85 - Surat Al-Buruj ()

|

(1) Ninaapa kwa mbingu yenye Buruji!

(2) Na kwa siku iliyoahidiwa!

(3) Na kwa shahidi na kinachoshuhudiwa!

(4) Wameangamizwa watu wa makhandaki.

(5) Yenye moto wenye kuni nyingi.

(6) Walipokuwa wamekaa hapo.

(7) Na wao ni mashahidi wa yale waliyokuwa wakiwafanyia Waumini.

(8) Nao hawakuona baya lolote kwao ila kuwa wakimuamini Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, Msifiwa.

(9) Ambaye anao ufalme wa mbingu na ardhi; na Mwenyezi Mungu ni shahidi wa kila kitu.

(10) Hakika waliowafitini Waumini wanaume na Waumini wanawake, kisha hawakutubu, basi watapata adhabu ya Jahannamu na watapata adhabu ya kuungua.

(11) Hakika walioamini na wakatenda mema watapata Bustani zenye mito ipitayo kati yake. Huko ndiko kufuzu kukubwa.

(12) Hakika kutesa kwa Mola wako Mlezi ni kukali.

(13) Yeye ndiye anayeanzisha na ndiye anayerejeza tena.

(14) Naye ni Mwenye kusamehe, Mwenye mapenzi.

(15) Mwenye Kiti cha Enzi, Mtukufu.

(16) Atendaye ayatakayo.

(17) Je! Zimekuwasilia habari za majeshi?

(18) Ya Firauni na Thamudi?

(19) Lakini waliokufuru wamo katika kukadhibisha.

(20) Na Mwenyezi Mungu nyuma yao amewazunguka.

(21) Bali hii ni Qur-ani tukufu.

(22) Katika Ubao Uliohifadhiwa.