53 - Surat An-Najm ()

|

(1) Ninaapa kwa nyota inapotua.

(2) Mwenzenu huyu hakupotea, wala hakukosea.

(3) Wala hatamki kwa matamanio.

(4) Hayakuwa haya ila ni ufunuo uliofunuliwa.

(5) Amemfundisha aliye Mwingi wa nguvu.

(6) Mwenye kutua, akatulia.

(7) Naye yuko juu kabisa upeo wa macho.

(8) Kisha akakaribia na akateremka.

(9) Akawa ni kama baina ya mipinde miwili, au karibu zaidi.

(10) Akamfunulia mja wake (Mwenyezi Mungu) alichomfunulia.

(11) Moyo haukusema uwongo uliyoyaona.

(12) Je, mnabishana naye kwa aliyoyaona?

(13) Na akamwona mara nyingine.

(14) Penye Mkunazi wa mwisho.

(15) Karibu yake ndiyo ipo Bustani ya mbinguni inayokaliwa.

(16) Kilipoufunika huo Mkunazi hicho kilichoufunika.

(17) Jicho halikuhangaika wala halikuruka mpaka.

(18) Kwa yakini aliona katika Ishara kubwa kabisa za Mola wake Mlezi.

(19) Je, mmemuona Lata na Uzza?

(20) Na Manaat, mwingine wa tatu?

(21) Je, nyinyi mnao wana wanaume na Yeye ndio awe na wanawake?

(22) Huo ni mgawanyo wa dhuluma!

(23) Hayo hayakuwa ila ni majina mliyowapa nyinyi na baba zenu. Mwenyezi Mungu hakuleta uthibitisho wowote juu ya hayo. Hawafuati ila dhana tu na kipendacho nafsi. Na kwa yakini uwongofu ulikwisha wafikia kutoka kwa Mola wao Mlezi.

(24) Ati mtu anakipata kila anachokitamani?

(25) Mwenyezi Mungu tu ndiye Mwenye dunia na Akhera.

(26) Na wako Malaika wangapi mbinguni, ambao uombezi wao hautafaa chochote isipokuwa baada ya Mwenyezi Mungu kutoa idhini kwa amtakaye na kumridhia.

(27) Hakika wale wasioamini Akhera bila ya shaka wao ndio wanawaita Malaika kwa majina ya kike.

(28) Nao hawana elimu yoyote kwa hayo isipokuwa wanafuata dhana tu. Na dhana haisaidii chochote mbele ya haki.

(29) Basi mwachilie mbali anayeupa kisogo ukumbusho wetu, na wala hataki ila maisha ya dunia.

(30) Huo ndio mwisho wao wa elimu. Hakika Mola wako Mlezi ndiye anayemjua zaidi mwenye kuipotea njia yake, na Yeye ndiye anayemjua zaidi mwenye kuongoka.

(31) Ni vya Mwenyezi Mungu vyote vilivyomo mbinguni na vilivyomo katika ardhi, ili awalipe wale waliotenda ubaya kwa waliyoyatenda, na wale waliotenda mema awalipe mema.

(32) Ambao wanajiweka mbali na madhambi makuu na vitendo vichafu, isipokuwa makosa hafifu. Hakika Mola wako Mlezi ni Mkunjufu wa maghfira, naye anakujueni sana tangu alipokuumbeni kutoka kwenye ardhi, na mlipokuwa mimba matumboni mwa mama zenu. Basi msijione watakatifu. Yeye anamjua sana mwenye kujikinga akawa mbali na maovu.

(33) Je, umemwona yule aliyegeuka akaenda zake?

(34) Na akapeana kidogo, kisha akajizuia?

(35) Je, anayo huyo elimu ya ghaibu, basi ndiyo anaona?

(36) Au hakuambiwa yaliyomo katika Vitabu vya Musa?

(37) Na vya Ibrahimu aliyetimiza ahadi?

(38) Ya kwamba hakika nafsi iliyobeba madhambi haibebi madhambi ya mwengine?

(39) Na ya kwamba hatapata mtu ila aliyoyafanya mwenyewe?

(40) Na kwamba vitendo vyake vitaonekana?

(41) Kisha ndio atalipwa malipo yake kwa hayo kwa ukamilifu.

(42) Na kwamba kwa Mola wako Mlezi ndiyo mwisho.

(43) Na kwamba Yeye ndiye anayeleta kicheko na kilio.

(44) Na kwamba Yeye ndiye anayefisha na kuhuisha.

(45) Na kwamba Yeye ndiye aliyeumba jozi, dume na jike

(46) Kutokana na mbegu ya uzazi inapomiminwa.

(47) Na kwamba ni juu yake ufufuo mwengine.

(48) Na kwamba ni Yeye ndiye anayetosheleza na kukinaisha.

(49) Na kwamba hakika Yeye ndiye Mola Mlezi wa nyota ya Shii'ra.

(50) Na kwamba Yeye ndiye aliyewaangamiza 'Adi wa kwanza.

(51) Na Thamudi hakuwabakisha.

(52) Na kabla yao kaumu ya Nuhu. Na hao hakika walikuwa ni madhalimu zaidi, na waovu zaidi.

(53) Na miji iliyopinduliwa, ni Yeye aliyeipindua.

(54) Vikaifunika vilivyofunika.

(55) Basi neema gani ya Mola wako Mlezi unayoifanyia shaka?

(56) Hili ni onyo katika maonyo yale yale ya zamani.

(57) Kiyama kimekaribia!

(58) Hapana wa kukifichua isipokuwa Mwenyezi Mungu.

(59) Je, mnayastaajabia maneno haya?

(60) Na mnacheka, wala hamlii?

(61) Nanyi mmeghafilika?

(62) Basi msujudieni Mwenyezi Mungu, na mumuabudu.