(1) Kuhimidiwa ni kwa Mwenyezi Mungu, ambaye alimteremshia mja wake Kitabu, wala hakukifanya kuwa na upogo.
(2) Kimenyooka sawa sawa, ili kionye adhabu kali kutoka kwake, na kiwabashirie Waumini watendao mema kwamba hakika wana ujira mzuri.
(3) Wakae humo milele.
(4) Na kiwaonye wasemao, "Mwenyezi Mungu amejifanyia mwana."
(5) Wao hawana elimu yoyote ya jambo hili, wala baba zao. Ni neno kubwa hilo litokalo vinywani mwao. Hawasemi isipokuwa uongo tu.
(6) Huenda ukajihiliki nafsi yako kwa ajili yao, kuwasikitikia kwa kuwa hawayaamini mazungumzo haya!
(7) Kwa hakika tumevifanya vilivyoko juu ya ardhi kuwa ni pambo lake ili tuwafanyie mtihani, ni nani kati yao ndio wenye vitendo vizuri zaidi.
(8) Na hakika Sisi tutavifanya vyote vilivyo juu ya ardhi kuwa kama nchi iliyopigwa na ukame.
(9) Kwani unadhani ya kwamba wale watu wa Pangoni na Maandishi walikuwa ni ajabu miongoni mwa ishara zetu?
(10) Vijana hao walipokimbilia kwenye pango, na wakasema, "Mola wetu Mlezi! Tupe rehema itokayo kwako, na tutengezee uwongofu katika jambo letu."
(11) Basi tukayaziba masikio yao kuwalaza humo pangoni kwa muda wa miaka kadhaa.
(12) Kisha tukawazindua ili tujue ni lipi katika makundi mawili yale ndilo lilihesabu sawa urefu wa muda waliokaa.
(13) Sisi tunakusimulia habari zao kwa haki. Hakika wao walikuwa ni vijana waliomuamini Mola wao Mlezi. Na Sisi tukawazidisha uwongofu.
(14) Na tukazitia nguvu nyoyo zao waliposimama na wakasema, "Mola wetu Mlezi ni Mola Mlezi wa mbingu na ardhi. Hatutamwita mwingine kabisa badala yake kuwa ni Mungu. Hivyo, itakuwa tumesema jambo la kuvuka mpaka.
(15) Hawa kaumu yetu walijifanyia miungu mingine badala yake Yeye. Kwa nini basi hawawatolei uthibitisho ulio dhahiri? Na ni nani aliye dhalimu zaidi kuliko anayemzulia uongo Mwenyezi Mungu?
(16) Na mkijitenga nao na vile wanavyoviabudu badala ya Mwenyezi Mungu, basi kimbilieni pangoni, awafungulie Mola wenu Mlezi katika rehema zake, na awatengenezee ya kuwafaa katika mambo yenu.
(17) Na unaliona jua linapochomoza, linainamia kuliani mwao kutoka hapo pangoni, na linapokuchwa, linawakwepa kushotoni, na wao wamo katika uwazi wa pango. Hizo ni katika ishara za Mwenyezi Mungu. Yule ambaye Mwenyezi Mungu anamwongoa, basi huyo ameongoka. Na yule ambaye anampoteza, basi hutampatia msimamizi wa kumwongoza.
(18) Nawe utawadhania wa macho, na hali wamelala. Nasi tunawageuza kulia na kushoto. Na mbwa wao amenyoosha miguu yake ya mbele kizingitini. Kama ungeliwatokea, hapana shaka ungeligeuka kuwakimbia, huku umejaa hofu juu yao.
(19) Na kwa namna hiyo tuliwainua usingizini ili wapate kuulizana wao kwa wao. Alisema msemaji katika wao: Mmekaa muda gani? Wakasema: Tumekaa siku moja au sehemu ya siku. Wakasema: Mola wenu Mlezi ndiye anayejua zaidi muda mliokaa. Hebu mtumeni mmoja wenu na hizi fedha zenu aende mjini, akatazame chakula chake kipi kilicho bora kabisa awaletee cha kula. Naye afanye mambo hayo kwa busara, wala asiwataje kabisa kwa yeyote.
(20) Kwani wao wakiwatambua, watawapiga mawe, au watawarudisha katika dini yao, na hapo hamtafanikiwa kabisa!
(21) Na namna hivo ndivyo tulivyowajulisha kwa watu ili wapate kujua ya kwamba ahadi ya Mwenyezi Mungu ni ya kweli, na kwamba Saa haina shaka. Walipokuwa wakigombania jambo lao wao kwa wao, wakasema: Jengeni jengo juu yao. Mola wao Mlezi anawajua vyema. Wakasema wale walioshinda katika shauri yao: Bila ya shaka tutajenga msikiti juu yao.
(22) Watasema: Walikuwa watatu, wa nne wao ni mbwa wao. Na wanasema: Walikuwa watano, wa sita wao ni mbwa wao. Wanabahatisha ghaibu. Na wanasema: Walikuwa saba, na wa nane wao ni mbwa wao. Sema: Mola wangu Mlezi ndiye anayejua sawa sawa hesabu yao. Hawawajui isipokuwa wachache tu. Basi usibishane juu yao isipokuwa kwa mabishano ya juu juu tu hivi. Wala usiulize habari zao kwa yeyote yule.
(23) Wala usiseme kamwe kwa jambo lolote lile: Hakika nitalifanya hilo kesho.
(24) Isipokuwa Mwenyezi Mungu akipenda. Na mkumbuke Mola wako Mlezi pale unaposahau, na sema: huenda Mola wangu Mlezi ataniongoa kwenye uwongozi ulio karibu zaidi kuliko huu.
(25) Na walikaa katika pango lao hilo miaka mia tatu, na wakazidisha tisa.
(26) Sema: Mwenyezi Mungu ndiye anayejua zaidi muda waliokaa. Ni zake tu siri za mbingu na ardhi. Kuona vyema kulikoje kwake na kusikia kuzuri kulikoje! Hawana mlinzi yeyote isipokuwa Yeye, wala hamshirikishi yeyote katika hukumu yake.
(27) Na soma yale uliyofunuliwa katika Kitabu cha Mola wako Mlezi. Hakuna yeyote awezaye kubadilisha maneno yake. Wala nawe hutapata makimbilio yoyote isipokuwa kwake.
(28) Na isubirishe nafsi yako pamoja na wale wanaomuomba Mola wao Mlezi asubuhi na jioni, hali ya kuwa wanataka uso wake. Wala macho yako yasiwaruke kwa kutaka pambo la uhai wa dunia. Wala usimtii tuliyemghafilisha moyo wake asitukumbuke, na akafuata matamanio yake, na mambo yake yakawa ni kupita mpaka tu.
(29) Na sema: Hii ni kweli itokayo kwa Mola wako Mlezi. Basi atakaye, aamini. Na atakaye, akatae. Hakika Sisi tumewaandalia wenye kudhulumu Moto ambao utawazunguka kama hema. Na wakiomba msaada, watasaidiwa kwa kupewa maji kama mafuta yaliyotibuka. Yatakayowababua nyuso zao. Ni kinywaji kiovu mno kilioje hicho! Ni matandiko mabaya mno ya kupumzikia yaliyoje hayo!
(30) Hakika wale walioamini na wakatenda mema, hakika Sisi hatupotezi ujira wa anayetenda mazuri.
(31) Hao watapata Bustani za milele, zinazopita mito kwa chini yao. Humo watapambwa kwa mavazi ya mikononi ya dhahabu, na watavaa nguo za kijani za hariri na atilasi, huku wakiegemea humo juu ya makochi. Hayo ndiyo malipo bora zaidi! Na ndiyo matandiko mazuri mno ya kupumzikia!
(32) Na wapigie mfano wa wanaume wawili: mmoja wao tulimpa vitalu viwili vya mizabibu, na tukavizungushia mitende, na kati yake tukatia mimea ya nafaka.
(33) Na hivyo vitalu viwili vikatoa mazao yake, wala hapana kitu katika hayo kilichotindikia. Na ndani yake tukapasua mito.
(34) Naye alikuwa na mazao mengi. Basi akamwambia mwenzake naye akibishana naye: Mimi nimekushinda wewe kwa mali na nguvu za watu!
(35) Na akaingia kitaluni kwake, huku anajidhulumu nafsi yake. Akasema: Sidhani kabisa kuwa haya yatawahi haribika milele.
(36) Wala sidhani kuwa hiyo Saa (ya Qiyama) itatokea. Na ikiwa nitarudishwa kwa Mola wangu Mlezi, bila ya shaka nitapata marejeo bora zaidi kuliko haya.
(37) Mwenzake akamwambia kwa kubishana naye: Je, unamkufuru aliyekuumba kutokana na udongo, tena kutokana na tone la manii, kisha akakufanya mwanamume aliye sawasawa?
(38) Lakini Yeye Mwenyezi Mungu ndiye Mola wangu Mlezi. Wala simshirikishi Mola wangu Mlezi na yeyote.
(39) Na lau kuwa ulipoingia kitaluni kwako, ungelisema: Mashaallah (alitakalo Mwenyezi Mungu huwa)! Hakuna nguvu yoyote isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu. Ikiwa unaniona mimi nina mali kidogo na watoto kuliko wewe.
(40) Basi huenda Mola wangu Mlezi akanipa kilicho bora kuliko kitalu chako, na akakitumia balaa kutoka mbinguni kwa hivyo kikageuka kuwa ardhi tupu inayoteleza.
(41) Au maji yake yakazama [katika ardhi], basi usiweze kuyatafuta ukayapata.
(42) Basi, yakateketezwa matunda yake, akabaki akipinduapindua viganja vyake, kwa vile alivyoyagharamia, huku miti yake imebwagika juu ya chanja zake. Akawa anasema: Laiti nisingelimshirikisha Mola wangu Mlezi na yeyote!
(43) Wala hakuwa na kikundi cha kumnusuru badala ya Mwenyezi Mungu, wala mwenyewe hakuweza kujinusuru.
(44) Huko ulinzi ni wa Mwenyezi Mungu wa Haki tu. Yeye ndiye mbora zaidi wa malipo, na wa mwisho ulio bora zaidi.
(45) Na wapigie mfano wa uhai wa dunia ambao ni kama maji tunayoyateremsha kutoka mbinguni, yakachanganyika na mimea ya ardhi, kisha mimea hiyo ikawa vibuwa vinavyopeperushwa na upepo. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye uweza juu ya kila kitu.
(46) Mali na wana ni pambo la uhai wa dunia. Na mema yanayobakia ni bora mbele ya Mola wako Mlezi kwa malipo, na bora kwa matumaini.
(47) Na siku tutakapoiondoa milima na ukaiona ardhi iwazi, na tukawafufua, wala hatutamwacha hata mmoja miongoni mwao.
(48) Na wakahudhurishwa mbele ya Mola wako Mlezi kwa safu (wakaambiwa): Mmetujia kama tulivyowaumba mara ya kwanza! Bali mlidai kwamba hatutawawekea miadi.
(49) Na kitawekwa kitabu. Basi utawaona wakosefu wanavyoogopa kwa yale yaliyomo. Na watasema: Ole wetu! Kitabu hiki kina nini! Hakiachi dogo wala kubwa isipokuwa hulidhibiti vyema? Na watayakuta yote waliyoyatenda yapo hadharani. Na Mola wako Mlezi hamdhulumu yeyote.
(50) Na tulipowaambia Malaika: Msujudieni Adam! Walimsjudia isipokuwa Iblisi. Yeye alikuwa miongoni mwa majini, na akavunja amri ya Mola wake Mlezi. Je, mnamchukua yeye na dhuria yake kuwa vipenzi badala yangu, hali wao ni adui zenu? Ni ovu mno badala hii ya madhalimu.
(51) Sikuwashuhudisha kuumbwa kwa mbingu na ardhi, wala kuumbwa kwa nafsi zao. Wala sikuwafanya wapotezao kuwa ni wasaidizi.
(52) Na siku atakaposema (Mwenyezi Mungu): Waiteni hao mliodai kuwa ni washirika wangu. Basi watawaita, na wao hawatawaitikia. Nasi tutaweka baina yao maangamio.
(53) Na wahalifu watauona Moto na watajua ya kwamba wao lazima wataingia humo; wala hawatapata pa kuuepukia.
(54) Na bila ya shaka tumewaelezea watu katika Qur-ani hii kila namna ya mfano. Lakini mwanaadamu amezidi kuliko kila kitu kwa ubishi.
(55) Na hakikuwazuia watu kuamini ulipowajia uwongofu, na kuomba maghfira kwa Mola wao Mlezi, isipokuwa iwafikie desturi ya wale wa mwanzo, au iwafikie adhabu jahara.
(56) Na hatuwatumi Mitume isipokuwa wawe wabashiri na waonyaji. Na wale waliokufuru wanabishana kwa batili, ili kwayo waivunje haki. Na walizifanya Ishara zangu na yale waliyoonywa kuwa ni mzaha.
(57) Na ni nani dhalimu zaidi kuliko yule anayekumbushwa Ishara za Mola wake Mlezi, naye akazipuuza na akasahau yaliyotangulizwa na mikono yake? Hakika Sisi tumeziba juu ya nyoyo zao ili wasifahamu, na uziwi kwenye masikio yao. Na ukiwaita kwenye uwongofu, hawataweza kabisa kuongoka.
(58) Na Mola wako Mlezi ni Msamehevu Mwenye rehema. Lau angeliwachukulia kwa mujibu wa yale waliyoyachuma, bila ya shaka angeliwafanyia haraka kuwaadhibu. Lakini wanayo miadi ambayo hawatapata makimbilio yoyote ya kuepukana nayo.
(59) Na miji hiyo tuliwaangamiza watu wake walipodhulumu. Na tukawawekea miadi ya maangamizo yao.
(60) Na pale Musa alipomwambia kijana wake, "Sitaacha kuendelea mpaka nifike zinapokutana bahari mbili, au nitaendelea kwa muda mrefu."
(61) Basi wawili hao walipofika zinapokutana hizo bahari mbili, walimsahau samaki wao, naye akashika njia yake akaponyokea baharini.
(62) Walipokwisha pita, alimwambia kijana wake: Tupe chakula chetu cha mchana. Kwa hakika tumepata machovu kweli kwa hii safari yetu.
(63) Akasema (kijana): Waona! Pale tulipopumzika penye jabali, basi mimi nilimsahau yule samaki. Na hakuna aliyenisahaulisha kumkumbuka isipokuwa Shetani tu. Naye akashika njia yake baharini kwa ajabu.
(64) (Musa) akasema: Hayo ndiyo tuliyokuwa tunayataka. Basi wakarudi nyuma kwa kufuata njia waliyojia.
(65) Basi wakamkuta mja katika waja wetu tuliyempa rehema kutoka kwetu, na tukamfunza mafunzo yaliyotoka kwetu.
(66) Musa akamwambia: Nikufuate ili unifunze katika ule uwongofu uliofunzwa wewe?
(67) Akasema: Hakika wewe hutaweza kuvumilia kuwa pamoja nami.
(68) Na utawezaje kuvumilia yale usiyoyajua vilivyo undani wake?
(69) Akasema: Inshaallah (Mwenyezi Mungu akipenda), utanikuta mvumilivu, wala sitaasi amri yako yoyote.
(70) Akasema: Basi ukinifuata, usiniulize kitu mpaka mimi nianze kukutajia.
(71) Basi wawili hao wakatoka, hata walipopanda jahazi (yule mtu), akalitoboa. (Musa) akasema: Unalitoboa ili uwazamishe watu wake? Hakika umefanya jambo baya mno.
(72) Akasema: Je, sikusema kwamba wewe hakika hutaweza kuvumilia kuwa pamoja nami?
(73) (Musa) akasema: Usinichukulie makosa kwa niliyosahau, wala usinipe uzito kwa jambo langu.
(74) Basi wakatoka wawili hao mpaka wakamkuta kijana, akamuua. (Musa) akasema: Ala! Umemuua mtu asiye na kosa, na wala hakuua nafsi yoyote! Ama hakika umefanya jambo baya kabisa!
(75) (Yule mtu) Akasema, "Je, sikukwambia kwamba hakika wewe hutaweza kusubiri kuwa pamoja nami?"
(76) (Musa) Akasema, "Nikikuuliza kuhusu kitu chochote baada ya haya, basi usifuatane nami. Kwani hakika umekwisha pata udhuru kutoka kwangu."
(77) Basi wakaondoka mpaka wakawafikia watu wa mji mmoja. Wakawaomba watu wake wawape chakula, nao wakakataa kuwakaribisha. Hapo wakakuta ukuta unataka kuanguka, (yule mja mwema) akausimamisha. (Musa) akasema, "Ungelitaka, ungelichukua ujira kwa haya."
(78) (Yule mtu) akasema: Huku ndiko kufarikiana baina yangu na wewe. Sasa nitakueleza maana ya yale ambayo hukuweza kuyastahamili.
(79) Ama lile jahazi, hilo lilikuwa la masikini fulani wafanyao kazi baharini. Kwa hivyo, nilitaka kulitia dosari, kwani nyuma yao alikuwako mfalme aliyekuwa akichukua kwa nguvu majahazi yote.
(80) Na ama yule kijana, wazazi wake walikuwa ni Waumini. Tukahofu aje kuwatia mashakani kwa kupindukia mipaka na ukafiri.
(81) Basi tulitaka Mola wao Mlezi awabadilishie aliye bora zaidi kuliko huyo kwa kutakasika, na aliye karibu zaidi kwa huruma.
(82) Na ama ukuta ule, huo ulikuwa ni wa vijana wawili mayatima kule mjini. Na chini yake ilikuwako hazina yao; na baba yao alikuwa ni mtu mwema. Basi Mola wako Mlezi alitaka wafikie utu uzima wao na wajitolee hazina yao wenyewe, hii ikiwa ni rehema itokayo kwa Mola wako Mlezi. Wala mimi sikutenda hayo kwa amri yangu. Hiyo ndiyo tafsiri ya hayo ambayo wewe hukuweza kuyasubiria.
(83) Na wanakuuliza kuhusu Dhul-Qarnain. Waambie: nitawasomea baadhi ya hadithi yake.
(84) Hakika Sisi tulimuimarisha katika ardhi na tukampa katika njia za kila kitu.
(85) asi akaifuata njia.
(86) Mpaka alipofika machweo ya jua, akaliona linatua katika chemchemi yenye matope meusi. Na pale akawakuta kaumu fulani. Tukasema: Ewe Dhul-Qarnain, ima uwaadhibu au uwafanyie uzuri.
(87) kasema: Ama aliyedhulumu, basi tutamuadhibu kisha atarudishwa kwa Mola wake Mlezi, naye atamuadhibu adhabu mbaya zaidi.
(88) Na ama yule mwenye kuamini na akatenda mema, basi huyo ana malipo mazuri, nasi tutamwambia lililo jepesi katika amri yetu.
(89) Kisha akaifuata njia.
(90) Hata alipofika machomozeo ya jua, akaliona linawachomozea kaumu ambao hatukuwawekea pazia ya kuwakinga kutokana nalo.
(91) Vivyo hivyo. Na Sisi tulizijua vilivyo habari zake zote.
(92) Kisha akaifuata njia.
(93) Hata alipofika katikati ya milima miwili, alikuta nyuma yake kaumu ambao walikaribia kutofahamu neno lolote.
(94) Wakasema: Ewe Dhul-Qarnain! Hakika Yaajuju na Maajuju wanafanya uharibifu katika ardhi. Basi je, tukupe ujira ili utie baina yetu na baina yao kizuizi?
(95) Akasema: yale ambayo Mola wangu Mlezi ameniimarisha ndani yake ndiyo bora zaidi. Lakini nisaidieni kwa nguvu. Nitaweka baina yenu na baina yao kizuizi imara.
(96) Nileteeni vipande vya chuma. Hata alipoijaza sawasawa nafasi iliyo katikati ya milima miwili hiyo, akasema, "Pulizeni moto" mpaka alipokifanya kuwa moto, akasema, " Nileteeni shaba iliyoyeyuka niimimine juu ya chuma hicho."
(97) Basi hawakuweza kukikwea, wala hawakuweza kukitoboa.
(98) Akasema, "Hii ni rehema kutoka kwa Mola wangu Mlezi. Na itakapokuja ahadi ya Mola wangu Mlezi, atakivunjavunja. Na ahadi ya Mola wangu Mlezi ni ya kweli."
(99) Na tutawaacha baadhi yao siku hiyo wachanganyike wao kwa wao, na litapulizwa baragumu, hapo tutawakusanya wote pamoja.
(100) Na siku hiyo tutawadhihirishia wazi Jahannamu makafiri waione.
(101) Wale ambao macho yao yalikuwa paziani hawanikumbuki, na wakawa hawawezi kusikia.
(102) Je, wanadhani wale waliokufuru kwamba watawafanya waja wangu kuwa vipenzi wao badala yangu Mimi? Hakika Sisi tumeiandaa Jahannamu iwe ndipo pahali pa kuteremkia pa makafiri.
(103) Sema: Je, tuwatajieni wenye hasara mno katika vitendo vyao?
(104) Ni wale ambao juhudi yao katika uhai wa dunia ilipotea bure, nao wanadhani kwamba wanafanya matendo mazuri.
(105) Hao ni wale waliozikufuru Ishara za Mola wao Mlezi na kukutana naye. Kwa hivyo matendo yao yakapotea bure, na wala Siku ya Qiyama hatutawasimamishia mizani yoyote.
(106) Hayo ndiyo malipo yao, Jahannam, kwa walivyokufuru na wakafanyia stihizai Ishara zangu na Mitume wangu.
(107) Hakika wale walioamini na wakatenda mema, mashukio yao yatakuwa kwenye Pepo za Firdausi.
(108) Watadumu humo; hawatataka kuondoka humo.
(109) Sema: Lau kuwa bahari ingekuwa ndiyo wino kwa maneno ya Mola wangu Mlezi, basi bahari ingelimalizika kabla ya kumalizika maneno ya Mola wangu Mlezi, hata tungeliileta mfano wa hiyo kuongezea.
(110) Sema, "Hakika mimi ni mwanadamu tu kama nyinyi. Ninaletewa Wahyi kwamba Mungu wenu ni Mungu Mmoja tu. Kwa hivyo, mwenye kutaraji kukutana na Mola wake Mlezi, basi na atende matendo mema, wala asimshirikishe yeyote katika ibada ya Mola wake Mlezi."