21 - Surat Al-Anbiya ()

|

(1) Imewakaribia watu hesabu yao, nao wako katika kughafilika wanapuuza.

(2) Hauwajii ukumbusho mpya kutoka kwa Mola wao Mlezi isipokuwa huusikiliza na huku wanafanya mchezo.

(3) Zimeghafilika nyoyo zao. Na wale waliodhulumu hunong'onezana kwa siri: Ni nani ati huyu isipokuwa ni mtu tu kama nyinyi! Je, mnauendea uchawi ilhali nyinyi mnaona?

(4) Alisema: Mola wangu Mlezi anayajua yasemwayo mbinguni na katika ardhi. Na Yeye ni Mwenye kusikia yote, Mwenye kujua vyema.

(5) Lakini wao walisema: Hizo ni ndoto za ovyo ovyo, bali amezizua tu, bali huyo ni mtunga mashairi. Basi atuletee miujiza kama walivyotumwa wale wa mwanzo.

(6) Hawakuamini kabla yao watu wa mji wowote tuliouangamiza. Basi, je, hawa ndio wataamini?

(7) Na hatukuwatuma kabla yako isipokuwa wanaume tuliowafunulia wahyi. Basi waulizeni wenye elimu ikiwa nyinyi hamjui.

(8) Wala hatukuwafanya miili isiyokula chakula, wala hawakuwa wenye kuishi milele.

(9) Kisha tukawatimizia miadi, na tukawaokoa wao na wale tuliowataka, na tukawaangamiza wale waliopitiliza mipaka.

(10) Na hakika tumewateremshia Kitabu ambacho ndani yake kuna ukumbusho wenu. Je, hamtumii akili?

(11) Na ni mingapi katika miji iliyokuwa ikidhulumu tumeiteketeza, na tukawasimamisha baada yao kaumu wengine.

(12) Basi walipoihisi adhabu yetu, tazama, wakaanza kuikimbia.

(13) Msikimbie! Na rejeeni kwenye yale yale mliyostareheshwa kwayo, na maskani zenu, ili mpate kuulizwa!

(14) Wakasema: Ole wetu! Hakika sisi tulikuwa madhalimu.

(15) Basi hakikuacha hicho kuwa ndicho kilio chao mpaka tukawafanya kama waliofyekwa, wamezimika.

(16) Na hatukuziumba mbingu na ardhi na vilivyo baina ya hivyo kwa mchezo.

(17) Kama tungelitaka kufanya pumbao, tungejifanyia Sisi wenyewe, lau kwamba tungelikuwa ni wafanyao hivyo.

(18) Bali tunaitupa haki juu ya batili, ikaivunja na mara ikatoweka. Na ole wenu kwa mnayoyazua.

(19) Na ni vyake Yeye tu vilivyomo mbinguni na katika ardhi. Na wale walioko kwake hawafanyi kiburi wakaacha kumuabudu, wala hawachoki.

(20) Wanamtakasa usiku na mchana, wala hawanyong'onyei.

(21) Au wamejifanyia miungu katika ardhi inayofufua?

(22) Lau wangelikuwamo humo miungu wengine isipokuwa Mwenyezi Mungu, basi bila ya shaka hizo mbingu na ardhi zingelihaliribika. Subahanallah (Ametakasika Mwenyezi Mungu), Bwana wa 'Arshi (Kiti cha Enzi) kutokana na hayo wanayoyazua.

(23) Yeye haulizwi kwa ayatendayo, na wao ndio wanaoulizwa kwa wayatendayo.

(24) Au wamejifanyia miungu mingine badala yake? Sema: Leteni ushahidi wenu! Haya ni ukumbusho wa hawa walio pamoja nami, na ukumbusho wa walio kabla yangu. Lakini wengi wao hawaijui haki, na kwa hivyo wanapeana mgongo.

(25) Na hatukumtuma kabla yako Mtume yeyote isipokuwa tulimfunulia ya kwamba hapana mungu isipokuwa Mimi. Basi niabuduni Mimi tu.

(26) Na wanasema: Arrahman (Mwingi wa rehema) alijifanyia mwana! Subhanahu (Ametakasika na hayo!) Bali hao (wanaowaita wana) ni waja waliotukuzwa.

(27) Hawamtangulii kwa neno, nao wanafanya amri zake.

(28) Anayajua yaliyo mbele yao na yaliyo nyuma yao. Wala hawamfanyii yeyote uombezi isipokuwa yule anayemridhia Yeye, nao kwa sababu ya kumhofu wanaogopa.

(29) Na yeyote kati yao atakayesema: Mimi ni mungu, badala yake, basi huyo tutamlipa malipo yake Jahannamu. Hivyo ndivyo tuwalipavyo madhalimu.

(30) Je, hao waliokufuru hawakuona kwamba mbingu na ardhi zilikuwa zimeambatana, kisha Sisi tukazibandua? Na tukajaalia kwa maji kila kilicho hai? Basi je, hawaamini?

(31) Na tukaweka katika ardhi milima iliyo thabiti ili isiwayumbishe, na tukaweka humo njia pana ili wapate kuongoka.

(32) Na tukaifanya mbingu kuwa dari iliyohifadhiwa, lakini wanazipuuza Ishara zake.

(33) Na Yeye ndiye aliyeumba usiku na mchana na jua na mwezi, vyote katika anga vinaogelea.

(34) Nasi hatukumjaalia mwanadamu yeyote kabla yako kuwa na uhai wa milele. Basi je, ukifa wewe, wao wataishi milele?

(35) Kila nafsi itaonja mauti; na tunawajaribu kwa mtihani wa maovu na heri. Na kwetu Sisi mtarejeshwa.

(36) Na wanapokuona wale waliokufuru, hawakufanyi wewe isipokuwa ni kitu cha masihara tu, (wakisema): Je, huyu ndiye anayeitaja miungu yenu? Na hali wao wanakufuru kumkumbuka Arrahman (Mwingi wa Rehema)!

(37) Mwanadamu ameumbwa na haraka. Nitawaonyesha Ishara zangu. Basi msinihimize.

(38) Na wanasema: Ahadi hii itatokea lini, ikiwa nyinyi mnasema kweli?

(39) Lau wangelijua wale waliokufuru wakati ambao hawatauzuia Moto kwenye nyuso zao wala migongo yao, na wala hawatanusuriwa!

(40) Bali utawafikia kwa ghafla, na utawashitua na wala hawataweza kuurudisha, wala hawatapewa muhula!

(41) Na Mitume walio kabla yako walikwisha dhihakiwa. Kwa hivyo wale waliowafanyia masikhara yaliwafika yale waliyokuwa wakiyafanyia dhihaka.

(42) Sema: Ni nani anayewalinda usiku na mchana kutokana na Arrahmani (Mwingi wa Rehema)? Bali wao wanapuuza kumkumbuka Mola wao Mlezi.

(43) Au wao wanao miungu watakaoweza kuwakinga kutokana nasi? Hao hawawezi kujinusuru wao wenyewe, wala hawatalindwa kutokana nasi!

(44) Bali tuliwastarehesha hawa na baba zao mpaka umri ukawa mrefu kwao. Je, hawaoni ya kwamba Sisi tunaijia ardhi tukiipunguza kutokea kwenye ncha zake? Basi je, hao ndio watashinda?

(45) Sema: Mimi ninawaonya kwa Wahyi. Na viziwi hawasikii wito wanapoonywa.

(46) Na wanapoguswa na mpulizo mmoja tu wa adhabu itokayo kwa Mola wako Mlezi, bila ya shaka wao husema: Ole wetu! Hakika tulikuwa wenye kudhulumu.

(47) Nasi tutaweka mizani za uadilifu kwa Siku ya Kiyama. Basi nafsi haitadhulumiwa kitu chochote. Hata ikiwa ni uzito wa chembe ya khardali tutaileta. Nasi tunatosha kuwa washika hisabu.

(48) Na kwa yakini tuliwapa Musa na Haaruni kipambanuzi, na mwangaza, na makumbusho kwa wachamungu,

(49) Ambao wanamkhofu Mola wao Mlezi faraghani, na wanaiogopa Saa ya Kiyama.

(50) Na haya ni makumbusho yaliyobarikiwa, tuliyoyateremsha. Basi je! Mnayakataa?

(51) Na hakika tulikwisha mpa Ibrahim uwongofu wake zamani, na tulikuwa tunamjua.

(52) Alipomwambia baba yake na watu wake: Ni nini haya masanamu mnayoshughulika kuyaabudu?

(53) Wakasema: Tumewakuta baba zetu wakiyaabudu.

(54) Akasema: Bila ya shaka nyinyi na baba zenu mmekuwa katika upotofu ulio dhaahiri.

(55) Wakasema: Je, umetujia kwa maneno ya kweli au wewe ni katika wachezao tu?

(56) Akasema: Bali Mola wenu Mlezi ni Mola Mlezi wa mbingu na ardhi ambaye ndiye aliyeziumba. Na mimi ni katika wenye kuyashuhudia hayo.

(57) Na naapa kwa Mwenyezi Mungu! Nitayafanyia vitimbi masanamu yenu haya baada ya mkishageuka kwenda zenu.

(58) Basi akayavunja vipande vipande, ila kubwa lao, ili wao walirudie.

(59) Wakasema: Nani aliyeifanyia haya miungu yetu? Hakika huyu ni katika waliodhulumu.

(60) Wakasema: Tumemsikia kijana mmoja akiwataja. Anaitwa Ibrahim.

(61) Wakasema: Mleteni mbele ya macho ya watu, ili wapate kumshuhudia!

(62) Wakasema: Je! Wewe umeifanyia haya miungu yetu, ewe Ibrahim?

(63) Akasema: Bali amefanya hayo huyu mkubwa wao. Basi waulizeni ikiwa wanaweza kutamka.

(64) Basi wakajirudi, wakasema: Hakika nyinyi mlikuwa madhalimu!

(65) Kisha wakarejea kwenye ule ule upotovu wao wakasema: Wewe unajua kwamba hawa hawesemi.

(66) Akasema: Basi nyinyi mnawaabudu asiyekuwa Mwenyezi Mungu wasiowafaa kitu wala kuwadhuru?

(67) Aibu yenu nyinyi na hivyo mnavyoviabudu badala ya Mwenyezi Mungu! Basi nyinyi hamtii akilini?

(68) Wakasema: Mchomeni moto, na muinusuru miungu yenu, ikiwa nyinyi ni watendao jambo!

(69) Sisi tukasema: Ewe moto! Kuwa baridi na salama kwa Ibrahim!

(70) Wao walimkusudia maovu, lakini Sisi tukawafanya wao ndio waliokhasiri.

(71) Na tukamwokoa yeye na Luuti tukawapeleka kwenye nchi tulioibariki kwa ajili ya walimwengu wote.

(72) Naye tukampa Is-haq, na Yaaqub kuwa ni ziada. Na wote tukawajaalia wawe watu wema.

(73) Na tukawafanya maimamu wakiongoa watu kwa amri yetu. Na tukawafunulia watende kheri, na washike Sala, na watoe Zaka; na walikuwa wanatuabudu Sisi tu."

(74) Na Lut tukampa hukumu na elimu na tukamwokoa kutokana na ule mji uliokuwa ukifanya machafu. Hakika hao walikuwa watu wabaya, wavukao mipaka.

(75) Na tukamuingiza katika rehema yetu. Hakika yeye ni miongoni mwa walio wema.

(76) Na Nuhu alipoita zamani, nasi tukamuitikia, na tukamwokoa yeye na watu wake kutokana na shida kubwa.

(77) Na tukamnusuru na watu waliozikanusha Ishara zetu. Hakika hao walikuwa watu wabaya. Basi tukawazamisha wote.

(78) Na Daud na Suleiman walipokata hukumu katika kadhiya ya konde walipolisha humo mbuzi wa watu usiku. Na Sisi tulikuwa wenye kushuhudia hukumu yao hiyo.

(79) Basi tukamfahamisha Suleiman. Na kila mmoja wao tulimpa hukumu na elimu. Na tuliifanya milima na ndege kuwa pamoja na Daud imnyenyekee na imtakase Mwenyezi Mungu. Na Sisi ndio tulioyafanya hayo.

(80) Na tukamfundisha kuunda mavazi ya vita kwa ajili yenu ili yawahifadhi katika kupigana kwenu. Je, mtakuwa wenye kushukuru?

(81) Na tukamsahilishia Suleiman upepo wa kimbunga wendao kwa amri yake kwenye ardhi tuliyoibarikia. Na Sisi ndio tunaojua kila kitu.

(82) Na pia mashetani wanaompigia mbizi na kufanya kazi nyenginezo. Na Sisi tulikuwa walinzi wao.

(83) Na Ayyubu, alipomwita Mola wake Mlezi, akasema: Mimi yamenipata madhara. Na Wewe ndiye unayerehemu kuliko wote wanaorehemu.

(84) Basi tukamwitikia, na tukamwondolea madhara aliyokuwa nayo, na tukampa watu wake na mfano wao pamoja nao kuwa ni rehema inayotoka kwetu, na ukumbusho kwa wafanyao ibada.

(85) Na Ismail, na Idris, na Dhulkifli - wote walikuwa miongoni mwa wanaooubiri.

(86) Na tukawaingiza katika rehema yetu. Hakika wao walikuwa katika watu wema.

(87) Na Dhun-Nun alipoondoka hali ameghadhabika, na akadhani ya kwamba hatutakuwa na uwezo juu yake. Basi aliita katika giza: Hapana mungu isipokuwa Wewe Subhanaka (Uliyetakasika). Hakika mimi nilikuwa miongoni mwa wenye kudhulumu.

(88) Basi tukamwitikia na tukamwokoa kutokana na dhiki. Na hivyo ndivyo tunavyowaokoa Waumini.

(89) Na Zakariya alipomwita Mola wake Mlezi: Mola wangu Mlezi! Usiniache peke yangu, na Wewe ndiye Mbora wa wanaorithi.

(90) Na mwanamke aliyeulinda uke wake, na tukampulizia katika roho yetu, na tukamfanya yeye na mwanawe kuwa ni Ishara kwa walimwengu.

(91) Na mwanamke aliyeulinda uke wake, na tukampulizia katika roho yetu, na tukamfanya yeye na mwanawe kuwa ni Ishara kwa walimwengu.

(92) Kwa hakika huu umma wenu ni umma mmoja, na Mimi ni Mola wenu Mlezi. Kwa hivyo niabuduni Mimi.

(93) Nao wakalikata jambo lao hili mapande mapande baina yao. Wote watarudi kwetu.

(94) Na atendaye mema naye ni Muumini basi haitakataliwa juhudi yake. Na hakika Sisi tunamwandikia.

(95) Na haiwi kwa wanamji tuliouangamiza, ya kwamba hawatarejea.

(96) Mpaka watakapofunguliwa Yaajuju na Maajuju wakawa wanateremka kutoka kila mlima.

(97) Na miadi ya haki ikakaribia. Hapo ndipo yatakapokodoka macho ya waliokufuru (na watasema): Ole wetu! Bila ya shaka tulikuwa tumeghafilika na haya, bali tulikuwa wenye kudhulumu.

(98) Hakika nyinyi na hao mnaowaabudu badala ya Mwenyezi Mungu ni kuni za Jahannamu; huko mtaingia tu.

(99) Lau kuwa hawa ni miungu, wasingeliingia. Na wote watadumu humo.

(100) Lao wao humo ni kupiga mayowe, na wala hawatasikia (jinginelo).

(101) Ama wale ambao wema wetu umewatangulia, hao watatenganishwa na hayo.

(102) Hawatausikia mvumo wake, na wao watadumu katika yale zinayoyatamani nafsi zao.

(103) Hicho Kitisho Kikubwa hakitowahuzunisha. Na Malaika watawapokea (kwa kuwaambia): Hii ndiyo Siku yenu mliyokuwa mkiahidiwa!

(104) Siku tutakapozikunja mbingu kama mkunjo wa karatasi za vitabu. Kama tulivyoanza uumbaji wa mwanzo, tutalirudisha tena. Ni ahadi iliyo juu yetu. Hakika Sisi ni watendao.

(105) Na hakika tulikwishaandika katika Zaburi baada ya Kumbukumbu, ya kwamba ardhi watairithi waja wangu walio wema.

(106) Hakika katika haya yapo mawaidha kwa watu wafanyao ibada.

(107) Nasi hatukukutuma ila uwe ni Rehema kwa walimwengu wote.

(108) Sema: Hakika imefunuliwa kwangu ya kwamba hakika Mungu wenu ni Mungu Mmoja tu. Je, Mmesilimu?

(109) Na kama wakigeuka, basi sema: Nimewatangazieni sawa sawa, wala sijui yako karibu au mbali hayo mliyoahidiwa.

(110) Hakika Yeye anajua kauli ya dhahiri na anajua myafichayo.

(111) Wala sijui pengine huu ni mtihani tu kwenu na starehe mpaka muda kidogo.

(112) Sema: Mola wangu Mlezi! Hukumu kwa haki. Na Mola wetu Mlezi ni Mwingi wa Rehema, aombwaye msaada juu ya mnayoyazua.