45 - Surat Al-Jathiyah ()

|

(1) Ha, Mim.

(2) Uteremsho wa Kitabu umetoka kwa Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, Mwenye hekima.

(3) Hakika katika mbingu na ardhi ziko Ishara kwa Waumini.

(4) Na katika umbo lenu na katika wanyama aliowatawanya, zimo Ishara kwa watu wenye yakini.

(5) Na kupishana usiku na mchana, na riziki anayoiteremsha Mwenyezi Mungu kutoka mbinguni, na kwayo akaifufua ardhi baada ya kufa kwake, na mabadiliko ya upepo, ni Ishara kwa watu wenye akili.

(6) Hizi Aya za Mwenyezi Mungu tunakusomea kwa haki; basi hadithi gani watakayoiamini baada ya Mwenyezi Mungu na Aya zake?

(7) Ole wake kila mzushi mwenye dhambi!

(8) Anayesikia Aya za Mwenyezi Mungu akisomewa, kisha anashikilia yale yale aliyokatazwa, na anajivuna, kama kwamba hakuzisikia. Basi mbashirie adhabu chungu!

(9) Na anapokijua kitu kidogo katika Aya zetu, hukifanyia mzaha. Watu hao ndio watakaokuwa na adhabu ya kufedhehesha.

(10) Na nyuma yao ipo Jahanamu. Na waliyoyachuma hayatawafaa hata kidogo, wala walinzi waliowashika badala ya Mwenyezi Mungu. Na watapata adhabu kubwa.

(11) Huu ni uwongofu. Na wale wale waliozikataa Ishara za Mola wao Mlezi watapata adhabu inayotokana na ghadhabu, iliyo chungu.

(12) Mwenyezi Mungu ndiye aliyeifanya bahari ikutumikieni, ili humo zipite merikebu kwa amri yake, na ili mtafute fadhila yake, na ili mpate kushukuru.

(13) Na amefanya vikutumikieni vilivyomo mbinguni na vilivyomo katika ardhi, vyote vimetoka kwake. Hakika katika hayo zimo Ishara kwa watu wanaofikiri.

(14) Waambie walioamini wawasamehe wale wasiozitaraji siku za Mwenyezi Mungu, ili awalipe kwa waliyokuwa wakiyachuma.

(15) Mwenye kutenda mema basi ni kwa ajili ya nafsi yake, na mwenye kutenda uovu ni juu yake mwenyewe. Kisha mtarudishwa kwa Mola wenu Mlezi.

(16) Na hakika tuliwapa Wana wa Israili Kitabu, hukumu na Unabii, na tukawaruzuku vitu vizuri vizuri, na tukawafadhilisha kuliko walimwengu wote.

(17) Na tukawapa maelezo wazi ya amri. Basi hawakuhitalifiana ila baada ya kuwajia elimu kwa sababu ya uhasidi uliokuwa baina yao. Hakika Mola wako Mlezi atahukumu baina yao Siku ya Kiyama katika mambo waliyokuwa wakihitilafiana.

(18) Kisha tukakuweka wewe juu ya Njia ya haya mambo, basi ifuate, wala usifuate matamanio ya wasiojua kitu.

(19) Kwa hakika hao hawatakufaa kitu mbele ya Mwenyezi Mungu. Na hakika wenye kudhulumu ni marafiki wao kwa wao. Na Mwenyezi Mungu ni rafiki msaidizi wa wamchao.

(20) Hizi ni dalili zilizo wazi kwa watu wote, na ni uwongofu na rehema kwa watu wenye yakini.

(21) Je, wanadhani wale wanaotenda maovu kuwa tutawafanya wawe sawa sawa na wale walioamini, na wakatenda mema, uhai wao na kufa kwao? Ni hukumu mbaya mno wanayoihukumu!

(22) Na Mwenyezi Mungu ameziumba mbingu na ardhi kwa haki, na ili kila nafsi ilipwe yale iliyoyachuma. Nao hawatadhulumiwa.

(23) Je, umemwona aliyefanya matamanio yake kuwa ndiye mungu wake, na Mwenyezi Mungu akampoteza pamoja na kuwa ana elimu, na akaziba masikio yake, na moyo wake, na akambandika vitanga machoni mwake? Basi ni nani atamwongoa huyo baada ya Mwenyezi Mungu? Je, hamkumbuki?

(24) Na walisema: 'Hapana ila huu uhai wetu wa duniani - twafa na twaishi, na hapana kinachotuangamiza isipokuwa dahari.' Lakini wao hawana elimu ya hayo, ila wao wanadhani tu.

(25) Na wakisomewa Aya zetu zilizo wazi hawana hoja ila kusema: 'Waleteni baba zetu, ikiwa nyinyi ni wasemao kweli.'

(26) Sema: 'Mwenyezi Mungu anawahuisha, kisha anawafisha, kisha anawakusanya Siku ya Kiyama isiyo na shaka. Lakini watu wengi hawajui.'

(27) Na Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye ufalme wa mbingu na ardhi. Na siku itakaposimama Saa ya Kiyama, siku hiyo wataangamia wenye kushikamana na upotovu.

(28) Na utauona kila umma umepiga magoti, na kila umma utaitwa kwenda kusoma kitabu chake: Leo mtalipwa mliyokuwa mkiyatenda.

(29) Hiki kitabu chetu kinasema juu yenu kwa haki. Hakika Sisi tulikuwa tukiyaandika mliyokuwa mkiyatenda.

(30) Ama walioamini na wakatenda mema, Mola wao Mlezi atawatia katika rehema yake. Huko ndiko kufuzu kuliko wazi.

(31) Na ama waliokufuru wataambiwa: 'Kwani hamkuwa mkisomewa Aya zangu nanyi mkapanda kichwa, na mkawa watu wakosefu?'

(32) Na ikisemwa: Hakika ahadi ya Mwenyezi Mungu ni kweli na Saa haina shaka, nyinyi mlikuwa mkisema: Hatuijui hiyo Saa, tunadhania dhana tu, wala hatuna yakini.

(33) Basi ubaya wa yale waliyoyatenda utawadhihirikia, na yatawafika yale waliyokuwa wakiyafanyia masihara.

(34) Na itasemwa: 'Leo tunawasahau kama nyinyi mlivyosahau mkutano wa siku yenu hii; na mahali penu ni Motoni, wala hamna wa kuwanusuru.'

(35) Hayo ni kwa sababu nyinyi mlizifanyia mzaha Aya za Mwenyezi Mungu, na maisha ya dunia yakawadanganya. Basi leo hawatatolewa humo wala hao hawatakubaliwa udhuru wao.

(36) Basi sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa mbingu na Mola Mlezi wa ardhi, na Mola Mlezi wa walimwengu wote.

(37) Na ukubwa ni wake Yeye tu, mbinguni na katika ardhi, naye ni Mwenye nguvu, Mwenye hekima.