(1) Alikunja kipaji na akageuka.
(2) Kwa sababu alimjia kipofu!
(3) Na nini kitakujuulisha pengine yeye atatakasika?
(4) Au atawaidhika, na mawaidha yamfae?
(5) Ama ajionaye hana haja,
(6) Wewe ndiyo unamshughulikia?
(7) Na si juu yako kama hakutakasika.
(8) Ama anayekujia kwa juhudi.
(9) Naye anaogopa,
(10) Ndiyo wewe unampuuza?
(11) Sivyo hivyo! Huku ni kukumbushana.
(12) Basi anayependa akumbuke.
(13) Yamo katika kurasa zilizoheshimiwa.
(14) Zilizoinuliwa, zilizotakaswa.
(15) Zimo mikononi mwa Malaika waandishi,
(16) Watukufu, wema.
(17) Ameangamia mwanaadamu! Nini kinachomkufurisha?
(18) Kwa kitu gani amemuumba?
(19) Kwa tone la manii, akamuumba na akamkadiria.
(20) Kisha akamsahilishia njia.
(21) Kisha akamfisha, akamtia kaburini.
(22) Kisha apendapo atamfufua.
(23) La! Hajamaliza aliyomuamuru.
(24) Hebu mtu na atazame chakula chake.
(25) Hakika Sisi tumemimina maji kwa nguvu.
(26) Tena tukaipasua pasua ardhi kwa nguvu.
(27) Kisha tukaotesha humo nafaka.
(28) Na zabibu, na mimea ya majani.
(29) Na mizaituni, na mitende.
(30) Na bustani zenye miti iliyosongana baraabara.
(31) Na matunda, na malisho ya wanyama.
(32) Kwa manufaa yenu na mifugo yenu.
(33) Basi utakapokuja ukelele.
(34) Siku ambayo mtu atamkimbia nduguye.
(35) Na mamaye na babaye.
(36) Na mkewe na wanawe.
(37) Kila mtu miongoni mwao siku hiyo atakuwa na lake la kumtosha.
(38) Siku hiyo ziko nyuso zitakazonawiri.
(39) Zitacheka, zitachangamka.
(40) Na nyuso siku hiyo zitakuwa na mavumbi.
(41) Giza totoro litazifunika.
(42) Hao ndio makafiri watenda maovu.