69 - Surat Al-Haqqah ()

|

(1) Tukio la haki.

(2) Nini hilo Tukio la haki?

(3) Na nini kitakujulisha nini hilo Tukio la haki?

(4) Thamudi na A'di waliukadhibisha Msiba unaositusha.

(5) Basi Thamudi waliangamizwa kwa balaa kubwa mno.

(6) Na ama A'di waliangamizwa kwa upepo mkali usiozuilika.

(7) Aliowapelekea masiku saba, na siku nane, mfululizo bila ya kusita. Utaona watu wamepinduka kama kwamba ni magongo ya mitende yaliyo wazi ndani.

(8) Basi je! Unamwona mmoja wao aliyebaki?

(9) Na Firauni na waliomtangulia, na miji iliyopinduliwa chini juu, walileta khatia.

(10) akamuasi Mtume wa Mola wao Mlezi, ndipo Yeye Mola akawakamata kwa mkamato uliozidi nguvu.

(11) Maji yalipofurika Sisi tulikupandisheni katika safina.

(12) Ili tuyafanye hayo kuwa ni waadhi kwenu na kila sikio linalosikia liyahifadhi.

(13) Na litapopulizwa barugumu mpulizo mmoja tu.

(14) Na ardhi na milima ikaondolewa, na ikavunjwa kwa mvunjo mmoja.

(15) Siku hiyo ndio Tukio litatukia.

(16) Na mbingu zitapasuka, kwani siku hiyo zitakuwa dhaifu kabisa.

(17) Na Malaika watakuwa pembezoni mwa mbingu; na wanane juu ya hawa watakuwa wamebeba Kiti cha Enzi cha Mola wako Mlezi.

(18) Siku hiyo mtahudhurishwa - haitafichika siri yoyote yenu.

(19) Basi ama atakayepewa kitabu chake kwa mkono wake wa kulia, atasema: Haya someni kitabu changu!

(20) Hakika nilijua ya kuwa nitapokea hisabu yangu.

(21) Basi yeye atakuwa katika maisha ya kupendeza.

(22) Katika Bustani ya juu.

(23) Matunda yake ya karibu.

(24) Waambiwe: Kuleni na mnywe kwa furaha kwa sababu ya mlivyotanguliza katika siku zilizopita.

(25) Na ama atakayepewa kitabu chake katika mkono wake wa kushoto, basi yeye atasema: Laiti nisingelipewa kitabu changu!

(26) Wala nisingelijua nini hisabu yangu.

(27) Laiti mauti ndiyo yangelikuwa ya kunimaliza kabisa.

(28) Mali yangu hayakunifaa kitu.

(29) Madaraka yangu yamenipotea.

(30) (Pasemwe): Mshikeni! Mtieni pingu!

(31) Kisha mtupeni Motoni!

(32) Tena mtatizeni katika mnyororo wenye urefu wa dhiraa sabini!

(33) Kwani huyo hakika alikuwa hamuamini Mwenyezi Mungu Mtukufu.

(34) Wala hahimizi kulisha masikini.

(35) Basi leo hapa hana jamaa wa kumwonea uchungu.

(36) Wala hana chakula ila usaha wa watu wa Motoni.

(37) Chakula hicho hawakili ila wakosefu.

(38) Basi ninaapa kwa mnavyoviona.

(39) Na msivyoviona.

(40) Kwa hakika hii ni kauli iliyoletwa na Mjumbe mwenye heshima.

(41) Wala si kauli ya mtunga mashairi. Ni machache sana mnayoyaamini.

(42) Wala si kauli ya kuhani. Ni machache mnayoyakumbuka.

(43) Ni uteremsho utokao kwa Mola Mlezi wa walimwengu wote.

(44) Na lau kama angelituzulia baadhi ya maneno tu.

(45) Bila ya shaka tungelimshika kwa mkono wa kulia.

(46) Kisha kwa hakika tungelimkata mshipa mkubwa wa moyo!

(47) Na hapana yeyote katika nyinyi ambaye angeliweza kutuzuia.

(48) Kwa hakika hii ni mawaidha kwa wacha Mungu.

(49) Na hakika Sisi bila ya shaka tunajua kwamba miongoni mwenu wapo wanaokadhibisha.

(50) Na hakika bila ya shaka itakuwa ni majuto kwa wanaokataa.

(51) Na hakika hii bila ya shaka ni haki ya yakini.

(52) Basi litakase jina la Mola wako Mlezi Mtukufu.