72 - Surat Al-Jinn ()

|

(1) Sema: Imefunuliwa kwangu ya kuwa kundi moja la majini lilisikiliza, na likasema: Hakika sisi tumeisikia Qur-ani ya ajabu!

(2) Inaongoza kwenye uwongofu, kwa hivyo tumeiamini, wala hatutamshirikisha yeyote na Mola wetu Mlezi.

(3) Na kwa hakika utukufu wa Mola wetu Mlezi umetukuka kabisa; hana mke wala mwana.

(4) Na kwa hakika wapumbavu miongoni mwetu walikuwa wakisema uwongo uliopindukia mipaka juu ya Mwenyezi Mungu.

(5) Nasi tulidhani kuwa watu na majini hawamzulii uongo Mwenyezi Mungu.

(6) Na hakika walikuwako wanaume katika watu waliokuwa wakitafuta kujikinga kwa wanaume wa kijini; kwa hivyo wakawazidisha madhambi.

(7) Na kwa hakika wao walidhani, kama mlivyodhani nyinyi, ya kuwa Mwenyezi Mungu hatamleta Mtume.

(8) Nasi tulizigusa mbingu, na tukaziona zimejaa walinzi wenye nguvu na vimondo.

(9) Na hakika tulikuwa tukikaa humo katika baadhi ya makao ili kusikiliza; lakini sasa anayetaka kusikiliza atakuta kimondo kinamvizia!

(10) Nasi hatujui kama wanatakiwa shari wale wanaokaa kwenye ardhi au Mola wao Mlezi anawatakia uwongofu.

(11) Na hakika katika sisi wamo walio wema, na wengine wetu ni kinyume na hivyo. Tumekuwa njia mbali mbali.

(12) Nasi tulijua kuwa hatutomshinda Mwenyezi Mungu duniani, wala hatuwezi kumponyoka kwa kukimbia.

(13) Nasi tulipousikia uwongofu tuliuamini. Basi mwenye kumuamini Mola wake Mlezi basi haogopi kupunjwa wala kudhulumiwa.

(14) Na hakika wamo katika sisi Waislamu, na wamo kati yetu wanaoacha haki. Basi waliosilimu, hao ndio waliotafuta uwongofu.

(15) Na ama wanaoacha haki, hao watakuwa kuni za Jahannamu.

(16) Na lau kama wangelisimama sawasawa juu ya njia tungeliwanywesha maji kwa wingi.

(17) Ili tuwajaribu kwa hayo. Na anayepuuza kumkumbuka Mola wake Mlezi atamsukuma kwenye adhabu ngumu.

(18) Na hakika misikiti ni ya Mwenyezi Mungu, basi msimuabudu yeyote pamoja na Mwenyezi Mungu.

(19) Na hakika Mja wa Mwenyezi Mungu aliposimama kumwomba, wao walikuwa karibu kumzonga!

(20) Sema: Hakika mimi namwomba Mola wangu Mlezi, wala simshirikishi Yeye na yeyote.

(21) Sema: Mimi sina mamlaka ya kukudhuruni wala kukuongozeni.

(22) Sema: Hakika hapana yeyote awezaye kunilinda na Mwenyezi Mungu, wala sitapata pa kukimbilia isipokuwa kwake Yeye tu.

(23) Ila nifikishe Ujumbe utokao kwa Mwenyezi Mungu na risala zake. Na wenye kumuasi Mwenyezi Mungu na Mtume wake, basi hakika hao watapata Moto wa Jahannamu wadumu humo milele.

(24) Hata watakapo yaona wanayoahidiwa, ndipo watakapojua ni nani mwenye msaidizi dhaifu, na mchache wa idadi.

(25) Sema: Sijui kama yapo karibu hayo mnayoahidiwa, au Mola wangu Mlezi atayawekea muda mrefu.

(26) Yeye ndiye Mwenye kujua ya siri, wala hamdhihirishii yeyote ghaibu yake.

(27) Isipokuwa Mtume wake aliyemridhia. Naye huyo humwekea walinzi mbele yake na nyuma yake.

(28) Ili Yeye ajue kwamba wao wamefikisha ujumbe wa Mola wao Mlezi, na Yeye anayajua vyema yote waliyo nayo, na amedhibiti idadi ya kila kitu.