(1) Litakapotokea hilo Tukio.
(2) Hapana cha kukanusha kutokea kwake.
(3) Literemshalo linyanyualo.
(4) Itakapotikiswa ardhi kwa mtikiso.
(5) Na milima itakaposagwasagwa.
(6) Basi iwe mavumbi yanayopeperushwa.
(7) Na nyinyi mtakuwa namna tatu.
(8) Basi watakuwepo wa kuliani; je, ni wepi wa kuliani?
(9) Na wa kushotoni; je, ni wepi wa kushotoni?
(10) Na wa mbele watakuwa mbele.
(11) Hao ndio watakaowekwa karibu (na Mwenyezi Mungu).
(12) Katika Bustani zenye neema.
(13) Fungu kubwa katika wa mwanzo.
(14) Na wachache katika wa mwisho.
(15) Watakuwa juu ya viti vya fakhari vilivyotonewa.
(16) Wakiviegemea wakielekeana.
(17) Wakitumikiwa na wavulana wa ujana wa milele.
(18) Kwa vikombe na mabirika na bilauri za vinywaji kutoka chemichemi safi.
(19) Hawataumwa kichwa kwa vinywaji hivyo wala hawatoleweshwa.
(20) Na matunda wayapendayo.
(21) Na nyama za ndege kama wanavyotamani.
(22) Na Mahurulaini.
(23) Walio kama mfano wa lulu zilizohifadhiwa.
(24) Ni malipo kwa waliyokuwa wakiyatenda.
(25) Humo hawatasikia porojo wala maneno ya dhambi.
(26) Isipokuwa maneno ya Salama, Salama.
(27) Na wale wa mkono wa kulia, ni yepi yatakuwa ya wa kuliani?
(28) Katika mikunazi isiyo na miba.
(29) Na migomba iliyopangiliwa.
(30) Na kivuli kilichotanda.
(31) Na maji yanayomiminika.
(32) Na matunda mengi.
(33) Hayatindikii wala hayakatazwi.
(34) Na matandiko yaliyonyanyuliwa.
(35) Hakika Sisi tutawaumba (Mahurulaini) upya.
(36) Na tutawafanya vijana.
(37) Wanapendana na waume zao, hirimu moja.
(38) Kwa ajili ya watu wa kuliani.
(39) Fungu kubwa katika wa mwanzo.
(40) Na fungu kubwa katika wa mwisho.
(41) Na watu wa kushotoni; je ni yepi ya wa kushotoni?
(42) Katika upepo wa moto, na maji yanayochemka.
(43) Na kivuli cha moshi mweusi.
(44) Si baridi wala cha kustarehesha.
(45) Hakika hao walikuwa kabla ya haya wakiishi maisha ya anasa.
(46) Na walikuwa wakiendelea tu kufanya madhambi makubwa.
(47) Na walikuwa wakisema: 'Tutakapokufa na tukawa udongo na mafupa, ati ndiyo tutafufuliwa?
(48) Au baba zetu wa zamani?'
(49) Sema: 'Hakika wa zamani na wa mwisho.'
(50) Bila ya shaka watakusanywa kwa wakati wa siku maalumu.
(51) Kisha nyinyi, mliopotea, mnaokanusha.
(52) Kwa yakini mtakula mti wa Zaqqumu.
(53) Na kwa mti huo mtajaza matumbo.
(54) Na juu yake mtakunywa maji yanayochemka.
(55) Tena mtakunywa kama wanavyokunywa ngamia wenye kiu.
(56) Hiyo ndiyo karamu yao ya kuwakaribisha Siku ya Malipo.
(57) Sisi tumekuumbeni; basi hamsadiki?
(58) Je, mnaiona mbegu ya uzazi mnayoidondokesha?
(59) Je, mnaiumba nyinyi, au ni Sisi ndio Waumbaji?
(60) Sisi tumekuwekeeni mauti; na wala Sisi hatushindwi.
(61) Kuwaleta wengine badala yenu na kukuumbeni nyinyi kwa umbo msilolijua.
(62) Na bila ya shaka mlikwisha jua umbo la kwanza, basi kwa nini hamkumbuki?
(63) Je, mnaona hivyo mnavyovipanda?
(64) Je, ni nyinyi mnayoyaotesha au ni Sisi ndio wenye kuotesha?
(65) Tungelitaka, tungeliyafanya yakawa mapepe, mkabaki mnastaajabu.
(66) Mkisema: 'Hakika sisi tumegharimika.'
(67) Bali sisi tumenyimwa.
(68) Je, mnayaona maji mnayoyanywa?
(69) Je, ni nyinyi mnaoyateremsha kutoka mawinguni au ni Sisi ndio wenye kuyateremsha?
(70) Tungelipenda, tungeliyafanya ya chumvi. Basi mbona hamshukuru?
(71) Je, mnauona moto mnaouwasha?
(72) Ni nyinyi mliouumba mti wake au Sisi ndio Waumbaji?
(73) Sisi tumeufanya uwe ni ukumbusho na manufaa kwa walioko nyikani.
(74) Basi litakase jina la Mola wako Mlezi aliye Mkuu.
(75) Basi ninaapa kwa maanguko ya nyota.
(76) Na hakika bila ya shaka hiki ni kiapo kikubwa, laiti mngelijua!
(77) Hakika hii bila ya shaka ni Qur-ani Tukufu.
(78) Katika Kitabu kilichohifadhiwa.
(79) Hapana akigusaye ila waliotakaswa.
(80) Ni uteremsho unaotoka kwa Mola Mlezi wa walimwengu wote.
(81) Ni maneno haya ndiyo nyinyi mnayapuuza?
(82) Na badala ya kushukuru kwa riziki yenu mnafanya kuwa mnakadhibisha?
(83) Yawaje basi itakapofika roho kwenye koo.
(84) Na nyinyi wakati huo mnatazama!
(85) Na Sisi tuko karibu zaidi naye kuliko nyinyi, lakini hamuoni.
(86) Na lau kuwa nyinyi hamumo katika mamlaka yangu.
(87) Kwa nini hamuirudishi hiyo roho, ikiwa nyinyi mnasema kweli?
(88) Kwa hivyo, akiwa miongoni mwa wale walio karibu na Mwenyezi Mungu.
(89) Basi ni raha, na manukato, na Bustani zenye neema.
(90) Na akiwa katika wale wa upande wa kulia.
(91) Basi ni Salamu kwako uliye miongoni mwa wale wa upande wa kulia.
(92) Na ama akiwa katika wale waliokadhibisha, wapotovu.
(93) Basi karamu ya makaribisho yake ni maji yanayochemka.
(94) Na kutiwa Motoni.
(95) Hakika hii ndiyo haki yenye yakini.
(96) Basi litakase jina la Mola wako Mlezi aliye Mkuu.