70 - Surat Al-Ma'arij ()

|

(1) Muulizaji aliuliza juu ya adhabu itakayotokea.

(2) Kwa makafiri - ambayo hapana awezaye kuizuia.

(3) Kutoka kwa Mwenyezi Mungu Mwenye mbingu za daraja.

(4) Malaika na Roho hupanda kwendea kwake katika siku ambayo kadiri yake ni miaka hamsini elfu!

(5) Basi subiri kwa subira njema.

(6) Hakika wao wanaiona iko mbali.

(7) Na Sisi tunaiona iko karibu.

(8) Siku ambayo mbingu zitakapokuwa kama maadeni iliyoyayushwa.

(9) Na milima itakuwa kama sufi.

(10) Wala jamaa hatamuuliza jamaa yake.

(11) Ijapokuwa wataonyeshwa waonane. Atatamani mkosefu lau ajikomboe na adhabu ya siku hiyo kwa kuwatoa fidia wanawe.

(12) Na mkewe, na nduguye.

(13) Na jamaa zake waliokuwa wakimkimu,

(14) Na wote waliomo duniani, kisha aokoke yeye.

(15) La, hasha! Kwa hakika huo ni Moto mkali kabisa,

(16) Unaobambua ngozi ya kichwa!

(17) Utamwita kila aliyegeuza mgongo na akageuka.

(18) Na akakusanya mali, kisha akayahifadhi.

(19) Hakika mtu ameumbwa na papara.

(20) Inapomgusa shari hupapatika.

(21) Na inapomgusa kheri huizuilia.

(22) Isipokuwa wanaosali,

(23) Ambao wanadumisha Sala zao,

(24) Na ambao katika mali yao iko haki maalumu.

(25) Kwa mwenye kuomba na anayejizuilia kuomba;

(26) Na ambao wanaisadiki Siku ya Malipo.

(27) Na ambao wanaiogopa adhabu itokayo kwa Mola wao Mlezi.

(28) Hakika adhabu ya Mola wao Mlezi si ya kuaminika nayo.

(29) Na ambao wanahifadhi tupu zao.

(30) Isipokuwa kwa wake zao, au iliyowamiliki mikono yao ya kuume, basi hao hawalaumiwi.

(31) Lakini wanaotaka kinyume cha haya, basi hao ndio wanaoruka mipaka.

(32) Na ambao wanazichunga amana zao na ahadi zao,

(33) Na ambao wanasimama imara katika ushahidi wao,

(34) Na ambao wanazihifadhi Sala zao.

(35) Hao ndio watakaoheshimiwa Peponi.

(36) Wana nini wale waliokufuru wanakutumbulia macho tu?

(37) Makundi kwa makundi upande wa kulia na upande wa kushoto!

(38) Kwani kila mmoja wao anatumai kuingizwa katika Pepo ya neema?

(39) La, hasha! Hakika Sisi tumewaumba kutokana na wanachokijua.

(40) Basi naapa kwa Mola Mlezi wa mashariki zote na magharibi zote kwamba Sisi tunaweza.

(41) Kuwabadili kwa walio bora kuliko wao; na Sisi hatushindwi.

(42) Basi waache wapige porojo na wacheze, mpaka wakutane na siku yao wanayoahidiwa,

(43) Siku watakapotoka makaburini kwa upesi kama kwamba wanakimbilia mfundo,

(44) Macho yao yatainama, fedheha itawafunika. Hiyo ndiyo Siku waliyokuwa wakiahidiwa.