15 - Surat Al-hijr ()

|

(1) Alif Lam Ra. Hizi ni Aya za Kitabu na Qur-ani inayobainisha.

(2) Huenda ikawa wale waliokufuru wakatamani kwamba wangekuwa Waislamu.

(3) Waache wale, na wastarehe, na yawazuge matumaini. Watakuja jua.

(4) Na hatukuuangamiza mji wowote ule isipokuwa ulikuwa na muda wake maalumu.

(5) Hawawezi umma wowote kuutangulia muda wao, wala kuchelewa.

(6) Na walisema, "Ewe uliyeteremshiwa Ukumbusho! Hakika wewe ni mwendawazimu.

(7) Mbona hutuletei Malaika ikiwa wewe ni miongoni mwa wakweli?

(8) Sisi hatuwateremshi Malaika isipokuwa kwa sababu ya haki, na hapo hawatapewa muhula.

(9) Hakika Sisi ndio tuliouteremsha Ukumbusho huu, na hakika Sisi ndio tutakoulinda.

(10) Na hakika tulikwisha watumia Mitume mataifa ya mwanzo.

(11) Na hakuwajia Mtume isipokuwa walikuwa wakimfanyia stihizai.

(12) Na kama hivi ndivyo tunavyoyaingiza katika nyoyo za wakosefu.

(13) Hawayaamini haya, na ilhali imekwisha wapitia desturi ya wa mwanzo.

(14) Na lau tungeliwafungulia mlango huko mbinguni, wakawa wanapanda kupitia humo,

(15) Basi wangelisema: Hakika macho yetu yameleweshwa tu. Bali sisi wenyewe ni kaumu tuliofanyiwa uchawi.

(16) Na hakika tumeweka katika mbingu vituo vya sayari, na tumezipamba kwa wenye kuangalia.

(17) Na tumezilinda kutokana na kila shetani aliyelaaniwa.

(18) Isipokuwa mwenye kusikiliza kwa kuibia, naye hufuatwa na kijinga cha moto kilicho dhahiri.

(19) Na ardhi tumeitandaza, na humo tumeweka milima madhubuti, na tumeotesha katika kila kitu kwa kiasi chake.

(20) Na tumewajaalia humo vitu vya maisha yenu, na ya hao ambao nyinyi sio wenye kuwaruzuku.

(21) Na hakuna chochote ila asili yake inatokana na Sisi; wala hatukiteremshi isipokuwa kwa kipimo maalumu.

(22) Na tunazipeleka pepo za kupandishia, na tunateremsha kutoka mbinguni maji, kisha tukakunywesheni maji hayo. Wala si nyinyi mnayoyaweka.

(23) Na hakika Sisi ndio tunaohuisha na tunaofisha. Na Sisi ndio Warithi.

(24) Na hakika tunawajua waliotangulia katika nyinyi, na tunawajua waliobaki nyuma.

(25) Na hakika Mola wako Mlezi ndiye atakayewakusanya. Hakika Yeye ni Mwenye hekima, Mjuzi.

(26) Na hakika tulimuumba Mtu kwa udongo unaotoa sauti, unaotokana na matope yaliyotiwa sura.

(27) Naye Jini tulimuumba hapo kabla kutokana na moto wa upepo moto.

(28) Na Mola wako Mlezi alipowaambia Malaika: Hakika Mimi nitamuumba mtu kwa udongo unaotoa sauti, unaotokana na matope yaliyotiwa sura.

(29) Basi nitakapomtengeneza sawasawa, na nikampulizia roho yangu, basi mmwangukie kumsujudia.

(30) Basi Malaika wote pamoja walimsujudia.

(31) Isipokuwa Iblisi. Yeye alikataa kuwa pamoja na waliosujudu.

(32) (Mwenyezi Mungu) akasema: Ewe Iblisi! Una nini hata hukuwa pamoja na waliosujudu?

(33) Akasema: Haiwi mimi nimsujudie mtu uliyemuumba kutokana na udongo unaotoa sauti, unaotokana na matope yaliyotiwa sura.

(34) (Mwenyezi Mungu) akasema: Basi toka humo, kwani hakika wewe umefukuziliwa mbali!

(35) Na hakika juu yako ipo laana mpaka Siku ya Malipo.

(36) Akasema (Iblisi): Mola wangu Mlezi! Nipe muhula mpaka siku watakapofufuliwa.

(37) (Mwenyezi Mungu) akasema: Hakika wewe ni katika waliopewa muhula.

(38) Mpaka siku ya wakati maalumu.

(39) Akasema: Mola wangu Mlezi! Ilivyokuwa umenitia makosani, basi hakika nitawapambia katika dunia na hakika nitawapoteza wote.

(40) Isipokuwa waja wako walioteuliwa miongoni mwao.

(41) Akasema: Hii ni njia ya kujia kwangu iliyonyooka.

(42) Hakika waja wangu, wewe hutakuwa na mamlaka juu yao, isipokuwa wale wapotofu waliokufuata.

(43) Na hakika Jahannamu ndipo mahali pao walipoahidiwa wote.

(44) Ina milango saba; na kwa kila mlango iko sehemu waliotengewa.

(45) Hakika wachamungu watakuwa katika Mabustani na chemchemi.

(46) (Wataambiwa:) Ingieni humo kwa salama na amani.

(47) Na tutaondoa chuki iliyokuwa vifuani mwao, wawe ndugu, juu ya viti vya enzi huku wameelekeana.

(48) Humo hayatawagusa machovu, wala hawatatolewa humo.

(49) Wape habari waja wangu ya kwamba Mimi ndiye Mwenye kusamehe zaidi, Mwingi wa kurehemu.

(50) Na kwamba adhabu yangu ndiyo adhabu iliyo chungu!

(51) Na wape habari za wageni wa Ibrahim.

(52) Walipoingia kwake na wakasema: Salama! Yeye akasema: Hakika sisi tunawaogopa.

(53) Wakasema: Usiogope. Hakika, Sisi tunakubashiria kijana mwenye elimu mno.

(54) Akasema: Mnanibashiria nami uzee umenishika! Basi kwa njia gani mnanibashiria?

(55) Wakasema: Tunakubashiria kwa haki, basi usiwe miongoni mwa wanaokata tamaa.

(56) Akasema: Na ni nani anayekata tamaa na rehema ya Mola wake Mlezi isipokuwa wapotovu?

(57) Akasema: Hebu mna jambo gani, enyi wajumbe?

(58) Wakasema: Hakika sisi tumetumwa kwa kaumu ya wahalifu!

(59) Isipokuwa watu wa familia ya Lut'. Bila ya shaka sisi tutawaokoa hao wote.

(60) Isipokuwa mkewe. Tumekwisha pitisha kwamba huyo hakika atakuwa miongoni mwa watakaobakia nyuma.

(61) Basi wale wajumbe walipowajia watu wa familia ya Lut'.

(62) (Lut') Alisema: Hakika nyinyi ni kaumu msiojulikana.

(63) Wakasema: Bali sisi tumekuletea yale waliyokuwa wakiyafanyia shaka.

(64) Na tumefika kwako kwa Haki, na hakika sisi ni wakweli.

(65) Basi ondoka na ahali zako usiku ungalipo, nawe ufuate nyuma yao, wala yeyote kati yenu asigeuke nyuma. Na mwende huko mnakoamrishwa.

(66) Na tukamfunulia hukumu hiyo, ya kwamba hata wa mwisho wao hao ikifika asubuhi atakuwa amekwisha katiliwa mbali.

(67) Na wakaja watu wa mji ule huku wamefurahi.

(68) Akasema: Hakika hawa ni wageni wangu. Basi msinifedheheshe.

(69) Na mcheni Mwenyezi Mungu, wala msinihizi.

(70) Wakasema: Kwani hatukukukataza (kuwakaribisha) walimwengu hawa?

(71) Akasema, "Hawa binti zangu, ikiwa nyinyi ni watendaji."

(72) Ninaapa kwa umri wako! Hakika hao walikuwa katika ulevi wao, wakihangaika ovyo.

(73) Basi ukelele ukawatwaa wakipambaukiwa.

(74) Kwa hivyo, tukaugeuza mji huo juu chini, na tukawanyeshea mvua ya mawe ya udongo wa kutoka Motoni.

(75) Hakika katika hayo zipo ishara kwa wanaotafakari na kuzingatia.

(76) Na hakika miji hii ipo kwenye njia inayopitiwa.

(77) Hakika katika hayo ipo ishara kwa Waumini.

(78) Na hakika watu wa Kichakani walikuwa wenye kudhulumu.

(79) Kwa hivyo tukawaadhibu. Na hakika miji miwili hii iko kwenye njia iliyo wazi.

(80) Na bila ya shaka wakaazi wa Hijr waliwakadhibisha Mitume.

(81) Na tuliwaletea ishara zetu, nao wakawa wanazipa migongo.

(82) Nao walikuwa wakichonga majumba katika milima kwa amani.

(83) Basi ukelele ukawatwaa asubuhi.

(84) Na hayakuwafaa yale waliyokuwa wakiyachuma.

(85) Na hatukuziumba mbingu na ardhi na vilivyomo ndani yake isipokuwa kwa haki. Na hakika Saa ya Qiyama itafika. Basi samehe msamaha mzuri.

(86) Hakika Mola wako Mlezi ndiye Muumbaji, Mwenye kujua zaidi.

(87) Na hakika tumekupa saba zinazosomwa mara kwa mara, na Qur-ani Tukufu.

(88) Kamwe usivinyoshee macho yako vitu tulivyowastarehesha kwavyo makundi fulani kati yao, wala usiwahuzunikie. Na wainamishie bawa lako (la huruma) Waumini.

(89) Na sema, "Hakika mimi ni mwonyaji mwenye kubainisha."

(90) Kama hivyo tuliwateremshia waliogawa.

(91) Ambao wakaifanya Qur-ani vipande vipande.

(92) Basi ninaapa kwa Mola wako Mlezi! Tutawauliza wote.

(93) Kuhusu yale waliyokuwa wakiyatenda.

(94) Basi wewe yadhihirishe yale uliyoamrishwa, na jitenge na washirikina.

(95) Hakika Sisi tunatosha kukukinga na wanaofanya stihizai.

(96) Ambao wanafanya mungu mwingine kuwa pamoja na Mwenyezi Mungu. Basi, watakuja jua!

(97) Na Sisi tunajua kwa hakika kuwa wewe kifua chako kinaona dhiki kwa hayo wayasemayo.

(98) Basi mtakase Mola wako Mlezi kwa kumhimidi, na uwe miongoni mwa wanaomsujudia.

(99) Na muabudu Mola wako Mlezi mpaka ikufikie Yakini.