(1) Ha, Mim.
(2) Uteremsho wa Kitabu uliotoka kwa Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, Mwenye hekima.
(3) Hatukuziumba mbingu na ardhi wala yaliyomo baina yake ila kwa haki na kwa muda maalumu. Na wale waliokufuru wanayapuuza yale wanayoonywa.
(4) Sema: 'Je, mwawaona wale mnaowaomba badala ya Mwenyezi Mungu? Nionyesheni wameumba nini katika ardhi; au hao wanao ushirika katika mbingu zote? Nileteeni Kitabu kilichokuwa kabla ya hiki, au alama yoyote ya elimu, ikiwa mnasema kweli.
(5) Na ni nani mpotofu mkubwa kuliko hao wanaoomba badala ya Mwenyezi Mungu wale ambao hawatawaitikia mpaka Siku ya Kiyama, na wala hata hawatambui maombi yao.
(6) Na ambao watu watakapokusanywa watakuwa maadui zao, na wataikataa ibada yao.
(7) Na wanaposomewa Aya zetu zilizo wazi, wale waliokufuru husema juu ya haki inapowajia: 'Huu ni uchawi dhahiri.'
(8) Au wanasema: 'Ameizua mwenyewe!' Sema: 'Ikiwa nimeizua mimi, basi nyinyi hamwezi kunifaa chochote mbele ya Mwenyezi Mungu. Yeye anajua zaidi hayo mnayoropokwa; anatosha kuwa shahidi baina yangu na nyinyi. Na Yeye ndiye Mwenye kusamehe mno, Mwingi wa kurehemu.'
(9) Sema: 'Mimi si kitu kigeni miongoni mwa Mitume. Wala sijui nitakavyofanywa mimi wala nyinyi. Mimi nafuata niliyofunuliwa tu kwa Wahyi, wala mimi si chochote ila ni mwonyaji wa wazi wazi.'
(10) Sema: 'Mnaonaje yakiwa haya ni kweli yametoka kwa Mwenyezi Mungu, nanyi mmeyakufuru, na akashuhudia shahidi miongoni mwa Wana wa Israili juu ya mfano wa haya, na akaamini, na nyinyi mnafanya kiburi? Hakika Mwenyezi Mungu hawaongoi watu wenye kudhulumu.'
(11) Na wale waliokufuru waliwaambia wale walioamini: 'Lau kuwa hii ni heri, wasingelitutangulia kuifikia.' Na walipokosa kuongoka, wakasema: 'Huu ni uzushi mkubwa wa zamani.'
(12) Na kabla yake kilikuwapo Kitabu cha Musa, kuwa chenye uwongozi na rehema. Na hiki ni Kitabu cha kusadikisha na kilichokuja kwa lugha ya Kiarabu, ili kiwaonye wale waliodhulumu, na kiwe ni bishara njema kwa watendao mema.
(13) Hakika wale waliosema: 'Mola wetu Mlezi ni Mwenyezi Mungu' kisha wakanyooka sawasawa, hawatakuwa na hofu, wala hawatahuzunika.
(14) Hao ndio watu wa Bustani za mbinguni, watadumu humo, kuwa ni malipo kwa yale waliyokuwa wakiyatenda.
(15) Na tumemuusia mwanadamu awatendee wema wazazi wake wawili. Mama yake amechukua mimba yake kwa taabu, na akamzaa kwa taabu. Na kuchukua mimba kwake hata kumwachisha ziwa ni miezi thelathini. Hata anapofika utu uzima wake, na akafikilia miaka arubaini, husema: 'Mola wangu Mlezi! Niwezeshe nishukuru neema zako ulizonineemesha mimi na wazazi wangu, na nitende mema unayoyapenda. Na unitengenezee dhuriya zangu. Hakika mimi nimetubu kwako, na hakika mimi ni miongoni mwa Waislamu.'
(16) Hao ndio tunaowapokelea bora ya vitendo vyao walivyovitenda, na tunayasamehe makosa yao. Watakuwa miongoni mwa watu wa Bustani za mbinguni. Miadi ya kweli hiyo waliyokuwa wakiahidiwa.
(17) Na yule aliyewafyonya wazazi wake: 'Uff kwenu nyote. Ati ndio mnanitisha kuwa nitafufuliwa, na hali vizazi vingi vimekwishapita kabla yangu!' Na hao wazazi humwomba msaada Mwenyezi Mungu (na humwambia mtoto wao): 'Ole wako! Amini! Hakika ahadi ya Mwenyezi Mungu ni kweli.' Na yeye husema: 'Hayakuwa haya ila ni visa vya watu wa kale.'
(18) Hao ndio ambao imehakikikishwa hukumu juu yao kama mataifa yaliyokwisha pita kabla yao miongoni mwa majini na watu. Hakika hao wamekuwa wenye kuhasiri.
(19) Na wote watakuwa na daraja zao mbalimbali kwa waliyoyatenda, na ili awalipe kwa ukamilifu kwa vitendo vyao, na wala hawatadhulumiwa.
(20) Na siku watakapoletwa wale waliokufuru kwenye Moto, wataambiwa: 'Nyinyi mlitwaa vitu vyenu vizuri katika uhai wa duniani, na mkajistarehesha navyo. Basi leo ndio mnalipwa adhabu ya fedheha kwa yale mlivyokuwa mkitakabari katika ardhi bila ya haki, na kwa sababu mlikuwa mkivuka mipaka.'
(21) Na mtaje ndugu wa kina 'Adi, alipowaonya watu wake kwenye vilima vya mchanga. Na kwa yakini waonyaji wengi walitokea kabla yake na baada yake kuwaambia: 'Msimuabudu isipokuwa Mwenyezi Mungu. Hakika mimi nawahofia ije kuwapateni adhabu ya siku iliyo kuu.'
(22) Wakasema: 'Je, umetujia ili ututenge mbali na miungu yetu? Basi tuletee hayo unayotuahidi ikiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli.'
(23) Akasema: 'Hakika ujua wa hayo uko kwa Mwenyezi Mungu. Mimi nawafikishieni yale niliyotumwa nayo. Lakini nawaona kuwa nyinyi mnafanya ujinga tu.'
(24) Basi walipoliona wingu likielekea kwenye mabonde yao, walisema: 'Hili ni wingu la kutunyeshea mvua!' Kumbe sivyo, haya ni hayo mliyotaka yawajie haraka: upepo ambao ndani yake imo adhabu chungu!
(25) Unaharibu kila kitu kwa amri ya Mola wake Mlezi. Wakawa hawaonekani ila nyumba zao tu. Hivyo ndivyo tuwalipavyo watu wahalifu!
(26) Na bila ya shaka tuliwaweka vizuri siyo kama tulivyokuwekeni nyinyi, na tuliwapa masikio, na macho, na nyoyo. Na hayakuwafaa kitu masikio yao, wala macho yao, wala nyoyo zao kwa lolote. Kwani hao walikuwa wakizikataa Ishara za Mwenyezi Mungu, na yale waliyokuwa wakiyafanyia masihara ndiyo yakawafika.
(27) Na hakika tuliiangamiza miji iliyo jirani zenu, na tulizitumia Ishara mbalimbali ili wapate kurejea.
(28) Basi mbona wale waliowashika badala ya Mwenyezi Mungu, kuwa ati hao ndio wawakurubishe, hawakuwanusuru? Bali waliwapotea! Na huo ndio uwongo mkubwa waliokuwa wakiuzua.
(29) Na wakati tulipowaleta kundi la majini kuja kwako kusikiliza Qur-ani. Basi walipoihudhuria, walisema: 'Sikilizeni!' Na ilipokwisha somwa, walirudi kwa kaumu yao kwenda kuwaonya.
(30) Wakasema: 'Enyi kaumu yetu! Hakika sisi tumesikia Kitabu kilichoteremshwa baada ya Musa, kinachosadikisha yale yaliyokuwa kabla yake, na kinachoongoza kwenye Haki na kwenye njia iliyonyooka.
(31) Enyi kaumu yetu! Muitikieni Mwenye kuitia kwa Mwenyezi Mungu, na muaminini, Mwenyezi Mungu atawasamehe, na atawakinga adhabu chungu.
(32) Na wasiomwitikia Mwitaji wa Mwenyezi Mungu, basi hao hawatashinda katika ardhi, wala hawatakuwa na walinzi mbele yake. Hao wamo katika upotovu ulio dhahiri.
(33) Je, hawaoni ya kwamba Mwenyezi Mungu, aliyeziumba mbingu na ardhi, na hakuchoka kwa kuziumba, kuwa ni Muweza wa kuwafufua wafu? Kwani? Hakika Yeye ni Muweza mno wa kila kitu.
(34) Na siku watakapoletwa makafiri Motoni, wakaambiwa: 'Je, haya si kweli?' Watasema: 'Ndivyo? Tunaapa kwa Mola wetu Mlezi, ni kweli!' Atasema: 'Basi onjeni adhabu kwa sababu ya vile mlivyokuwa mkikufuru.'
(35) Basi subiri, kama walivyosubiri Mitume wenye stahmala kubwa, wala usiwafanyie haraka. Siku watakayoyaona hayo waliyoahidiwa, itakuwa kama kwamba hawakukaa ulimwenguni ila saa moja ya mchana. Huu ndio ufikisho! Kwani huangamizwa wengine isipokuwa watu wavukao mipaka tu?