(1) Hakika wamefaulu Waumini.
(2) Ambao ni wanyenyekevu katika Swala zao.
(3) Na ambao hujiepusha na mambo ya upuuzi.
(4) Na ambao wanatoa Zaka.
(5) Na ambao wanazilinda tupu zao.
(6) Isipokuwa kwa wake zao au kwa wale iliyowamiliki mikono yao ya kulia. Kwani hao si wenye kulaumiwa.
(7) Lakini anayetaka kinyume cha haya, basi hao ndio wavukao mipaka.
(8) Na ambao wanazitunza amana zao na ahadi zao.
(9) Na ambao Swala zao wanazihifadhi.
(10) Hao ndio warithi.
(11) Ambao watairithi Pepo ya Firdausi, nao watadumu humo.
(12) Na kwa yakini tumemuumba mtu kutokana na asili ya udongo.
(13) Kisha tukamfanya kuwa tone la mbegu ya uzazi katika mahali patulivu palipo madhubuti.
(14) Kisha tukaliumba tone hilo kuwa damu iliyoganda, na tukaiumba damu hiyo kuwa pande la nyama, kisha tukaliumba pande hilo la nyama kuwa mifupa, na mifupa hiyo tukaivisha nyama. Kisha tukamfanya kuwa kiumbe mwingine. Basi Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa baraka, Mbora zaidi wa waumbaji.
(15) Kisha hakika nyinyi baada ya hayo mtakufa.
(16) Kisha hakika nyinyi Siku ya Qiyama mtafufuliwa.
(17) Na kwa yakini tumeziumba juu yenu njia saba. Nasi hatukuwa wenye kughafilika na viumbe.
(18) Na tumeteremsha kutoka mbinguni maji kwa kiasi na tukayatuliza katika ardhi. Na hakika Sisi tunaweza kuyaondoa.
(19) Kwa maji hayo tukawafanyia bustani za mitende na mizabibu, mnapata humo matunda mengi, na katika hayo mnakula.
(20) Na mti utokao katika mlima wa Sinai, unaotoa mafuta na kuwa kitoweo kwa walao.
(21) Na hakika mnayo mazingatio makubwa katika wanyama hoa. Tunawanywesha nyinyi katika vile viliovymo matumboni mwao, na nyinyi mnapata katika hao manufaa mengi, na pia mnawala.
(22) Na juu yao na juu ya marikebu mnabebwa.
(23) Na hakika tulimtuma Nuhu kwa kaumu yake, akasema, "Enyi kaumu yangu! Muabuduni Mwenyezi Mungu. Nyinyi hamna mungu yeyote asiyekuwa Yeye. Basi je, hamwogopi?"
(24) Wakasema wale wakuu waliokufuru katika kaumu yake, "Huyu si chochote isipokuwa ni mtu tu kama nyinyi. Anataka kujipa ubora juu yenu. Na lau kuwa Mwenyezi Mungu angetaka, basi kwa yakini angeliteremsha Malaika. Hatukusikia haya kwa baba zetu wa mwanzoni."
(25) Huyu si lolote isipokuwa ni mwanamume mwenye wazimu. Basi mngojeeni tu kwa muda."
(26) Akasema (Nuhu), "Mola wangu Mlezi! Ninusuru kwa kuwa wamenikanusha."
(27) Tukamfunulia wahyi kwamba, "Unda jahazi mbele ya macho yetu na ufunuo wetu! Na itakapofika amri yetu na ikafurika tanuri, hapo waingize ndani yake kutoka kwa kila jozi, dume na jike, na ahali zako, isipokuwa yule ambaye katika wao juu yake imekwisha tangulia kauli. Wala usiniongeleshe kuhusu hao waliodhulumu. Kwani hao bila ya shaka watazamishwa.
(28) Basi utakapotulia sawasawa wewe na wale walio pamoja nawe humo merikebuni, sema: Alhamdulillahi (Sifa zote njema ni za Mwenyezi Mungu), aliyetuokoa kutoka kwa kaumu madhalimu!
(29) Na sema: Mola wangu Mlezi! Niteremshe mteremsho wenye baraka, na Wewe ndiye Mbora wa wateremshaji.
(30) Hakika katika hayo zipo ishara. Na kwa yakini Sisi ni wenye kuwajaribu.
(31) Kisha baada yao tukaanzisha kizazi kingine.
(32) Kisha tukawatumia Mtume miongoni mwao, kuwaambia: Muabuduni Mwenyezi Mungu! Hamna mungu yeyote asiyekuwa Yeye. Je, hamchi?
(33) Na wakubwa katika kaumu yake, wale waliokufuru na wakakadhibisha mkutano wa Akhera, na tukawastarehesha katika uhai wa dunia hii, walisema: Huyu si chochote isipokuwa ni mtu kama nyinyi. Anakula katika mnavyokula, na anakunywa katika mnavyokunywa.
(34) Kwa hivyo, nyinyi mkimtii mtu kama nyinyi, basi hakika mtakuwa hasarani.
(35) Hivi anawaahidi ati mtakapokufa na mkawa udongo na mifupa, kuwa hakika mtatolewa?
(36) Hayawi! Hayawi hayo mnayoahidiwa.
(37) Hapana isipokuwa uhai wetu wa duniani tu, tunakufa na kuishi tu. Wala sisi hatutafufuliwa.
(38) Huyu si lolote isipokuwa ni mwanamume anayemzulia Mwenyezi Mungu uongo, wala sisi sio wa kumuamini.
(39) Akasema: Mola wangu Mlezi! Ninusuru kwa sababu wananikanusha.
(40) (Mwenyezi Mungu) akasema: Baada ya muda mchache watakuwa wenye kujuta.
(41) Basi ukawanyakua ukelele kwa haki, na tukawafanya kama takataka zinazoelea juu ya maji. Ikapotelea mbali kaumu ya madhalimu!
(42) Kisha tukaleta baada yao vizazi vingine.
(43) Hapana umma uwezao kutanguliza muda wake wala kuuchelewesha.
(44) Kisha tukawatuma Mitume wetu, mmoja baada ya mmoja. Kila umma alipowafikia Mtume wao, walimkadhibisha. Tukawafuatanisha hawa baada ya hawa, na tukawafanya kuwa hadithi za kusimuliwa. Basi wakapotelea mbali kaumu wasioamini.
(45) Kisha tukamtuma Musa na kakaye, Haarun, pamoja na ishara zetu na hoja zilizo wazi.
(46) Kumwendea Firauni na wakuu wake. Lakini wakatakabari, nao walikuwa kaumu majeuri.
(47) Wakasema, "Je, tuwaamini watu wawili hawa kama sisi, na ambao kaumu yao ni watumwa wetu?"
(48) Basi wakawakadhibisha, na wakawa miongoni mwa walioangamizwa.
(49) Na hakika tulimpa Musa Kitabu ili wapate kuongoka.
(50) Na tukamfanya mwana wa Mariamu na mama yake kuwa ni Ishara, na tukawapa makimbilio kwenda mahali palipoinuka penye utulivu na chemchemi za maji.
(51) Enyi Mitume! Kuleni vyakula vizuri na tendeni mema. Hakika Mimi ninajua vyema mnayoyatenda.
(52) Na kwa yakini huu Umma wenu ni Umma mmoja, na Mimi ni Mola wenu Mlezi, basi nicheni Mimi.
(53) Lakini walikatiana jambo lao mapande mbalimbali. Kila kundi likifurahia kwa waliyo nayo.
(54) Basi waache katika ghafla yao kwa muda.
(55) Je, wanadhani ya kuwa kwa vile tunavyowapa mali na watoto.
(56) Ndiyo tunawahimizia kheri? Lakini wenyewe hawatambui.
(57) Kwa hakika hao ambao kwa kumwogopa Mola wao Mlezi wananyenyekea.
(58) Na wale ambao Ishara za Mola wao Mlezi wanaziamini.
(59) Na wale ambao Mola wao Mlezi hawamshirikishi.
(60) Na wale ambao wanatoa kile walichopewa, na hali nyoyo zao zinaogopa kwa kuwa watarejea kwa Mola wao Mlezi.
(61) Basi wote hao ndio wanaokimbilia katika mambo ya heri, na ndio watakaotangulia kuyafikia.
(62) Na hatuitwiki nafsi isipokuwa kwa kiasi cha uwezo wake. Na tunacho kitabu kisemacho kweli. Nao hawatadhulumiwa.
(63) Lakini nyoyo zao zimefunikwa hazitambui hayo, na wanavyo vitendo vingenvyo wanavyovifanya.
(64) Hata tutakapowatia katika adhabu wale waliodekezwa kwa starehe kati yao, hapo ndipo watakapoyayatika.
(65) Msiyayatike leo! Hakika nyinyi hamtanusurika nasi.
(66) Hakika zilikuwa Aya zangu mkisomewa, nanyi mkirudi nyuma juu ya visigino vyenu.
(67) Na huku mkiitakabari na usiku mkiizungumza (Qur-ani) kwa dharau.
(68) Je, hawakuifikiri kauli, au yamewajia ambayo hayakuwafikia baba zao wa zamani?
(69) Au hawakumjua Mtume wao, ndiyo maana wanamkataa?
(70) Au wanasema: Ana wazimu? Bali amewajia kwa Haki, na wengi wao wanaichukia Haki.
(71) Na lau kuwa Haki ingelifuata matamanio yao, basi zingeliharibika mbingu na ardhi na waliomo ndani yake. Bali tumewaletea ukumbusho wao, nao wanajitenga mbali na ukumbusho wao.
(72) Au unawaomba ujira? Lakini ujira wa Mola wako Mlezi ni bora ,na Yeye ndiye Mbora wa wanaoruzuku.
(73) Na kwa yakini, wewe unawaita kwenye Njia iliyonyooka.
(74) Na hakika wale wasioiamini Akhera wanajitenga na Njia hiyo.
(75) Na lau tungeliwarehemu na tukawaondolea shida waliyo nayo, bila ya shaka wangeliendelea katika upotofu wao, vile vile wakitangatanga.
(76) Na hakika tuliwatia adhabu kali; lakini hawakuelekea kwa Mola wao Mlezi wala hawakunyenyekea.
(77) Mpaka tulipowafungulia mlango wa adhabu, hapo ndipo wakawa wenye kukata tamaa.
(78) Na Yeye ndiye aliyewaumbia kusikia na kuona na nyoyo za kufahamu. Ni kuchache mno kushukuru kwenu.
(79) Na Yeye ndiye aliye aliyewaeneza katika ardhi, na kwake Yeye mtakusanywa.
(80) Na Yeye ndiye anayehuisha na kufisha, na ni yake Yeye mabadiliko ya usiku na mchana. Basi je, hamfahamu?
(81) Bali wanasema kama walivyosema watu wa kwanza.
(82) Walisema: Je, tukisha kufa tukawa udongo na mifupa, ndio tutafufuliwa?
(83) Tuliahidiwa haya sisi na baba zetu wa zamani. Hayakuwa haya ila ni visa vya uwongo vya watu wa zamani.
(84) Sema: Ni ya nani ardhi na vilivyomo ndani yake, kama nyinyi mnajua?
(85) Watasema: Ni vya Mwenyezi Mungu! Sema: Basi, je, hamkumbuki?
(86) Sema: Ni nani Mola Mlezi wa mbingu saba na Mola Mlezi wa A'rshi kuu.
(87) Watasema: Ni vya Mwenyezi Mungu. Sema, Basi, je, hamwogopi?
(88) Sema: Ni nani mkononi mwake umo Ufalme wa kila kitu, naye ndiye anayelinda, wala hakilindwi asichotaka, kama mnajua?
(89) Watasema, "Ufalme huo" ni wa Mwenyezi Mungu. Sema: Basi vipi mnadanganyika?"
(90) Bali tumewaletea Haki, na kwa yakini hao ni waongo.
(91) Mwenyezi Mungu hana mwana yeyote, wala hanaye mungu mwingine. Ingekuwa hivyo basi kila mungu angelichukua alivyoumba, na baadhi yao wangeliwashinda wengine. Mwenyezi Mungu ameepukana na sifa wanazomsifu.
(92) Mjuzi wa siri na dhahiri, na ametukuka juu ya hayo wanayomshirikisha nayo.
(93) Sema: Mola wangu Mlezi! Ukinionyesha adhabu waliyoahidiwa.
(94) Mola wangu Mlezi! Usinijalie katika watu madhalimu hao.
(95) Na hakika Sisi ni waweza wa kukuonyesha tuliyowaahidi.
(96) Kinga maovu kwa kutenda yaliyo mema zaidi. Sisi tunayajua wayasemayo.
(97) Na sema: Mola wangu Mlezi! Najikinga kwako na wasiwasi wa mashetani.
(98) Na najikinga kwako, Mola wangu Mlezi, wasinikaribie.
(99) Mpaka yanapomfikia mmoja wao mauti, husema: Mola wangu Mlezi! Nirudishe.
(100) Ili nitende mema sasa badala ya yale niliyoyaacha. Wapi! Hii ni kauli aisemayo Yeye tu. Na nyuma yao kipo kizuizi mpaka siku watakapofufuliwa.
(101) Basi litakapopulizwa baragamu, hapo hautakuwapo ujamaa baina yao siku hiyo, wala hawataulizana.
(102) Ama wale ambao mizani zao zitakuwa nzito, hao ndio wenye kufanikiwa.
(103) Na wale ambao mizani zao zitakuwa nyepesi, hao ndio waliozitia hasarani nafsi zao, na katika Jahannamu watadumu.
(104) Moto utababua nyuso zao, nao watakuwa na nyuso zilizo kunjana.
(105) Je, hazikuwa Aya zangu mkisomewa, na nyinyi mkizikanusha?
(106) Watasema: Mola wetu Mlezi! Tulizidiwa na uovu wetu na tukawa watu tuliopotea.
(107) Mola wetu Mlezi! Tutoe humu Motoni. Na tufanyapo tena basi kweli sisi ni wenye kudhulumu.
(108) Atasema Mwenyezi Mungu: Tokomeeni humo, wala msinisemeze.
(109) Bila ya shaka lilikuwapo kundi katika waja wangu likisema: Mola wetu Mlezi! Tumeamini; basi tusamehe na uturehemu, nawe ndiwe Mbora wa wanaorehemu.
(110) Lakini nyinyi mliwakejeli hata wakawasahaulisheni kunikumbuka, na mlikuwa mkiwacheka.
(111) Hakika Mimi leo nimewalipa kwa vile walivyosubiri. Bila ya shaka hao ndio wenye kufuzu.
(112) Atasema: Mlikaa muda gani katika ardhi kwa hisabu ya miaka?
(113) Watasema: Tulikaa siku moja au sehemu ya siku. Basi waulize wanaoweka hisabu.
(114) Atasema: Nyinyi hamkukaa huko duniani ila kidogo, laiti ingelikuwa mnajua.
(115) Je, mlidhani ya kwamba tuliwaumba bure, na ya kwamba nyinyi kwetu hamtarudishwa?
(116) Ametukuka Mwenyezi Mungu, Mfalme wa Haki, hapana mungu yeyote isipokuwa Yeye, Mola Mlezi wa 'Arshi Tukufu.
(117) Na anayemuomba - pamoja na Mwenyezi Mungu - mungu mwenginewe, hana ushahidi wa hili; basi bila ya shaka hisabu yake iko kwa Mola wake Mlezi. Kwa hakika makafiri hawafanikiwi.
(118) Nawe sema, "Mola wangu Mlezi, Samehe na urehemu nawe ni Mbora wa wanaorehemu."