50 - Surat Qaf ()

|

(1) Qaaf. Ninaapa kwa Qur-ani tukufu!

(2) Bali wanastaajabu kwamba amewafikia mwonyaji kutoka miongoni mwao, na wakasema makafiri: 'Hili ni jambo la ajabu!

(3) Ati tukifa na tukawa udongo...? Kurejea huko kuko mbali!'

(4) Hakika Sisi tunajua kiasi cha kila kinachopunguzwa na ardhi kutokana nao. Na kwetu kipo Kitabu kinachohifadhi vyema yote.

(5) Lakini waliikanusha Haki ilipowajia; kwa hivyo wamo katika mambo ya mchanganyiko.

(6) Je, hawaangalii mbingu zilizo juu yao! Vipi tulivyozijenga, na tukazipamba. Wala hazina nyufa.

(7) Na ardhi tumeitandaza na tukaiwekea milima, na tukaiotesha mimea mizuri ya kila namna.

(8) Yawe haya ni kifumbua macho na ukumbusho kwa kila mja mwenye kurejea (kwa Mwenyezi Mungu).

(9) Na tumeteremsha kutoka mbinguni maji yaliyobarikiwa, na kwa hayo tukaotesha mabustani na nafaka za kuvunwa.

(10) Na mitende mirefu yenye makole yaliyozaa kwa wingi.

(11) Ili iwe ni riziki kwa waja wangu. Na tukaifufua kwa maji nchi iliyokuwa imekufa. Kama hivyo ndivyo utakavyokuwa ufufuaji.

(12) Kabla yao walikadhibisha kaumu ya Nuhu na wakazi wa Rassi na Thamudi.

(13) Na A'di na Firauni na kaumu ya Luti.

(14) Na wakazi wa Machakani, na watu wa Tubbaa'. Wote hao waliwakanusha Mitume, kwa hivyo onyo likathibitika juu yao.

(15) Kwani tulichoka kwa kuumba mara ya kwanza? Bali wao wamo katika shaka tu juu ya umbo jipya.

(16) Na hakika tulimuumba mtu, nasi tunayajua yanayomtia wasiwasi katika nafsi yake. Na Sisi tuko karibu naye kuliko mshipa wa shingoni mwake.

(17) Wanapopokea wapokeaji wawili, wanaokaa kuliani na kushotoni.

(18) Hatamki neno ila karibu yake yupo mwangalizi tayari.

(19) Na uchungu wa kutoka roho utamjia kwa haki. Hayo ndiyo uliyokuwa ukiyakimbia.

(20) Na litapulizwa baragumu. Hiyo ndiyo Siku ya Miadi.

(21) Na kila nafsi itakuja na pamoja nayo mchungaji na shahidi.

(22) (Aambiwe): 'Kwa hakika ulikuwa umeghafilika mbali na haya. Basi leo tumekuondolea pazia lako, na kwa hivyo kuona kwako leo ni kukali mno.'

(23) Na mwenzake atasema: 'Huyu niliye naye mimi keshatayarishwa.

(24) Mtupeni katika Jahanamu kila kafiri mwenye inda.

(25) Akatazaye mno heri, arukaye mipaka, mwenye kutia shaka.

(26) Aliyeweka mungu mwengine pamoja na Mwenyezi Mungu. Basi mtupeni katika adhabu kali.'

(27) Mwenzake aseme: 'Ewe Mola wetu Mlezi! Sikumpoteza mimi, bali yeye mwenyewe alikuwa katika upotovu wa mbali.'

(28) (Mwenyezi Mungu) aseme: 'Msigombane mbele yangu. Tayari niliwaletea mbele onyo langu.

(29) Mbele yangu haibadilishwi kauli, wala Mimi siwadhulumu waja wangu.

(30) Siku tutakapoiambia Jahanamu: 'Je, umejaa?' Nayo itasema: 'Je, kuna ziada?'

(31) Na Bustani ya mbinguni italetwa karibu mno kwa ajili ya wacha Mungu, haitakuwa mbali.

(32) Haya ndiyo mnayoahidiwa kwa kila mwenye kurejea mno kwa Mwenyezi Mungu na akajilinda vyema.

(33) Mwenye kumwogopa mno Mwingi wa rehema hali kuwa hamwoni, na akaja kwa moyo uliotubia.

(34) (Ataambiwa) ingieni humo kwa salama. Hiyo ndiyo siku ya kudumu daima dawamu.

(35) Humo watapata wakitakacho, na kwetu yako ya ziada.

(36) Na kaumu ngapi tuliziangamiza kabla yao, waliokuwa na nguvu zaidi kuliko hawa! Nao walitanga tanga katika nchi nyingi. Je, walipata pa kukimbilia?

(37) Hakika katika hayo upo ukumbusho kwa mwenye moyo au akatega sikio naye yupo anashuhudia.

(38) Na bila ya shaka Sisi tumeziumba mbingu na ardhi na vilivyo baina yake katika siku sita; na wala hayakutugusa machofu yoyote.

(39) Basi vumilia kwa hayo wasemayo, na mtakase kwa kumsifu Mola wako Mlezi kabla ya kuchomoza jua na kabla ya kuchwa.

(40) Na katika usiku pia mtakase, na baada ya kusujudu.

(41) Na sikiliza siku atakaponadi mwenye kunadi kutoka mahali karibu.

(42) Siku watakaposikia ukelele wa haki. Hiyo ndiyo siku ya kufufuka.

(43) Hakika Sisi tunahuisha na tunafisha, na kwetu Sisi ndio marejeo.

(44) Siku itapowapasukia ardhi mbio mbio! Mkusanyo huo kwetu ni mwepesi.

(45) Sisi tunajua kabisa wayasemayo. Wala wewe si mwenye kuwatawalia kwa ujabari. Basi mkumbushe kwa Qur-ani anayeliogopa onyo.