(1) Hakika sisi tumekufungulia Ushindi wa dhahiri.
(2) Ili Mwenyezi Mungu akusamehe makosa yako yaliyotangulia na yajayo, na akutimizie neema zake, na akuongoe katika njia iliyonyooka.
(3) Na Mwenyezi Mungu akunusuru nusura yenye nguvu.
(4) Yeye ndiye aliyeteremsha utulivu katika nyoyo za Waumini ili wazidi Imani juu ya Imani yao. Na Mwenyezi Mungu ndiye mwenye majeshi ya mbingu na ardhi. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye elimu mno, Mwenye hekima.
(5) Ili awaingize Waumini wanaume na Waumini wanawake katika Bustani za mbinguni zipitazo mito chini yake, wadumu humo, na awafutie makosa yao. Na huko ndiko kufuzu kukubwa mbele ya Mwenyezi Mungu.
(6) Na awape adhabu wanafiki wanaume na wanafiki wanawake, na washirikina wanaume na washirikina wanawake, wanaomdhania Mwenyezi Mungu dhana mbaya. Utawafikia mgeuko mbaya, na Mwenyezi Mungu awakasirikie, na awalaani, na awaandalie Jahanamu. Na hayo ni marudio maovu kabisa.
(7) Na Mwenyezi Mungu ana majeshi ya mbingu na ardhi. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye hekima.
(8) Hakika tumekutuma wewe uwe Shahidi, na Mbashiri, na Mwonyaji.
(9) Ili mumuamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na mumsaidie, na mumheshimu, na mumtakase asubuhi na jioni.
(10) Bila ya shaka wale wanaokupa kiapo cha utii, kwa hakika wanampa Mwenyezi Mungu kiapo cha utii. Mkono wa Mwenyezi Mungu uko juu ya mikono yao. Kwa hivyo, avunjaye ahadi hizi, basi anavunja kwa kuidhuru nafsi yake. Na anayetekeleza aliyomuahadi Mwenyezi Mungu, basi Mwenyezi Mungu atamlipa ujira mkubwa.
(11) Watakuambia mabedui waliobaki nyuma: 'Zimetushughulisha mali zetu na ahali zetu, basi tuombee msamaha.' Wanasema kwa ndimi zao yasiyokuwamo katika nyoyo zao. Sema: 'Ni nani awezaye kukusaidieni chochote kwa Mwenyezi Mungu akitaka Yeye kuwadhuru au akitaka kuwanufaisha? Bali Mwenyezi Mungu anazo habari za mnayoyatenda.'
(12) Lakini mlidhani kwamba Mtume na Waumini hawatarudi kabisa kwa ahali zao, na mkapambiwa hayo katika nyoyo zenu, na mkadhania dhana mbaya, na mkawa watu wanaoangamia.
(13) Na asiyemuamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, basi kwa hakika Sisi tumewaandalia makafiri Moto mkali.
(14) Na Mwenyezi Mungu ndiye mwenye ufalme wa mbingu na ardhi. Humsamehe amtakaye, na humuadhibu amtakaye. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe muno, Mwingi wa kurehemu.
(15) Wale waliobaki nyuma watasema: 'Mtakapokwenda kuchukua ngawira, tuacheni tukufuateni!' Wanataka kuyabadili maneno ya Mwenyezi Mungu. Sema: 'Hamtatufuata kabisa. Mwenyezi Mungu alikwisha sema hivi zamani.' Hapo watasema: 'Bali nyinyi mnatuhusudu.' Sivyo, bali walikuwa hawafahamu ila kidogo.
(16) Waambie wale walioachwa nyuma katika mabedui: 'Mtakuja itwa kwenda kupigana na watu wakali kwa vita, mpigane nao au wasalimu amri. Basi mkimtii, Mwenyezi Mungu atawapa ujira mzuri. Na mkigeuka kama mlivyogeuka kwanza, atawaadhibu kwa adhabu iliyo chungu.'
(17) Kipofu hana lawama, wala kiguru hana lawama, wala mgonjwa hana lawama. Na mwenye kumtii Mwenyezi Mungu na Mtume wake, atamuingiza katika Mabustani ya mbinguni yapitayo mito chini yake. Na atakayegeuka upande, atamuadhibu kwa adhabu chungu.
(18) Kwa hakika Mwenyezi Mungu amewapa radhi Waumini walipokupa ahadi ya utii chini ya mti, na alijua yaliyomo nyoyoni mwao. Basi akateremsha utulivu juu yao, na akawalipa kwa Ushindi wa karibu.
(19) Na ngawira nyingi watakazozichukua. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye hekima.
(20) Mwenyezi Mungu anawaahidi ngawira nyingi mtakazozichukua, basi amewatangulizia hizi kwanza, na akaizuia mikono ya watu isiwafikie, na ili hayo yawe ni Ishara kwa Waumini, na akawaongoza njia iliyonyooka.
(21) Na yale mengine hamwezi kuyapata bado, Mwenyezi Mungu amekwisha yazingira. Na Mwenyezi Mungu ni Muweza mno wa kila kitu.
(22) Na lau makafiri wangelipigana nanyi, basi bila ya shaka wangeligeuza migongo, kisha wasingelipata mlinzi wala msaidizi.
(23) Huo ndio mwendo wa Mwenyezi Mungu uliokwisha pita zamani, wala hutapata mabadiliko katika mwendo wa Mwenyezi Mungu.
(24) Na Yeye ndiye aliyeizuia mikono yao kwenu, na mikono yenu kwao, katika bonde la Makka baada ya kuwapeni Ushindi juu yao. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kuyaona mno myatendayo.
(25) Hao ndio waliokufuru na wakawazuia msiingie Msikiti Mtakatifu, na wakawazuilia dhabihu kufika mahala pao. Na lau si wanaume Waumini na wanawake Waumini msiowajua mkawasaga na mkaingia makosani kutokana nao bila ya kujua... Mwenyezi Mungu (amefanya haya) ili amuingize amtakaye katika rehema yake. Lau wangelitengana, bila ya shaka tungeliwaadhibu wale waliokufuru kwa adhabu chungu.
(26) Pale wale waliokufuru walipotia katika nyoyo zao hasira, hasira za kijinga, Mwenyezi Mungu aliteremsha utulivu juu ya Mtume wake na juu ya Waumini, na akawalazimisha neno la kumcha Mungu. Na wao walikuwa ndio wenye haki nalo na wenye kustahili. Na Mwenyezi Mungu ni mwenye kujua mno kila kitu.
(27) Hakika Mwenyezi Mungu amemtimizia Mtume wake ndoto ya haki. Bila ya shaka nyinyi mtauingia Msikiti Mtakatifu, Inshallah (Mwenyezi Mungu akipenda), kwa amani, na hali mmenyoa vichwa vyenu na mmepunguza nywele. Hamtakuwa na hofu. Yeye anajua msiyoyajua. Basi atawapea kabla ya haya Ushindi karibuni.
(28) Yeye ndiye aliyemtuma Mtume wake kwa uwongofu na Dini ya Haki, ili aipe ushindi juu ya dini zote. Na Mwenyezi Mungu anatosha kuwa Shahidi.
(29) Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu. Na wale walio pamoja naye wana nguvu mbele ya makafiri, na wanahurumiana wao kwa wao. Utawaona wakiinama na kusujudu wakitafuta fadhila na radhi za Mwenyezi Mungu. Alama zao zi katika nyuso zao, kutokana na athari ya kusujudu. Huu ndio mfano wao katika Taurati. Na mfano wao katika Injili ni kama mmea uliotoa chipukizi lake, kisha ukalitia nguvu, ukawa mnene, ukasimama sawa juu ya ubuwa wake, ukawafurahisha wakulima, ili kuwakasirisha kwa ajili yao makafiri. Mwenyezi Mungu amewaahidi wale walioamini na wakatenda mema katika wao msamaha na ujira mkubwa.