(1) Ewe uliyejigubika!
(2) Simama uonye!
(3) Na Mola wako Mlezi mtukuze!
(4) Na nguo zako, zisafishe.
(5) Na yaliyo machafu yahame!
(6) Wala usitoe kwa kutaraji kuzidishiwa.
(7) Na kwa ajili ya Mola wako Mlezi, subiri!
(8) Basi litakapopulizwa barugumu,
(9) Siku hiyo, basi, itakuwa siku ngumu.
(10) Kwa makafiri haitakuwa nyepesi.
(11) Niache peke yangu na niliyemuumba.
(12) Na nikamjaalia awe na mali mengi.
(13) Na wana wanaoonekana.
(14) Na nikamtegenezea mambo vizuri kabisa.
(15) Kisha anatumai nimzidishie!
(16) Hasha! Kwani hakika yeye alikuwa akizifanyia inadi Aya zetu!
(17) Nitamtesa kwa mateso yasiowezekana.
(18) Kwani hakika yeye alifikiri na akapima.
(19) Basi ameangamia! Vipi alivyopima!
(20) Tena ameangamia! Vipi alivyopima!
(21) Kisha akatazama.
(22) Kisha akakunja kipaji, na akanuna.
(23) Kisha akaipa kisogo haki, na akatakabari.
(24) Na akasema: Haya si chochote ila ni uchawi ulionukuliwa.
(25) Haya si chochote ila kauli ya binaadamu.
(26) Nitakuja mtia kwenye Moto wa Saqar.
(27) Na nini kitakujuulisha ni nini huo Moto wa Saqar?
(28) Haubakishi wala hausazi.
(29) Unababua ngozi iwe nyeusi.
(30) Juu yake wapo kumi na tisa.
(31) Na hatukuwafanya walinzi wa Motoni ila ni Malaika, wala hatukuifanya idadi yao hiyo ila kuwatatanisha waliokufuru, wapate kuwa na yakini waliopewa Kitabu, na wazidi Imani wale walioamini, wala wasiwe na shaka waliopewa Kitabu na Waumini, na wapate kusema wenye maradhi katika nyoyo zao na makafiri: Mwenyezi Mungu amekusudia nini kwa mfano huu? Ndiyo kama hivyo Mwenyezi Mungu humwacha apotee amtakaye, na humwongoa amtakaye. Na hapana yeyote anayejua majeshi ya Mola wako Mlezi ila Yeye tu. Na haya si chochote ila ni ukumbusho kwa binaadamu.
(32) Hasha! Naapa kwa mwezi!
(33) Na kwa usiku unapokucha!
(34) Na kwa asubuhi inapopambazuka!
(35) Hakika huo Moto ni katika mambo yaliyo makubwa kabisa!
(36) Ni onyo kwa binaadamu.
(37) Kwa anayetaka miongoni mwenu kutangulia au kuchelewa.
(38) Kila nafsi imo rahanini kwa mabaya iliyoyachuma.
(39) Isipokuwa watu wa kuliani.
(40) Hao watakuwa katika Mabustani, wawe wanaulizana
(41) Habari za wakosefu:
(42) Ni nini kilichokupelekeni Motoni?
(43) Waseme: Hatukuwa miongoni waliokuwa wakisali.
(44) Wala hatukuwa tukiwalisha masikini.
(45) Na tulikuwa tukizama pamoja na waliozama katika maovu.
(46) Na tulikuwa tukiikanusha siku ya malipo.
(47) Mpaka yakini ilipotufikia.
(48) Basi hautawafaa kitu uombezi wa waombezi.
(49) Basi wana nini hata wanapuuza onyo hili?
(50) Kana kwamba wao ni mapunda waliotimuliwa.
(51) Wanaomkimbia simba!
(52) Ati kila mmoja katika wao anataka apewe nyaraka zilizofunuliwa.
(53) Hasha! Kwani wao hawaiogopi Akhera?
(54) Hasha! Kwa hakika huu ni ukumbusho!
(55) Basi anayetaka atakumbuka.
(56) Na hawatakumbuka isipokuwa Mwenyezi Mungu atake. Uchamngu ni kwake Yeye, na msamaha ni wake Yeye.