona uzito kati yenu, basi amnyonyeshee mwanamke mwingine.
(7) Mwenye wasaa atoe kiasi ya wasaa wake, na mwenye dhiki, atoe katika kile ambacho Mwenyezi Mungu alimpa. Mwenyezi Mungu hamjukumishi mtu ila kwa kiasi cha alichompa. Mwenyezi Mungu atajaalia baada ya dhiki faraja.
(8) Na miji mingapi iliyovunja amri ya Mola wake Mlezi na Mitume wake, basi tuliihisabia hisabu ngumu na tukaiadhibu kwa adhabu kali.
(9) Basi ikauonja ubaya wa mambo yake; na mwisho wa mambo yao ilikuwa hasara.
(10) Mwenyezi Mungu aliwaandalia adhabu kali. Basi mcheni Mwenyezi Mungu, enyi wenye akili, mlioamini! Hakika Mwenyezi Mungu amekuteremshieni Ukumbusho.
(11) Mtume anayekusomeeni Aya za Mwenyezi Mungu zinazobainisha, ili kuwatoa wale walioamini na wakatenda mema kutoka vizani kuwapeleka kwenye nuru. Na mwenye kumuamini Mwenyezi Mungu na akatenda mema, atamwingiza katika Bustani za mbinguni zipitazo mito kati yake, wadumu humo milele. Mwenyezi Mungu amekwisha mpa riziki nzuri.
(12) Mwenyezi Mungu ni yule ambaye ameziumba mbingu saba, na ardhi kwa mfano wa hizo. Amri zake zinashuka baina yake, ili mjue kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwenye uweza mno juu ya kila kitu, na kwamba Mwenyezi Mungu amekizunguka kila kitu kukijua vilivyo kwa elimu yake.