52 - Surat At-Tur ()

|

(1) Ninaapa kwa mlima wa T'ur.

(2) Na Kitabu kilichoandikwa.

(3) Katika ngozi iliyokunjuliwa.

(4) Na kwa Nyumba iliyojengwa.

(5) Na kwa dari iliyonyanyuliwa.

(6) Na kwa bahari iliyojazwa.

(7) Hakika adhabu ya Mola wako Mlezi hapana shaka itatokea.

(8) Hapana wa kuizuia.

(9) Siku zitakapotikisika mbingu kwa mtikiso.

(10) Na milima iwe inakwenda kwa mwendo mkubwa.

(11) Basi ole wao siku hiyo hao wanaokadhibisha.

(12) Ambao wanacheza katika mambo ya upuuzi.

(13) Siku watakaposukumwa kwenye Moto kwa msukumo wa nguvu.

(14) (Waambiwe): Huu ndio ule Moto mliokuwa mkiukadhibisha!

(15) Je, huu ni uchawi, au hamwoni tu?

(16) Uingieni, mkistahamili au msistahamili - ni mamoja kwenu. Hakika mnalipwa kwa mliyokuwa mkiyatenda.

(17) Hakika wacha Mungu watakuwa katika Mabustani na neema.

(18) Wakifurahi kwa yale aliyowapa Mola wao Mlezi. Na Mola wao Mlezi atawalinda na adhabu ya Motoni.

(19) Kuleni na kunyweni kwa raha kabisa kwa sababu ya mliyokuwa mkiyatenda.

(20) Watakuwa wameegemea juu ya viti vya enzi vilivyopangwa kwa safu. Na tutawaoza mahurulaini.

(21) Na wale walioamini na dhuriya zao wakawafuata kwa Imani, tutawakutanisha nao dhuriya zao, na wala hatutawapunja hata kidogo katika vitendo vyao. Kila mtu lazima atapata alichokichuma.

(22) Na tutawapa matunda, na nyama kama watakavyopenda.

(23) Watapeana humo bilauri zisizo na vinywaji vya kuleta maneno ya upuuzi wala dhambi.

(24) Iwe wanawapitia watumishi wao kama kwamba ni lulu zilizomo katika chaza.

(25) Wataelekeana wakiulizana.

(26) Waseme: Hakika tulikuwa zamani pamoja na ahali zetu tukiogopa mno.

(27) Basi Mwenyezi Mungu akatufanyia hisani na akatulinda mbali adhabu ya upepo wa Moto.

(28) Hakika sisi zamani tulikuwa tukimwomba Yeye tu. Hakika Yeye ndiye Mwema Mwingi wa kurehemu.

(29) Basi kumbusha! Kwani wewe, kwa neema ya Mola wako Mlezi, si kuhani wala mwendawazimu.

(30) Au wanasema: Huyu ni mtunga mashairi, tunamtarajia kupatilizwa na dahari.

(31) Sema: Tarajieni, na mimi pia ni pamoja nanyi katika kutarajia.

(32) Au hizo akili zao ndio zinawaamrisha haya, au wao basi ni watu majeuri tu?

(33) Au ndiyo wanasema: 'Ameitunga hii!' Bali basi tu hawaamini!

(34) Basi nawalete masimulizi kama haya ikiwa wao wanasema kweli.

(35) Au wao wameumbwa pasipo kutokana na kitu chochote, au ni wao ndio waumbaji?

(36) Au wao wameziumba mbingu na ardhi? Bali hawana yakini.

(37) Au wanazo hazina za Mola wako Mlezi au wao ndio wenye madaraka?

(38) Au wanazo ngazi za kusikilizia? Basi huyo msikilizaji wao na alete hoja iliyo wazi!

(39) Au Yeye Mwenyezi Mungu ana wasichana, na nyinyi ndio mna wavulana?

(40) Au wewe unawaomba ujira, na kwa hivyo ndio wanaelemewa na uzito wa gharama?

(41) Au wanayo elimu ya ghaibu, nao wameandika?

(42) Au wanataka kufanya vitimbi tu? Lakini hao waliokufuru ndio watakaotegeka.

(43) Au wanaye mungu asiyekuwa Mwenyezi Mungu? Ametaksika Mwenyezi Mungu mbali na hao wanaowashirikisha naye.

(44) Na hata wangeona pande linatoka mbinguni linaanguka wangesema: Ni mawingu yaliyobebana.

(45) Basi waache mpaka wakutane na siku yao watakapohilikishwa.

(46) Siku ambayo hila zao hazitawafaa hata kidogo, wala wao hawatanusuriwa.

(47) Na hakika wale waliodhulumu watapata adhabu nyingine isiyokuwa hii, lakini wengi wao hawajui.

(48) Na ingojee hukumu ya Mola wako Mlezi. Kwani wewe hakika uko mbele ya macho yetu,

(49) Na usiku pia mtakase, na zinapokuchwa nyota.