60 - Surat Al-Mumtahanah ()

|

(1) Enyi mlioamini! Msiwafanye adui zangu na adui zenu kuwa marafiki mkiwapa mapenzi, na hali wao wamekwisha ikataa haki iliyokujieni, wakamfukuza Mtume na nyinyi kwa sababu mnamuamini Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wenu. Mnapotoka kwa ajili ya Jihadi katika Njia yangu na kutafuta radhi yangu, mnafanya urafiki nao kwa siri, na Mimi nayajua mnayoyaficha na mnayodhihirisha. Na mwenye kufanya hayo kati yenu, basi ameipotea njia ya sawa.

(2) Wakikuwezeni, wanakuwa maadui zenu, na wanakukunjulieni mikono yao na ndimi zao kwa uovu. Na wanapenda muwe makafiri.

(3) Hawatakufaeni jamaa zenu, wala watoto wenu Siku ya Kiyama. Mwenyezi Mungu atapambanua baina yenu, na Mwenyezi Mungu anayaona mno mnayoyatenda.

(4) Hakika nyinyi mna mfano mzuri kwenu kwa Ibrahim na wale waliokuwa pamoja naye, walipowaambia watu wao: Hakika sisi tumejitenga nanyi na hayo mnayoyaabudu badala ya Mwenyezi Mungu. Tunakukataeni; na umekwisha dhihiri uadui na chuki baina yetu na nyinyi mpaka mtakapomuamini Mwenyezi Mungu peke yake. Isipokuwa kauli ya Ibrahim kumwambia baba yake: Hakika nitakuombea msamaha, wala similiki chochote kwa ajili yako mbele ya Mwenyezi Mungu. Mola wetu Mlezi! Juu yako tumetegemea, na kwako tumeelekea, na kwako ndiyo marejeo.

(5) Mola wetu Mlezi! Usitufanyie mtihani kwa waliokufuru. Na tusamehe, Mola wetu Mlezi. Hakika Wewe ndiye Mwenye nguvu, Mwenye hekima.

(6) Kwa yakini umekuwa mfano mzuri kwenu katika mwendo wao, kwa anayemtarajia Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho. Na mwenye kugeuka, basi hakika Mwnyezi Mungu ni Mwenye kujitosha, Msifiwa mno.

(7) Asaa Mwenyezi Mungu akatia mapenzi baina yenu na hao maadui zenu, na Mwenyezi Mungu ni Mweza, na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe zaidi, Mwenye kurehemu mno.

(8) Mwenyezi Mungu hakukatazini kuwafanyia wema na uadilifu wale ambao hawakukupigeni vita, wala hawakukutoeni makwenu. Hakika Mwenyezi Mungu huwapenda wafanyao uadilifu.

(9) Hakika Mwenyezi Mungu anakukatazeni kufanya urafiki wa kusaidiana nao, na wale waliokupigeni vita kwa sababu ya dini, na wakakutoeni makwenu, na wakasaidia katika kufukuzwa kwenu. Na wanaowafanya hao marafiki, basi hao ndio madhalimu.

(10) Enyi mlioamini! Wakikujilieni wanawake Waumini waliohama, basi wafanyieni mtihani - Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kujua zaidi Imani yao. Mkiwa mnawajua kuwa ni Waumini, basi msiwarudishe kwa makafiri. Wanawake hao si halali kwa hao makafiri, wala hao makafiri hawahalalikii wanawake Waumini. Na wapeni hao wanaume mahari waliotoa. Wala hapana makosa kwenu kuwaoa mkiwapa mahari yao. Wala msiwaweke wanawake makafiri katika kifungo cha ndoa zenu. Na takeni mlichokitoa, na wao watake walichokitoa. Hiyo ndiyo hukumu ya Mwenyezi Mungu anayokuhukumuni. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujua mno, Mwenye hekima.

(11) Na akitoroka yeyote katika wake zenu kwenda kwa makafiri, tena ikatokea mkapata ngawira, basi wapeni waliokimbiwa na wake zao kiasi cha mahari waliyoyatoa. Na mcheni Mwenyezi Mungu ambaye mnamuamini.

(12) Ewe Nabii! Watakapokujia wanawake Waumini wanakuahidi ya kwamba hawatamshirikisha Mwenyezi Mungu na chochote, wala hawataiba, wala hawatazini, wala hawatawauwa watoto wao, wala hawataleta uzushi wanaouzua tu wenyewe baina ya mikono yao na miguu yao, wala hawatakuasi katika jambo jema, basi peana nao ahadi, na uwatakie maghfira kwa Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa maghfira, Mwenye kurehemu mno.

(13) Enyi mlioamini! Msiwafanye marafiki wa kusaidiana nao katika watu ambao Mwenyezi Mungu amewakasirikia. Hao wamekwisha kata tamaa ya Akhera, kama makafiri walivyowakatia tamaa watu wa makaburini.