63 - Surat Al-Munafiqun ()

|

(1) Wanapokujia wanafiki husema: Tunashuhudia ya kuwa wewe ni Mtume wa Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu anajua kuwa wewe ni Mtume wake, na Mwenyezi Mungu anashuhudia ya kuwa hakika wanafiki ni waongo.

(2) Wamevifanya viapo vyao ni ngao, na wao wakaizuia Njia ya Mwenyezi Mungu. Hakika ni mabaya kabisa waliyokuwa wakiyafanya.

(3) Hayo ni kwa sababu ya kuwa waliamini, kisha wakakufuru; kwa hivyo umeziziba nyoyo zao. Kwa hivyo hawafahamu lolote.

(4) Na unapowaona, miili yao inakupendeza, na wakisema, unasikiliza usemi wao. Lakini wao ni kama magogo yaliyoegemezwa. Wao hudhania kila ukelele unaopigwa ni kwa ajili yao. Hao ni maadui; tahadhari nao. Mwenyezi Mungu awaangamizilie mbali! Vipi wanapotoka mbali na haki?

(5) Na wanapoambiwa: Njooni ili Mtume wa Mwenyezi Mungu akuombeeni maghfira, huvigeuza vichwa vyao, na unawaona wanageuka nao wamejaa kiburi.

(6) Sawa sawa kwao, ukiwatakia maghfira au hukuwatakia maghfira, Mwenyezi Mungu hatawaghufiria. Hakika Mwenyezi Mungu hawaongoi watu wavukao mipaka.

(7) Hao ndio wanaosema: Msitoe mali kwa ajili ya walioko kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu, ili waondokelee mbali! Na Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye hazina za mbingu na ardhi, lakini wanafiki hawafahamu.

(8) Wanasema: Tukirejea Madina mwenye utukufu zaidi bila ya shaka atamfukuza aliye mnyonge. Na Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye utukufu - Yeye, na Mtume wake, na Waumini. Lakini wanafiki hawajui.

(9) Enyi mlioamini! Yasikusahaulisheni mali yenu, wala watoto wenu, kumkumbuka Mwenyezi Mungu. Na wenye kufanya hayo, basi hao ndio waliohasiri.

(10) Na toeni katika tulichokupeni kabla hayajamfikia mmoja wenu mauti, tena hapo akasema: 'Mola wangu Mlezi! Huniakhirishi muda kidogo, nipate kutoa sadaka sana, na niwe katika watu wema?'

(11) Wala Mwenyezi Mungu hataiakhirisha nafsi yoyote unapofika muda wake. Na Mwenyezi Mungu anazo habari za mnayoyatenda.